Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 16

Tetea Ukweli Kuhusu Kifo

Tetea Ukweli Kuhusu Kifo

“[Tunalitofautisha] neno la kweli lililoongozwa na roho na neno lenye kosa lililoongozwa na roho.”—1 YOH. 4:6.

WIMBO 73 Tupe Ujasiri

MUHTASARI *

Badala ya kushiriki katika desturi zinazomchukiza Mungu, wafariji watu wako wa ukoo mpendwa wenu anapokufa (Tazama fungu la 1 na 2) *

1-2. (a) Shetani amewadanganya watu jinsi gani? (b) Tutazungumzia nini katika makala hii?

SHETANI, “baba ya uwongo,” amekuwa akiwadanganya watu tangu wanadamu walipoumbwa. (Yoh. 8:44) Baadhi ya uwongo anaoendeleza ni mafundisho ya uwongo kuhusu kifo na kuhusu uhai baada ya kifo. Mafundisho hayo ndiyo msingi wa desturi nyingi zinazopendwa na watu leo na pia ushirikina. Kwa sababu hiyo, baadhi ya ndugu na dada zetu wamelazimika ‘kufanya pigano kali kwa ajili ya imani’ mtu fulani katika familia yao au jamii anapokufa.​—Yuda 3.

2 Ukikabili majaribu kama hayo, ni nini kinachoweza kukusaidia usimame imara na kuunga mkono mambo ambayo Biblia inafundisha kuhusu kifo? (Efe. 6:11) Unaweza kumfariji na kumwimarisha jinsi gani Mkristo mwenzako anayeshinikizwa ajihusishe katika desturi zinazomchukiza Mungu? Makala hii itazungumzia mwongozo ambao Yehova ametupatia. Kwanza, acheni tuzungumzie mambo ambayo Biblia inafundisha kuhusu kifo.

UKWELI KUHUSU HALI YA WAFU

3. Uwongo wa kwanza ulisababisha nini?

3 Mungu hakukusudia wanadamu wafe. Lakini ili waishi milele, Adamu na Hawa walipaswa kumtii Yehova aliyewapa amri hii rahisi: “Kuhusu mti wa ujuzi wa mema na mabaya, usile matunda yake, kwa maana siku utakapokula matunda yake hakika utakufa.” (Mwa. 2:16, 17) Kisha Shetani akatokea. Akizungumza kupitia nyoka, Shetani alimwambia Hawa hivi: “Hakika hamtakufa.” Inasikitisha kwamba Hawa aliamini uwongo huo na akala matunda hayo. Baadaye, mume wake pia akala matunda hayo. (Mwa. 3:4, 6) Kwa njia hiyo, dhambi na kifo vikaingia kwenye jamii ya wanadamu.​—Rom. 5:12.

4-5. Shetani anaendelea kuwadanganya wanadamu jinsi gani?

4 Adamu na Hawa walikufa kama Mungu alivyokuwa amesema. Lakini Shetani aliendelea kueneza uwongo kuhusu kifo. Baada ya muda fulani, alitunga uwongo mbalimbali kuhusu kifo. Mojawapo ya uwongo huo ni fundisho la kwamba mwili hufa lakini sehemu fulani ya mtu huendelea kuishi mahali fulani kwenye makao ya roho. Mafundisho mbalimbali kuhusu uwongo huo yamewapotosha watu wengi tangu ulipotungwa mpaka leo hii.​—1 Tim. 4:1.

5 Kwa nini watu wengi hivyo wamedanganyika? Shetani amefanikiwa kueneza uwongo huo kwa sababu anajua jinsi tunavyohisi kuhusu kifo. Kwa kuwa tuliumbwa tuishi milele, hatupendi kufa. (Mhu. 3:11) Tunakiona kifo kuwa adui.​—1 Kor. 15:26.

6-7. (a) Je, Shetani amefanikiwa kuficha ukweli kuhusu kifo? Eleza. (b) Kweli ya Biblia hutusaidiaje tusiwaogope wafu?

