Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 50

“Utakuwa Pamoja Nami Katika Paradiso”

“Utakuwa Pamoja Nami Katika Paradiso”

“Kwa kweli ninakuambia leo, utakuwa pamoja nami katika Paradiso.”​—LUKA 23:43.

WIMBO 145 Ahadi ya Mungu ya Paradiso

MUHTASARI a

1. Muda mfupi kabla ya Yesu kufa, alimwambia nini mhalifu aliyekuwa kando yake? (Luka 23:39-43)

 YESU na wahalifu wawili waliokuwa kando yake, walikuwa wakiteseka walipokuwa wakifa kifo cha polepole. (Luka 23:32, 33) Wahalifu hao wawili walikuwa wamemdhihaki Yesu, basi ni wazi kwamba hawakuwa wanafunzi wake. (Mt. 27:44; Marko 15:32) Lakini mmoja wao alibadilisha mtazamo wake. Alisema hivi: “Yesu, unikumbuke utakapoingia katika Ufalme wako.” Yesu akamjibu hivi; “Kwa kweli ninakuambia leo, utakuwa pamoja nami katika Paradiso.” (Soma Luka 23:39-43.) Hakuna jambo linalothibitisha kwamba mhalifu huyo alikuwa amekubali ujumbe kuhusu “Ufalme wa mbinguni” ambao Yesu alihubiri wakati wa huduma yake. Na Yesu hakusema kamwe kwamba mwanamume huyo angeingia katika Ufalme. (Mt. 4:17) Yesu alikuwa akizungumza kuhusu Paradiso ya wakati ujao duniani. Kwa nini tunaweza kusema hivyo?

Tunaweza kufikia mkataa gani kumhusu mhalifu aliyezungumza na Yesu na kuhusu mambo ambayo mhalifu huyo alijua? (Tazama fungu la 2 na 3)

2. Ni nini kinachoonyesha kwamba yule mhalifu aliyetubu alikuwa Myahudi?

2 Inaelekea kwamba mhalifu huyo aliyetubu alikuwa Myahudi. Alimwambia hivi mhalifu mwenzake: “Je, wewe humwogopi Mungu hata kidogo, kwa kuwa umepata hukumu ileile?” (Luka 23:40) Wayahudi walimwabudu Mungu mmoja, lakini watu wa mataifa waliamini kwamba kuna miungu mingi. (Kut. 20:2, 3; 1 Kor. 8:5, 6) Ikiwa wahalifu hao walikuwa watu wa mataifa, huenda mhalifu huyo angeuliza hivi, “Je, wewe huogopi miungu hata kidogo?” Isitoshe, Yesu alitumwa, si kwa watu wa mataifa, bali kwa “kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli.” (Mt. 15:24) Mungu alikuwa amewafunulia Waisraeli kwamba angewafufua wafu. Huenda yule mhalifu aliyetubu alijua jambo hilo na kama maneno yake yanavyoonyesha, alifikiri kwamba Yehova angemfufua Yesu atawale katika Ufalme wa Mungu. Inaonekana mwanamume huyo alitumaini kwamba Mungu angemfufua yeye pia.

3. Inaelekea yule mhalifu alifikiria kuhusu nini Yesu alipotaja Paradiso? Eleza. (Mwanzo 2:15)

3 Akiwa Myahudi, yule mhalifu aliyetubu alijua kuhusu Adamu na Hawa na Paradiso ambayo Yehova alikuwa ameumba kwa ajili yao. Basi, inawezekana kwamba mhalifu huyo aliamini Paradiso ambayo Yesu alitaja ingekuwa bustani maridadi hapa duniani.​—Soma Mwanzo 2:15.

4. Maneno ambayo Yesu alimwambia yule mhalifu yanapaswa kutuchochea tufikirie kuhusu nini?

4 Maneno ambayo Yesu alimwambia yule mhalifu yanapaswa kutuchochea tufikirie jinsi maisha yatakavyokuwa katika Paradiso. Kwa kweli, tunaweza kujifunza jambo fulani kuhusu Paradiso kutokana na utawala wenye amani wa Mfalme Sulemani. Na tunaweza kutarajia kwamba Yesu, yule mtu mkuu kuliko Sulemani, atashirikiana na watawala wenzake kuleta hali bora sana duniani. (Mt. 12:42) Ni wazi kwamba wale “kondoo wengine” wanapaswa kutamani kujua mambo wanayopaswa kufanya ili wastahili kuishi milele katika Paradiso.​—Yoh. 10:16.

