Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 17

Kubali Msaada wa Yehova wa Kuwapinga Roho Waovu

Kubali Msaada wa Yehova wa Kuwapinga Roho Waovu

“Tunapambana . . . dhidi ya majeshi ya roho waovu katika mahali pa kimbingu.”—EFE. 6:12.

WIMBO 55 Msiwaogope!

MUHTASARI *

1. Taja mojawapo ya mambo yenye kugusa moyo zaidi yanayoonyesha kwamba Yehova anatujali, kama andiko la Waefeso 6:10-13 linavyoonyesha. Eleza.

MOJAWAPO ya mambo yenye kugusa moyo zaidi yanayoonyesha kwamba Yehova anatujali tukiwa watumishi wake ni msaada anaotupatia ili tuwapinge maadui wetu. Maadui wetu wakuu ni Shetani na roho wake waovu. Yehova anatuonya kuhusu maadui hao, naye hutupatia kile tunachohitaji ili tuwapinge. (Soma Waefeso 6:10-13.) Tunapokubali msaada wa Yehova na kumtegemea kikamili, tunaweza kufanikiwa kumpinga Ibilisi. Tunaweza kuwa na uhakika kama ule ambao mtume Paulo alikuwa nao. Aliandika hivi: “Ikiwa Mungu yuko upande wetu, ni nani atakayekuwa dhidi yetu?”​—Rom. 8:31.

2. Tutazungumzia nini katika makala hii?

2 Tukiwa Wakristo wa kweli, hatusisimuliwi na mambo yanayomhusu Shetani na roho wake waovu. Badala yake, tunaelekeza fikira zetu katika kujifunza kumhusu Yehova na kumtumikia. (Zab. 25:5) Hata hivyo, tunahitaji kujua mbinu za msingi ambazo Shetani hutumia. Kwa nini? Ili tuepuke kudanganywa naye. (2 Kor. 2:11; maelezo ya chini) Katika makala hii, tutazungumzia njia moja kuu ambayo Shetani na roho waovu hutumia ili kuwapotosha watu. Pia, tutazungumzia jinsi tunavyoweza kuwapinga kwa mafanikio.

JINSI ROHO WAOVU WANAVYOWAPOTOSHA WATU

3-4. (a) Kuwasiliana na roho ni nini? (b) Idadi ya watu wanaoamini nguvu za kuwasiliana na roho ni kubwa kadiri gani?

3 Njia moja kuu ambayo Shetani na roho waovu hutumia ili kuwapotosha watu ni kupitia zoea la kuwasiliana na roho. Wale wanaojihusisha na zoea hilo hudai kwamba wanajua au kudhibiti mambo ambayo kwa kawaida wanadamu hawawezi kuyajua au kuyadhibiti. Kwa mfano, baadhi ya watu hudai kwamba wanaweza kujua hali za wakati ujao kwa kufanya uaguzi au kutazama nyota. Wengine hufanya ionekane ni kana kwamba wanawasiliana na watu waliokufa. Wengine hufanya mazingaombwe au uchawi, na hujaribu kuutumia ili kuwaloga wengine. *

4 Idadi ya watu wanaoamini nguvu za kuwasiliana na roho ni kubwa kadiri gani? Utafiti uliofanywa katika nchi 18 za Amerika ya Latini na Karibea ulionyesha kwamba theluthi moja ya watu waliofanyiwa utafiti wanaamini mazingaombwe, nguvu za uchawi, au ulozi, na idadi nyingine inayolingana na hiyo wanaamini kwamba inawezekana kuwasiliana na roho. Utafiti mwingine ulifanywa katika nchi 18 barani Afrika. Katika nchi hizo, zaidi ya nusu ya idadi ya watu waliofanyiwa utafiti huo walisema kwamba wanaamini nguvu za uchawi. Bila shaka, ni lazima tuwe macho ili tusinaswe na zoea la kuwasiliana na roho, haidhuru tunaishi wapi. Ukweli wa mambo ni kwamba Shetani ameazimia kuipotosha “dunia nzima inayokaliwa.”​—Ufu. 12:9.

