Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 52

Akina Dada Vijana​—⁠Mnawezaje Kuwa Wakristo Wakomavu?

Akina Dada Vijana​—⁠Mnawezaje Kuwa Wakristo Wakomavu?

“Vilevile wanawake wanapaswa . . . wawe wenye kiasi katika mazoea, na waaminifu katika mambo yote.”—1 TIM. 3:11.

WIMBO 133 Mwabudu Yehova Ujanani

MUHTASARI a

1. Ili kufikia ukomavu wa Kikristo, ni lazima tufanye nini?

 TUNASTAAJABISHWA na jinsi mtoto anavyokua haraka na kuwa mtu mzima. Inaonekana ni kama watoto wanakua tu bila kufanya jitihada yoyote. Hata hivyo, jitihada inahitajika ili kuwa Mkristo mkomavu. b (1 Kor. 13:11; Ebr. 6:1) Ili kufikia lengo hilo, tunahitaji kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova. Pia, tunahitaji roho takatifu ili tusitawishe sifa zinazompendeza Yehova, tuwe na ustadi unaofaa, na tujitayarishe kwa ajili ya majukumu ya wakati ujao.—Met. 1:5.

2. Tunajifunza nini kwenye Mwanzo 1:​27, na tutazungumzia nini katika makala hii?

2 Yehova alimuumba mwanamume na mwanamke. (Soma Mwanzo 1:27.) Ni wazi kwamba wanaume na wanawake wanatofautiana kimwili, lakini wanatofautiana kwa njia nyingine pia. Kwa mfano, Yehova aliwapatia wanaume na wanawake majukumu hususa, hivyo wanahitaji sifa na ustadi ili waweze kutimiza majukumu yao. (Mwa. 2:18) Katika makala hii, tutachunguza mambo ambayo dada kijana anaweza kufanya ili kuwa Mkristo mkomavu. Katika makala inayofuata, tutachunguza mambo ambayo ndugu kijana anaweza kufanya.

SITAWISHA SIFA ZA KIROHO

Kuiga sifa za wanawake waaminifu, kama vile Rebeka, Esta, na Abigaili, kutakusaidia kuwa mwanamke Mkristo mkomavu (Tazama fungu la 3-4)

3-4. Akina dada vijana wanaweza kupata wapi mifano mizuri ya kuiga? (Tazama pia picha.)

3 Biblia inawataja wanawake wengi wa pekee waliompenda Yehova na kumtumikia. (Tazama makala kwenye jw.org yenye kichwa “Wanawake Katika Biblia—Tunaweza Kujifunza Nini Kutoka Kwao?”) Kama andiko la msingi linavyoshauri, wanawake hao walikuwa “wenye kiasi katika mazoea” na “waaminifu katika mambo yote.” Kwa kuongezea, akina dada vijana wanaweza kupata katika kutaniko lao wanawake Wakristo wakomavu ambao ni mfano mzuri wa kuigwa.

4 Akina dada vijana, je, mnaweza kutafuta kutanikoni wanawake Wakristo wakomavu ambao mnaweza kuiga mfano wao? Chunguzeni sifa zao zinazovutia; kisha mfikirie jinsi mnavyoweza kuonyesha sifa hizo. Katika mafungu yanayofuata, tutazungumzia sifa tatu muhimu ambazo wanawake wakomavu wanapaswa kuwa nazo.

