Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 28

WIMBO 123 Kutii Utaratibu wa Kitheokrasi Kwa Ushikamanifu

Je, Unaweza Kuitambua Kweli?

Je, Unaweza Kuitambua Kweli?

“Simameni imara . . . mkiwa mmejifunga kiunoni mshipi wa ile kweli.”EFE. 6:14.

JAMBO KUU

Kujifunza jinsi ya kutambua tofauti kati ya kweli tuliyojifunza kutoka kwa Yehova na uwongo unaoendelezwa na Shetani na wapinzani wetu.

1. Unahisije kuhusu kweli?

 WATU wa Yehova wanaipenda kweli inayopatikana katika Neno la Mungu. Na imani yetu inategemea kweli hiyo. (Rom. 10:17) Tumeamini kwamba Yehova ameliweka kutaniko la Kikristo kuwa “nguzo na tegemezo la ile kweli.” (1 Tim. 3:15) Na kwa hiari tunajitiisha kwa “wale wanaoongoza” kati yetu wanapotufafanulia kweli kutoka katika Biblia na kutupatia mwongozo unaopatana na mapenzi ya Mungu.—Ebr. 13:17.

2. Kulingana na Yakobo 5:​19, ni hatari gani tunayoweza kukabili baada ya kujifunza kweli?

2 Hata hivyo, baada ya kuikubali kweli na kukubali kwamba tunahitaji kufuata mwongozo unaotegemeka wa tengenezo la Mungu, bado tunaweza kupotoshwa. (Soma Yakobo 5:19.) Shetani angependa sana tuache kutumaini Biblia au mwongozo tunaopata kutoka katika tengenezo la Mungu.—Efe. 4:14.

3. Kwa nini tunapaswa kushikamana na ile kweli? (Waefeso 6:​13, 14)

3 Soma Waefeso 6:​13, 14. Hivi karibuni, Shetani atatumia propaganda zenye nguvu kuyapotosha mataifa yote ili yampinge Yehova. (Ufu. 16:​13, 14) Pia, tunaweza kutarajia kwamba Shetani ataongeza jitihada zake za kuwapotosha watu wa Yehova. (Ufu. 12:9) Kwa sababu hiyo, ni muhimu tujifunze kutambua tofauti iliyopo kati ya ukweli na uwongo na tuwe watiifu kwa ile kweli. (Rom. 6:17; 1 Pet. 1:22) Ni lazima tufanye hivyo ili tuokoke dhiki kuu!

4. Tutachunguza nini katika makala hii?

4 Katika makala hii, tutachunguza sifa mbili tunazohitaji ambazo zitatusaidia kuitambua kweli inayopatikana katika Biblia na kukubali mwongozo wa tengenezo la Mungu. Kisha tutazungumzia mapendekezo matatu tunayopaswa kufuata ili kuendelea kushikamana na ile kweli.

SIFA ZINAZOHITAJIKA ILI KUITAMBUA KWELI

5. Kumwogopa Yehova kunatusaidiaje kuitambua kweli?

5 Kumwogopa Yehova. Tunapomwogopa Yehova kwa njia inayofaa, tutampenda sana hivi kwamba hatutafanya jambo lolote ambalo litamkasirisha. Tunajitahidi sana kujifunza tofauti kati ya mambo yaliyo sawa na yasiyo sawa, kati ya ukweli na uwongo, ili tupate kibali cha Yehova. (Met. 2:​3-6; Ebr. 5:14) Hisia za kuwaogopa wanadamu hazipaswi kamwe kuwa na nguvu kuliko upendo wetu kwa Yehova, kwa sababu mara nyingi mambo yanayowafurahisha wanadamu humkasirisha Yehova.

