Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 29

Muunge Mkono Mwangalizi Wetu Yesu

Muunge Mkono Mwangalizi Wetu Yesu

“Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani.”​—MT. 28:18.

WIMBO 13 Kristo, Kielelezo Chetu

MUHTASARI a

1. Mapenzi ya Yehova ni nini leo?

 LEO, mapenzi ya Mungu ni kwamba habari njema za Ufalme zihubiriwe katika dunia yote. (Marko 13:10; 1 Tim. 2:3, 4) Hii ni kazi ya Yehova, na kazi hii ni muhimu sana hivi kwamba amemchagua Mwana wake mpendwa aiongoze. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba chini ya mwongozo wa Yesu, kazi ya kuhubiri itatimizwa kama Yehova anavyotaka kabla mwisho haujafika.​—Mt. 24:14.

2. Tutazungumzia nini katika makala hii?

2 Katika makala hii, tutaona jinsi Yesu anavyomtumia ‘mtumwa wake mwaminifu na mwenye busara’ kuandaa chakula cha kiroho na kuwapanga wafuasi wake ili wafanye kazi kubwa zaidi ya kuhubiri katika historia ya wanadamu. (Mt. 24:45) Tutaona pia mambo ambayo kila mmoja wetu anaweza kufanya ili kumuunga mkono Yesu na mtumwa mwaminifu.

YESU ANAONGOZA KAZI YA KUHUBIRI

3. Yesu amepewa mamlaka gani?

3 Yesu anaongoza kazi ya kuhubiri. Kwa nini tuna uhakika huo? Muda mfupi kabla ya kwenda mbinguni, Yesu alikutana na baadhi ya wafuasi wake waaminifu kwenye mlima fulani huko Galilaya. Aliwaambia hivi: “Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani.” Kisha ona jambo alilosema: “Basi, nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.” (Mt. 28:18, 19) Hivyo, mamlaka ya kuongoza kazi ya kuhubiri, ni mojawapo ya mambo ambayo Yesu amepewa.

4. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba bado Yesu anaongoza kazi ya kuhubiri?

4 Yesu alisema kwamba kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi ingefanywa katika “mataifa yote” na kwamba angekuwa pamoja na wafuasi wake “sikuzote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mt. 28:20) Maneno hayo yanaonyesha wazi kwamba kazi ya kuhubiri ingeendelea chini ya uongozi wa Yesu hadi siku zetu.

5. Tunahusikaje katika kutimizwa kwa Zaburi 110:3?

5 Yesu hakuwa na wasiwasi kwamba kungekuwa na upungufu wa wafanyakazi katika kipindi cha umalizio wa mfumo wa mambo. Alijua kwamba unabii huu wa mtunga zaburi ungetimizwa: “Watu wako watajitoa kwa hiari katika siku ya jeshi lako.” (Zab. 110:3) Ikiwa unashiriki katika kazi ya kuhubiri, unamuunga mkono Yesu na mtumwa mwaminifu, na unasaidia kutimizwa kwa unabii huo. Kazi hiyo inaendelea kufanywa, ingawa kuna changamoto.

6. Wahubiri wa Ufalme wanakabili changamoto gani leo?

6 Changamoto moja ambayo wahubiri wa Ufalme wanakabili ni upinzani. Waasi-imani, viongozi wa kidini, na wanasiasa wamewafanya watu wengi wawe na maoni yasiyofaa kuhusu kazi yetu. Ikiwa watu wetu wa ukoo, watu tunaofahamiana nao, na wafanyakazi wenzetu wameathiriwa na habari hizo za uwongo, huenda wakatushinikiza tuache kumtumikia Yehova na tuache kuhubiri. Katika baadhi ya nchi, upinzani huu unahusisha vitisho, kushambuliwa, kukamatwa, na hata kufungwa gerezani. Hatushangai tunapotendewa hivyo. Yesu alitabiri hivi: “Mtachukiwa na mataifa yote kwa sababu ya jina langu.” (Mt. 24:9) Kwa kweli, tunapochukiwa kwa njia hiyo, ni uthibitisho kwamba tuna kibali cha Yehova. (Mt. 5:11, 12) Ibilisi ndiye anayechochea upinzani huo. Lakini hawezi kumshinda Yesu! Kwa msaada wa Yesu, habari njema zinawafikia watu wa mataifa yote. Fikiria uthibitisho uliopo.