5. Kwa nini sifa ya unyenyekevu ni muhimu kwa mwanamke Mkristo mkomavu?

5 Unyenyekevu ni sifa muhimu ya kuwa Mkristo mkomavu. Ikiwa mwanamke ni mnyenyekevu, atafurahia uhusiano mzuri na Yehova na watu wengine pia. (Yak. 4:6) Kwa mfano, mwanamke anayempenda Yehova, kwa unyenyekevu anachagua kuunga mkono kanuni ya ukichwa ambayo Baba yake wa mbinguni alianzisha. (1 Kor. 11:3) Kanuni hiyo inatumika kwa njia hususa katika kutaniko na katika familia pia. c

6. Akina dada vijana wanaweza kujifunza nini kuhusu unyenyekevu kutoka kwa Rebeka?

6 Fikiria mfano wa Rebeka. Alikuwa mwanamke mwenye hekima, alifanya maamuzi kwa ujasiri, na katika maisha yake yote hakusita kuchukua hatua kwa njia inayofaa. (Mwa. 24:58; 27:​5-17) Hata hivyo, alikuwa na heshima na ujitiisho. (Mwa. 24:​17, 18, 65) Ikiwa kwa unyenyekevu utaunga mkono mipango ya Yehova kama alivyofanya Rebeka, utakuwa mfano mzuri katika familia yako na kutanikoni pia.

7. Akina dada vijana wanawezaje kuiga mfano wa Esta inapohusu kuonyesha sifa ya kiasi?

7 Sifa ya kiasi ni sifa nyingine inayohitajika kwa Wakristo wote wakomavu. Biblia inasema kwamba “wenye kiasi wana hekima.” (Met. 11:2) Esta alikuwa mwanamke mwaminifu mwenye sifa ya kiasi. Sifa ya kiasi ilimlinda asitende kwa kimbelembele. Alisikiliza ushauri wa binamu yake mwenye umri mkubwa, Mordekai, na aliufuata. (Esta 2:​10, 20, 22) Unaweza kuonyesha sifa hiyo ya kiasi kwa kutafuta ushauri mzuri na kuutumia.—Tito 2:​3-5.

8. Kulingana na 1 Timotheo 2:​9, 10, sifa ya kiasi itamsaidiaje dada kufanya maamuzi mazuri inapohusu mavazi na kujipamba?

8 Esta alionyesha sifa ya kiasi katika njia nyingine. Alikuwa “mrembo na mwenye umbo zuri”; hata hivyo, hakutenda kwa njia iliyofanya wengine wamkazie fikira. (Esta 2:​7, 15) Mwanamke Mkristo anawezaje kunufaika na mfano wa Esta? Njia moja inatajwa kwenye 1 Timotheo 2:​9, 10. (Soma.) Mtume Paulo aliwaagiza wanawake Wakristo wavalie kwa kiasi na utimamu wa akili. Maneno ya Kigiriki yaliyotumiwa hapa yanadokeza kwamba mavazi ya mwanamke Mkristo yangepaswa kuwa ya heshima na yangeonyesha kwamba anajali hisia au maoni ya wengine. Tunajivunia dada zetu Wakristo wakomavu ambao wanavalia kwa kiasi!

9. Tunajifunza nini kutokana na mfano wa Abigaili?

9 Utambuzi ni sifa nyingine ambayo akina dada wote Wakristo wakomavu huonyesha. Utambuzi ni nini? Ni uwezo wa kufanya maamuzi mazuri, yaani, uwezo wa kutofautisha lililo sawa na lisilo sawa na kisha kutenda kwa hekima. Fikiria mfano wa Abigaili. Mume wake alifanya uamuzi mbaya ambao ungekuwa na matokeo mabaya kwa watu wote wa nyumba yake. Abigaili alichukua hatua haraka. Uamuzi wake mzuri uliokoa uhai. (1 Sam. 25:​14-23, 32-35) Pia, sifa ya utambuzi inatusaidia kujua wakati wa kuzungumza na wakati wa kukaa kimya. Na inatusaidia kupendezwa kibinafsi na wengine kwa njia isiyopita kiasi.—1 The. 4:11.

JIFUNZE USTADI UTAKAOKUSAIDIA

Je, umenufaika kwa kujifunza kusoma na kuandika vizuri? (Tazama fungu la 11)

10-11. Kusoma na kuandika vizuri kunaweza kukunufaishaje wewe na wengine? (Tazama pia picha.)

