Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 30

WIMBO 36 Tuulinde Moyo Wetu

Mambo Muhimu Tunayojifunza Kutokana na Wafalme wa Israeli

Mambo Muhimu Tunayojifunza Kutokana na Wafalme wa Israeli

“Nanyi mtaona tena tofauti kati ya mtu mwadilifu na mtu mwovu, kati ya yule anayemtumikia Mungu na yule asiyemtumikia.”MAL. 3:18.

JAMBO KUU

Kujifunza maoni ya Yehova kuhusu wafalme wa Israeli ili tuweze kuelewa mambo anayotarajia kutoka kwa waabudu wake leo.

1-2. Biblia inafunua nini kuhusu baadhi ya wafalme wa Israeli?

 BIBLIA inawataja wanaume zaidi ya 40 ambao walitawala wakiwa wafalme wa Israeli. a Rekodi hiyo inafunua kwa unyoofu habari fulani hususa kuhusu baadhi yao. Kwa mfano, hata wafalme wazuri walifanya mambo fulani mabaya. Mfikirie mfalme mzuri Daudi. Yehova alisema hivi: ‘Mtumishi wangu Daudi alinifuata kwa moyo wake wote, akitenda tu yaliyokuwa sawa machoni pangu.’ (1 Fal. 14:8) Hata hivyo, Daudi alifanya uzinzi na mke wa mtu na akapanga njama ili mume wake auawe vitani.—2 Sam. 11:​4, 14, 15.

2 Kwa upande mwingine, wafalme wengi ambao hawakuwa waaminifu walifanya mambo fulani mazuri. Mfikirie Rehoboamu. Yehova alimwona kuwa mfalme ambaye “alitenda maovu.” (2 Nya. 12:14) Hata hivyo, Rehoboamu alitii agizo la Mungu la kutenganisha yale makabila kumi kutoka kwenye ufalme wake. Pia, aliwanufaisha watu wa Mungu kwa kuimarisha majiji katika ufalme wake.—1 Fal. 12:​21-24; 2 Nya. 11:​5-12.

3. Ni swali gani muhimu linalojitokeza, na tutazungumzia nini katika makala hii?

3 Swali hili muhimu linajitokeza. Ikiwa wafalme wa Israeli walifanya mambo fulani mazuri na mabaya, Yehova alitumia msingi gani kuamua ikiwa mfalme fulani ni mwaminifu? Jibu la swali hilo litatusaidia kuelewa Yehova anatarajia nini kutoka kwetu. Tutazungumzia mambo matatu ambayo inaelekea Yehova alitumia alipoamua ikiwa mfalme fulani alikuwa mzuri au mbaya. Mambo hayo ni: hali yao ya moyoni, toba yao, na jinsi walivyoshikamana na ibada ya kweli.

MIOYO YAO ILIKUWA KAMILI KUMWELEKEA YEHOVA

4. Ni tofauti gani moja iliyopo kati ya wafalme waaminifu na wasio waaminifu?

4 Wafalme waliomfurahisha Yehova walimwabudu kwa moyo kamili. b Mfalme mzuri Yehoshafati “[alimtafuta] Yehova kwa moyo wake wote.” (2 Nya. 22:9) Maandiko yanasema hivi kumhusu Yosia: “Kabla ya Yosia hakukuwa na mfalme yeyote aliyekuwa kama yeye, ambaye alimrudia Yehova kwa moyo wake wote.” (2 Fal. 23:25) Namna gani kuhusu Sulemani, ambaye baadaye alikuja kufanya mambo mabaya? Biblia inasema: “Moyo wake haukuwa kamili.” (1 Fal. 11:4) Na Biblia inasema hivi kumhusu Abiyamu, mfalme mwingine ambaye hakuwa mwaminifu: “Moyo wake haukuwa kamili kwa Yehova.”—1 Fal. 15:3.