5. Yehova anahisije kuhusu zoea la kuwasiliana na roho?

5 Yehova ni “Mungu wa ukweli.” (Zab. 31:5) Hivyo, anahisije kuhusu zoea la kuwasiliana na roho? Anachukizwa nalo! Yehova aliwaambia hivi Waisraeli: “Asipatikane miongoni mwenu mtu yeyote anayemteketeza motoni mwanawe au binti yake, mtu yeyote anayefanya uaguzi, mtu yeyote anayefanya uchawi, mtu yeyote anayetafuta ishara za ubashiri, mlozi, mtu yeyote anayewafunga wenzake kwa uchawi, mtu yeyote anayetafuta ushauri kutoka kwa watu wanaowasiliana na roho, mpiga ramli, au mtu yeyote anayetafuta habari kuhusu wafu. Kwa maana mtu yeyote anayefanya mambo haya ni chukizo kwa Yehova.” (Kum. 18:10-12) Wakristo hawako chini ya Sheria ambayo Yehova aliwapa Waisraeli. Hata hivyo, tunajua kwamba hisia zake kuhusu zoea la kuwasiliana na roho hazijabadilika.​—Mal. 3:6.

6. (a) Shetani hutumiaje zoea la kuwasiliana na roho ili kuwadhuru watu? (b) Kulingana na Mhubiri 9:5, ukweli kuhusu hali ya wafu ni nini?

6 Yehova anatuonya tuepuke zoea la kuwasiliana na roho kwa sababu anajua kwamba Shetani hulitumia ili kuwadhuru watu. Shetani hutumia zoea hilo kuendeleza mafundisho yake ya uwongo—kutia ndani uwongo wa kwamba wafu wanaendelea kuishi mahali pengine. (Soma Mhubiri 9:5.) Pia, Shetani hutumia zoea hilo ili kuwaogopesha watu na kuwafanya wamwache Yehova. Lengo lake ni kuwafanya watu wanaojihusisha na zoea la kuwasiliana na roho wawaamini roho waovu badala ya kumwamini Yehova.

JINSI TUNAVYOWAPINGA ROHO WAOVU

7. Yehova anatueleza nini?

7 Kama tulivyoona awali, Yehova anatueleza mambo tunayohitaji kujua ili tuepuke kupotoshwa na Shetani na roho waovu. Acheni tuzungumzie baadhi ya mambo tunayoweza kufanya ili tumpinge Shetani na roho waovu.

8. (a) Taja njia kuu ya kuwapinga roho waovu. (b) Andiko la Zaburi 146:4 linafunuaje uwongo wa Shetani kuhusu hali ya wafu?

8 Soma Neno la Mungu na kulitafakari. Hiyo ndiyo njia kuu ya kupinga uwongo unaoenezwa na roho waovu. Neno la Mungu ni kama upanga mkali unaoweza kufunua uwongo ambao Shetani anaendeleza. (Efe. 6:17) Kwa mfano, Neno la Mungu linafunua uwongo wa kwamba watu waliokufa wanaweza kuwasiliana na watu walio hai. (Soma Zaburi 146:4.) Pia, linatukumbusha kwamba ni Yehova pekee anayeweza kutabiri kwa usahihi mambo ya wakati ujao. (Isa. 45:21; 46:10) Tukisoma Neno la Mungu na kulitafakari kwa ukawaida, tutakuwa tayari kupinga na kuchukia uwongo ambao roho waovu wanataka tuamini.

9. Tunapaswa kuepuka mazoea gani ya kuwasiliana na roho?

9 Kataa kufanya jambo lolote linalohusiana na zoea la kuwasiliana na roho. Tukiwa Wakristo wa kweli, hatujihusishi na jambo lolote linalohusiana na zoea la kuwasiliana na roho. Kwa mfano, hatuendi kwa watu wanaowasiliana na roho au kutumia njia nyingine yoyote kuwasiliana na watu waliokufa. Kama tulivyoona katika makala iliyotangulia, tunaepuka desturi za mazishi zinazounga mkono imani ya kwamba watu waliokufa wanaendelea kuishi mahali pengine. Pia, hatujihusishi na unajimu au ubashiri ili kujaribu kujua mambo ya wakati ujao. (Isa. 8:19) Tunajua kwamba mazoea hayo yote ni hatari sana na yanaweza kufanya tuanze kushirikiana moja kwa moja na Shetani na roho waovu.

