Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 25

WIMBO 7 Yehova, Nguvu Yetu

Kumbuka Kwamba Yehova Ndiye “Mungu Aliye Hai”

Kumbuka Kwamba Yehova Ndiye “Mungu Aliye Hai”

“Yehova yuko hai!”ZAB. 18:46.

JAMBO KUU

Tunanufaika sana tunapokumbuka kwamba Mungu tunayemwabudu ndiye “Mungu aliye hai.”

1. Ni nini kinachowasaidia watu wa Yehova kuendelea kumwabudu Yehova licha ya matatizo wanayokabili?

 BIBLIA inafafanua siku zetu kuwa “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Tim. 3:1) Watu wa Yehova wanakabiliana na changamoto ambazo kila mtu anakabili katika mfumo huu wa mambo, lakini pia wanakabiliana na upinzani na mateso. Ni nini kinachotusaidia kuendelea kumwabudu Yehova licha ya matatizo hayo? Jambo moja kuu ni kwamba tunajua Yehova ndiye “Mungu aliye hai.”—Yer. 10:10; 2 Tim. 1:12.

2. Ni katika njia gani Yehova ni Mungu aliye hai?

2 Yehova ni Mtu halisi anayetutegemeza wakati wa majaribu na anatafuta fursa za kutusaidia. (2 Nya. 16:9; Zab. 23:4) Kumwona Yehova kuwa Mungu aliye hai kunaweza kutusaidia kukabiliana na jaribu lolote tunalopata kwa mafanikio. Fikiria jinsi Mfalme Daudi alivyojionea jambo hilo.

3. Daudi alimaanisha nini aliposema kwamba “Yehova yuko hai”?

3 Daudi alimjua Yehova na alimtegemea. Maadui wake, kutia ndani Mfalme Sauli, walipojaribu kumuua, Daudi alisali kwa Yehova ili kupata msaada. (Zab. 18:6) Baada ya Mungu kujibu sala yake na kumwokoa, Daudi alisema hivi: “Yehova yuko hai!” (Zab. 18:46) Daudi alipotumia maneno hayo, hakuwa akikubali tu kwamba Mungu yuko. Kitabu kimoja cha marejeo kinasema kwamba Daudi alikuwa akionyesha uhakika wake katika Yehova “akiwa mungu aliye hai ambaye sikuzote hutenda kwa niaba ya watu wake.” Naam, Daudi alijua kutokana na mambo aliyojionea maishani kwamba Mungu wake alikuwa hai, na uhakika huo ulichochea upya azimio lake la kumtumikia na kumsifu Yehova.—Zab. 18:​28, 29, 49.

4. Tunanufaikaje kwa kumwona Yehova kuwa Mungu aliye hai?

4 Kuwa na uhakika kwamba Yehova ndiye Mungu aliye hai kunaweza kutusaidia kumtumikia kwa bidii. Tutakuwa na nguvu za kuvumilia majaribu na kichocheo cha kuendelea kufanya kazi kwa bidii katika utumishi wake. Pia, tutaazimia kuendelea kuwa karibu na Yehova.

MUNGU ALIYE HAI ATAKUIMARISHA

5. Ni jambo gani linaloweza kutupatia uhakika tunapokabili majaribu? (Wafilipi 4:13)

5 Tutaweza kuvumilia jaribu lolote, liwe kubwa au dogo, ikiwa tutakumbuka kwamba Yehova yuko hai na kwamba yuko tayari kututegemeza. Isitoshe, hakuna jaribu lolote tunalokabili ambalo linaweza kumshinda Mungu wetu. Yeye ni Mweza-Yote, na anaweza kutupatia nguvu za kuvumilia. (Soma Wafilipi 4:13.) Hivyo, jambo hilo linatupatia uhakika tunapokabili majaribu. Tunapojionea msaada wa Yehova tunapokabili majaribu madogo, hilo linatuhakikishia kwamba atatusaidia pia tutakapokabili majaribu makubwa zaidi.