5. Kumtumikia Yehova kwa moyo kamili kunamaanisha nini?

5 Basi, inamaanisha nini kumtumikia Yehova kwa moyo kamili? Mtu mwenye moyo kamili kumwelekea Yehova hamwabudu kidesturi. Badala yake, anamtumikia kwa sababu amejitoa kwake na anampenda. Zaidi ya hilo, anaendelea kujitoa kwake na kumpenda katika maisha yake yote.

6. Tunawezaje kudumisha moyo ulio kamili kumwelekea Yehova? (Methali 4:23; Mathayo 5:​29, 30)

6 Tunawezaje kuwaiga wafalme waaminifu na kudumisha moyo ulio kamili kumwelekea Yehova? Kwa kuepuka mambo yanayoweza kutuathiri. Kwa mfano, burudani zisizofaa zinaweza kuugawanya moyo wetu. Pia, tunahitaji kuwa waangalifu tusiathiriwe na marafiki wabaya na mwelekeo wa kupenda mali. Tukitambua kwamba jambo fulani linaanza kudhoofisha upendo wetu kwa Yehova, tunapaswa kuchukua hatua haraka ili kulirekebisha.—Soma Methali 4:23; Mathayo 5:​29, 30.

7. Kwa nini ni muhimu tuepuke mambo yanayoweza kutuathiri?

7 Hatupaswi kuruhusu moyo wetu ugawanyike. Tusipokuwa waangalifu, tunaweza kujidanganya kwamba tukiongeza utendaji wetu wa kiroho, hatutahitaji kuepuka mambo yanayoweza kutuathiri. Kwa mfano, jiwazie ukiwa nje siku yenye upepo na baridi kali sana. Unapofika nyumbani, unavaa sweta au jaketi. Lakini je, kufanya hivyo kutakusaidia kwa kadiri gani ikiwa utaacha mlango ukiwa wazi? Hewa baridi iliyo nje itaingia haraka nyumbani kwako. Somo ni nini? Tunahitaji kufanya mengi zaidi ya kula chakula cha kiroho “kinachotupatia joto” au kuimarisha uhusiano wetu pamoja na Yehova. Ni lazima pia tufunge mlango ili kuzuia “hewa baridi,” yaani, uvutano mbaya, au mitazamo isiyompendeza Mungu, isiingie katika moyo wetu na kuugawanya.—Efe. 2:2.

WALITUBU DHAMBI ZAO

8-9. Mfalme Daudi na Mfalme Hezekia waliitikiaje walipokaripiwa? (Tazama picha kwenye .)

8 Kama ilivyotajwa mapema, Mfalme Daudi alitenda dhambi nzito. Lakini nabii Nathani alipomweleza jinsi Yehova alivyohisi kuhusu dhambi yake, Daudi alitubu kwa unyenyekevu. (2 Sam. 12:13) Kupitia maneno yake yaliyoandikwa kwenye Zaburi ya 51, tunaona kwamba alitubu kwa unyoofu. Daudi hakuwa akijifanya kwamba anasikitishwa na kosa alilofanya ili kumdanganya Nathani au kuepuka adhabu.—Zab. 51:​3, 4, 17, utangulizi.

9 Mfalme Hezekia pia alimtendea Yehova dhambi. Biblia inasema hivi: “Moyo wake uliingiwa na kiburi, jambo lililomfanya yeye pamoja na watu wa Yuda na wa Yerusalemu wapatwe na ghadhabu.” (2 Nya. 32:25) Kwa nini Hezekia alianza kuwa na kiburi? Huenda alianza kujiona bora kuliko wengine kwa sababu ya mali zake, ushindi wake dhidi ya Waashuru, au kwa sababu aliponywa ugonjwa wake kimuujiza. Huenda alichochewa na kiburi kuwaonyesha Wababiloni mali zake, jambo lililosababisha akaripiwe na nabii Isaya. (2 Fal. 20:​12-18) Lakini kama Daudi, Hezekia alitubu kwa unyenyekevu. (2 Nya. 32:26) Matokeo ni kwamba Yehova alimwona kuwa mfalme mwaminifu ambaye “aliendelea kutenda yaliyokuwa sawa.”—2 Fal. 18:3.

