Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 12

WIMBO 77 Nuru Katika Ulimwengu Wenye Giza

Epuka Giza​—⁠Baki Katika Nuru

Epuka Giza​—⁠Baki Katika Nuru

“Wakati fulani mlikuwa giza, lakini sasa ninyi ni nuru.”EFE. 5:8.

JAMBO KUU

Tunaweza kujifunza nini kutokana na maneno giza na nuru yanayotajwa katika Waefeso sura ya 5?

1-2. (a) Paulo alikuwa katika hali gani alipowaandikia barua Wakristo walioishi jijini Efeso? (b) Tutachunguza maswali gani?

 ALIPOKUWA kwenye kifungo cha nyumbani jijini Roma, mtume Paulo alitaka kuwatia moyo waabudu wenzake. Hangeweza kukutana nao uso kwa uso, hivyo aliwaandikia barua. Mojawapo ya barua hizo aliwaandikia Wakristo walioishi jijini Efeso, karibu mwaka wa 60 au 61 W.K.—Efe. 1:1; 4:1.

2 Karibu miaka kumi mapema, Paulo alikuwa jijini Efeso akihubiri na kufundisha habari njema. (Mdo. 19:​1, 8-10; 20:​20, 21) Aliwapenda sana ndugu zake na alitaka kuwasaidia waendelee kuwa waaminifu kwa Yehova. Lakini kwa nini aliwaandikia Wakristo watiwa-mafuta kuhusu giza na nuru? Na ni masomo gani ambayo Wakristo wote wanaweza kujifunza kutokana na ushauri huo? Acheni tuchunguze majibu ya maswali hayo.

KUTOKA KWENYE GIZA HADI KWENYE NURU

3. Paulo alitumia maneno gani katika barua yake kwa Waefeso?

3 Paulo aliwaandikia Wakristo huko Efeso hivi: “Wakati fulani mlikuwa giza, lakini sasa ninyi ni nuru.” (Efe. 5:8) Paulo hapa alitumia maneno giza na nuru ili kufafanua hali mbili zinazotofautiana. Acheni tuchunguze kwa nini Paulo angeweza kusema kwamba ‘wakati fulani Waefeso walikuwa giza.’

4. Ni katika maana gani Waefeso walikuwa gizani kwa sababu ya dini ya uwongo?

4 Gizani kwa sababu ya dini ya uwongo. Kabla ya kujifunza kweli na kuwa Wakristo, Waefeso ambao Paulo aliwaandikia barua walikuwa watumwa wa mafundisho ya dini za uwongo na ushirikina. Jiji la Efeso lilikuwa na hekalu maarufu la Artemi, ambalo watu wa kale waliliona kuwa mojawapo ya maajabu saba ya ulimwengu. Watu walienda katika hekalu hilo ili kuabudu sanamu. Kutengeneza na kuuza vihekalu vya dini ya uwongo vya mungu wa kike Artemi, ilikuwa biashara yenye faida kubwa. (Mdo. 19:​23-27) Zaidi ya hayo, jiji hilo lilijulikana kwa kufanya uchawi.—Mdo. 19:19.

5. Ni katika maana gani Waefeso walikuwa gizani kwa sababu ya maadili mapotovu?

5 Gizani kwa sababu ya maadili mapotovu. Waefeso walijulikana kwa kuwa na maadili na mwenendo mpotovu. Ilikuwa kawaida kusikia maneno machafu katika kumbi za michezo za jiji na hata kwenye sherehe za dini. (Efe. 5:3) Wakaaji wengi wa jiji hilo walikuwa “wamepotoka kabisa kimaadili,” msemo ambao kihalisi unamaanisha “hawahisi tena maumivu.” (Efe. 4:​17-19) Kabla ya kujua kwa usahihi mambo yaliyo sawa na yasiyo sawa, dhamiri za Waefeso hazikuwasumbua kabisa au hawakufikiri kwamba wanawajibika mbele za Yehova. Kwa sababu hizo Paulo angeweza kusema kwamba ‘walikuwa gizani kiakili na wametenganishwa na uzima ambao ni wa Mungu.’

6. Kwa nini Paulo angeweza kuwaambia Waefeso kwamba ‘sasa wao ni nuru’?

6 Hata hivyo, baadhi ya Waefeso hawakuendelea kubaki gizani. Paulo aliandika kwamba ‘sasa wao ni nuru kuhusiana na Bwana.’ (Efe. 5:8) Walikuwa wamekubali nuru ya kweli ya Kimaandiko. (Zab. 119:105) Waefeso hao waliacha mazoea ya dini zao za uwongo na mwenendo mpotovu. Walikuwa wamekuwa “waigaji wa Mungu” na walifanya yote wawezayo ili kumwabudu na kumfurahisha.—Efe. 5:1.