Waige Wakristo wa mapema kwa kuharibu kitu chochote ulicho nacho kinachohusiana na mambo ya uchawi na kwa kukataa burudani zinazohusisha zoea la kuwasiliana na roho waovu (Tazama fungu la 10 hadi 12)

10-11. (a) Baadhi ya watu katika karne ya kwanza walifanya nini walipojifunza kweli? (b) Kulingana na andiko la 1 Wakorintho 10:21, kwa nini tunapaswa kuwaiga Wakristo wa mapema, na tunaweza kuwaigaje?

10 Haribu vitu vyote vinavyohusiana na mambo ya uchawi. Katika karne ya kwanza, baadhi ya watu walioishi katika jiji la Efeso walikuwa na zoea la kuwasiliana na roho. Walipojifunza kweli, walifanya mabadiliko makubwa. “Idadi kubwa ya wale waliozoea kufanya uchawi wakakusanya vitabu vyao pamoja na kuviteketeza mbele ya kila mtu.” (Mdo. 19:19) Watu hao walichukulia kwa uzito suala la kuwapinga roho waovu. Vitabu vyao vya mambo ya uchawi vilikuwa vimewagharimu pesa nyingi. Lakini badala ya kuwapa wengine vitabu hivyo au kuviuza, waliviteketeza. Walihangaikia zaidi kumfurahisha Yehova badala ya kiasi cha pesa walichogharimika kuvinunua.

11 Tunaweza kuwaigaje Wakristo hao wa karne ya kwanza? Ni jambo la hekima kuharibu kitu chochote tulicho nacho kinachohusiana na mambo ya uchawi. Vitu hivyo vinatia ndani hirizi, talasimu, au vitu vingine ambavyo watu huvaa au kumiliki ili wajilinde dhidi ya roho waovu.​—Soma 1 Wakorintho 10:21.

12. Tunapaswa kujiuliza maswali gani kuhusu burudani tunazochagua?

12 Chunguza kwa makini burudani unazochagua. Jiulize: ‘Je, mimi husoma vitabu, magazeti, au makala za Intaneti zinazozungumzia mambo ya uchawi? Vipi kuhusu muziki ninaosikiliza, sinema na vipindi vya televisheni ninavyotazama, au michezo ya video ninayocheza? Je, burudani yoyote ninayochagua ina mambo yanayohusiana na zoea la kuwasiliana na roho? Je, inahusisha wanyonya-damu (vampires), mazimwi, au mambo yanayopita uwezo wa kibinadamu? Je, burudani hiyo inaonyesha kwamba mazingaombwe, uchawi, au laana ni vitumbuizo visivyo na madhara?’ Bila shaka, si burudani zote zinazohusisha masimulizi ya kuwaziwa au mambo yasiyo halisi zinazohusiana moja kwa moja na zoea la kuwasiliana na roho. Unapochanganua burudani yako, azimia kuepuka kabisa kitu chochote kinachomchukiza Yehova. Tungependa kufanya yote tunayoweza ili “kudumisha dhamiri safi” mbele za Mungu wetu.​—Mdo. 24:16. *

13. Tunapaswa kuepuka kufanya nini?

13 Epuka kuwasimulia wengine kuhusu roho waovu. Kuhusiana na hilo, tunapaswa kumwiga Yesu. (1 Pet. 2:21) Kabla ya kuja duniani Yesu aliishi mbinguni, na alijua mengi kuhusu Shetani na roho waovu. Lakini hakuwasimulia wengine mambo ambayo roho hao waovu walikuwa wamefanya. Yesu alitaka kuwa shahidi wa Yehova, si wakili wa kumtangaza Shetani. Tunaweza kumwiga Yesu kwa kuepuka kueneza hadithi kuhusu roho waovu. Badala ya kueneza hadithi kama hizo, kupitia maneno yetu tutaonyesha kwamba “moyo [wetu] umesisimuliwa na jambo jema,” yaani, ile kweli.​—Zab. 45:1.