Mfalme Daudi na Mfalme Hezekia walitubu kwa unyenyekevu walipofuatwa na kuelezwa kuhusu dhambi zao (Tazama fungu la 8-9)


10. Mfalme Amazia aliitikiaje aliporekebishwa?

10 Tofauti na Daudi na Hezekia, Mfalme Amazia wa Yuda alitenda yaliyokuwa sawa “lakini si kwa moyo kamili.” (2 Nya. 25:2) Tatizo lilikuwa nini? Baada ya Yehova kumsaidia kuwashinda Waedomu, Amazia alianza kuinamia miungu yao. c Kisha nabii wa Yehova alipomfuata ili kuzungumza naye, kwa ukaidi mfalme huyo alimfukuza.—2 Nya. 25:​14-16.

11. Kulingana na 2 Wakorintho 7:​9, 11, ni lazima tufanye nini ili tupate msamaha? (Tazama pia picha.)

11 Mifano hiyo inatufundisha nini? Tunahitaji kutubu dhambi zetu na kufanya yote tuwezayo ili kuepuka kuzirudia tena. Namna gani ikiwa tunapata shauri kutoka kwa wazee wa kutaniko; hata ikiwa ni kuhusu jambo linaloonekana kuwa dogo? Hatupaswi kuhisi kwamba Yehova au wazee hawatupendi. Hata wafalme wazuri wa Israeli walihitaji karipio na ushauri. (Ebr. 12:6) Tunaporekebishwa, tunapaswa (1) kuitikia kwa unyenyekevu, (2) kufanya mabadiliko yanayohitajika, na (3) kuendelea kumtumikia Yehova kwa moyo wetu wote. Ikiwa tutatubu dhambi zetu, Yehova atatusamehe.—Soma 2 Wakorintho 7:​9, 11.

Tunaporekebishwa, tunapaswa (1) kuitikia kwa unyenyekevu, (2) kufanya mabadiliko yanayohitajika, na (3) kuendelea kumtumikia Yehova kwa moyo wote (Tazama fungu la 11) f


WALISHIKAMANA NA IBADA YA KWELI

12. Ni jambo gani hasa lililowatofautisha wafalme waaminifu na wafalme wasio waaminifu?

12 Wafalme ambao Yehova aliwaona kuwa waaminifu walishikamana na ibada ya kweli. Nao waliwatia moyo watu wa Yehova wafanye vivyo hivyo. Bila shaka, kama tulivyoona, wao pia walifanya makosa. Lakini walikuwa wakimwabudu Yehova peke yake na hata walijitahidi sana ili kuondoa ibada ya sanamu nchini. d

13. Kwa nini Yehova alimhukumu Mfalme Ahabu kuwa si mwaminifu?

13 Namna gani kuhusu wafalme ambao Yehova aliwahukumu kuwa si waaminifu? Ni wazi kwamba si kila jambo walilofanya lilikuwa baya. Hata mfalme mwovu Ahabu alionyesha unyenyekevu kwa kadiri fulani na alijuta kwa sababu alihusika katika mauaji ya Nabothi. (1 Fal. 21:​27-29) Pia, alijenga majiji na kushinda maadui wa Israeli. (1 Fal. 20:​21, 29; 22:39) Lakini Ahabu alijulikana kwa kuendeleza ibada ya uwongo akichochewa na mke wake. Hakutubu kamwe kwa sababu ya kosa hilo.—1 Fal. 21:​25, 26.

14. (a) Kwa nini Yehova alimwona Mfalme Rehoboamu kuwa si mwaminifu? (b) Wafalme wasio waaminifu walifanana kwa njia gani?