10 Mwanamke Mkristo anahitaji kuwa na ustadi utakaomsaidia. Baadhi ya stadi ambazo msichana anajifunza akiwa mtoto, zitaendelea kumnufaisha katika maisha yake yote. Fikiria mifano michache.

11 Jifunze kusoma na kuandika vizuri. Katika baadhi ya tamaduni, watu wanaona kwamba si muhimu kwa wanawake kujifunza kusoma na kuandika. Hata hivyo, huo ni ustadi muhimu sana kwa kila Mkristo. d (1 Tim. 4:13) Hivyo, usiruhusu jambo lolote likuzuie kujifunza kusoma na kuandika vizuri. Utanufaikaje? Ustadi huo unaweza kukusaidia kupata kazi na kuidumisha. Utakusaidia kuwa mwanafunzi na mwalimu mzuri wa Neno la Mungu. Faida muhimu zaidi ni kwamba ustadi huo utakusaidia kumkaribia Yehova unaposoma Neno lake na kulitafakari.—Yos. 1:8; 1 Tim. 4:15.

12. Methali 31:26 inawezaje kukusaidia kuwasiliana vizuri na wengine?

12 Sitawisha ustadi wa kuwasiliana vizuri. Wakristo wanahitaji kuwasiliana vizuri. Kuhusu jambo hilo, mwanafunzi Yakobo alitoa ushauri unaofaa kwetu aliposema hivi: “Kila mtu lazima awe mwepesi wa kusikia, si mwepesi wa kusema.” (Yak. 1:19) Unaposikiliza kwa makini wengine wanapozungumza unawaonyesha “hisia-mwenzi.” (1 Pet. 3:8) Ikiwa huna uhakika kama umeelewa kile ambacho mtu amesema au jinsi anavyohisi, muulize maswali kwa busara. Kisha tua kidogo na ufikiri kabla ya kuongea. (Met. 15:​28, maelezo ya chini) Jiulize hivi: ‘Je, jambo ninalotaka kusema ni la kweli na linajenga? Je, ni maneno ya busara na fadhili?’ Jifunze kutoka kwa akina dada wakomavu wanaosikiliza kwa makini na kuzungumza kwa fadhili. (Soma Methali 31:26.) Kazia uangalifu jinsi wanavyozungumza. Ukijifunza vizuri ustadi huu, utakuwa na uhusiano mzuri na wengine.

Mwanamke ambaye amejifunza kusimamia nyumba yake ni baraka kwa familia yake na kutaniko (Tazama fungu la 13)

13. Unawezaje kujifunza jinsi ya kusimamia nyumba? (Tazama pia picha.)

13 Jifunze kusimamia nyumba. Katika maeneo mengi, wanawake hufanya kazi nyingi za nyumbani. Mama yako au dada mwingine mwenye uzoefu anaweza kukusaidia kujifunza stadi zinazohitajika. Dada anayeitwa Cindy, anasema hivi: “Mojawapo ya zawadi zenye thamani kubwa zaidi ambazo mama yangu alinipa ni kunifundisha shangwe inayotokana na kufanya kazi ngumu. Kujifunza stadi kama vile kupika, kusafisha, kushona nguo, na kufanya ununuzi kulifanya maisha yangu yawe rahisi zaidi na kunifungulia nafasi ya kufanya mengi zaidi katika utumishi wa Yehova. Pia, mama alinifundisha jinsi ya kuwa mkaribishaji-wageni, na hilo limenisaidia kukutana na ndugu na dada wazuri ambao ningeweza kuiga mifano yao.” (Met. 31:​15, 21, 22) Mwanamke mwenye bidii na mkaribishaji-wageni ambaye amejifunza kusimamia nyumba yake ni baraka kwa familia yake na kutaniko pia.—Met. 31:​13, 17, 27; Mdo. 16:15.