Hatuhitaji kuwaogopa roho waovu. Yehova, Yesu, na malaika wana nguvu nyingi zaidi (Tazama fungu la 14 na 15) *

14-15. (a) Kwa nini hatupaswi kuwaogopa roho waovu? (b) Kuna uthibitisho gani kwamba Yehova anawalinda watu wake leo?

14 Usiwaogope roho waovu. Katika ulimwengu wa leo, mambo mabaya yanaweza kutupata. Ghafla, tunaweza kupatwa na aksidenti, ugonjwa, au hata kifo. Lakini hatupaswi kufikiri kwamba mambo hayo yamesababishwa na roho hao wasioonekana. Biblia hueleza kwamba “wakati na matukio yasiyotarajiwa” humpata yeyote. (Mhu. 9:11) Yehova ameonyesha kwamba ana nguvu nyingi kuliko roho waovu. Kwa mfano, Mungu hakumruhusu Shetani amuue Ayubu. (Ayu. 2:6) Katika siku za Musa, Yehova alionyesha kwamba ana nguvu nyingi kuliko makuhani wachawi wa Misri. (Kut. 8:18; 9:11) Kwa nguvu za Yehova, Yesu aliyetukuzwa alionyesha jinsi alivyo na nguvu nyingi kuliko Shetani na roho waovu alipowatupa chini duniani. Na hivi karibuni watatupwa katika shimo refu lisilo na mwisho ambapo hawataweza kumdhuru yeyote.​—Ufu. 12:9; 20:2, 3.

15 Tunajionea uthibitisho mwingi kwamba Yehova anawalinda watu wake leo. Fikiria hili: Tunahubiri na kufundisha kweli katika sehemu zote za dunia. (Mt. 28:19, 20) Kwa njia hiyo, tunafunua kazi za uovu za Ibilisi. Kwa hakika ikiwa Shetani angeweza, angekomesha utendaji wetu wote, lakini hawezi. Hivyo, hatuhitaji kuwaogopa roho waovu. Tunajua kwamba “macho ya Yehova yanaenda huku na huku duniani kote ili adhihirishe nguvu zake kwa niaba ya wale ambao moyo wao ni kamili kumwelekea yeye.” (2 Nya. 16:9) Ikiwa sisi ni waaminifu kwa Yehova, roho waovu hawawezi kutusababishia madhara ya kudumu.

BARAKA KWA WALE WANAOKUBALI MSAADA WA YEHOVA

16-17. Toa mfano unaoonyesha ujasiri unaohitajika ili kuwapinga roho waovu.

16 Tunahitaji ujasiri ili kuwapinga roho waovu, hasa tunapopingwa na marafiki au watu wetu wa ukoo wasio na nia mbaya. Lakini Yehova huwabariki wale wanaoonyesha ujasiri kama huo. Fikiria mfano wa Erica, dada anayeishi nchini Ghana. Erica alikuwa na umri wa miaka 21 alipokubali kujifunza Biblia. Akiwa binti ya kuhani wa kichawi, alitarajiwa kushiriki katika desturi ya kishirikina iliyohusisha kula nyama iliyotolewa kama dhabihu ya matambiko kwa miungu ya baba yake. Erica alipokataa kufanya hivyo, familia yake iliona kwamba ameidharau miungu hiyo. Familia yake iliamini kwamba miungu ingewaadhibu kwa kuwasababishia magonjwa ya akili na ya kimwili.