7. Ni katika njia gani hali yetu inafanana na Wakristo wengi walioishi jijini Efeso?

7 Kwa njia hiyohiyo, kabla hatujajifunza kweli tulikuwa katika giza kwa sababu ya dini za uwongo na maadili mapotovu. Baadhi yetu tulisherehekea sikukuu za dini za uwongo; na wengine tuliishi maisha mapotovu kiadili. Lakini baada tu ya kujifunza viwango vya Yehova vya mema na mabaya, tulifanya mabadiliko. Tulianza kuishi kupatana na viwango vyake vya uadilifu. Matokeo ni kwamba tumenufaika sana. (Isa. 48:17) Hata hivyo, kwa sasa tunaendelea kukabili changamoto. Tunahitaji kukaa mbali na giza tuliloliacha na kuendelea “kutembea kama watoto wa nuru.” Tunawezaje kufanya hivyo?

Image digitally reproduced with the permission of the Papyrology Collection, Graduate Library, University of Michigan, P.Mich.inv. 6238. Licensed under CC by 3.0

Mambo ambayo Paulo aliwaandikia Waefeso ni ushauri wenye upendo ambao tunaweza kutumia leo (Tazama fungu la 7) b


EPUKA GIZA

8. Kulingana na Waefeso 5:​3-5, Waefeso walihitaji kuepuka nini?

8 Soma Waefeso 5:​3-5. Ili wawe mbali na giza linalotokana na maadili mapotovu, Wakristo huko Efeso walihitaji kuendelea kukataa mazoea yasiyomfurahisha Yehova. Jambo hilo lilitia ndani kuepuka mwenendo mpotovu wa kingono, na pia maneno machafu. Paulo aliwakumbusha Waefeso kwamba walihitaji kuepuka mazoea hayo ikiwa walitaka kuwa na “urithi wowote katika Ufalme wa Kristo na wa Mungu.”

9. Kwa nini tunapaswa kukataa kufanya jambo lolote litakalotuongoza kwenye maadili mapotovu?

9 Sisi pia ni lazima tuendelee kupambana ili tusinaswe “katika matendo yasiyozaa matunda, ambayo ni ya giza.” (Efe. 5:11) Ukweli ni kwamba visa mbalimbali vinaonyesha kuwa kadiri mtu anavyotazama, kusikiliza, au kuzungumza kuhusu mambo machafu na mapotovu kiadili, ndivyo inavyokuwa rahisi zaidi kwake kufanya dhambi. (Mwa. 3:6; Yak. 1:​14, 15) Katika nchi moja, ndugu wengi walikuwa “marafiki” kwenye mtandao fulani wa kijamii. Mwanzoni, wengi wao waliandika jumbe kuhusu mambo ya kiroho. Hata hivyo, baada ya muda walianza kuzungumzia mambo yasiyomfurahisha Yehova. Mazungumzo yao yalihusu hasa ngono. Baadaye, wengi kati ya ndugu hao walikiri kwamba mazungumzo hayo machafu yaliwaongoza wafanye uasherati.

10. Shetani anajaribu kutudanganya jinsi gani? (Waefeso 5:6)

10 Ulimwengu wa Shetani unajaribu kutudanganya na kutufanya tuamini kwamba mambo ambayo Yehova anayaona kuwa machafu na mapotovu si mabaya. (2 Pet. 2:19) Jambo hilo halitushangazi! Mbinu moja ambayo Ibilisi ameitumia kwa muda mrefu ni kuwachanganya watu ili wasitambue mambo yaliyo sawa na yasiyo sawa. (Isa. 5:20; 2 Kor. 4:4) Haishangazi kwamba sinema nyingi, vipindi vya televisheni, na tovuti zinaendeleza mawazo yaliyo kinyume na viwango vya uadilifu vya Yehova! Shetani anajaribu kutudanganya tufikiri kwamba matendo na mwenendo mchafu, unakubalika, na pia unafurahisha na hauna madhara.—Soma Waefeso 5:6.

11. Kisa cha Angela kinaonyeshaje umuhimu wa kutumia ushauri wenye hekima unaopatikana katika Waefeso 5:7? (Tazama pia picha.)