6 Licha ya jitihada za Shetani, ukweli kuhusu kifo haujafichika. Kwa kweli, leo kuliko wakati mwingine wowote, watu wengi wanajua na wanatangaza mambo ambayo Biblia inafundisha kuhusu hali ya wafu na tumaini la wafu. (Mhu. 9:5, 10; Mdo. 24:15) Kweli hizo hutufariji na kutusaidia tusiwe na woga na wasiwasi usio wa lazima. Kwa mfano, hatuwaogopi wafu wala hatuogopi kwamba watapatwa na mambo mabaya. Tunajua kwamba hawako hai na hawawezi kumdhuru yeyote. Ni kana kwamba wako katika usingizi mzito. (Yoh. 11:11-14) Pia, tunajua kwamba wafu hawana habari kuhusu jinsi muda unavyozidi kusonga. Hivyo, wakati wa ufufuo, hata wale ambao wamekufa kwa karne nyingi watahisi ni kana kwamba walikuwa wamelala kwa kipindi kifupi tu, kama kupepesa kwa jicho.

7 Je, hukubali kwamba ukweli kuhusu hali ya wafu uko wazi, ni rahisi, na unaeleweka? Ukweli huo ni tofauti kabisa na uwongo wenye kutatanisha wa Shetani! Mbali na kuwapotosha watu, Shetani amemchongea Muumba wetu kwa uwongo wake. Ili tuelewe vizuri zaidi madhara ambayo Shetani amesababisha, tutazungumzia maswali haya: Shetani amemchongeaje Yehova kupitia uwongo wake? Uwongo huo umewafanyaje watu wafikiri kwamba si lazima wawe na imani katika dhabihu ya fidia ya Kristo? Uwongo huo umewafanyaje wanadamu wazidi kuteseka na kuwa na huzuni?

UWONGO WA SHETANI UMELETA MADHARA MAKUBWA

8. Kama inavyoonyeshwa kwenye andiko la Yeremia 19:5, uwongo wa Shetani kuhusu wafu umefanyaje Yehova aonekane kuwa mwovu?

8 Shetani amemchongea Yehova kwa kusema uwongo kuhusu hali ya wafu. Uwongo huo unatia ndani fundisho la uwongo kwamba wafu huteseka katika moto wa mateso. Mafundisho kama hayo yanamfanya Mungu aonekane kuwa mwovu! Jinsi gani? Kihalisi, mafundisho hayo yanamfanya Mungu mwenye upendo aonekane kuwa na utu wa Ibilisi. (1 Yoh. 4:8) Jambo hilo linakufanya uhisije? Na jambo muhimu hata zaidi, hilo linamfanya Yehova ahisije? Tunajua kwamba anachukia aina zote za ukatili.​—Soma Yeremia 19:5.

9. Uwongo wa Shetani umeathirije maoni ya watu kuhusu dhabihu ya fidia ya Kristo inayotajwa kwenye Yohana 3:16 na 15:13?

9 Uwongo wa Shetani kuhusu kifo huwafanya watu wafikiri kwamba si lazima wawe na imani katika dhabihu ya fidia ya Kristo. (Mt. 20:28) Uwongo mwingine unaoenezwa na Shetani ni kwamba wanadamu wana nafsi isiyoweza kufa. Ikiwa hilo lingekuwa kweli, basi kila mtu angeishi milele. Isingekuwa lazima kwa Kristo kutoa uhai wake kuwa fidia kwa ajili yetu ili tupate uzima wa milele. Zingatia akilini kwamba dhabihu ya Kristo ndiyo zawadi kubwa zaidi kupita zote ya upendo ambayo jamii ya wanadamu ilipewa. (Soma Yohana 3:16; 15:13.) Wazia jinsi Yehova na Mwana wake wanavyohisi kuhusu mafundisho yanayofanya zawadi hiyo ionekane kuwa isiyo ya lazima!

