Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Fuata Mwongozo wa Mungu Kuhusu Kileo

Fuata Mwongozo wa Mungu Kuhusu Kileo

HAPANA shaka unathamini zawadi mbalimbali za Yehova, kutia ndani uhuru wa kuchagua jinsi utakavyofurahia zawadi hizo. Kulingana na Biblia, divai ni zawadi kutoka kwa Mungu. Na hata inasema hivi: “Mkate umekusudiwa kuleta kicheko, na divai hufanya maisha yafurahishe.” (Mhu. 10:19; Zab. 104:15) Hata hivyo, huenda umejionea kwamba baadhi ya watu wamekuwa na matatizo yanayotokana na kutumia kileo. Zaidi ya hilo, viwango na maoni kuhusu matumizi ya kileo yanatofautiana kotekote duniani na katika tamaduni mbalimbali. Basi, Wakristo wanapaswa kufuata mwongozo gani wenye hekima?

Licha ya mahali tunapoishi au utamaduni wetu, tunaporuhusu maoni ya Yehova yaongoze mawazo na maamuzi yetu, kwa hakika tutanufaika na kuwa na maisha yenye furaha.

Kama ambavyo huenda umejionea, watu wengi ulimwenguni wanakunywa mara kwa mara na kupita kiasi. Huenda baadhi ya watu wanatumia kileo kwa sababu kinawastarehesha au kuwatuliza. Wengine wanakunywa ili kukabiliana na matatizo. Na katika maeneo mengine, kunywa kileo kwa wingi kunaonwa kuwa jambo linalofaa au linafanya mtu aonwe kuwa mwanamume halisi.

Hata hivyo, Wakristo wana mwongozo wenye hekima kutoka kwa Muumba wao mwenye upendo. Kwa mfano, ametuonya kuhusu matokeo yenye kuhuzunisha ya kunywa kupita kiasi. Huenda tumesoma kuhusu ufafanuzi ulio wazi kwenye Methali 23:​29-35, wa mtu aliyelewa na baadhi ya matatizo aliyopata. a Daniel, mzee Mkristo anayeishi barani Ulaya, anakumbuka jinsi maisha yake yalivyokuwa kabla ya kuwa Mkristo wa kweli, anasema hivi: “Kunywa kupita kiasi kulisababisha nifanye maamuzi mabaya na kupitia hali zenye kuumiza ambazo zimeniacha nikiwa na majeraha ya kihisia.”

Wakristo wanawezaje kutumia vizuri uhuru wao wa kuchagua na kuepuka matatizo yanayotokana na kunywa kileo kupita kiasi? Tunapaswa kuruhusu maoni ya Mungu yaongoze mawazo na matendo yetu.

Acheni tuchunguze yale ambayo Biblia inasema kuhusu kileo na sababu ambazo zinawachochea baadhi ya watu kunywa.

VIWANGO VYA BIBLIA

Neno la Mungu halishutumu kunywa kileo kwa kiasi. Kwa kweli, Biblia inakubali kwamba kunywa divai ni jambo linaloweza kutufurahisha. Tunasoma hivi: “Ule chakula chako kwa shangwe, na unywe divai yako kwa moyo mchangamfu.” (Mhu. 9:7) Pindi fulani Yesu alikunywa divai, na hata watumishi wengine waaminifu wa Yehova walikunywa divai.—Mt. 26:​27-29; Luka 7:34; 1 Tim. 5:23.

Hata hivyo, Neno la Mungu linaonyesha tofauti iliyo wazi kati ya kunywa kileo kwa kiasi na kulewa. Inasema hivi waziwazi: “Msilewe divai.” (Efe. 5:18) Na hata inaonyesha kwamba “walevi . . . hawataurithi Ufalme wa Mungu.” (1 Kor. 6:10) Naam, Yehova anashutumu vikali kunywa kupita kiasi na ulevi. Badala ya kufuata utamaduni wetu, tunafanya maamuzi kwa kutegemea maoni ya Mungu.