11 Shetani anataka tushirikiane na watu ambao watafanya iwe vigumu kwetu kushikamana na viwango vya Yehova. Ndiyo sababu Paulo aliwahimiza Waefeso hivi: “Msishirikiane nao,” yaani, watu wanaofanya mambo mabaya machoni pa Yehova. (Efe. 5:7) Tunahitaji kukumbuka kwamba watu tunaoshirikiana nao, si wale tu tunaokutana nao uso kwa uso. Wanatia ndani wale ambao tunawasiliana nao kwenye mitandao ya kijamii, hatari ambayo Waefeso wa kale hawakuwa nayo. Angela a, anayeishi barani Asia, alitambua jinsi mitandao ya kijamii ilivyo hatari. Anakiri hivi: “Unaweza kuwa mtego ambao unabadili njia yako ya kufikiri bila hata wewe mwenyewe kutambua. Nilifikia hatua kwamba haikunisumbua kuwa na ‘marafiki’ ambao hawakuheshimu kanuni za Biblia. Mwishowe, nilianza kufikiri kwamba ilikuwa sawa kufuatia mtindo wa maisha ambao haukumfurahisha Yehova.” Inafurahisha kwamba wazee wenye upendo walimsaidia Angela kufanya mabadiliko aliyohitaji. Anasema hivi: “Sasa ninajaza akili yangu mambo ya kiroho badala ya mambo yaliyo kwenye mitandao ya kijamii.”

Uwezo wetu wa kushikamana na viwango vya Yehova unategemea sana marafiki tunaochagua (Tazama fungu la 11)


12. Ni nini kitakachotusaidia kushikamana na viwango vya Yehova vya mema na mabaya?

12 Tunapaswa kupinga mawazo ya ulimwengu kwamba mwenendo mpotovu kiadili unakubalika. Tunajua kwamba mawazo hayo si sahihi. (Efe. 4:​19, 20) Itafaa tujiulize hivi: ‘Je, ninakuwa mwangalifu na kuepuka kushirikiana isivyo lazima na wafanyakazi wenzangu, wanafunzi wenzangu, au watu wengine ambao hawaheshimu viwango vya uadilifu vya Yehova? Je, ninashikamana na viwango vya Yehova kwa ujasiri hata ikiwa baadhi ya watu wanasema nina ubaguzi kwa sababu ya kufanya hivyo?’ Kama inavyoonyeshwa kwenye 2 Timotheo 2:​20-22, tunahitaji pia kuwa waangalifu tunapochagua watu tunaoshirikiana nao ndani ya kutaniko la Kikristo. Tunahitaji kukumbuka kwamba baadhi ya watu hawawezi kutusaidia tuendelee kuwa waaminifu katika utumishi wetu kwa Yehova.

TEMBEENI “KAMA WATOTO WA NURU”

13. Inamaanisha nini ‘kuendelea kutembea kama watoto wa nuru’? (Waefeso 5:​7-9)

13 Paulo aliwatia moyo Wakristo huko Efeso, waendelee kukataa giza, na pia ‘waendelee kutembea kama watoto wa nuru.’ (Soma Waefeso 5:​7-9.) Hilo linamaanisha nini? Kwa ufupi, inamaanisha kujiendesha kama Wakristo wa kweli nyakati zote. Njia moja itakayotusaidia kufikia lengo hilo ni kwa kusoma na kujifunza Biblia kwa bidii pamoja na machapisho yanayotegemea Biblia. Ni muhimu hasa kukazia uangalifu mfano na mafundisho ya Yesu Kristo ambaye ndiye “nuru ya ulimwengu.”—Yoh. 8:12; Met. 6:23.

14. Roho takatifu inawezaje kutusaidia?

14 Pia, tunahitaji msaada wa roho takatifu ya Mungu ili tuweze kuendelea kujiendesha “kama watoto wa nuru.” Kwa nini? Kwa sababu si rahisi kuendelea kuwa safi katika ulimwengu huu uliopotoka kimaadili. (1 The. 4:​3-5, 7, 8) Roho takatifu inaweza kutusaidia kupambana na mawazo ya ulimwengu, kutia ndani falsafa zake na maoni yake yanayopingana na mawazo ya Mungu. Roho takatifu pia inaweza kutusaidia kutokeza “kila namna ya wema na uadilifu.”—Efe. 5:9.