14. Unajifunza nini kutokana na mfano wa Crystal, na unapaswa kukazia fikira nini?

14 Jifunze kujitegemea na kuridhika. Sifa hizo ni muhimu sana kwa Wakristo wote wakomavu. (Flp. 4:11) Dada anayeitwa Crystal, anasema hivi: “Wazazi wangu walinisaidia kuchagua mambo nitakayosoma katika elimu ya sekondari ili niweze kujifunza ustadi utakaonisaidia. Baba yangu alinitia moyo nisome masomo ya uhasibu, ambayo yalisaidia sana.” Zaidi ya kujifunza ustadi unaohitaji ili kupata kazi, jitahidi kujifunza kupanga bajeti na kushikamana nayo. (Met. 31:​16, 18) Kazia fikira malengo ya kiroho kwa kuepuka madeni yasiyo ya lazima na kuridhika na maisha rahisi.—1 Tim. 6:8.

JITAYARISHE KWA AJILI YA MAJUKUMU YA WAKATI UJAO

15-16. Akina dada waseja wanawanufaishaje wengine? (Marko 10:​29, 30)

15 Kusitawisha sifa nzuri za kiroho na kuwa na ustadi unaofaa, kutakusaidia kutimiza vizuri majukumu yako ya wakati ujao. Fikiria mifano michache ya mambo unayoweza kufanya.

16 Unaweza kuendelea kuwa mseja kwa kipindi fulani cha wakati. Kulingana na maneno ya Yesu, baadhi ya wanawake wamechagua kutoolewa, hata ingawa useja hauonwi kuwa jambo zuri katika utamaduni wao. (Mt. 19:​10-12) Huenda wengine wakaendelea kuwa waseja kwa sababu ya hali. Uwe na hakika kwamba Yehova na Yesu wanawathamini Wakristo waseja. Ulimwenguni kote, dada waseja ni mfano mzuri katika makutaniko. Upendo wao kwa wengine na jinsi wanavyowahangaikia kutoka moyoni kunawachochea wanawake hao Wakristo wawe dada na mama wa kiroho kwa wengi.—Soma Marko 10:​29, 30; 1 Tim. 5:2.

17. Dada kijana anaweza kujitayarishaje sasa ili kuingia katika utumishi wa wakati wote?

17 Unaweza kuwa mtumishi wa wakati wote. Wanawake Wakristo wanatimiza sehemu kubwa katika kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote. (Zab. 68:11) Je, unaweza kupanga sasa kuingia katika utumishi wa wakati wote? Unaweza kutumikia ukiwa painia, mjenzi, au Mwanabetheli. Sali kuhusu lengo lako. Zungumza na wale ambao wamefikia lengo kama hilo, na ujifunze unapaswa kufanya nini ili ustahili. Kisha panga mipango hususa. Kufikia lengo lako kutakufungulia nafasi nyingi zenye kusisimua katika utumishi wa Yehova.

Ikiwa unafikiria kufunga ndoa, unapaswa kumchagua mwenzi wako kwa makini sana (Tazama fungu la 18)

18. Kwa nini dada anapaswa kumchagua mume wake kwa makini sana? (Tazama pia picha.)

18 Unaweza kuchagua kufunga ndoa. Sifa na ustadi tuliozungumzia utakusaidia uwe mke mwema. Bila shaka, ikiwa unafikiria kufunga ndoa, unapaswa kuchagua mwenzi wako kwa makini sana. Huo ni mojawapo ya maamuzi muhimu zaidi ambayo utafanya maishani. Kumbuka, utakuwa chini ya ukichwa wa mwanamume unayefunga ndoa naye. (Rom. 7:2; Efe. 5:​23, 33) Hivyo jiulize: ‘Je, mwanamume huyo ni Mkristo mkomavu? Je, anatanguliza masilahi ya kiroho maishani mwake? Je, anafanya maamuzi ya hekima? Je, anaweza kukiri makosa yake? Je, anaheshimu wanawake? Je, ana ustadi unaohitajika ili kunitegemeza kiroho, kimwili, na kihisia? Je, anatimiza majukumu yake vizuri? Kwa mfano, ana majukumu gani kutanikoni na anayatimizaje?’ (Luka 16:10; 1 Tim. 5:8) Bila shaka, ikiwa unataka kupata mume mzuri, unahitaji kuwa mke mzuri pia.

