Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 10

WIMBO 13 Kristo, Kielelezo Chetu

‘Endelea Kumfuata’ Yesu Baada ya Ubatizo

‘Endelea Kumfuata’ Yesu Baada ya Ubatizo

“Mtu yeyote akitaka kunifuata, lazima ajikane mwenyewe, aubebe mti wake wa mateso siku baada ya siku na aendelee kunifuata.”LUKA 9:23.

JAMBO KUU

Makala hii inaweza kutusaidia sisi sote kutafakari maana ya wakfu wetu. Inaweza kuwasaidia kihususa wale ambao wamebatizwa hivi karibuni waendelee kuwa waaminifu.

1-2. Mtu anapata baraka gani baada ya kubatizwa?

 TUNAFURAHI sana tunapobatizwa na kuwa sehemu ya familia ya Yehova. Wale walio na pendeleo hilo wanaweza kukubaliana na maneno ya mtunga zaburi Daudi aliyesema hivi: ‘Mwenye furaha ni yule ambaye Yehova amemchagua na kumleta karibu ili akae katika nyua zake.’—Zab. 65:4.

2 Yehova hamleti mtu yeyote tu kwenye nyua zake. Kama tulivyozungumzia katika makala iliyotangulia, anachagua kuwa karibu na wale ambao wamethibitisha kwamba wanataka kuwa na uhusiano wa karibu pamoja naye. (Yak. 4:8) Unapojiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa, unakuwa karibu na Yehova kwa njia ya pekee. Unaweza kuwa na uhakika kwamba baada ya kubatizwa, ‘atakumwagia baraka hivi kwamba hutakosa chochote.’—Mal. 3:10; Yer. 17:​7, 8.

3. Wakristo waliojiweka wakfu na kubatizwa wana wajibu gani mzito? (Mhubiri 5:​4, 5)

3 Bila shaka, ubatizo ndio mwanzo tu wa maisha yako ya kumtumikia Yehova. Baada ya kuchukua hatua hiyo, utatamani kujitahidi kuishi kulingana na ahadi uliyotoa ulipojiweka wakfu, hata utakapokabili vishawishi au majaribu ya imani. (Soma Mhubiri 5:​4, 5.) Ukiwa mwanafunzi wa Yesu, utafuata kadiri uwezavyo mfano na maagizo ya Yesu kwa ukaribu zaidi. (Mt. 28:​19, 20; 1 Pet. 2:21) Makala hii itakusaidia kufanya hivyo.

‘ENDELEA KUMFUATA’ YESU LICHA YA MAJARIBU NA VISHAWISHI

4. Ni katika maana gani wanafunzi wa Yesu wanabeba “mti wa mateso”? (Luka 9:23)

4 Baada ya kubatizwa, haimaanishi kwamba maisha yako yatakuwa bila matatizo. Kwa kweli, Yesu alieleza wazi kwamba wanafunzi wake wangebeba “mti wa mateso.” Isitoshe, wangefanya hivyo “siku baada ya siku.” (Soma Luka 9:23.) Je, Yesu alisema kwamba wafuasi wake wangeteseka sikuzote? Hapana. Badala yake, alikuwa tu akikazia kwamba pamoja na baraka ambazo wafuasi wake wangefurahia, wangekabili pia changamoto. Huenda baadhi ya changamoto hizo zitakuwa ngumu sana.—2 Tim. 3:12.

5. Yesu aliahidi baraka gani kwa wale wanaojidhabihu?

5 Huenda tayari umekabili upinzani kutoka kwa watu wa familia, au labda umeacha kufuatilia mambo fulani ya kimwili ili utangulize masilahi ya Ufalme. (Mt. 6:33) Ikiwa ndivyo, uwe na uhakika kwamba Yehova anatambua mambo yote unayofanya kwa ajili yake. (Ebr. 6:10) Inawezekana umejionea ukweli wa maneno haya ya Yesu: “Hakuna mtu aliyeacha nyumba au ndugu au dada au mama au baba au watoto au mashamba kwa ajili yangu na kwa ajili ya habari njema ambaye hatapata mara 100 sasa katika kipindi hiki—nyumba, ndugu, dada, mama, watoto, mashamba, pamoja na mateso—na katika mfumo wa mambo unaokuja, uzima wa milele.” (Marko 10:​29, 30) Kwa kweli, baraka ambazo umepata ni nyingi zaidi ukilinganisha na jambo lolote ulilojidhabihu.—Zab. 37:4.