MAISHA YATAKUWAJE KATIKA PARADISO?

5. Unatazamia nini kuhusiana na maisha katika Paradiso?

5 Ni nini kinachokuja akilini mwako unapofikiria kuhusu maisha katika Paradiso? Labda unawazia mazingira maridadi, kama bustani ya Edeni. (Mwa. 2:7-9) Huenda unakumbuka unabii ambao Mika aliandika kwamba watu wa Mungu wataketi “kila mtu chini ya mzabibu wake na chini ya mtini wake.” (Mika 4:3, 4) Huenda pia ukakumbuka mistari ya Biblia inayosema kwamba kutakuwa na chakula kwa wingi. (Zab. 72:16; Isa. 65:21, 22) Basi, huenda ukajiwazia ukiwa kwenye bustani maridadi, ukiwa umekaa kwenye meza iliyojaa chakula kitamu. Huenda ukawazia hewa safi yenye harufu nzuri ya mimea na maua. Na inaelekea kwamba unasikia sauti za kicheko za watu wa familia na marafiki​—kutia ndani wale waliofufuliwa—​wakifurahia kuwa pamoja. Mambo hayo yote si ndoto tu. Kwa hakika, mambo hayo yote yatatokea duniani. Hata hivyo, maisha katika Paradiso yatatia ndani pia kazi yenye kufurahisha.

Tutafanya kazi muhimu ya kuwafundisha wale watakaofufuliwa (Tazama fungu la 6)

6. Tutafanya nini katika Paradiso? (Tazama picha.)

6 Yehova ametuumba tukiwa na uwezo wa kufurahia kazi. (Mhu. 2:24) Tutakuwa na kazi nyingi sana hasa wakati wa Utawala wa Miaka Elfu Moja wa Kristo. Wale watakaookoka dhiki kuu, pamoja na mamilioni ya watu watakaofufuliwa, watahitaji mavazi, chakula, na mahali pa kuishi. Ili kutimiza uhitaji huo, tutahitaji kufanya kazi nyingi yenye kufurahisha. Kama vile Adamu na Hawa walivyopaswa kutunza makao yao ya bustani, tutakuwa na pendeleo la kuifanya dunia kuwa Paradiso. Wazia pia jinsi itakavyofurahisha kuwafundisha mamilioni ya watu watakaofufuliwa ambao hawajui mengi kumhusu Yehova na kusudi lake na kuwasaidia waaminifu walioishi muda mrefu kabla ya wakati wa Yesu wajifunze mengi zaidi!

7. Tunaweza kuwa na uhakika kuhusu jambo gani, na kwa nini?

7 Tunaweza kuwa na uhakika kwamba maisha katika Paradiso ya wakati ujao yatakuwa yenye amani, ufanisi, na mpangilio mzuri. Kwa nini? Kwa sababu tayari Yehova ametupatia kionjo cha jinsi maisha yatakavyokuwa chini ya utawala wa Mwana wake. Tunaweza kuona hilo katika simulizi la utawala wa Mfalme Sulemani.

UTAWALA WA SULEMANI​—KIONJO CHA PARADISO

8. Maneno yaliyo kwenye Zaburi 37:10, 11, 29 yalitimizwaje baada ya Mfalme Daudi kuyaandika? (Tazama “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika gazeti hili.)