6. Kuwaogopa wanadamu kulisababishaje wakuu kumi wa Israeli wapotoshe ukweli?

6 Ikiwa tunawaogopa wanadamu kuliko tunavyomwogopa Mungu, tunaweza kupeperushwa mbali kutoka katika kweli. Fikiria mfano wa wakuu 12 ambao walitumwa kupeleleza nchi ambayo Yehova alikuwa ameahidi kuwapa Waisraeli. Kwa wale wapelelezi kumi, hisia za kuwaogopa Wakanaani zilikuwa na nguvu kuliko upendo wao kwa Yehova. Waliwaambia hivi Waisraeli wenzao: “Hatuwezi kwenda kupigana na watu hao, kwa sababu wana nguvu kuliko sisi.” (Hes. 13:​27-31) Kwa maoni ya wanadamu, Wakanaani walikuwa na nguvu kuliko Waisraeli—hilo lilikuwa kweli. Lakini kusema kwamba Waisraeli hangeweza kuwashinda maadui wao kunaonyesha kwamba hawakumfikiria Yehova. Wapelelezi hao kumi walipaswa kukazia fikira kile ambacho Yehova alitaka Waisraeli wafanye. Pia, walipaswa kutafakari mambo ambayo Yehova alikuwa amewafanyia muda mfupi uliopita. Kisha wangetambua kwamba Wakanaani hawakuwa na nguvu zozote walipolinganishwa na Yehova, Mungu Mweza-Yote. Tofauti na wapelelezi hao wasio na imani, Yoshua na Kalebu walitaka kupata kibali cha Yehova. Waliwaambia watu hivi: “Ikiwa Yehova amependezwa nasi, kwa hakika atatuingiza katika nchi hii na kutupatia iwe yetu.”—Hes. 14:​6-9.

7. Tunawezaje kuimarisha sifa ya kumwogopa Yehova? (Tazama pia picha.)

7 Ili tuimarishe sifa ya kumwogopa Yehova, tunahitaji kukazia fikira kumpendeza yeye tunapofanya maamuzi yetu yote. (Zab. 16:8) Unaposoma masimulizi ya Biblia, jiulize hivi: ‘Ikiwa ningekuwa katika hali hiyo, ningefanya uamuzi gani?’ Kwa mfano, jiwazie ukiwa unasikiliza ripoti mbaya ya wale wakuu kumi wa Israeli. Je, ungeamini ripoti hiyo na kuanza kuwaogopa wanadamu, au je, upendo wako kwa Yehova na tamaa yako ya kumfurahisha ingekuwa na nguvu zaidi? Kizazi kizima cha Waisraeli kilishindwa kutambua kwamba Yoshua na Kalebu walikuwa wakisema ukweli. Matokeo ni kwamba, walipoteza pendeleo la kuingia katika Nchi ya Ahadi.—Hes. 14:​10, 22, 23.

Wewe ungemwamini nani? (Tazama fungu la 7)


8. Ni sifa gani ambayo ni lazima tujitahidi kusitawisha, na kwa nini?

8 Unyenyekevu. Yehova hufunua kweli yake kwa watu wanyenyekevu. (Mt. 11:25) Kwa unyenyekevu, tulikubali msaada wa kujifunza kweli. (Mdo. 8:​30, 31) Hata hivyo, ni lazima tuwe waangalifu ili tusiwe na kiburi. Tunapokuwa na kiburi, huenda tukaanza kufikiri kwamba maoni yetu ya kibinafsi ni sahihi au ni yenye hekima, sawa tu na kanuni za Kimaandiko na mwongozo kutoka katika tengenezo la Yehova.

9. Tunawezaje kudumisha unyenyekevu wetu?

9 Ili kudumisha unyenyekevu wetu, tunahitaji kukumbuka kwamba sisi ni wadogo sana kwa kulinganishwa na ukuu wa Yehova. (Zab. 8:​3, 4) Pia, tunaweza kusali kwa Yehova atusaidie tuwe wanyenyekevu zaidi na tuwe tayari kufundishwa. Yehova atatusaidia tutangulize mawazo yake yanayopatikana katika Neno lake na tengenezo lake, badala ya mawazo yetu. Katika usomaji wako wa Biblia, tafuta mambo yanayothibitisha kwamba Yehova anapenda unyenyekevu na anachukia kiburi, kujisifu, na majivuno. Na ujitahidi sana kuendelea kuwa mnyenyekevu ikiwa utapata pendeleo la utumishi ambalo litafanya uwe na mamlaka ya kadiri fulani au ujulikane.