6. Kwa nini unahitaji kuendelea kupambana na “tamaa ya mwili” baada ya ubatizo?

6 Baada ya kubatizwa, bado utahitaji kupambana na “tamaa ya mwili.” (1 Yoh. 2:16) Hiyo ni kwa sababu wewe bado si mkamilifu. Huenda wakati mwingine ukahisi kama alivyohisi mtume Paulo. Aliandika hivi: “Kwa kweli naipenda sheria ya Mungu kulingana na mtu niliye kwa ndani, lakini ninaona ndani ya mwili wangu sheria nyingine ikipigana na sheria ya akili yangu na kunichukua mateka kwa sheria ya dhambi iliyo ndani ya mwili wangu.” (Rom. 7:​22, 23) Huenda ukahisi umevunjika moyo kwa sababu ya mwelekeo wako wa kutenda dhambi. Hata hivyo, kufikiria kuhusu ahadi uliyomwahidi Yehova ulipojiweka wakfu kwake kutaimarisha azimio lako la kupambana dhidi ya kishawishi. Ukweli ni kwamba ahadi uliyotoa ulipojiweka wakfu, itakusaidia utakapokabili vishawishi. Jinsi gani?

7. Kujiweka wakfu kwa Yehova kutakusaidiaje kuendelea kuwa mwaminifu kwake?

7 Unapojiweka wakfu kwa Yehova, unajikana mwenyewe. Hilo linamaanisha kukataa tamaa na malengo ya kibinafsi ambayo hayampendezi Yehova. (Mt. 16:24) Hivyo, unapokabili jaribu huhitaji kutumia muda mwingi kufikiria cha kufanya. Tayari utakuwa umeamua cha kufanya—kuwa mwaminifu kwa Yehova. Utashikamana na azimio lako la kumpendeza Yehova. Kwa njia hiyo, utakuwa kama Ayubu. Hata ingawa alikabili majaribu makali sana, alisema hivi kwa uhakika: “Sitaukana utimilifu wangu!”—Ayu. 27:5.

8. Kutafakari sala uliyotoa ulipojiweka wakfu kutakusaidiaje kupinga kishawishi?

8 Ukitafakari sala uliyotoa ulipojiweka wakfu kwa Yehova, utapata nguvu za kushinda kishawishi chochote. Kwa mfano, je, utamchezea kimapenzi mwenzi wa ndoa wa mtu mwingine? Bila shaka hapana! Tayari ulishamwahidi Yehova kwamba hutafanya jambo kama hilo. Ikiwa hutaruhusu tamaa mbaya zisitawi, hutahitaji kupambana baadaye ili kuzing’oa. ‘Utajiepusha’ na “kijia cha waovu.”—Met. 4:​14, 15.

9. Kutafakari sala uliyotoa ulipojiweka wakfu kutakusaidiaje kuendelea kutanguliza utendaji wako wa kiroho?

9 Namna gani ukipata kazi ambayo itakuzuia kuhudhuria mikutano kwa ukawaida? Utajua jambo la kufanya. Kabla ya kupata kazi hiyo, tayari ulishaamua kwamba hutakubali kazi ambayo itakuzuia kuhudhuria mikutano. Hivyo, hutashawishiwa kukubali kazi kama hiyo, kisha ujitahidi kutafuta njia za kufanya uamuzi huo mbaya uonekane kuwa mzuri. Ukikumbuka azimio la Yesu la kumpendeza Baba yake, utakataa haraka na kwa uthabiti jambo lolote ambalo unajua halitampendeza Mungu ambaye umejiweka wakfu kwake.—Mt. 4:10; Yoh. 8:29.

10. Yehova atakusaidiaje ‘uendelee kumfuata’ Yesu baada ya kubatizwa?

10 Ukweli ni kwamba majaribu na vishawishi vinakupa nafasi ya kuonyesha kwamba umeazimia ‘kuendelea kumfuata’ Yesu. Unapofanya hivyo, unaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atakusaidia. Biblia inasema hivi: “Mungu ni mwaminifu, naye hatawaacha mjaribiwe kupita mnavyoweza kuhimili, bali pamoja na majaribu hayo ataifanya pia njia ya kutokea ili mweze kuyavumilia.”—1 Kor. 10:13.

