Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 29

WIMBO 121 Tunahitaji Sifa ya Kujizuia

Endelea Kujilinda Dhidi ya Majaribu

Endelea Kujilinda Dhidi ya Majaribu

“Endeleeni kukesha na kusali bila kuacha, ili msiingie katika majaribu.”MT. 26:41.

JAMBO KUU

Kutusaidia kutambua umuhimu wa kuepuka kutenda dhambi na pia kutambua hatua zinazoongoza kwenye dhambi.

1-2. (a) Yesu aliwapatia wanafunzi wake onyo gani? (b) Kwa nini wanafunzi walimwacha Yesu? (Tazama pia picha.)

 “BILA shaka, roho inataka lakini mwili ni dhaifu.” a (Mt. 26:41b) Aliposema maneno hayo, Yesu alionyesha anaelewa kwamba sisi si wakamilifu. Lakini maneno yake pia yalitia ndani onyo hili: Jihadhari dhidi ya kujiamini kupita kiasi. Mapema usiku huo, wanafunzi walikuwa wameeleza kwa uhakika azimio lao la kushikamana na Bwana wao. (Mt. 26:35) Walikuwa na nia nzuri. Hata hivyo, hawakutambua jinsi ambavyo ingekuwa rahisi kwao kuacha kushikamana na azimio lao waliposhinikizwa. Hivyo, Yesu aliwaonya hivi: “Endeleeni kukesha na kusali bila kuacha, ili msiingie katika majaribu.”—Mt. 26:41a.

2 Kwa kusikitisha, wanafunzi hao walishindwa kuendelea kukesha. Yesu alipokamatwa, je, walishikamana naye au waliogopa na kukimbia? Kwa kuwa hawakuchukua tahadhari, wanafunzi hao walifanya kile ambacho walisema hawangefanya kamwe—walimwacha Yesu.—Mt. 26:56.

Yesu aliwahimiza wanafunzi wake waendelee kukesha na kujilinda dhidi ya majaribu, lakini walimwacha (Tazama fungu la 1-2)


3. (a) Kwa nini ni lazima tuepuke kujiamini kupita kiasi ili tuendelee kuwa washikamanifu kwa Yehova? (b) Tutachunguza nini katika makala hii?

3 Hatupaswi kujiamini kupita kiasi. Ni kweli kwamba tumeazimia kutofanya jambo lolote lisilompendeza Yehova. Hata hivyo, sisi si wakamilifu na tunaweza kushawishiwa kufanya mambo mabaya. (Rom. 5:12; 7:​21-23) Bila kutarajia, tunaweza kukabili hali ambazo zitafanya tuvutiwe na kushawishiwa kufanya mambo mabaya. Ili tuendelee kuwa washikamanifu kwa Yehova na Mwana wake, tunahitaji kufuata ushauri wa Yesu wa kuendelea kujilinda dhidi ya kishawishi cha kutenda dhambi. Makala hii inaweza kutusaidia kufanya hivyo. Kwanza, tutachunguza mambo ambayo ni lazima tujilinde nayo. Kisha, tutachunguza jinsi ya kujilinda dhidi ya majaribu. Mwishowe, tutajifunza jinsi ya kuendelea kujilinda.

ENDELEA KUJILINDA—DHIDI YA MAMBO GANI?

4-5. Kwa nini tunapaswa kujilinda dhidi ya kufanya hata dhambi ndogo?

4 Hata dhambi zinazoonekana kuwa ndogo, zinaweza kudhoofisha uhusiano wetu pamoja na Yehova. Pia, zinaweza kusababisha tutende dhambi nzito zaidi.