8 Mfalme Daudi aliongozwa na roho kuandika jinsi ambavyo maisha yangekuwa wakati wa utawala wa mfalme mwenye hekima na mwaminifu wa wakati ujao. (Soma Zaburi 37:10, 11, 29.) Mara nyingi, sisi huwasomea watu Zaburi 37:11 tunapozungumza kuhusu Paradiso ya wakati ujao. Tuna sababu nzuri ya kufanya hivyo kwa sababu Yesu alinukuu andiko hilo katika Mahubiri yake ya Mlimani, akionyesha kwamba litakuwa na utimizo wakati ujao. (Mt. 5:5) Lakini maneno ya Daudi yalifunua pia jinsi ambavyo maisha yangekuwa katika siku za Mfalme Sulemani. Mfalme Sulemani alipotawala Israeli, watu wa Mungu walifurahia amani nyingi na usitawi katika nchi iliyokuwa ‘inatiririka maziwa na asali.’ Mungu alikuwa amesema hivi: “Mkiendelea kufuata sheria zangu . . . , nitaleta amani nchini, nanyi mtalala na hakuna yeyote atakayewaogopesha.” (Law. 20:24; 26:3, 6) Ahadi hizo zilitimia wakati wa utawala wa Sulemani. (1 Nya. 22:9; 29:26-28) Pia, kulikuwa na ahadi kwamba waovu ‘hawangekuwepo tena.’ (Zab. 37:10) Basi, maneno yanayopatikana kwenye Zaburi 37:10, 11, 29 yalitimizwa zamani na pia yatatimizwa wakati ujao.

9. Malkia wa Sheba alisema nini kuhusu utawala wa Mfalme Sulemani?

9 Habari kuhusu amani na usitawi ambao Waisraeli walifurahia chini ya utawala wa Sulemani zilimfikia malkia wa Sheba. Mtawala huyo aliyeishi nchi ya mbali alifunga safari kwenda Yerusalemu ili ajionee hali hiyo. (1 Fal. 10:1) Baada ya kukagua ufalme wa Sulemani, alisema hivi: “Sikuwa nimeambiwa hata nusu yake. . . . Wenye furaha ni watu wako, na wenye furaha ni watumishi wako wanaosimama mbele yako daima, wakiisikiliza hekima yako!” (1 Fal. 10:6-8) Lakini hali ambazo zilikuwepo wakati wa utawala wa Sulemani zilikuwa kionjo tu cha mambo ambayo Yehova atawafanyia wanadamu chini ya utawala wa Yesu, Mwana Wake.

10. Ni kwa njia gani Yesu ni Mfalme bora kuliko Sulemani?

10 Yesu anamzidi Sulemani katika kila njia. Sulemani alikuwa mwanadamu asiye mkamilifu aliyefanya makosa mazito ambayo mwishowe yaliwasababishia watu wa Mungu hali ngumu. Lakini Yesu ni Mtawala mkamilifu ambaye hawezi kufanya makosa. (Luka 1:32; Ebr. 4:14, 15) Yesu aliendelea kuwa mwaminifu licha ya majaribu makali sana ambayo Shetani alimletea. Kristo amethibitisha kwamba hatafanya kamwe dhambi au kufanya jambo lolote litakalowaletea madhara raia zake washikamanifu. Kwa kweli, ni pendeleo kubwa kuwa na Mfalme bora kama huyo.

11. Yesu atatawala pamoja na nani?

11 Yesu atashirikiana na watawala wenzake 144,000 kuwatunza wanadamu na kutimiza kusudi la Mungu kwa dunia. (Ufu. 14:1-3) Watawala hao walikabiliana na majaribu na mateso mengi walipokuwa wanaume na wanawake, basi wataelewa vizuri hali yetu. Watawala hao watatimiza jukumu gani hasa?

WATIWA-MAFUTA WATATIMIZA JUKUMU GANI?

12. Yehova atawapatia kazi gani wale 144,000?

12 Jukumu ambalo Yesu na watawala wenzake wamepewa ni kubwa zaidi kuliko jukumu ambalo Sulemani alipewa. Mfalme huyo wa Israeli alitawala mamilioni ya watu katika nchi moja tu. Hata hivyo, watawala katika Ufalme wa Mungu watatawala mabilioni ya watu watakaoishi ulimwengu pote. Kwa kweli, Yehova amewapatia wale 144,000 pendeleo kubwa sana!