Baadhi ya watu wanahisi kwamba wanaweza kunywa kiasi kingi cha kileo bila kulewa. Hata hivyo, jambo hilo ni hatari sana. Maandiko yanaonyesha wazi kwamba kuwa “watumwa wa divai nyingi” kunaweza kumfanya mwanamume (au mwanamke) apotoshwe kimaadili na kiroho. (Tito 2:3; Met. 20:1) Hata Yesu alitoa onyo kwamba “kunywa kupita kiasi” kunaweza kumzuia mtu kuingia katika ulimwengu mpya wa Mungu. (Luka 21:​34-36) Hivyo, ni nini kinachoweza kumsaidia Mkristo aepuke matatizo yanayoweza kutokea kwa urahisi kwa sababu ya kunywa kileo?

CHUNGUZA NIA NA MAZOEA YAKO

Ni hatari kwa mtu kuruhusu utamaduni wake uamue maoni yake kuhusu kunywa. Kwa hekima, Wakristo wanafanya mambo yanayomfurahisha Yehova inapohusu mambo kama vile kula na kunywa. Biblia inatukumbusha hivi: “Iwe mnakula au mnakunywa au mnafanya jambo lingine lolote, fanyeni mambo yote kwa utukufu wa Mungu.” (1 Kor. 10:31) Yafuatayo ni baadhi ya maswali na kanuni za Biblia tunazopaswa kufikiria:

Je, ninakunywa ili nikubaliwe na wengine? Kutoka 23:2 inasema: “Usiufuate umati.” Katika mstari huo, Yehova alikuwa akiwaonya Waisraeli dhidi ya kuwafuata watu ambao hawakumfurahisha. Himizo hilo linawafaa pia Wakristo leo. Ikiwa tutaruhusu watu wengine wafinyange mawazo na maamuzi yetu kuhusu kileo, hatimaye tunaweza kupoteza uhusiano wetu wa karibu pamoja na Yehova na kuacha kuishi kulingana na viwango vyake.—Rom. 12:2.

Je, ninakunywa kileo ili kuonyesha jinsi nilivyo mwenye nguvu? Katika baadhi ya tamaduni, kunywa kileo mara kwa mara na kwa kupita kiasi ni jambo la kawaida na linalokubalika. (1 Pet. 4:3) Lakini ona jambo linaloonyeshwa kwenye 1 Wakorintho 16:13: “Kaeni macho, simameni imara katika imani, endeleeni kuwa kama wanaume, iweni na nguvu.” Je, kweli kileo kinaweza kumsaidia mtu kuwa na nguvu? La hasha. Kileo kinaweza kwa urahisi kudhoofisha uwezo wa mtu wa kufikiri na kufanya maamuzi mazuri. Hivyo, badala ya kuwa ishara inayoonyesha nguvu, kunywa kileo kupita kiasi kunaonyesha mtu ni dhaifu. Isaya 28:7 inasema kwamba mtu ambaye amepotea njia kwa sababu ya kileo anapepesuka na kujikwaa.

Nguvu za kweli zinatoka kwa Yehova na zinahusisha kuwa macho na kusimama imara katika imani. (Zab. 18:32) Mkristo mnyoofu anaweza kufanya hivyo kwa kuendelea kuwa macho na kuchukua hatua mara moja ili kujilinda dhidi ya madhara ya kiroho. Yesu alionyesha nguvu kama hizo alipokuwa duniani, na watu wengi walimheshimu na kumwona kuwa mwanamume halisi mwenye nguvu na ujasiri.

Je, ninatumia kileo kama njia ya kukimbia matatizo yangu? Mtunga zaburi aliongozwa na roho kuandika hivi: “Mahangaiko yaliponilemea, [Yehova] ulinifariji na kunibembeleza.” (Zab. 94:19) Ikiwa unalemewa na matatizo, mtegemee Yehova ili kupata kitulizo, si kileo. Njia nzuri ya kufanya hivyo ni kwa kusali kwa Yehova mara nyingi zaidi. Pia, wengi wamenufaika kwa kutafuta ushauri unaofaa kutoka kwa rafiki mkomavu kutanikoni. Ukweli ni kwamba kunywa kileo ili kukabiliana na matatizo kunaweza kudhoofisha azimio la mtu la kutenda lililo jema. (Hos. 4:11) Daniel, aliyetajwa awali, anakiri hivi: “Nilipambana na mahangaiko na hisia za hatia. Nilikunywa ili kukabiliana na hali hiyo, lakini matatizo yaliongezeka na nikapoteza marafiki na kuacha kujiheshimu.” Mwishowe ni jambo gani lililomsaidia Daniel? Anasema hivi: “Nilitambua kwamba nilimhitaji Yehova karibu yangu, si kileo. Hatimaye, niliweza kukabiliana na matatizo yangu na kuyashinda.” Ukweli ni kwamba sikuzote Yehova yuko karibu yetu ili kutupatia kitulizo, hata ikiwa tumepoteza kabisa tumaini.—Flp. 4:​6, 7; 1 Pet. 5:7.