5 Sisi sote tunaweza kushawishiwa kutenda dhambi. Lakini kila mmoja wetu ana mambo ambayo yanaweza kumshawishi kwa urahisi zaidi, iwe ni kutenda dhambi nzito, kujihusisha katika mwenendo fulani usio safi, au kuathiriwa na njia ya ulimwengu ya kufikiri. Kwa mfano, huenda mtu fulani anapambana dhidi ya kishawishi cha kufanya uasherati. Inawezekana mwingine anapambana dhidi ya kishawishi cha kufanya mambo yasiyo safi, kama vile kupiga punyeto au kutazama ponografia. Pia, huenda mwingine anapambana na hisia za kuwaogopa wanadamu, kiburi, kukasirika haraka, au jambo lingine. Kama Yakobo alivyosema, “kila mtu hujaribiwa kwa kuvutwa na kushawishiwa na tamaa yake mwenyewe.”Yak. 1:14.

6. Tunapaswa kujichunguza kwa unyoofu kuhusu nini?

6 Je, unajua wewe unashawishiwa kwa urahisi na mambo gani? Ni jambo la hatari kupuuza udhaifu wetu au kufikiri kwamba tuna nguvu nyingi sana hivi kwamba tunaweza kujidhibiti tusifanye dhambi. (1 Yoh. 1:8) Isitoshe, Paulo anaonyesha kwamba hata walio “na sifa za kustahili kiroho” wanaweza kushindwa na jaribu ikiwa hawaendelei kujilinda. (Gal. 6:1) Ni lazima tujichunguze kwa unyoofu na kutambua mambo ambayo yanaweza kutushawishi kwa urahisi kufanya dhambi.—2 Kor. 13:5.

7. Tunapaswa kukazia uangalifu sana mambo gani? Toa mfano.

7 Tunapaswa kufanya nini mara tu tunapotambua mambo ambayo yanaweza kutushawishi kwa urahisi zaidi kufanya dhambi? Imarisha azimio lako la kupinga kishawishi hicho! Kwa mfano, katika nyakati za Biblia, upande wa kuta za jiji ambapo ilikuwa rahisi zaidi kushambuliwa na maadui ulikuwa upande wenye malango. Hivyo, sehemu ya malango ililindwa zaidi. Vivyo hivyo, tunapaswa kukazia uangalifu sana mambo ambayo tunajua ni udhaifu wetu.—1 Kor. 9:27.

JINSI YA KUJILINDA

8-9. Kijana anayefafanuliwa katika Methali sura ya 7 angewezaje kuepuka kutenda dhambi nzito? (Methali 7:​8, 9, 13, 14, 21)

8 Tunawezaje kujilinda? Tufikirie mambo ambayo tunaweza kujifunza kutokana na mwanamume kijana anayetajwa katika Methali sura ya 7. Alifanya uasherati na mwanamke mwasherati. Mstari wa 22 unatuambia kwamba “ghafla” kijana huyo alimfuata. Lakini mistari inayotangulia inaonyesha kwamba kabla ya hapo alikuwa amefanya mambo kadhaa ambayo hatua kwa hatua yalimwongoza kwenye dhambi.

9 Ni mambo gani yaliyomwongoza kwenye dhambi? Kwanza, jioni, “alipita barabarani karibu na njia panda anapoishi mwanamke huyo [mwasherati].” Kisha, akashika njia inayoelekea nyumbani kwa mwanamke huyo. (Soma Methali 7:​8, 9.) Halafu, alipomwona mwanamke huyo, hakuondoka. Badala yake, alikubali mwanamke huyo ampige busu na alimsikiliza alipozungumza kuhusu dhabihu za ushirika alizotoa. Huenda mwanamke huyo alimwambia hivyo ili kijana huyo afikiri kwamba yeye si mtu mbaya. (Soma Methali 7:​13, 14, 21.) Ikiwa kijana huyo angeepuka mambo yaliyomwongoza kwenye dhambi, angeweza kujilinda dhidi ya vishawishi hivyo na kuepuka kutenda dhambi.