7. Unaona uthibitisho gani kwamba andiko la Ufunuo 14:6, 7 linatimizwa?

7 Tukiwa wahubiri wa Ufalme tunakabili pia changamoto ya kizuizi cha lugha. Katika ufunuo ambao alimpa mtume Yohana, Yesu alitabiri kwamba katika siku zetu habari njema ingeshinda kizuizi hicho. (Soma Ufunuo 14:6, 7.) Jinsi gani? Tunawapa watu wengi iwezekanavyo fursa ya kukubali ujumbe wa Ufalme. Leo, watu duniani pote wanaweza kusoma habari zinazotegemea Biblia kwenye tovuti yetu ya jw.org, kwa sababu ina habari katika lugha zaidi ya 1,000! Baraza Linaloongoza lilitoa idhini ya kutafsiri kitabu Furahia Maisha Milele!, kifaa chetu kikuu cha kufanya wanafunzi, katika lugha zaidi ya 700! Chakula cha kiroho kimeandaliwa pia kupitia video kwa ajili ya viziwi na machapisho katika maandishi ya vipofu. Tunajionea unabii wa Biblia ukitimizwa. Watu “kutoka katika lugha zote za mataifa” wanajifunza kuzungumza “lugha safi” ya kweli za Biblia. (Zek. 8:23; Sef. 3:9) Yote hayo yanatimizwa chini ya uongozi wa Yesu Kristo.

8. Kazi ya kuhubiri imekuwa na matokeo gani kufikia sasa?

8 Leo, zaidi ya watu milioni nane katika nchi 240 wanashirikiana na tengenezo la Yehova, na kila mwaka makumi ya maelfu wanabatizwa! Hata hivyo, jambo muhimu zaidi kuliko idadi, ni sifa za Kikristo, yaani, “utu mpya” ambao wanafunzi hao wapya wanasitawisha. (Kol. 3:8-10) Wengi waliacha maadili mapotovu, ukatili, ubaguzi, na uzalendo. Unabii ulio katika Isaya 2:4 unatimizwa; ‘hawajifunzi vita tena kamwe.’ Tunapojitahidi kuvaa utu mpya, tunawavuta watu kwenye tengenezo la Mungu, na kuthibitisha kwamba tunamfuata mwangalizi wetu Kristo Yesu. (Yoh. 13:35; 1 Pet. 2:12) Mambo hayo hayajitokezi yenyewe tu. Yesu anatupatia msaada tunaohitaji.

YESU AMWEKA RASMI MTUMWA

9. Kulingana na Mathayo 24:45-47, ni unabii gani uliotolewa kuhusu wakati wa mwisho?

9 Soma Mathayo 24:45-47. Yesu alitabiri kwamba katika wakati wa mwisho, angemweka rasmi “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ili aandae chakula cha kiroho. Basi, tunatazamia kwamba mtumwa huyo angekuwa akifanya kazi kwa bidii leo. Na hivyo ndivyo ilivyo. Mwangalizi wetu ametumia kikundi kidogo cha wanaume watiwa-mafuta kuwaandalia watu wa Mungu na wale wanaopendezwa ‘chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa.’ Wanaume hao hawajioni kuwa mabwana wa imani ya wengine. (2 Kor. 1:24) Badala yake, wanatambua kwamba Yesu Kristo ndiye “kiongozi na kamanda” wa watu wake.​—Isa. 55:4.