Ikiwa unakunywa kileo pindi fulani, unaweza kutumia maswali yafuatayo ili kujichunguza: ‘Je, mtu wa familia au rafiki wa karibu amenieleza kwamba ana wasiwasi kuhusu mazoea yangu ya kunywa kileo?’ Ikiwa ndivyo, hilo linaweza kuonyesha kwamba umeanza kusitawisha zoea au tatizo ambalo bado hujalitambua. ‘Je, ninakunywa zaidi ya nilivyokuwa nikinywa awali?’ Hali hiyo inaweza kumpata mtu ambaye kwa sasa si mraibu wa kileo, lakini huenda anaelekea huko. ‘Je, ni vigumu kwangu kutotumia kileo kwa siku kadhaa au kwa muda mrefu zaidi?’ Ikiwa ndivyo, basi huenda kunywa kileo kumekuwa zoea sugu au uraibu. Huenda ukahitaji msaada wa wataalamu ili kushinda tatizo hilo.

Baadhi ya Wakristo wameamua kuepuka kunywa kileo cha aina yoyote kwa sababu ya hatari au matatizo yanayohusiana na kunywa. Huenda wengine wakachagua kutokunywa kwa sababu tu hawapendi ladha yake. Ikiwa yeyote kati ya wale unaoshirikiana nao anafanya uamuzi kama huo, unaweza kumwonyesha fadhili kwa kuheshimu uamuzi wake bila kumkosoa.

Au huenda umeona ni jambo la hekima kujiwekea mipaka. Huenda Mkristo akaamua kudhibiti kiasi atakachokunywa. Au huenda akaamua ni mara ngapi atakunywa, labda mara moja kwa juma au kwa kiasi wakati wa mlo. Wengine wamejiwekea mipaka ya aina za vileo watakavyotumia, kama vile kuamua kunywa kwa kiasi divai au bia, lakini si pombe kali, hata inapochanganywa na vinywaji vingine visivyo na kileo. Mtu anapoweka mipaka iliyo wazi inapohusu kutumia kileo, itakuwa rahisi zaidi kwake kushikamana nayo. Na Mkristo mkomavu hapaswi kuaibika ikiwa amefanya maamuzi hayo na kuazimia kushikamana nayo.

Tunapaswa pia kukumbuka kuwaonyesha wengine ufikirio. Waroma 14:21 inasema: “Ni vema kutokula nyama au kunywa divai au kufanya jambo lolote ambalo litamkwaza ndugu yako.” Unawezaje kutumia shauri hilo? Waonyeshe wengine upendo wa kindugu. Ikiwa unahisi kwamba kutumia kileo kutamkwaza mtu mwingine, je, upendo hautakuchochea kuamua kutokunywa? Hivyo, utaonyesha unawajali wengine na kuheshimu hisia zao, na unatafuta, si faida yako mwenyewe, bali ya wengine.—1 Kor. 10:24.

Isitoshe, huenda serikali ikawa na sheria zinazopaswa kumwongoza Mkristo anapofanya maamuzi. Huenda sheria hizo zikataja umri ambao mtu hapaswi kunywa kileo au zikakataza kuendesha gari au kutumia aina fulani za mashine wakati umekunywa.—Rom. 13:​1-5.

Yehova ametuonyesha heshima kwa kutupatia uhuru wa kufurahia zawadi nyingi ambazo ametupatia. Hilo linatia ndani zawadi ya kutumia uhuru wa kuchagua tunapoamua tutakula au kunywa nini. Acheni maamuzi yetu yaonyeshe kwamba tunathamini uhuru huo kwa kuutumia kwa njia itakayomfurahisha Baba yetu wa mbinguni.

a Ripoti ya shirika la afya la Centers for Disease Control and Prevention la Marekani inasema kwamba madhara ya muda mfupi ya kunywa kileo kupita kiasi yanatia ndani mauaji, kujiua, kushambuliwa kingono, kutendewa kwa ukatili na mtu wa karibu, mwenendo hatari wa kingono, na mimba kuharibika.