10. Leo, huenda mtu akafanyaje kosa lilelile alilofanya yule kijana?

10 Simulizi la Sulemani linaonyesha jambo linaloweza kumpata mtumishi yeyote wa Yehova. Huenda akatenda dhambi nzito na baadaye akahisi kwamba kila kitu kilitokea “ghafla.” Au huenda akasema, “Ilitokea tu bila kutarajia.” Hata hivyo, ikiwa atafikiria kuhusu jinsi mambo yalivyotukia, inaelekea atagundua kwamba alifanya mambo fulani yasiyo ya hekima ambayo yalimwongoza kutenda dhambi. Huenda mambo hayo yakatia ndani marafiki wabaya, burudani zisizofaa, au kutembelea sehemu zisizomfaa Mkristo—iwe ni mtandaoni au sehemu halisi. Huenda pia mtu huyo aliacha kusali, kusoma Biblia, kuhudhuria mikutano, au kushiriki katika huduma. Kama kijana aliyezungumziwa kwenye Methali, huenda mtu huyo hakutenda dhambi “ghafla” kama alivyofikiri.

11. Tunapaswa kufanya nini ili tusitumbukie katika dhambi?

11 Tunajifunza nini? Tunahitaji kuepuka kutenda dhambi, na pia hatua zinazoongoza kwenye dhambi hiyo. Sulemani pia anataja jambo hilohilo baada ya kusimulia kisa cha yule kijana na mwanamke mwasherati. Akimrejelea yule mwanamke, alisema hivi: “Msipotee njia na kufuata vijia vyake.” (Met. 7:25) Na hata alisema: “Kaeni mbali naye; msiukaribie mlango wa nyumba yake.” (Met. 5:​3, 8) Naam, tunajilinda dhidi ya kutenda dhambi kwa kuepuka kabisa hali zinaongoza kwenye dhambi. b Huenda hilo likatia ndani kuepuka hali au utendaji fulani ambao si kosa kwa Mkristo kufanya, lakini tunajua kwamba unaweza kutuongoza kwenye dhambi.—Mt. 5:​29, 30.

12. Ayubu aliazimia kufanya nini, na hilo lilimsaidiaje kujilinda dhidi ya kishawishi? (Ayubu 31:1)

12 Tunahitaji kufanya uamuzi thabiti ili kuepuka hali zinazoweza kutuongoza kwenye dhambi. Hivyo ndivyo Ayubu alivyofanya. ‘Alifanya agano na macho yake’ ili kamwe asimtazame mwanamke na kumtamani. (Soma Ayubu 31:1.) Kushikamana na uamuzi huo kungemsaidia kuepuka kabisa hatari ya kufanya uzinzi. Sisi pia tunaweza kuazimia kuepuka jambo lolote linaloweza kutuongoza kwenye dhambi.

13. Kwa nini ni lazima tuilinde njia yetu ya kufikiri? (Tazama pia picha.)

13 Ni lazima pia tuilinde njia yetu ya kufikiri. (Kut. 20:17) Baadhi ya watu wanaamini kwamba si kosa kujiwazia wakifanya jambo lisilofaa maadamu hawalifanyi jambo hilo kihalisi. Mtu anayeendelea kujiwazia akifanya jambo fulani baya, atatamani hata zaidi kufanya jambo hilo. Kwa maneno mengine, anajitengenezea kishawishi ambacho sasa anahitaji kukipinga. Bila shaka, pindi fulani mawazo mabaya yataingia akilini. Jambo la muhimu ni kupinga mawazo hayo mara moja na kufikiria mambo mazuri. Tunapofanya hivyo, tunazuia mawazo yasiyofaa yasitokeze tamaa zenye nguvu ambazo ni vigumu kuzishinda na huenda hata zikasababisha tutende dhambi nzito.—Flp. 4:8; Kol. 3:2; Yak. 1:​13-15.

Tunahitaji kuepuka jambo lolote linaloweza kutuongoza kwenye dhambi (Tazama fungu la 13)


14. Ni jambo gani lingine linaloweza kutusaidia kujilinda dhidi ya kishawishi?

14 Ni jambo gani lingine tunaloweza kufanya ili kujilinda dhidi ya kishawishi? Tunahitaji kusadiki kabisa kwamba sikuzote tutanufaika tutakapotii sheria za Yehova. Huenda pindi fulani tukapambana sana ili kupatanisha mawazo na tamaa zetu na mambo ambayo Mungu anakubali. Lakini tunapojitahidi kufanya hivyo, tutakuwa na amani ya akili na furaha ya kweli.