JINSI YA KUENDELEA KUMFUATA YESU

11. Mojawapo ya njia bora za kuendelea kumfuata Yesu ni ipi? (Tazama pia picha.)

11 Yesu alikuwa na bidii na aliendelea kumkaribia Yehova katika sala. (Luka 6:12) Kwa kweli, mojawapo ya njia bora za kuendelea kumfuata Yesu baada ya ubatizo wako ni kusitawisha mazoea ya kufanya mambo yatakayokusaidia umkaribie zaidi Yehova. Biblia inasema hivi: “Kwa kadiri ambavyo tumefanya maendeleo, na tuendelee kutembea kwa utaratibu katika mwendo huohuo.” (Flp. 3:16) Mara kwa mara, utasikia kuhusu mambo yaliyoonwa ya ndugu na dada ambao wamepanua utumishi wao mtakatifu. Labda walihudhuria Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme au walihamia maeneo yenye uhitaji mkubwa. Ikiwa hali zako zinakuruhusu, hilo ni lengo zuri sana la kujiwekea. Watu wa Yehova wanatafuta fursa mbalimbali za kupanua huduma yao. (Mdo. 16:9) Namna gani ikiwa hali zako za sasa hazikuruhusu kufanya hivyo? Usihisi kwamba wewe ni duni kuliko wale wanaofanya hivyo. (Mt. 10:22) Usisahau kwamba unamfurahisha sana Yehova unapofanya utumishi wake kwa bidii kulingana na uwezo na hali zako. Hiyo ni njia muhimu ya kuendelea kumfuata Yesu baada ya ubatizo.—Zab. 26:1.

Baada ya ubatizo, weka lengo la kufanya mambo yatakayokusaidia uwe karibu zaidi na Yehova (Tazama fungu la 11)


12-13. Unaweza kufanya nini ikiwa bidii yako inaanza kupungua? (1 Wakorintho 9:​16, 17) (Tazama pia sanduku “ Usitoke Katika Shindano.”)

12 Utafanya nini ikiwa unahisi sala zako hazitoki moyoni, au hufurahii utumishi kama ilivyokuwa zamani? Namna gani ikiwa hufurahii usomaji wako wa Biblia kama ilivyokuwa zamani? Ikiwa hali hiyo inakupata baada ya ubatizo, usifikie mkataa kwamba umepoteza roho ya Yehova. Kwa kuwa wewe si mkamilifu, hisia zako zinaweza kubadilika mara kwa mara. Ikiwa bidii yako inaanza kupungua, tafakari mfano wa mtume Paulo. Ingawa alijitahidi kumwiga Yesu, alijua kwamba nyakati nyingine huenda hangekuwa na tamaa kubwa ya kufanya kile alichohitaji kufanya. (Soma 1 Wakorintho 9:​16, 17.) Alisema hivi: “Hata nikifanya hivyo bila kupenda, bado nimekabidhiwa usimamizi.” Kwa maneno mengine, Paulo aliazimia kutimiza huduma yake licha ya jinsi ambavyo huenda angehisi wakati huo.

13 Vivyo hivyo, usifanye maamuzi kwa kutegemea tu jinsi unavyohisi. Azimia kufanya lililo sawa licha ya jinsi unavyohisi. Ikiwa utaendelea kufanya yaliyo sawa, baada ya muda huenda hisia zako zikabadilika. Vyovyote vile, kudumisha ratiba nzuri ya kiroho kutakusaidia uendelee kumfuata Yesu baada ya ubatizo. Pia, uvumilivu wako katika utumishi wa Yehova utawatia moyo waabudu wenzako.—1 The. 5:11.

“ENDELEENI KUJIJARIBU . . . ENDELEENI KUTHIBITISHA”

14. Unapaswa kuchunguza nini kwa ukawaida, na kwa nini? (2 Wakorintho 13:5)

14 Pia, baada ya kubatizwa ni jambo muhimu sana kujichunguza kwa ukawaida. (Soma 2 Wakorintho 13:5.) Chunguza mara kwa mara maisha na mazoea yako ili uone ikiwa unasali kwa ukawaida, unasoma na kujifunza Biblia, unahudhuria mikutano, na kushiriki katika huduma. Jaribu kutafuta njia za kufurahia na kunufaika zaidi na utendaji huo wa kiroho. Kwa mfano, jiulize maswali kama vile: ‘Je, ninaweza kuwafafanulia wengine mafundisho ya msingi ya Biblia? Je, kuna mambo yoyote ninayoweza kufanya ili huduma yangu iwe yenye kufurahisha zaidi? Ni kwa kadiri gani ninataja mambo hususa katika sala zangu na je, sala zangu zinaonyesha kwamba ninamtegemea kikamili Yehova? Je, ninahudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida? Ninawezaje kuboresha jinsi ninavyoshiriki na kukaza fikira ninapokuwa kwenye mikutano?’