10. Uwongo wa Shetani kuhusu kifo umewafanyaje watu wazidi kuteseka na kuwa na huzuni?

10 Uwongo wa Shetani umewafanya watu wazidi kuteseka na kuwa na huzuni. Huenda wazazi wanaoomboleza kwa sababu ya kufiwa na mtoto wao wakaambiwa kwamba Mungu amemchukua mtoto huyo ili awe malaika mbinguni. Je, uwongo huo wa kishetani hufanya maumivu yao yapungue au hufanya yaongezeke? Fundisho la uwongo kuhusu moto wa mateso limetumiwa kuhalalisha mateso ya kikatili, kama vile kuwatundika mtini na kuwateketeza kwa moto wale wanaopinga mafundisho ya kanisa. Kulingana na kitabu kinachozungumzia Baraza la Kuhukumu Waasi wa Kidini la Hispania, baadhi ya watu waliotekeleza ukatili huo waliamini kwamba walikuwa tu wakiwapa waasi “kionjo cha moto wa mateso usiozimika” ili waweze kutubu kabla ya kufa, na hivyo kuokolewa kutoka kwenye moto huo. Katika baadhi ya nchi, watu huhisi kwamba ni lazima wawaabudu, wawaheshimu, au kuwaomba baraka mababu zao waliokufa. Wengine hutaka kuwatuliza mababu zao waliokufa ili wasiwaadhibu. Inasikitisha kwamba imani zinazotegemea uwongo huo wa kishetani haziwapi watu faraja ya kweli. Badala yake, huwafanya watu wawe na mahangaiko au hata woga usio wa lazima.

TUNAWEZA KUITETEA KWELI YA BIBLIA JINSI GANI?

11. Watu wa ukoo au marafiki wetu wasio na nia mbaya wanaweza kutushinikiza tutende kinyume na Neno la Mungu jinsi gani?

11 Kumpenda Mungu na Neno lake huimarisha azimio letu la kumtii Mungu hata wakati watu wa ukoo au marafiki wasio na nia mbaya wanapojaribu kutushinikiza tujihusishe katika desturi zisizo za Kimaandiko kuhusu wafu. Huenda wakajaribu kutuaibisha, labda kwa kusema kwamba hatukumpenda au kumheshimu yule aliyekufa. Au huenda wakasema kwamba matendo yetu yanaweza kumfanya mtu aliyekufa awadhuru kwa njia fulani wale walio hai. Tunaweza kuiteteaje kweli ya Biblia? Fikiria jinsi unavyoweza kutumia kanuni za Biblia zifuatazo.

12. Ni desturi zipi kuhusu wafu ambazo hazipatani hata kidogo na Maandiko?

12 Azimia ‘kujitenga’ na imani na desturi zisizo za Kimaandiko. (2 Kor. 6:17) Katika nchi moja ya Karibea, watu wengi huamini kwamba baada ya mtu kufa, huenda “mzimu” wake ukabaki kwa muda fulani na kuwaadhibu wale waliomtendea vibaya. Kulingana na kitabu kimoja, huenda “mzimu” wake “ukaisababishia jamii matatizo makubwa.” Barani Afrika, watu huwa na desturi ya kufunika vioo katika nyumba ya mtu aliyekufa na kugeuza picha ili zitazame ukutani. Kwa nini? Baadhi ya watu wanadai kwamba wafu hawapaswi kuona sura yao! Tukiwa watumishi wa Yehova hatuamini hata kidogo hekaya zozote au kushiriki katika desturi zozote zinazoendeleza uwongo wa Shetani!​—1 Kor. 10:21, 22.

Kufanya utafiti kwa makini kwenye machapisho yanayotegemea Biblia na kuzungumza kwa upole na watu wa ukoo ambao si Mashahidi kunaweza kukusaidia uepuke matatizo (Tazama fungu la 13 na 14) *

13. Kama inavyotajwa kwenye andiko la Yakobo 1:5, unapaswa kufanya nini ikiwa una shaka kuhusu desturi fulani?

13 Ikiwa una shaka kuhusu desturi au zoea fulani, sali kwa Yehova na umwombe akupatie hekima yake. (Soma Yakobo 1:5.) Kisha fanya utafiti ukitumia machapisho yetu. Ikiwa ni lazima, waombe ushauri wazee wa kutaniko lako. Hawatakuambia jambo unalopaswa kufanya, lakini wanaweza kukusaidia upate kanuni zitakazokufaa, kama zile zilizozungumziwa katika makala hii. Ukichukua hatua hizo, utazoeza “nguvu [zako] za utambuzi,” na nguvu hizo zitakusaidia “kutofautisha mambo yaliyo sawa na mambo yasiyo sawa.”​—Ebr. 5:14.