15. Kusitawisha tamaa zinazofaa kutatusaidiaje kujilinda dhidi ya kishawishi?

15 Tunahitaji kusitawisha tamaa zinazofaa. Ikiwa tutajifunza ‘kuchukia maovu, na kupenda yaliyo mema,’ tutaimarisha azimio letu la kufanya yaliyo sawa na kuepuka hali zinazoongoza kwenye dhambi. (Amo. 5:15) Pia, tamaa zinazofaa zitatuimarisha ili tuendelee kuwa thabiti tunapokabili hali zinazotushawishi ambazo hatungeweza kutarajia au kuzizuia.

16. Utendaji wa kiroho unawezaje kutusaidia kuendelea kujilinda? (Tazama pia picha.)

16 Tunawezaje kusitawisha tamaa zinazofaa? Tunaweza kufanya hivyo kwa kuwa na mengi ya kufanya katika utendaji wetu wa kiroho. Tunapokuwa kwenye mikutano ya Kikristo na katika huduma, si rahisi kushawishiwa kufanya mambo mabaya. Badala yake, utendaji huo unaimarisha tamaa yetu ya kumfurahisha Yehova. (Mt. 28:​19, 20; Ebr. 10:​24, 25) Tunaposoma, kujifunza, na kutafakari Neno la Mungu, tunaimarisha upendo wetu kwa yaliyo mema na kuchukia yaliyo mabaya. (Yos. 1:8; Zab. 1:​2, 3; 119:​97, 101) Kumbuka kwamba Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: “[Salini] bila kuacha, ili msiingie katika majaribu.” (Mt. 26:41) Tunapotumia muda kusali kwa Baba yetu wa mbinguni, tunampa fursa ya kutusaidia na tunaimarisha azimio letu la kumfurahisha.—Yak. 4:8.

Ratiba nzuri ya mambo ya kiroho inatuimarisha ili tuweze kupinga vishawishi (Tazama fungu la 16) c


ENDELEA KUJILINDA

17. Ni udhaifu gani ambao Petro alihitaji kuendelea kupambana nao?

17 Inaelekea kwamba tunaweza kushinda kabisa baadhi ya udhaifu au mielekeo yetu ya dhambi. Lakini huenda tukahitaji kupambana kwa muda mrefu dhidi ya udhaifu wetu mwingine. Fikiria mfano wa mtume Petro. Alinaswa na mtego wa kuwaogopa wanadamu alipomkana Yesu mara tatu. (Mt. 26:​69-75) Ilionekana kwamba Petro alikuwa ameshinda woga huo alipotoa ushahidi kwa ujasiri mbele ya Sanhedrini. (Mdo. 5:​27-29) Hata hivyo, miaka kadhaa baadaye, kwa sababu ya “kuwaogopa wale waliotahiriwa,” aliacha kula pamoja na Wakristo wasio Wayahudi kwa muda fulani. (Gal. 2:​11, 12) Woga wa Petro ulikuwa umerudi. Huenda hakuwa ameushinda kabisa.

18. Ni nini kinachoweza kutokea tunapofikiri kwamba tumeshinda mwelekeo fulani mbaya?

18 Huenda tukapatwa na hali kama hiyo. Jinsi gani? Mwelekeo ambao tulidhani tumeushinda unaweza kurudi na kutushawishi tena. Kwa mfano, ndugu mmoja anakiri hivi: “Sikutazama ponografia kwa miaka kumi, basi nilikuwa na uhakika kwamba tatizo langu lilikuwa limekwisha. Lakini uraibu huo ulikuwa umezama tu, ukisubiri hali ambazo zingeruhusu uibuke tena.” Inafurahisha kwamba hakukata tamaa. Alitambua kwamba alihitaji kujitahidi kila siku ili kupambana na udhaifu wake—huenda kwa maisha yake yote katika mfumo huu wa mambo. Kwa msaada wa mke wake na wazee wa kutaniko lake, amekuwa akijitahidi hata zaidi kupinga kishawishi cha kutazama ponografia.