15. Tunaweza kupokea roho takatifu kwa njia gani? (Waefeso 5:​19, 20)

15 Njia moja tunayoweza kupata roho takatifu ni kwa kumwomba Yehova. Yesu alisema kwamba Yehova ‘atawapa roho takatifu wale wanaomwomba.’ (Luka 11:13) Na tunapomsifu Yehova pamoja kwenye mikutano ya Kikristo, tunapokea pia roho takatifu. (Soma Waefeso 5:​19, 20.) Na roho takatifu ya Mungu itatuchochea tuishi kwa njia inayompendeza Mungu.

16. Ni nini kitakachotusaidia tufanye maamuzi ya hekima? (Waefeso 5:​10, 17)

16 Tunapotaka kufanya maamuzi muhimu, tunahitaji “kuyafahamu mapenzi ya Yehova” na kisha tutende kupatana nayo. (Soma Waefeso 5:​10, 17.) Tunapotafuta kanuni za Biblia zinazohusu hali yetu, kwa kweli tutakuwa tukitafuta mawazo ya Mungu kuhusu jambo hilo. Kisha, kadiri tunavyotumia kanuni za Mungu, ndivyo tutakavyoweza kufanya maamuzi mazuri.

17. Tunawezaje kutumia wakati wetu kwa hekima? (Waefeso 5:​15, 16) (Tazama pia picha.)

17 Paulo pia aliwashauri Wakristo huko Efeso watumie wakati wao kwa hekima. (Soma Waefeso 5:​15, 16.) “Yule mwovu,” adui yetu Shetani, angependa tutumie muda mwingi kufuatilia mambo ya ulimwengu huu, hivi kwamba tukose wakati wa kufanya utumishi wetu kwa Mungu. (1 Yoh. 5:19) Inaweza kuwa rahisi sana kwa Mkristo kutanguliza mali, elimu, au kazi yake badala ya kutafuta fursa za kumtumikia Yehova. Ikiwa jambo hilo litatokea, itaonyesha kwamba Mkristo huyo ameathiriwa na njia ya kufikiri ya ulimwengu. Kwa kweli, mali, elimu, au kazi si mambo mabaya, lakini hayapaswi kamwe kutangulizwa maishani mwetu. Ili tutembee “kama watoto wa nuru,” tunahitaji ‘kutumia vizuri kabisa wakati wetu,’ yaani, kukazia fikira mambo ambayo kwa kweli ni muhimu.

Wakristo huko Efeso walihimizwa watumie muda wao kwa hekima (Tazama fungu la 17)


18. Donald alichukua hatua zipi ili atumie vizuri zaidi wakati wake?

18 Tafuta fursa za kumtumikia Yehova kikamili zaidi. Hivyo ndivyo alivyofanya Donald, anayeishi nchini Afrika Kusini. Anasema hivi: “Nilichunguza hali yangu na kutoa dua kwa Yehova anisaidie niwe na matokeo zaidi katika huduma. Nilisali ili nipate kazi itakayoniruhusu kuwa na muda mwingi wa kuhubiri. Kwa msaada wa Yehova, nilipata kazi inayofaa. Kisha mimi na mke wangu tulianza utumishi wa wakati wote.”

19. Tunawezaje kuendelea kutembea “kama watoto wa nuru”?

19 Ni lazima barua ya Paulo kwa Waefeso iliwasaidia waendelee kuwa waaminifu kwa Yehova. Na ushauri huo ulioongozwa na roho unaweza kutusaidia sisi pia. Kama tulivyoona, unaweza kutusaidia kuchagua kwa hekima burudani inayofaa na watu tutakaoshirikiana nao. Unaweza kutuchochea kuendelea kuzama katika nuru ya kweli kwa kuwa na programu endelevu ya kujifunza Biblia. Na ushauri huo wa Paulo umekazia umuhimu wa roho takatifu ambayo inaweza kutusaidia tutokeze sifa nzuri. Kutumia maishani mambo ambayo Paulo aliandika, kunaweza kutusaidia tufanye maamuzi ya hekima ambayo yanapatana na njia ya kufikiri ya Yehova. Kwa kufanya mambo hayo, tutaweza kuepuka giza la ulimwengu huu na kubaki katika nuru!

UNGEJIBUJE?

  • Maneno “giza” na “nuru” yanayotajwa katika Waefeso 5:8 yanarejelea nini?

  • Tunawezaje kuepuka “giza”?

  • Tunawezaje ‘kuendelea kutembea kama watoto wa nuru’?

WIMBO 95 Nuru Inazidi Kuongezeka

a Baadhi ya majina yamebadilishwa.

b MAELEZO YA PICHA: Kwenye picha tunaona nakala ya kale ya barua ya mtume Paulo kwa Waefeso.