6. Ni matukio gani ambayo Daudi alikabili alipokuwa kijana yaliyoongeza uhakika wake katika Yehova?

6 Fikiria matukio mawili ambayo yalimsaidia Daudi kuwa na uhakika zaidi katika Yehova. Daudi alipokuwa kijana mdogo akichunga kondoo wa baba yake, dubu na pia simba waliwachukua kondoo. Katika pindi hizo mbili, kwa ujasiri Daudi aliwakimbiza wanyama hao na kuwaokoa kondoo. Hata hivyo, hakudai kwamba ushindi huo ulikuwa wake. Alijua kwamba Yehova ndiye aliyempatia nguvu za kufanya hivyo. (1 Sam. 17:​34-37) Daudi hakusahau kamwe matukio hayo. Kwa kuyatafakari matukio hayo, Daudi alikuwa na uhakika kwamba Mungu aliye hai angemwimarisha wakati ujao.

7. Kuwa na mtazamo unaofaa kulimsaidiaje Daudi kukabiliana na Goliathi?

7 Baadaye, huenda bado akiwa tineja, Daudi alitembelea kambi ya jeshi la Israeli. Aliwaona wanajeshi wakiwa na woga kwa sababu ya Goliathi, jitu kutoka kwa Wafilisti, ambaye alikuwa amekuja ‘kutukana vikosi vya Israeli.’ (1 Sam. 17:​10, 11) Wanajeshi hao walimwogopa kwa sababu walikazia fikira jinsi Goliathi alivyokuwa mkubwa na maneno aliyokuwa akiwaambia. (1 Sam. 17:​24, 25) Hata hivyo, Daudi aliona mambo kwa njia tofauti. Aliona kwamba Goliathi hakuwa tu akitukana vikosi vya Israeli, bali alikuwa akivitukana “vikosi vya Mungu aliye hai.” (1 Sam. 17:26) Daudi alikuwa akimfikiria kwanza Yehova. Aliamini kwamba Mungu ambaye alimsaidia alipokuwa mchungaji, angemsaidia tena katika kisa hiki. Akiwa na uhakika kwamba Mungu angemtegemeza, Daudi alimkabili Goliathi, na bila shaka, alishinda!—1 Sam. 17:​45-51.

8. Tunawezaje kumweka Yehova akilini tunapokabili majaribu? (Tazama pia picha.)

8 Sisi pia tunaweza kukabiliana na majaribu ikiwa tutakumbuka kwamba Mungu aliye hai yuko tayari kutusaidia. (Zab. 118:6) Tunaweza kuimarisha uhakika wetu katika jambo hilo kwa kutafakari mambo aliyofanya wakati uliopita. Soma masimulizi ya Biblia yanayokukumbusha jinsi Yehova alivyowaokoa waabudu wake. (Isa. 37:​17, 33-37) Pia, soma au tazama ripoti zilizo kwenye tovuti yetu ya jw.org zinazoonyesha jinsi Yehova alivyowategemeza ndugu na dada katika siku zetu. Zaidi ya hayo, kumbuka nyakati ambazo Yehova alitenda kwa niaba yako. Huenda ukahisi kwamba Yehova hajakutendea jambo lenye kustaajabisha kama vile kukuokoa kutokana na dubu au simba. Hata hivyo, ukweli ni kwamba Yehova amekuwa akikusaidia maishani mwako! Amekuvuta ili uwe na uhusiano mzuri pamoja naye. (Yoh. 6:44) Hata sasa, ni kwa sababu tu ya msaada wake bado unaendelea kumtumikia. Hivyo, mwombe Yehova akusaidie kukumbuka pindi ambazo alijibu sala zako, alikupatia msaada kwa wakati uliofaa, au alikutegemeza ulipokabili hali ngumu. Kutafakari kuhusu mambo hayo kutaimarisha uhakika wako kwamba Yehova ataendelea kutenda kwa niaba yako.

Majaribu tunayokabili ni sehemu ya lile suala kuu zaidi (Tazama fungu la 8-9)


9. Tunaweza kuwa na mtazamo gani unaofaa kuhusu majaribu yetu? (Methali 27:11)

9 Kumwona Yehova kuwa Mungu aliye hai kutatusaidia kuwa na mtazamo unaofaa kuhusu majaribu yetu. Jinsi gani? Tutaanza kuona majaribu yetu kuwa sehemu ya lile suala kuu zaidi kati ya Yehova na Shetani. Ibilisi anadai kwamba tutakapokabili hali ngumu, tutamwacha Yehova. (Ayu. 1:​10, 11; soma Methali 27:11.) Lakini tunapokabiliana na majaribu yetu kwa mafanikio, tunaonyesha kwamba tunampenda Yehova na tunathibitisha kwamba Ibilisi ni mwongo. Je, unakabili upinzani wa serikali, hali ngumu ya kiuchumi, au watu unaowahubiria hawapendezwi na habari njema, au jaribu lolote lingine? Ikiwa ndivyo, kumbuka kwamba hali yako inakupatia fursa ya kuufanya moyo wa Yehova ushangilie. Pia, kumbuka kwamba Yehova hataruhusu ujaribiwe kupita unavyoweza kuhimili. (1 Kor. 10:13) Atakupatia nguvu za kuvumilia.