13. Kazi ya wale watakaotawala pamoja na Yesu itatia ndani jukumu gani la pekee?

13 Kama Yesu, wale 144,000 watatumikia wakiwa wafalme na makuhani. (Ufu. 5:10) Chini ya Sheria ya Musa, kimsingi makuhani walikuwa na jukumu la kulinda afya ya kimwili ya watu huku wakihakikisha kwamba watu walikuwa na afya nzuri kiroho. Sheria ilikuwa “kivuli cha mambo mema yatakayokuja,” basi inapatana na akili kufikia mkataa kwamba wale watakaotawala pamoja na Yesu watasaidia kutimiza jukumu la pekee la kushughulikia mahitaji ya kimwili na ya kiroho ya watu wa Mungu. (Ebr. 10:1) Hatujui jinsi wafalme na makuhani hao watakavyowasiliana na raia wa Ufalme watakaoishi duniani. Hata hivyo, tunaweza kuwa na uhakika kwamba mpango ambao Yehova ataweka katika Paradiso ya wakati ujao, utahakikisha kwamba wale walio duniani wanapata mwongozo wanaohitaji.​—Ufu. 21:3, 4.

“KONDOO WENGINE” WANAPASWA KUFANYA NINI ILI WASTAHILI KUISHI KATIKA PARADISO?

14. Kuna uhusiano gani kati ya “kondoo wengine” na ndugu za Kristo?

14 Yesu aliwarejelea wale ambao watatawala pamoja naye kuwa “kundi dogo.” (Luka 12:32) Pia, alizungumza kuhusu kikundi cha pili, ambacho alikirejelea kuwa “kondoo wengine.” Vikundi hivyo viwili vinafanyiza kundi moja lenye umoja. (Yoh. 10:16) Tayari vikundi hivyo viwili vimekuwa vikifanya kazi pamoja, na wataendelea kushirikiana dunia itakapokuwa Paradiso. Bila shaka, wakati huo, wale wa “kundi dogo” watakuwa mbinguni na wale “kondoo wengine” watakuwa na tumaini la kufurahia maisha milele duniani. Lakini kuna mambo ambayo “kondoo wengine” wanahitaji kufanya sasa ili wastahili kuishi katika Paradiso.

Hata sasa tunaweza kuonyesha kwamba tunajitayarisha kuishi katika Paradiso ya wakati ujao (Tazama fungu la 15) b

15. (a) “Kondoo wengine” wanashirikianaje na ndugu za Kristo? (b) Unawezaje kuiga mfano wa ndugu aliye dukani? (Tazama picha.)

15 Yule mhalifu aliyetubu alikufa kabla ya kupata fursa ya kuthibitisha kabisa kwamba alithamini mambo ambayo Kristo alimfanyia. Kinyume chake, sisi tunaofanyiza “kondoo wengine” tuna fursa nyingi sasa za kuonyesha jinsi tunavyohisi kumhusu Yesu. Kwa mfano, tunaonyesha kwamba tunampenda kupitia jinsi tunavyowatendea ndugu zake watiwa-mafuta. Yesu alisema kwamba angewahukumu kondoo kwa msingi huo. (Mt. 25:31-40) Tunaweza kuwaunga mkono ndugu za Kristo kwa kuwasaidia kwa bidii kufanya kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi. (Mt. 28:18-20) Hivyo, tungependa kutumia vizuri vifaa vya kujifunzia Biblia ambavyo tumeandaliwa, kama vile kitabu Furahia Maisha Milele! Ikiwa kwa sasa huongozi funzo la Biblia, kwa nini usijiwekee lengo la kuwatajia watu wengi iwezekanavyo kuhusu mpango wa kujifunza Biblia?

16. Tunaweza kufanya nini ili kujitayarisha kuwa raia wa Ufalme wa Mungu?

16 Hatuhitaji kusubiri hadi tutakapoishi katika Paradiso ili tuwe aina ya watu ambao Yehova angependa wawe huko. Hivi sasa tunaweza kujitahidi kuwa wanyoofu katika mambo tunayosema na kutenda na kuishi maisha yenye usawaziko. Na tunaweza kuwa washikamanifu kwa Yehova, kwa mwenzi wetu wa ndoa, na kwa Wakristo wenzetu. Kadiri tunavyojitahidi kufuata kwa ukaribu viwango vya Mungu tunapoishi katika ulimwengu huu mwovu, ndivyo itakavyokuwa rahisi zaidi kwetu kuishi kulingana na viwango hivyo katika Paradiso. Pia, tunaweza kusitawisha uwezo na ustadi na hivyo kuonyesha kwamba tunajitayarisha kuishi wakati huo. Tazama makala, “Je, Uko Tayari ‘Kuirithi Dunia’?” inayopatikana kwenye gazeti hili.