17 Familia ya Erica ilijaribu kumlazimisha afuate desturi hiyo, lakini alikataa, ingawa kufanya hivyo kungemaanisha aondoke nyumbani. Mashahidi fulani walimkaribisha aishi pamoja nao. Kwa njia hiyo, Yehova alimbariki Erica kwa kumpa familia mpya, yaani, waamini wenzake waliokuwa kama ndugu na dada zake. (Marko 10:29, 30) Ingawa watu wake wa ukoo walimkataa na hata wakateketeza vitu vyake, Erica aliendelea kuwa mshikamanifu kwa Yehova, akabatizwa, na sasa yeye ni painia wa kawaida. Hawaogopi roho waovu. Na anaeleza hivi kuhusu familia yake: “Kila siku ninasali ili familia yangu ijionee baraka za kumjua Yehova na uhuru unaotokana na kumtumikia Mungu wetu mwenye upendo.”

18. Tunapata baraka zipi kwa kumtumaini Yehova?

18 Si kila mmoja wetu atakayelazimika kukabili jaribu kubwa kama hilo la imani. Hata hivyo, sisi sote tunahitaji kuwapinga roho waovu na kumtumaini Yehova. Tukifanya hivyo tutapata baraka nyingi, na hatutapotoshwa na uwongo wa Shetani. Pia, hatutawaogopa roho waovu hivi kwamba tuache kumtumikia Yehova. Zaidi ya yote, tutaimarisha urafiki wetu pamoja na Yehova. Mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “Jitiisheni kwa Mungu; lakini mpingeni Ibilisi, naye atawakimbia ninyi. Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.”​—Yak. 4:7, 8.

WIMBO 150 Mtafute Mungu Upate Ukombozi

^ fu. 5 Akichochewa na upendo, Yehova ametuonya kuhusu roho waovu na madhara wanayoweza kusababisha. Roho waovu hujaribu kuwapotosha watu jinsi gani? Ni hatua gani tunazoweza kuchukua ili kuwapinga? Makala hii itazungumzia jinsi Yehova anavyoweza kutusaidia ili tusiathiriwe na roho waovu.

^ fu. 3 UFAFANUZI WA MANENO: Maneno kuwasiliana na roho yanarejelea imani na mazoea yanayohusianishwa na roho waovu. Pia, yanarejelea imani ya kwamba roho za watu waliokufa huendelea kuishi baada ya mwili kufa na kwamba zinaweza kuwasiliana na watu walio hai, hasa kupitia mtu fulani (anayewasiliana na roho). Vilevile, kuwasiliana na roho kunatia ndani mazoea kama vile uchawi na kufanya uaguzi. Neno uchawi au mazingaombwe kama linavyotumika katika makala hii linarejelea mazoea yanayohusianishwa na nguvu za roho waovu, au nguvu zinazopita uwezo wa kibinadamu. Linaweza kutia ndani laana, kuwafunga wengine kwa uchawi au kuwafungua kutokana na uchawi. Halirejelei michezo ya kiini macho au kidanganya-macho ambayo baadhi ya watu hufanya ili kuwatumbuiza wengine.

^ fu. 12 Wazee wa makutaniko hawapaswi kuweka sheria zao kuhusu burudani. Badala yake, Mkristo mmoja-mmoja anapaswa kutumia dhamiri yake iliyozoezwa na Biblia anapochagua habari atakazosoma, sinema na vipindi vya televisheni atakavyotazama, au michezo ya video atakayocheza. Vichwa vya familia wenye hekima huhakikisha kwamba burudani zinazofurahiwa na familia zao zinapatana na kanuni za Biblia.​—Tazama makala kwenye jw.org/sw yenye kichwa, “Je, Mashahidi wa Yehova Huwakataza Wafuasi Wao Sinema, Vitabu, au Nyimbo Fulani?” kwenye KUTUHUSU > MASWALI YANAYOULIZWA MARA NYINGI.

^ fu. 54 MAELEZO YA PICHA: Mchoro unaoonyesha Yesu akiwa Mfalme mwenye nguvu mbinguni akiongoza jeshi la malaika. Kiti cha Ufalme cha Yehova kiko juu yao.