14 Mfikirie mfalme mwingine ambaye hakuwa mwaminifu—Rehoboamu. Kama ilivyotajwa mwanzoni, alitimiza mambo mengi mazuri wakati wa utawala wake. Lakini mara tu ufalme wake ulipoimarika, aliiacha Sheria ya Yehova na kufuata ibada ya uwongo. (2 Nya. 12:1) Baada ya hapo, wakati fulani alimwabudu Yehova na wakati mwingine aliabudu miungu ya uwongo. (1 Fal. 14:​21-24) Rehoboamu na Ahabu hawakuwa wafalme pekee walioiacha ibada ya kweli. Kwa kweli, wafalme wengi ambao hawakuwa waaminifu walikuwa na hatia ya kuunga mkono ibada ya uwongo kwa njia fulani. Ni wazi kwamba machoni pa Yehova, kushikamana na ibada ya kweli ilikuwa mojawapo ya sababu kuu iliyoamua ikiwa mfalme alikuwa mzuri au mbaya.

15. Kwa nini kushikamana na ibada ya kweli ni jambo muhimu kwa Yehova?

15 Kwa nini suala la ibada lilikuwa muhimu sana kwa Yehova? Sababu moja ni kwamba wafalme walikuwa na jukumu la kuwaongoza watu wa Mungu kwenye ibada ya kweli. Pia, ibada ya uwongo ilifanya watu watende dhambi nyingine nzito na matendo mengine ya ukosefu wa haki. (Hos. 4:​1, 2) Zaidi ya hayo, wafalme na raia wao walikuwa wamewekwa wakfu kwa Yehova. Hivyo, walipokosa kuwa waaminifu na kujihusisha katika ibada ya uwongo, Biblia inasema ni kana kwamba walikuwa wakifanya uzinzi. (Yer. 3:​8, 9) Mtu anapofanya uzinzi kihalisi, anamtendea dhambi mwenzi wake kwa njia inayomuumiza sana kibinafsi. Vivyo hivyo, mtumishi wa Yehova aliyejiweka wakfu ambaye anajihusisha katika ibada ya uwongo anamtendea Yehova dhambi kwa njia ya moja kwa moja na inayomuumiza kibinafsi. eKum. 4:​23, 24.

16. Ni jambo gani hasa linalomtofautisha mwadilifu na mwovu machoni pa Yehova?

16 Tunajifunza nini? Bila shaka, ni lazima tuazimie kuepuka ibada ya uwongo. Pia, ni lazima tushikamane na ibada ya kweli na kuendelea kuwa na bidii katika utumishi. Nabii Malaki alieleza waziwazi ni nini kinachomtofautisha mtu mwema na mbaya machoni pa Yehova. Aliandika hivi: “Nanyi mtaona tena tofauti kati ya mtu mwadilifu na mtu mwovu, kati ya yule anayemtumikia Mungu na yule asiyemtumikia.” (Mal. 3:18) Hivyo, hatupaswi kuruhusu mambo yoyote—kutia ndani udhaifu na makosa yetu—yatuvunje moyo hivi kwamba tuache kumtumikia Mungu. Kuacha kumtumikia Yehova ni dhambi nzito.

17. Kwa nini tunapaswa kuwa waangalifu sana tunapochagua mwenzi wa ndoa?

17 Ikiwa wewe ni mseja na unafikiria kufunga ndoa, je, unaona jinsi maneno ya Malaki kuhusu kumtumikia Mungu yanavyohusiana na mtu utakayemchagua kuwa mwenzi wako wa ndoa? Huenda mtu akawa na sifa fulani nzuri, lakini ikiwa hamtumikii Mungu wa kweli, je, kwa sasa mtu huyo anaonwa kuwa mwadilifu machoni pa Yehova? (2 Kor. 6:14) Ikiwa utafunga naye ndoa, je, atakusaidia kuendelea kuwa mwaminifu kwa Yehova? Fikiria jambo hili: Huenda wake wapagani wa Mfalme Sulemani walikuwa na sifa fulani nzuri. Lakini hawakumwabudu Yehova, na hatua kwa hatua waliugeuza moyo wa Sulemani, naye akaanza kuabudu miungu ya uwongo.—1 Fal. 11:​1, 4.