19. Kwa nini jukumu la “msaidizi” ni lenye kuheshimika?

19 Biblia inasema kwamba mke mzuri ni “msaidizi” wa mume wake na “kikamilisho” chake. (Mwa. 2:18) Je, ufafanuzi huo unamshushia mke heshima? Hapana! Jukumu la mke la kuwa msaidizi ni lenye heshima. Kumbuka, hata Yehova mara nyingi anaitwa “msaidizi” katika Biblia. (Zab. 54:4; Ebr. 13:6) Mke ni msaidizi wa kweli wa mume wake anapomuunga mkono na kumsaidia kutekeleza maamuzi yanayohusu familia. Na kwa kuwa mke anampenda Yehova, anajitahidi kuwasaidia wengine waone sifa nzuri za mume wake. (Met. 31:​11, 12; 1 Tim. 3:11) Unaweza kujitayarisha kwa ajili ya jukumu hilo la wakati ujao kwa kuimarisha upendo wako kwa Yehova na kwa kuwa msaidizi wa wengine nyumbani na kutanikoni.

20. Mama anaweza kuisaidiaje familia yake?

20 Unaweza kuwa mama. Baada ya kufunga ndoa, wewe na mume wako mnaweza kuwa na watoto. (Zab. 127:3) Hivyo, ni jambo la hekima kufikiria kuhusu hilo mapema. Sifa na stadi tulizozungumzia katika makala hii zitakusaidia ukiwa mke na mama. Upendo, fadhili, na subira yako itachangia amani na furaha nyumbani kwako ambapo watoto wako watahisi wakiwa salama na watasitawi.—Met. 24:3

Wanawake wengi vijana ambao wamefundishwa kupitia Maandiko na wanatumia mambo waliyojifunza, wamekuwa Wakristo wakomavu (Tazama fungu la 21)

21. Tunahisije kuhusu dada zetu, na kwa nini? (Tazama picha kwenye jalada.)

21 Tunawapenda sana enyi akina dada kwa mambo yote mnayofanya kwa ajili ya Yehova na watu wake. (Ebr. 6:10) Mnajitahidi kusitawisha sifa za kiroho, kujifunza ustadi utakaowasaidia katika maisha yenu na maisha ya wengine, na kujitayarisha vizuri kwa ajili ya majukumu mnayoweza kupata wakati ujao. Mna thamani kubwa katika tengenezo la Yehova!

WIMBO 137 Wanawake Waaminifu, Dada Wakristo

a Enyi dada vijana, mnathaminiwa kutanikoni. Mnaweza kufikia ukomavu wa Kikristo kwa kusitawisha sifa zinazompendeza Mungu, kujifunza ustadi utakaowasaidia, na kujitayarisha kwa ajili ya kutimiza majukumu ya wakati ujao. Matokeo ni kwamba mtafurahia baraka nyingi katika utumishi wa Yehova.

b UFAFANUZI WA MANENO: Mtu aliyefikia ukomavu wa Kikristo anaongozwa na roho ya Mungu, si hekima ya ulimwengu. Anaiga mfano wa Yesu, anajitahidi kudumisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova, na kuwaonyesha wengine upendo wa kujidhabihu.

d Ili kupata habari zaidi kuhusu umuhimu wa kusoma, tazama makala kwenye jw.org yenye kichwa “Kwa Nini Kusoma Ni Muhimu kwa Watoto—Sehemu 1: Kusoma au Kutazama?