JINSI TUNAVYOWEZA KUSHIKAMANA NA KWELI

10. Yehova amewatumia nani kutoa maagizo na mwongozo kwa watu wake?

10 Endelea kuutumaini mwongozo wa kitheokrasi. Katika Israeli la kale, Yehova alimtumia Musa na kisha Yoshua kuwasilisha maagizo kwa watu Wake. (Yos. 1:​16, 17) Waisraeli walibarikiwa walipowaona wanaume hao kuwa wawakilishi wa Yehova Mungu. Karne nyingi baadaye kutaniko la Kikristo lilipoanzishwa, mitume 12 walitoa mwongozo. (Mdo. 8:​14, 15) Kisha, kikundi hicho kiliongezeka na kutia ndani wazee wengine waliokuwa Yerusalemu. Kwa kufuata mwongozo uliotolewa na wanaume hao waaminifu, “makutaniko yakaendelea kuimarishwa katika imani na kuongezeka idadi siku baada ya siku.” (Mdo. 16:​4, 5) Katika siku zetu, sisi pia tunabarikiwa tunapofuata mwongozo wa kitheokrasi unaotoka kwenye tengenezo la Yehova. Lakini Yehova atahisije ikiwa tunakataa kuwatambua wale ambao amewaweka rasmi? Tunaweza kujibu swali hilo kwa kuchunguza kilichotokea Waisraeli walipokuwa wakielekea kwenye Nchi ya Ahadi.

11. Ni nini kilichowapata Waisraeli wa kale ambao hawakumheshimu Musa, ambaye alichaguliwa na Yehova awaongoze? (Tazama pia picha.)

11 Pindi moja, Waisraeli walipokuwa safarini kuelekea kwenye Nchi ya Ahadi, wanaume maarufu walimpinga Musa na jukumu alilopewa na Yehova. Walisema hivi: “Kusanyiko lote ni takatifu [si Musa tu], watu wote, na Yehova yuko miongoni mwao.” (Hes. 16:​1-3) Ingawa ilikuwa kweli kwamba “kusanyiko lote” lilikuwa takatifu, Yehova alikuwa amemchagua Musa awaongoze watu Wake. (Hes. 16:28) Kwa kumpinga Musa, kwa kweli waasi hao walikuwa wakimpinga Yehova. Hawakukazia fikira jambo ambalo Yehova alitaka; bali walikazia fikira jambo ambalo wao walitaka—mamlaka zaidi na kutambuliwa. Mungu aliwaangamiza viongozi wa uasi huo pamoja na maelfu ya watu wengine waliowaunga mkono. (Hes. 16:​30-35, 41, 49) Leo, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova hapendezwi na watu wasioheshimu mipango ya tengenezo lake.

Wewe ungemuunga mkono nani? (Tazama fungu la 11)


12. Kwa nini tunaweza kuendelea kulitumaini tengenezo la Yehova?

12 Tunaweza kuendelea kulitumaini tengenezo la Yehova. Inapoonekana wazi kwamba kuna uhitaji wa kurekebisha uelewaji wetu wa kweli fulani ya Biblia au jinsi kazi ya Ufalme inavyofanywa, wale wanaoongoza hawasiti kufanya mabadiliko yanayohitajika. (Met. 4:18) Wanafanya hivyo kwa sababu wanataka kumfurahisha Yehova kuliko jambo lingine lolote. Pia, wanafanya yote wanayoweza ili maamuzi yao yategemee Neno la Mungu, yaani, kiwango au kigezo ambacho ni lazima watu wote wa Yehova wakifuate.

13. “Kigezo cha maneno yenye manufaa” kinarejelea nini, na ni lazima tufanye nini?

13 “Endelea kushika kigezo cha maneno yenye manufaa.” (2 Tim. 1:13) “Kigezo cha maneno yenye manufaa” kinarejelea mafundisho ya Kikristo yanayopatikana katika Biblia. (Yoh. 17:17) Mafundisho hayo ndiyo msingi wa kila jambo tunaloamini. Tengenezo la Yehova limetufundisha kushikamana na kigezo hicho. Tukiendelea kufanya hivyo, tutabarikiwa.