14. Tunaweza kuepuka kuwakwaza watu jinsi gani?

14 “Fanyeni mambo yote kwa utukufu wa Mungu. Epukeni kuwa vikwazo.” (1 Kor. 10:31, 32) Tunapoamua ikiwa tutajihusisha katika mila au desturi fulani, tunapaswa pia kufikiria jinsi uamuzi wetu utakavyoathiri dhamiri za wengine, na hasa Wakristo wenzetu. Hatungependa kamwe kumkwaza yeyote! (Marko 9:42) Pia, hatungependa kuwakwaza isivyo lazima watu ambao si Mashahidi. Upendo utatuchochea tuzungumze nao kwa heshima, na jambo hilo litamtukuza Yehova. Hatungependa kamwe kuzozana na watu au kudhihaki desturi zao. Kumbuka, upendo una nguvu! Tunapoonyesha upendo kwa njia yenye ufikirio na heshima, tunaweza kulainisha hata mioyo ya wapinzani wetu.

15-16. (a) Kwa nini ni jambo la hekima kuwajulisha wengine mambo unayoamini? Toa mfano. (b) Maneno ya Paulo kwenye Waroma 1:16 yanatuhusuje?

15 Wajulishe watu katika eneo unaloishi kwamba wewe ni Shahidi wa Yehova. (Isa. 43:10) Itakuwa rahisi zaidi kwako kushughulika na watu wa ukoo na majirani ambao wamekasirika ikiwa wanajua kwamba wewe ni mwabudu wa Yehova Mungu. Francisco, ndugu anayeishi nchini Msumbiji aliandika hivi: “Tulipojifunza kweli, mimi pamoja na mke wangu, Carolina, tuliwaambia watu wa familia yetu kwamba hatutaendelea kuwaabudu wafu. Uamuzi wetu ulijaribiwa dada ya Carolina alipokufa. Kulingana na desturi za eneo letu, maiti huoshwa kimila. Kisha ni lazima mtu wa ukoo wa karibu na mtu aliyekufa alale kwa siku tatu mahali ambapo maji yaliyotumiwa kumwosha yalimwagwa. Desturi hizo zimekusudiwa kutuliza roho ya mtu aliyekufa. Familia ya Carolina ilimtarajia alale mahali ambapo maji hayo yalimwagwa.”

16 Francisco na mke wake walifanya nini? Francisco anaeleza hivi: “Kwa sababu tunampenda Yehova na tunatamani kumfurahisha, tulikataa kushiriki katika desturi hiyo. Watu wa familia ya Carolina walikasirika sana. Walitushutumu kwamba hatuwaheshimu wafu na wakasema kwamba hawatatutembelea tena au kutusaidia. Kwa kuwa hapo awali tulikuwa tumezungumza nao kuhusu imani yetu, hatukujadiliana nao kuhusu jambo hilo walipokuwa wamekasirika. Hata baadhi ya watu wa ukoo walitutetea, wakisema kwamba tayari tulikuwa tumeeleza msimamo wetu. Baada ya muda, watu wa ukoo wa Carolina walitulia, na tulifanikiwa kurudisha amani. Hata baadhi yao wametutembelea nyumbani na kutuomba machapisho ya Biblia.” Naam, na tusiaibikie kamwe msimamo tulio nao wa kutetea ukweli kuhusu kifo.​—Soma Waroma 1:16.

WAFARIJI NA KUWATEGEMEZA WALE WANAOOMBOLEZA

Marafiki wa kweli huwafariji na kuwategemeza wale waliofiwa na wapendwa wao (Tazama fungu la 17 hadi 19) *

17. Ni nini kinachoweza kutusaidia tuwe rafiki wa kweli kwa Mkristo mwenzetu anayeomboleza?

17 Mkristo mwenzetu anapofiwa na mpendwa wake, tunapaswa kujitahidi kadiri tuwezavyo kuwa “rafiki wa kweli . . . , ndugu ambaye amezaliwa kwa ajili ya nyakati za taabu.” (Met. 17:17) Tunawezaje kuwa “rafiki wa kweli,” hasa ikiwa ndugu au dada anayeomboleza anashinikizwa ajihusishe katika desturi zisizo za Kimaandiko? Kuna kanuni mbili za Biblia zinazoweza kutusaidia kuwafariji wale waliofiwa.