17. Je, tunapaswa kulemewa na dhambi tulizofanya zamani? Eleza.

17 Pia, tunapaswa kujitahidi kushinda hisia za hatia ambazo huenda tukahisi kwa sababu ya dhambi nzito tulizofanya zamani. Bila shaka, hatungependa kamwe kuiona dhabihu ya fidia kuwa kisingizio cha kuendelea “kutenda dhambi kimakusudi.” (Ebr. 10:26-31) Lakini tunaweza kuwa na uhakika kwamba ikiwa tumetubu kikweli baada ya kufanya dhambi nzito, tumetafuta msaada ambao Yehova huandaa, na tumebadili mwenendo wetu, Yehova ametusamehe kwa njia kubwa. (Isa. 55:7; Mdo. 3:19) Kumbuka maneno haya ambayo Yesu aliwaambia Mafarisayo: “Sikuja kuwaita waadilifu, bali watenda dhambi.” (Mt. 9:13) Dhabihu ya fidia ina nguvu za kutosha kufunika dhambi zetu zote.

UNAWEZA KUISHI MILELE KATIKA PARADISO

18. Ungependa kuzungumzia nini pamoja na mhalifu aliyekufa kando ya Yesu?

18 Je, unaweza kujiwazia ukiwa katika Paradiso, ukiongea na yule mhalifu aliyezungumza na Yesu? Bila shaka, nyote wawili mngeeleza jinsi ambavyo mnathamini dhabihu ya Yesu. Huenda ukamwomba akuambie mengi zaidi kuhusu mambo yaliyotokea wakati wa saa chache za mwisho za maisha ya Yesu duniani na jinsi alivyohisi Yesu alipojibu ombi lake. Naye huenda akakuomba umweleze jinsi maisha yalivyokuwa katika siku za mwisho za mfumo wa Shetani. Litakuwa pendeleo kubwa kujifunza Neno la Mungu pamoja na watu walio kama mwanamume huyo!​—Efe. 4:22-24

Wakati wa Utawala wa Miaka Elfu Moja, ndugu anafurahia kuboresha uwezo ambao alitarajia kwa hamu kusitawisha (Tazama fungu la 19)

19. Kwa nini maisha katika Paradiso hayatachosha? (Tazama picha kwenye jalada.)

19 Maisha katika Paradiso hayatachosha kamwe. Sikuzote tutafurahia kukutana na watu mbalimbali na tutakuwa na kazi yenye kuridhisha. Jambo bora zaidi ni kwamba kila siku tutaendelea kumjua Baba yetu wa mbinguni vizuri zaidi na kufurahia mambo ambayo ametuandalia. Sikuzote tutakuwa na mengi ya kujifunza kumhusu na pia tutajifunza mengi kuhusu uumbaji wake. Kadiri tutakavyoendelea kuishi, ndivyo upendo wetu kwa Mungu utakavyozidi kuongezeka. Tunamshukuru sana Yehova na Yesu kwa kutupatia ahadi kwamba tunaweza kuishi milele katika Paradiso!

WIMBO 22 Ufalme Umesimamishwa​—Na Uje!

a Je, mara kwa mara wewe hufikiria jinsi maisha yatakavyokuwa katika Paradiso? Tunatiwa moyo tunapofanya hivyo. Kadiri tunavyofikiria kuhusu mambo ambayo Yehova ametuahidi, ndivyo tutakavyokuwa na shauku tunapowafundisha wengine kuhusu ulimwengu mpya. Makala hii itatusaidia kuimarisha imani yetu katika ahadi ya Yesu kuhusu paradiso ya wakati ujao.

b MAELEZO YA PICHA: Ndugu aliye na tumaini la kushiriki katika kazi ya kuwafundisha wale watakaofufuliwa tayari anawafundisha wengine.