Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Uko Tayari ‘Kuirithi Dunia’?

Je, Uko Tayari ‘Kuirithi Dunia’?

SISI sote tunatazamia kwa hamu kutimizwa kwa ahadi hii ya Yesu: “Wenye furaha ni wale walio wapole, kwa kuwa watairithi dunia.” (Mt. 5:5) Watiwa-mafuta watairithi dunia kwa kutawala mbinguni wakiwa wafalme pamoja na Yesu. (Ufu. 5:10; 20:6) Leo, Wakristo wengi wa kweli wanatazamia kuirithi dunia na kuishi humo milele wakiwa wakamilifu, kwa amani, na furaha. Ili kutimiza kikamili jambo hilo, watahitaji kufanya kazi mbalimbali muhimu. Fikiria mambo matatu watakayohitaji kufanya: kuitiisha dunia, kuwaandalia mahitaji wale watakaofufuliwa, na kuwafundisha watakaofufuliwa. Pia, fikiria jinsi ambavyo hata sasa unaweza kuonyesha kwamba unatamani kushiriki kufanya kazi hizo.

JE, UKO TAYARI KUITIISHA DUNIA?

Yehova alipowaagiza wanadamu “[waijaze] dunia na kuitiisha,” alionyesha kwamba hatimaye dunia nzima ingekuwa paradiso. (Mwa. 1:28) Wale watakaoirithi dunia watahitaji kutii amri hiyo. Dunia haitakuwa paradiso mwanzoni​—kwa sababu leo bustani ya Edeni haipo. Hivyo, kutakuwa na kazi nyingi ya kufanya ili kusafisha maeneo ambayo sasa yameharibiwa. Hiyo itakuwa kazi kubwa sana!

Hilo linatukumbusha kazi ambayo Waisraeli walikuwa nayo waliporudi kutoka Babiloni. Nchi yao haikuwa na wakaaji kwa miaka 70. Lakini Isaya alitabiri kwamba kwa msaada wa Yehova, wangefaulu kuirudisha katika hali nzuri. Unabii huo ulisema hivi: “Ataifanya nyika yake kuwa kama Edeni na jangwa lake tambarare kama bustani ya Yehova.” (Isa. 51:3) Waisraeli walifanikiwa kufanya kazi hiyo. Vivyo hivyo, kwa msaada wa Yehova, wale watakaoirithi dunia watafanikiwa kuitiisha. Hata sasa unaweza kuonyesha kwamba unatamani kufanya kazi hiyo.

Njia moja ni kwa kufanya yote unayoweza ili kudumisha nyumba na mazingira yako yakiwa safi na nadhifu. Unaweza kufanya hivyo hata ikiwa jirani zako hawafanyi hivyo. Pia, unaweza kusaidia kwa kufanya usafi na kudumisha Jumba lenu la Ufalme na Jumba la Makusanyiko. Ikiwa hali zako zinakuruhusu, unaweza pia kutuma ombi la kuwa mjitoleaji katika eneo lenu ili kusaidia kutoa msaada majanga ya asili yanapotokea. Kwa njia hiyo, utaonyesha kwamba uko tayari kusaidia kunapokuwa na uhitaji. Unaweza kujiuliza hivi, ‘Je ninaweza kujifunza ustadi fulani ambao nitautumia ikiwa nitapata baraka ya kuirithi dunia?’

JE, UKO TAYARI KUWAANDALIA MAHITAJI WALE WATAKAOFUFULIWA?

Mara tu baada ya kumfufua binti ya Yairo, Yesu alisema kwamba mtoto huyo anapaswa kupewa chakula. (Marko 5:42, 43) Haikuwa kazi ngumu kumtunza msichana huyo mwenye umri wa miaka 12. Hata hivyo, fikiria kazi itakayohusika wakati ahadi hii ya Yesu itakapotimizwa: “Wote walio katika makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti yake na kutoka.” (Yoh. 5:28, 29) Ingawa Biblia haitaji habari nyingi, tunaweza kuwazia kwamba wale watakaofufuliwa watahitaji msaada ili kupata chakula, makao, na mavazi. Hata sasa, je, unaweza kuonyesha kwamba uko tayari kusaidia? Unaweza kufikiria maswali yafuatayo.