19. Tunaweza kufanya nini ili udhaifu fulani ambao bado hatujaushinda usituongoze kwenye dhambi?

19 Tunaweza kufanya nini ili udhaifu fulani ambao bado hatujaushinda usituongoze kwenye dhambi? Tunaweza kufuata ushauri huu wa Yesu kuhusu vishawishi: “Endeleeni kukesha,” yaani, jilindeni dhidi ya vishawishi. Hata katika pindi unazohisi kwamba una nguvu, endelea kuepuka hali zinazoweza kukushawishi kutenda dhambi. (1 Kor. 10:12) Endelea kutumia mambo ambayo tayari yamekusaidia kushinda vishawishi. Methali 28:14 inasema: “Mwenye furaha ni mtu aliye chonjo sikuzote.”2 Pet. 3:14.

MANUFAA YA KUENDELEA KUJILINDA

20-21. (a) Tutapata manufaa gani ikiwa tutaendelea kujilinda dhidi ya majaribu? (b) Tukifanya sehemu yetu, Yehova naye atatufanyia nini? (2 Wakorintho 4:7)

20 Tunaweza kuwa na uhakika kwamba tunapoendelea kujilinda dhidi ya vishawishi tutanufaika sikuzote. Tunapotenda dhambi, huenda tukapata ‘furaha ya muda,’ lakini kuishi kulingana na viwango vya Yehova kutatupatia furaha nyingi zaidi. (Ebr. 11:25; Zab. 19:8) Hiyo ni kwa sababu tumeumbwa ili tuishi kulingana na njia zake. (Mwa. 1:27) Hivyo, tutakuwa na dhamiri safi na tutakuwa na tumaini la kuishi milele.—1 Tim. 6:12; 2 Tim. 1:3; Yuda 20, 21.

21 Ni kweli kwamba “mwili ni dhaifu,” lakini hilo halimaanishi kuwa hatuna msaada wowote. Yehova yuko tayari kutupatia nguvu tunazohitaji. (Soma 2 Wakorintho 4:7.) Hata hivyo, umeona kwamba nguvu ambazo Mungu hutupatia ni zinazopita zile za kawaida. Hivyo, ni wajibu wetu kuwa na nguvu za kawaida, yaani, jitihada ambazo sisi wenyewe tunafanya kila siku ili kujilinda dhidi ya kishawishi. Tukifanya sehemu yetu, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atajibu sala zetu na kutupatia nguvu zaidi tunapozihitaji. (1 Kor. 10:13) Naam, kwa msaada wa Yehova, tunaweza kujilinda dhidi ya majaribu.

WIMBO 47 Sali kwa Yehova Kila Siku

a UFAFANUZI WA MANENO: “Roho” inayotajwa kwenye Mathayo 26:41 ni nguvu zilizo ndani yetu zinazofanya tuhisi au kutenda kwa njia fulani. “Mwili” ni hali yetu ya kutokuwa wakamilifu. Hivyo, huenda tukawa tumeazimia kufanya jambo lililo sawa, lakini ikiwa hatutakuwa waangalifu, tunaweza kushawishiwa kufanya jambo ambalo Biblia inasema ni kosa.

b Mtu ambaye amefanya dhambi nzito anaweza kupata msaada katika kitabu Furahia Maisha Milele! somo la 57 jambo kuu la 1-3, na katika makala “‘Tazama Mbele Moja kwa Moja’ Kwenye Wakati Ujao” kwenye gazeti la Mnara wa Mlinzi la Novemba 2020, uku. 27-29, fungu la 12-17.

c MAELEZO YA PICHA: Ndugu anasoma andiko la siku asubuhi, anasoma Biblia mchana anapokuwa kwenye mapumziko kazini, na anahudhuria mkutano wa katikati ya juma jioni.