18. Ni nini kilichomfanya Yesu atokwe na machozi, na tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wake?

18 “Lieni na wale wanaolia.” (Rom. 12:15) Huenda ikawa vigumu kujua jambo la kumwambia mtu aliyelemewa na huzuni. Nyakati nyingine machozi yetu yanaweza kusema mengi kuliko maneno yetu. Lazaro, rafiki ya Yesu alipokufa, Maria, Martha, na wengine walimlilia ndugu yao na rafiki yao mpendwa. Yesu alipofika siku nne baadaye, yeye pia ‘alitokwa na machozi,’ hata ingawa alijua kwamba punde si punde angemfufua Lazaro. (Yoh. 11:17, 33-35) Machozi ya Yesu yalifunua jinsi Baba yake alivyohisi. Pia, yaliwathibitishia watu wa familia hiyo kwamba Yesu anawapenda, jambo ambalo bila shaka liliwafariji Maria na Martha. Vivyo hivyo, ndugu zetu wanapohisi kwamba tunawapenda na kuwajali, wanatambua kwamba hawako peke yao bali wako miongoni mwa marafiki wanaowajali na kuwategemeza.

19. Tunapomfariji Mkristo mwenzetu anayeomboleza, tunaweza kulitumiaje andiko la Mhubiri 3:7?

19 “Wakati wa kunyamaza na wakati wa kuongea.” (Mhu. 3:7) Njia nyingine ya kumfariji Mkristo mwenzetu anayeomboleza ni kuwa msikilizaji mzuri. Mruhusu ndugu yako amimine moyo wake, na usikasirishwe na “mazungumzo [yake] ya ovyoovyo.” (Ayu. 6:2, 3) Huenda anakabili mkazo mkubwa sana wa kihisia kutoka kwa watu wake wa ukoo ambao si Mashahidi. Hivyo, sali pamoja naye. Msihi “Msikiaji wa sala” ampe nguvu na uwezo wa kufikiri vizuri. (Zab. 65:2) Hali zikiruhusu, someni Biblia pamoja. Au soma pamoja naye makala inayomfaa kutoka katika machapisho yetu, kama vile simulizi la maisha lenye kutia moyo.

20. Tutazungumzia nini katika makala inayofuata?

20 Ni pendeleo kubwa kwelikweli kujua ukweli kuhusu wafu na kuhusu wakati ujao mzuri ajabu ambao wale walio katika makaburi ya ukumbusho watafurahia! (Yoh. 5:28, 29) Basi, kupitia maneno na matendo yetu, acheni tutetee kwa ujasiri kweli ya Biblia na tutumie kila fursa inayojitokeza kuwaambia wengine kuihusu. Katika makala inayofuata tutazungumzia njia nyingine ambayo Shetani hujaribu kuwafanya watu wabaki katika giza la kiroho, yaani, kuwasiliana na roho waovu. Tutajifunza kwa nini tunahitaji kuepuka mazoea na burudani zinazohusiana na mtego huo wa roho waovu.

WIMBO 24 Njooni Kwenye Mlima wa Yehova

^ fu. 5 Shetani na roho wake waovu wamewadanganya watu kuhusu hali ya wafu. Uwongo wao kuhusu hali ya wafu umesababisha watu wafuate desturi nyingi zisizo za Kimaandiko. Makala hii itakusaidia uendelee kuwa mwaminifu kwa Yehova wengine wanapojaribu kukushinikiza ujihusishe katika desturi kama hizo.

^ fu. 55 MAELEZO YA PICHA: Mtu wa ukoo anapoomboleza kifo cha mpendwa wake, watu wa familia yake ambao ni Mashahidi wanamfariji.

^ fu. 57 MAELEZO YA PICHA: Baada ya kufanya utafiti kuhusu desturi za mazishi, Shahidi anawaeleza kwa upole watu wa familia yake kuhusu imani yake.

^ fu. 59 MAELEZO YA PICHA: Wazee wa kutaniko la Kikristo wanamfariji na kumtegemeza Shahidi aliyefiwa na mpendwa wake.