18. Wazazi wanapaswa kuwafundisha nini watoto wao?

18 Wazazi, mnaweza kutumia mifano ya wafalme wanaotajwa kwenye Biblia kuwasaidia watoto wenu wawe na bidii kwa ajili ya ibada ya Yehova. Wasaidie watambue kwamba Yehova alimwona mfalme kuwa mzuri au mbaya ikitegemea kwa sehemu kubwa jinsi mfalme huyo alivyounga mkono ibada ya kweli. Wafundishe watoto wako kupitia maneno na mfano wako kwamba mambo ya kiroho—kama vile, kujifunza Biblia, kuhudhuria mikutano, na kushiriki katika huduma ya shambani—ni muhimu zaidi kuliko utendaji mwingine wowote. (Mt. 6:33) Usipofanya hivyo, watoto wako wanaweza kufikia mkataa kwamba kuwa Shahidi wa Yehova ni sawa tu na kufuata “dini ya wazazi.” Matokeo ni kwamba huenda wakaacha kutanguliza ibada ya kweli maishani mwao au kuiacha kabisa.

19. Kuna tumaini gani kwa mtu yeyote ambaye ameacha kumtumikia Yehova? (Tazama pia sanduku “ Unaweza Kumrudia Yehova!”)

19 Je, mtu aliyeacha kumtumikia Yehova hana tumaini lolote? Hapana, kwa sababu anaweza kutubu na kumrudia Yehova. Ili kufanya hivyo, huenda akahitaji kuwa mnyenyekevu na kukubali msaada kutoka kwa wazee wa kutaniko. (Yak. 5:14) Atajitahidi kadiri anavyoweza ili kupata tena kibali cha Yehova!

20. Yehova atatuonaje ikiwa tutawaiga wafalme waaminifu?

20 Basi, tumejifunza nini kutokana na wafalme wa Israeli? Tunaweza kuwa kama wafalme waaminifu ikiwa tutaendelea kujitoa kamili kwa Yehova. Acheni tujifunze kutokana na makosa yetu, tutubu, na kufanya marekebisho yanayohitajika. Na tukumbuke umuhimu wa kushikamana na ibada ya Mungu wa pekee wa kweli. Ikiwa utaendelea kuwa mwaminifu kwa Yehova, atakuona wewe kuwa mtu anayefanya mambo yaliyo sawa machoni pake.

WIMBO 45 Kutafakari kwa Moyo Wangu

a Katika makala hii, maneno “wafalme wa Israeli” yanarejelea wafalme wote ambao waliwatawala watu wa Yehova, iwe walitawala katika ufalme wa Yuda wa makabila mawili, ufalme wa Israeli wa makabila kumi, au makabila yote 12.

b UFAFANUZI WA MANENO: Mara nyingi Biblia inatumia neno “moyo” kumfafanua yule mtu wa ndani, kutia ndani tamaa, mawazo, mwelekeo, mtazamo, uwezo, nia, na malengo ya mtu.

c Inaonekana kwamba wafalme wapagani walikuwa na zoea la kuabudu miungu ya mataifa ambayo waliyashinda.

d Mfalme Asa alitenda dhambi nzito. (2 Nya. 16:​7, 10) Hata hivyo, Biblia inasema Asa alifanya mambo yaliyo sawa machoni pa Yehova. Ingawa mwanzoni alikataa kurekebishwa, inawezekana kwamba baadaye alitubu. Kwa ujumla, sifa zake nzuri zilikuwa nyingi kuliko mambo mabaya aliyofanya. Jambo muhimu ni kwamba Asa alimwabudu tu Yehova na alijitahidi kuondoa ibada ya sanamu katika ufalme wake.—1 Fal. 15:​11-13; 2 Nya. 14:​2-5.

e Tunaona kwamba ibada ni jambo muhimu sana kwa Yehova kwa sababu amri mbili za kwanza katika Sheria ya Musa ziliwakataza watu kuabudu kitu chochote au mtu yeyote isipokuwa Yehova.—Kut. 20:​1-6.

f MAELEZO YA PICHA: Mzee kijana akizungumza na ndugu kuhusu zoea lake la kunywa kileo. Kwa unyenyekevu ndugu huyo anakubali shauri, anafanya mabadiliko yanayohitajika, na anaendelea kumtumikia Yehova kwa uaminifu.