Unaweza kufanya nini leo ili kuonyesha kwamba uko tayari kuirithi dunia?

Tangazo linapotolewa kwamba mwangalizi wa mzunguko atatembelea kutaniko lenu, je, wewe hujitolea kumkaribisha kwa ajili ya chakula? Watumishi wa pekee wa wakati wote wanapopewa migawo mipya kutoka Betheli kwenda shambani au mwangalizi wa mzunguko anapomaliza kutumikia katika kazi ya kusafiri, je, unaweza kuwasaidia kupata makao? Ikiwa kusanyiko la eneo au kusanyiko la pekee litafanywa katika eneo lenu, je, unaweza kujitolea kufanya kazi kabla au baada ya kusanyiko au kuwa tayari kuwakaribisha wajumbe?

JE, UKO TAYARI KUWAFUNDISHA WALE WATAKAOFUFULIWA?

Kulingana na Matendo 24:15, tunatarajia kwamba mabilioni ya watu watafufuliwa. Wengi wao watakuwa wale ambao hapo awali hawakupata nafasi ya kumjua Yehova. Watapata nafasi hiyo baada ya kufufuliwa. a Watumishi waaminifu wa Yehova walio na uzoefu, watashiriki kufanya kazi hiyo ya kufundisha. (Isa. 11:9) Charlotte, ambaye ameshiriki kuhubiri huko Ulaya, Amerika Kusini, na Afrika, anatazamia kwa hamu kufanya kazi hiyo. Anasema hivi kwa furaha: “Ninatazamia kuwafundisha watu watakaofufuliwa. Ninaposoma kuhusu mtu ambaye aliishi zamani, mara nyingi mimi hujiambia: ‘Ikiwa mtu huyo angemjua Yehova, maisha yake yangekuwa tofauti sana.’ Natazamia kwa hamu kuwaambia watu watakaofufuliwa mambo ambayo hawakupata nafasi ya kujifunza.”

Hata watumishi waaminifu wa Yehova walioishi kabla ya Yesu kuja duniani watakuwa na mengi ya kujifunza. Fikiria kuhusu shangwe na pendeleo la kumfafanulia Danieli utimizo wa unabii ambao aliandika lakini hakuelewa maana yake. (Dan. 12:8) Au fikiria kuhusu kumsaidia Ruthu na Naomi wajifunze jinsi familia yao ilivyohusika katika ukoo uliomtokeza masihi? Itakuwa shangwe sana kushiriki katika programu hiyo ya kufundisha ulimwenguni pote, bila mikazo na mambo yanayotukengeusha leo katika ulimwengu huu mwovu!

Unawezaje kuonyesha sasa kwamba uko tayari kushiriki katika programu hiyo? Njia moja ni kwa kujitahidi kuboresha ustadi wako wa kufundisha na kwa kushiriki kwa ukawaida katika kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote inayofanywa leo. (Mt. 24:14) Hata ikiwa umri au hali nyingine zinakuzuia kufanya mengi wakati huu, jitihada zako zinaweza kuonyesha kwamba uko tayari kuwafundisha wale watakaofufuliwa.

Naam, swali muhimu ni, Je, kweli unatazamia kwa hamu kuirithi dunia? Je, unasisimka kwa sababu ya tumaini la kuitiisha dunia, na pia kuwaandalia mahitaji na kuwafundisha wale watakaofufuliwa? Unaweza kuonyesha kwamba uko tayari kwa kutumia fursa unazopata leo, kushiriki kwenye kazi ambazo zinafanana na zile ambazo utafanya utakapoirithi dunia!

a Tazama makala ‘Kuwaleta Wengi Kwenye Uadilifu’ katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Septemba 2022.