14. Baadhi ya Wakristo waliachaje kushikamana na “kigezo cha maneno yenye manufaa”?

14 Ni nini kinachoweza kutokea ikiwa tutaacha kushika “kigezo cha maneno yenye manufaa”? Fikiria mfano ufuatao. Katika karne ya kwanza, inaonekana baadhi ya Wakristo walisambaza uvumi kwamba siku ya Yehova ilikuwa imefika. Huenda kulikuwa na barua iliyosema hivyo, ambayo watu walifikiri iliandikwa na mtume Paulo. Bila kuhakikisha ukweli wa jambo hilo, baadhi ya Wakristo jijini Thesalonike waliamini uvumi huo na hata waliusambaza. Hawangeweza kudanganywa ikiwa wangekumbuka mambo ambayo Paulo aliwafundisha alipokuwa pamoja nao. (2 The. 2:​1-5) Paulo aliwashauri ndugu zake wasiamini kila kitu walichosikia. Ili wasidanganywe tena wakati ujao, Paulo alimalizia barua yake ya pili kwa Wathesalonike kwa kuwaambia maneno haya: “Hii ni salamu yangu, mimi Paulo, kwa mkono wangu mwenyewe, ambayo ni ishara katika kila barua; hivi ndivyo ninavyoandika.”—2 The. 3:17.

15. Tunawezaje kujilinda dhidi ya uwongo unaoonekana kana kwamba ni ukweli? Toa mfano. (Tazama pia picha.)

15 Tunaweza kujifunza nini kutokana na maneno ya Paulo kwa Wathesalonike? Tunaposikia jambo fulani ambalo halipatani na kile ambacho tumejifunza katika Biblia, au uvumi fulani wenye kusisimua, tunahitaji kutumia utambuzi. Katika Muungano wa Sovieti, pindi moja maadui wetu walisambaza barua ambayo ilionekana imetoka makao makuu ya ulimwenguni pote. Barua hiyo iliwatia moyo baadhi ya akina ndugu wajitenge, na kuunda tengenezo linalojitegemea. Barua hiyo ilionekana kuwa ya kweli. Lakini ndugu waaminifu hawakudanganywa. Walitambua kwamba ujumbe wa barua hiyo haukupatana na mambo ambayo walikuwa wamefundishwa. Leo, maadui wa ile kweli wanatumia Intaneti na mitandao ya kijamii ili kutuvuruga na kutugawanya. Badala ya ‘kutikiswa upesi kutoka kwenye kufikiri kwetu,’ tunaweza kujilinda kwa kuchunguza kwa makini ikiwa mambo tunayosikia au kusoma yanapatana na kweli ambazo tayari tumejifunza.—2 The. 2:2; 1 Yoh. 4:1.

Usidanganywe na uwongo ambao unaonekana kana kwamba ni ukweli (Tazama fungu la 15) a


16. Kulingana na Waroma 16:​17, 18, tunapaswa kufanya nini ikiwa baadhi ya watu wanaiacha kweli?

16 Endelea kushirikiana kwa umoja na wale ambao ni washikamanifu kwa Yehova. Mungu anataka tumwabudu kwa umoja. Tutaendelea kuwa na umoja ikiwa tutashikamana na kweli. Yeyote anayeeneza habari zinazopingana na ile kweli anasababisha migawanyiko kutanikoni, hivyo Mungu anatuonya ‘tujiepushe nao.’ La sivyo, sisi pia tunaweza kupeperushwa mbali na kweli.—Soma Waroma 16:​17, 18.

17. Tunanufaikaje kwa kuitambua kweli na kushikamana nayo?

17 Tunapoitambua kweli na kushikamana nayo kabisa, tutaendelea kuwa karibu na Yehova na kuimarisha imani yetu. (Efe. 4:​15, 16) Tutalindwa dhidi ya mafundisho ya uwongo na propaganda za Shetani, na tutaendelea kuwa salama chini ya utunzaji wa Yehova wakati wa dhiki kuu. Endeleeni kushikamana sana na ukweli, “na Mungu wa amani atakuwa pamoja nanyi.”—Flp. 4:​8, 9.

WIMBO 122 Iweni Imara, Thabiti!

a MAELEZO YA PICHA: Igizo: Miaka mingi iliyopita, akina ndugu katika Muungano wa Sovieti, walipokea barua iliyoonekana imetoka makao makuu ya ulimwenguni pote, lakini kwa kweli ilitoka kwa adui zao. Katika siku zetu, adui zetu wanaweza kutumia Intaneti kusambaza habari za uwongo kuhusu tengenezo la Yehova.