10. Ni chapisho gani kwenye picha ambalo lilikusadikisha uanze kutembea katika njia inayoongoza kwenye uzima wa milele?

10 Tangu mwaka wa 1919, mtumwa huyo mwaminifu ameandaa machapisho mbalimbali ambayo yamewapatia kwa mara ya kwanza watu wanaopendezwa chakula cha kiroho chenye lishe. Mwaka wa 1921, mtumwa huyo aliandaa kitabu The Harp of God ili kuwasaidia watu wanaopendezwa wajifunze mafundisho ya msingi ya Biblia. Kadiri mambo yalivyobadilika, machapisho zaidi yaliandaliwa. Ni chapisho gani ambalo lilikusaidia wewe umjue na kumpenda Baba yako wa mbinguni? Je, ni kitabu “Mungu na Awe wa Kweli,Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele, Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani, Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, Biblia Inafundisha Nini Hasa?, Biblia Inatufundisha Nini?, au ni Furahia Maisha Milele!, chapisho letu jipya kabisa? Machapisho hayo yote yalikusudiwa kutimiza uhitaji hususa yalipotolewa.

11. Kwa nini ni muhimu kwetu sote kupokea chakula cha kiroho?

11 Si wale tu walioanza kujifunza hivi karibuni wanaohitaji chakula kigumu cha kiroho. Sisi sote tunakihitaji. Mtume Paulo aliandika hivi: “Chakula kigumu ni cha watu wakomavu.” Paulo aliongezea kwamba kutumia mambo tunayojifunza katika Biblia, kungetusaidia “kutofautisha mambo yaliyo sawa na mambo yasiyo sawa.” (Ebr. 5:14) Katika nyakati hizi ngumu ambapo viwango vya maadili vimeshuka kabisa, inaweza kuwa vigumu sana kushikamana na viwango vya Yehova. Lakini Yesu anahakikisha kwamba tunapata nguvu tunazohitaji kupitia chakula cha kiroho kinachovutia. Chanzo cha chakula hicho ni Biblia, Neno la Mungu lililoongozwa na roho. Mtumwa mwaminifu anatayarisha na kugawa chakula hiki chini ya mwongozo wa Yesu.

12. Kama Yesu, tumeliheshimu jina la Mungu jinsi gani?

12 Kama Yesu, tunaliheshimu jina la Mungu kama linavyostahili kuheshimiwa. (Yoh. 17:6, 26) Kwa mfano, mwaka wa 1931 tulianza kuitwa kwa jina Mashahidi wa Yehova linalotegemea Maandiko, na hivyo kuonyesha kwamba tunataka kutambulika kwa jina la Baba yetu wa mbinguni. (Isa. 43:10-12) Na tangu Oktoba mwaka huo, jina la Mungu limekuwa katika jalada la kila toleo la gazeti hili. Isitoshe, Biblia Takatifu​—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya imelirudisha jina la Mungu mahali panapofaa katika Neno lake. Hilo ni kinyume kabisa na makanisa ya dini zinazodai kuwa za Kikristo ambazo zimeondoa jina Yehova katika tafsiri zao nyingi za Biblia!

YESU ANAWAPANGA WAFUASI WAKE

13. Ni nini kinachokusadikisha kwamba Yesu anamtumia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” leo? (Yohana 6:68)

13 Kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” Yesu amefanyiza tengenezo la pekee hapa duniani ili kuendeleza ibada safi. Unahisije kuhusu tengenezo hilo? Labda una maoni kama ya mtume Petro ambaye alimwambia Yesu hivi: “Tutaenda kwa nani? Wewe una maneno ya uzima wa milele.” (Yoh. 6:68) Tungekuwa wapi leo ikiwa hatungeanza kushirikiana na tengenezo la Yehova? Kupitia tengenezo hili, Kristo anahakikisha kwamba tunalishwa vizuri kiroho. Pia, anatuzoeza ili tutimize huduma yetu kwa njia nzuri. Isitoshe, anatusaidia kuvaa “utu mpya” ili tumfurahishe Yehova.​—Efe. 4:24.