MUNGU ALIYE HAI ATAKUTHAWABISHA

10. Mungu aliye hai atawafanyia nini wale wanaomwabudu?

10 Yehova ni Mthawabishaji wa wale wanaomwabudu. (Ebr. 11:6) Kwa sasa anatusaidia kuridhika na kuwa na amani, na atatupatia uzima wa milele wakati ujao. Tunaweza kumtumaini Yehova, tukiwa na uhakika kwamba anatamani na ana uwezo wa kututhawabisha. Na uhakika huo unatusaidia kuwa na mengi ya kufanya katika ibada yetu, kama tu watumishi waaminifu wa Mungu walivyofanya zamani. Hivyo ndivyo alivyofanya Timotheo katika karne ya kwanza.—Ebr. 6:​10-12.

11. Ni nini kilichomchochea Timotheo kufanya kazi kwa bidii kutanikoni? (1 Timotheo 4:10)

11 Soma 1 Timotheo 4:10. Timotheo alimtumaini Mungu aliye hai. Hivyo, alikuwa na sababu nzuri ya kufanya kazi kwa bidii na kujitahidi sana. Alifanya nini? Mtume Paulo alimtia moyo afanye maendeleo katika kufundisha na kusoma mbele ya watu. Pia, Timotheo alipaswa kuwawekea mfano mzuri waabudu wenzake, vijana kwa wazee. Na alipewa migawo fulani migumu, ambayo ilitia ndani kutoa shauri kwa uthabiti lakini kwa upendo kwa wale waliolihitaji. (1 Tim. 4:​11-16; 2 Tim. 4:​1-5) Timotheo angeweza kuwa na uhakika kwamba Yehova angemthawabisha hata ikiwa wakati mwingine kazi yake isingeonwa au kuthaminiwa na watu wengine.—Rom. 2:​6, 7.

12. Ni jambo gani linaloweza kuwachochea wazee waendelee kufanya kazi yao kwa bidii? (Tazama pia picha.)

12 Leo pia, wazee wanaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova anaona na anathamini kazi yao nzuri. Zaidi ya kazi ya uchungaji, kufundisha, na kuhubiri, wazee wengi wanasaidia katika miradi ya ujenzi na katika kazi ya kutoa msaada wakati wa majanga. Wengine wanatumikia katika Vikundi vya Kutembelea Wagonjwa au Halmashauri za Uhusiano na Hospitali. Wazee ambao wanajitoa kwa ajili ya kazi hizo wanaliona kutaniko kuwa mpango wa Yehova, na si shirika linaloongozwa na wanadamu. Matokeo ni kwamba wanajitoa kwa nafsi yote katika migawo yao na wana uhakika kabisa kwamba Mungu atawathawabisha kwa yale wanayofanya.—Kol. 3:​23, 24.

Mungu aliye hai atakuthawabisha unapofanya kazi kwa bidii kwa ajili ya kutaniko (Tazama fungu la 12-13)


13. Yehova anahisije kuhusu jitihada zetu za kibinafsi katika utumishi wake?

13 Ni kweli kwamba si wote wanaweza kuwa wazee wa kutaniko, lakini sisi sote tuna jambo ambalo tunaweza kumtolea Yehova. Na Mungu wetu anathamini tunapofanya yote tuwezayo ili kumtumikia. Anaona tunapotoa michango kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote, hata ikiwa hatuwezi kutoa mchango mkubwa. Anafurahi tunapojitahidi kushinda hisia zetu za haya na kunyoosha mikono ili kutoa maelezo kwenye mikutano, na anafurahi tunapoachilia kosa na kusamehe. Hata unapohisi kwamba huwezi kufanya mengi kama ambavyo ungependa, uwe na uhakika kwamba Yehova anathamini kile unachoweza kufanya. Na kwa sababu hiyo anakupenda, na atakuthawabisha.—Luka 21:​1-4.