15-16. Umejifunza nini kutokana na kisa cha ndugu mmoja kuhusu kupinga kishawishi?

15 Ni jambo muhimu pia kuchunguza udhaifu wako kwa unyoofu. Ndugu anayeitwa Robert, anaeleza jambo alilojionea linalotusaidia kuelewa jambo hilo, anasema hivi: “Nilipokuwa na umri wa miaka 20 hivi, nilipata kazi ya muda. Siku moja baada ya kazi, mfanyakazi mwenzangu wa kike alinialika nyumbani kwake. Mwanamke huyo aliniambia kwamba tungekuwa peke yetu na ‘tungefurahia kuwa pamoja.’ Mwanzoni, nilitoa udhuru usio na msingi thabiti, lakini hatimaye nilimwambia hapana na nilimfafanulia sababu.” Robert alipinga kishawishi hicho, na tunampongeza kwa jambo hilo. Hata hivyo, baadaye alitafakari kuhusu tukio hilo na alitambua kwamba angeweza kulishughulikia kwa njia nzuri zaidi. Anakiri hivi: “Sikukataa ombi lake kwa uthabiti au kwa uharaka kama Yosefu alivyofanya alipokataa ombi la mke wa Potifa. (Mwa. 39:​7-9) Kwa kweli, nilishangaa jinsi ilivyokuwa vigumu kwangu kukataa ombi lake. Tukio hilo lilinisaidia kutambua kwamba nilihitaji kuimarisha urafiki wangu na Yehova.”

16 Unaweza kunufaika ukijichunguza kama alivyofanya Robert. Hata kama ulifanikiwa kupinga kishawishi, jiulize hivi, ‘Ilinichukua muda gani kukataa kishawishi hicho?’ Ikiwa unatambua kwamba unahitaji kufanya marekebisho fulani, usivunjike moyo. Shukuru kwamba sasa umetambua udhaifu huo. Sali kuhusu jambo hilo, na uchukue hatua ili kuimairisha azimio lako la kuishi kulingana na viwango vya maadili vya Yehova.—Zab. 139:​23, 24.

17. Jina la Yehova lilihusikaje katika kisa cha Robert?

17 Kuna jambo lingine tunalojifunza kutokana na jambo lililompata Robert. Anaendelea kusema hivi: “Baada ya kukataa mwaliko wake, mwanamke huyo aliniambia hivi, ‘Umefaulu mtihani!’ Nilimuuliza alimaanisha nini. Mwanamke huyo aliniambia kwamba rafiki yake, ambaye zamani alikuwa Shahidi, alimwambia kwamba ikiwa watapata nafasi, Mashahidi wote vijana wanaweza kufanya dhambi kisiri. Hivyo, mwanamke huyo alimwambia rafiki yake kwamba angenijaribu ili kuthibitisha kama jambo hilo ni kweli. Pindi hiyo nilifurahi sana kwamba sikuliletea suto jina la Yehova.”

18. Umeazimia kufanya nini baada ya kubatizwa? (Tazama pia sanduku “ Mfululizo Utakaoufurahia.”)

18 Unapojiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa, unaonyesha kwamba unataka kulitakasa jina lake hata hali ziweje. Na unaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova anajua majaribu unayokabili na vishawishi unavyopinga. Atabariki jitihada zako za kuendelea kuwa mwaminifu. Amini kwamba anaweza kukupatia nguvu za kufanya hivyo kupitia roho yake takatifu. (Luka 11:​11-13) Kwa msaada wa Yehova, utaweza kuendelea kumfuata Yesu baada ya kubatizwa.

UNGEJIBUJE?

  • Ni katika maana gani Wakristo wanabeba ‘mti wa mateso siku baada ya siku’?

  • Unaweza kufanya nini ili ‘uendelee kumfuata’ Yesu baada ya kubatizwa?

  • Kutafakari sala uliyotoa ulipojiweka wakfu kutakusaidiaje kuendelea kuwa mwaminifu?

WIMBO 89 Sikiliza, Tii, Upate Baraka