14. Umenufaikaje kwa kuwa sehemu ya tengenezo la Yehova wakati wa janga la COVID-19?

14 Yesu anaandaa mwongozo wenye hekima ili kutusaidia kukabiliana na majanga. Manufaa ya mwongozo huo yalionekana wakati wa janga la COVID-19. Ingawa watu wengi ulimwenguni hawakuwa na uhakika kuhusu jambo la kufanya, Yesu alihakikisha kwamba tunapokea mwongozo ulio wazi ili kuwa salama. Tulitiwa moyo tuvae barakoa tunapokuwa katika maeneo ya umma na kudumisha umbali unaofaa kutoka kwa wengine. Wazee wa kutaniko walikumbushwa wadumishe mawasiliano na wote kutanikoni kwa ukawaida na kujitahidi kutambua mahitaji yao ya kimwili na kiroho. (Isa. 32:1, 2) Tulipokea mwongozo zaidi na kutiwa moyo kupitia ripoti za Baraza Linaloongoza.

15. Tulipewa mwongozo gani kuhusu kufanya mikutano na kushiriki katika kazi ya kuhubiri wakati wa janga la COVID-19, na matokeo yamekuwaje?

15 Pia, wakati wa janga hilo, tulipokea mwongozo ulio wazi kuhusu kufanya mikutano ya kutaniko na kushiriki katika kazi ya kuhubiri. Bila kupoteza muda, tulianza kuhudhuria mikutano ya Kikristo, makusanyiko ya mzunguko, na makusanyiko ya eneo kupitia video kwenye intaneti. Pia, tulianza kutoa ushahidi hasa kupitia kuandika barua na kupiga simu. Yehova alibariki jitihada zetu. Ofisi nyingi za tawi zimeripoti kwamba kumekuwa na ongezeko kubwa la idadi ya wahubiri. Isitoshe, wengi wamejionea mambo yenye kutia moyo katika kipindi hicho.​—Tazama sanduku “ Yehova Hubariki Kazi Yetu ya Kuhubiri.”

16. Tunaweza kuwa na uhakika gani?

16 Huenda wengine walihisi kwamba tengenezo lilikuwa linachukua tahadhari kupita kiasi kuhusiana na janga hilo. Lakini tena na tena, ilionekana wazi kwamba mwongozo tuliopokea ulikuwa wenye hekima. (Mt. 11:19) Na tunapotafakari jinsi Yesu anavyowaongoza watu wake kwa upendo, tuna uhakika kwamba hata hali ziweje wakati ujao, Yehova na Mwana wake watakuwa pamoja nasi.​—Soma Waebrania 13:5, 6.

17. Unahisije kuhusu kufanya kazi chini ya mwongozo wa Yesu?

17 Tumebarikiwa sana kufanya kazi chini ya mwongozo wa Yesu! Tunashirikiana na tengenezo ambalo linashinda vizuizi vyote vya kitamaduni, kitaifa, na lugha. Tunalishwa vizuri kiroho na tunazoezwa kikamili ili kufanya kazi ya kuhubiri. Kila mmoja wetu anafundishwa jinsi ya kuvaa utu mpya, na tunajifunza kupendana. Tuna kila sababu ya kujivunia mwangalizi wetu Yesu!

WIMBO 16 Msifuni Yah kwa Mwana Wake Mtiwa Mafuta

a Leo, mamilioni ya wanaume, wanawake, na watoto wanatangaza kwa bidii habari njema. Je, wewe ni mmoja wao? Ikiwa ndivyo, unafanya kazi chini ya uangalizi wa Bwana wetu Yesu Kristo. Katika makala hii, tutachunguza uthibitisho kwamba Yesu anaongoza kazi ya kuhubiri leo. Kutafakari kuhusu habari hii kutatusaidia kuazimia kuendelea kumtumikia Yehova chini ya mwongozo wa Kristo.