ENDELEA KUMKARIBIA MUNGU ALIYE HAI

14. Kuendelea kumkaribia Yehova kunatusaidiaje kuendelea kuwa waaminifu? (Tazama pia picha.)

14 Ikiwa Yehova ni halisi kwetu, itakuwa rahisi zaidi kuendelea kuwa waaminifu kwake. Ilikuwa hivyo kwa Yosefu. Alikataa kwa uthabiti kufanya uasherati. Mungu alikuwa halisi kwake, na hakutaka kumchukiza. (Mwa. 39:9) Ili Yehova awe halisi kwetu, tunahitaji kutenga wakati wa kusali na kujifunza Neno lake. Tukifanya hivyo urafiki wetu kwake utakua. Kama Yosefu, tunapokuwa na uhusiano wa karibu na Yehova, hatutafanya jambo lolote ambalo litamkasirisha.—Yak. 4:8.

Kumkaribia Mungu aliye hai kutakusaidia kuendelea kuwa mwaminifu (Tazama fungu la 14-15)


15. Tunajifunza somo gani kutokana na kile kilichowapata Waisraeli wakiwa nyikani? (Waebrania 3:12)

15 Wale ambao wanasahau kwamba Yehova ni Mungu aliye hai wanaweza kupeperushwa kwa urahisi kutoka kwake. Fikiria kilichowapata Waisraeli walipokuwa nyikani. Walijua kwamba Yehova yuko, lakini walianza kutilia shaka ikiwa angewaandalia mahitaji yao. Hata waliuliza: “Je, Yehova yuko katikati yetu au la?” (Kut. 17:​2, 7) Mwishowe, walimwasi Mungu. Kwa kweli, hatutaki kufuata mfano wao wa kutotii, ambao ni onyo kwetu.—Soma Waebrania 3:12.

16. Ni jambo gani linaloweza kujaribu imani yetu?

16 Ulimwengu huu unafanya iwe vigumu kwetu kuendelea kuwa karibu na Yehova. Wengi hupinga wazo la kwamba Mungu yupo. Mara nyingi, wale wanaopuuza matakwa ya Mungu wanaonekana kuwa na maisha mazuri. Tunapoona jambo hilo, imani yetu inaweza kujaribiwa. Ingawa tunaamini kwamba Mungu yupo, huenda tukatilia shaka ikiwa atatenda kwa niaba yetu. Mwandikaji wa Zaburi ya 73 alijiuliza jambo hilo. Aliwaona watu waliomzunguka wakipuuza sheria za Mungu na bado walionekana wakifurahia maisha. Matokeo ni kwamba, alianza kutilia shaka ikiwa kuna manufaa yoyote ya kumtumikia Mungu.—Zab. 73:​11-13.

17. Ni nini kitakachotusaidia kuendelea kumkaribia Yehova?

17 Hatimaye, ni nini kilichomsaidia mtunga zaburi kurekebisha mtazamo wake? Alitafakari kuhusu kile ambacho kingewapata wale wanaomsahau Yehova. (Zab. 73:​18, 19, 27) Pia, alichunguza manufaa yanayotokana na kumtumikia Mungu. (Zab. 73:24) Sisi pia tunaweza kutafakari kuhusu baraka ambazo Yehova ametupatia. Wazia jinsi ambavyo maisha yetu yangekuwa ikiwa hatungemtumikia Yehova. Kufanya hivyo kutatusaidia kuendelea kuwa waaminifu na kukubaliana na maneno ya mtunga zaburi aliyesema hivi: “Kwa upande wangu, kumkaribia Mungu ni jambo jema kwangu.”—Zab. 73:28.

18. Kwa nini hatuhitaji kuogopa mambo yatakayotukia wakati ujao?

18 Tunaweza kukabiliana na changamoto zozote tunazopata katika siku hizi za mwisho kwa sababu ‘tunamtumikia Mungu wa kweli aliye hai.’ (1 The. 1:9) Mungu wetu ni Mtu halisi ambaye anatenda kwa niaba ya wale wanaomwabudu yeye. Alishikamana pamoja na watumishi wake wa zamani, naye yuko pamoja nasi leo. Hivi karibuni, kutakuwa na dhiki kuu zaidi ambayo haijawahi kutukia duniani. Lakini hatutaikabili tukiwa peke yetu. (Isa. 41:10) Acheni sisi sote “tuwe hodari na kusema: ‘Yehova ni msaidizi wangu; sitaogopa.’”—Ebr. 13:​5, 6.

WIMBO 3 Tumaini, Nguvu, na Uhakika Wetu