Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 9

WIMBO 75 “Mimi Hapa! Nitume Mimi!”

Je, Uko Tayari Kujiweka Wakfu kwa Yehova?

Je, Uko Tayari Kujiweka Wakfu kwa Yehova?

“Nitamlipa Yehova nini kwa mema yote aliyonitendea?”ZAB. 116:12.

JAMBO KUU

Makala hii inaweza kukusaidia kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova ili utamani kujiweka wakfu kwake na kubatizwa.

1-2. Ni lazima mtu afanye nini kabla ya kubatizwa?

 KATIKA miaka mitano iliyopita, watu zaidi ya milioni moja wamebatizwa na kuwa Mashahidi wa Yehova. Kama mwanafunzi wa karne ya kwanza Timotheo, wengi wao wamefundishwa kweli “tangu utoto mchanga.” (2 Tim. 3:​14, 15) Wengine wamejifunza na Mashahidi wa Yehova wakiwa watu wazima, na baadhi wakiwa wamezeeka. Miaka kadhaa iliyopita, mwanamke mmoja alijifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova na kubatizwa akiwa na umri wa miaka 97!

2 Ikiwa wewe ni mwanafunzi wa Biblia au unalelewa na wazazi ambao ni Mashahidi wa Yehova, je, unafikiria kubatizwa? Hilo ni lengo nzuri sana! Lakini kabla ya kubatizwa, utahitaji kujiweka wakfu kwa Yehova. Makala hii itafafanua kujiweka wakfu kunahusisha nini. Pia, itakusaidia kuona kwa nini huna sababu ya kusita kuchukua hatua hiyo pamoja na ya kubatizwa, ikiwa uko tayari kufanya hivyo.

KUJIWEKA WAKFU KUNAMAANISHA NINI?

3. Toa mifano ya Biblia ya watu waliojiweka wakfu kwa Yehova.

3 Katika Biblia, kuweka wakfu humaanisha kutenga kwa ajili ya kusudi takatifu. Waisraeli walikuwa taifa lililowekwa wakfu kwa Yehova. Lakini baadhi ya watu katika taifa hilo walikuwa wamewekwa wakfu kwa Yehova katika njia ya pekee. Kwa mfano, Haruni alivaa “ishara takatifu ya wakfu”—bamba linalong’aa la dhahabu lililowekwa upande wa mbele wa kilemba chake. Bamba hilo la dhahabu lilionyesha kwamba alikuwa amechaguliwa amtumikie Yehova kwa njia ya pekee—akiwa kuhani mkuu wa Israeli. (Law. 8:9) Wanadhiri pia walikuwa wamejiweka wakfu kwa Yehova katika njia ya pekee. Neno “Mnadhiri,” linatokana na neno la Kiebrania nazirʹ linalomaanisha “Aliyewekwa Kando,” au “Aliyewekwa Wakfu.” Wanadhiri walihitaji kutii maagizo hususa ambayo yaliandikwa katika Sheria ya Musa.—Hes. 6:​2-8.

4. (a) Ni katika njia gani wale ambao wamejiweka wakfu kwa Yehova wametengwa kwa ajili ya kusudi takatifu? (b) Inamaanisha nini ‘kujikana’ mwenyewe? (Tazama pia picha.)

4 Unapojiweka wakfu kwa Yehova unachagua kuwa mwanafunzi wa Yesu Kristo na jambo kuu zaidi maishani mwako linakuwa kufanya mapenzi ya Mungu. Wakfu wa Kikristo unahusisha nini? Yesu alisema: “Mtu yeyote akitaka kunifuata, lazima ajikane mwenyewe.” (Mt. 16:24) Msemo wa Kigiriki unaotafsiriwa “lazima ajikane mwenyewe” unaweza pia kurejelewa kuwa “kutoishi tena kwa ajili yetu wenyewe.” Ukiwa mtumishi wa Yehova aliyejiweka wakfu, utahitaji kukataa kitu chochote kisichopatana na mapenzi yake. (2 Kor. 5:​14, 15) Hilo linatia ndani kukataa “matendo ya mwili,” kama vile uasherati. (Gal. 5:​19-21; 1 Kor. 6:18) Je, kutii maagizo hayo kunafanya maisha yako yawe magumu? Hapana, hutahisi hivyo ikiwa unampenda Yehova na unasadiki kwamba sheria zake ni kwa ajili ya manufaa yako. (Zab. 119:97; Isa. 48:​17, 18) Ndugu mmoja anayeitwa Nicholas anaelezea jambo hilo kwa njia hii, “Unaweza kuona viwango vya Yehova kama kizuizi cha gereza kinachokuzuia kufanya mambo kama unavyotaka au kama vyuma vya banda la simba vinavyokulinda kutokana na hatari.”

Je, unaviona viwango vya Yehova kama kizuizi cha gereza kinachokuzuia kufanya mambo kama unavyotaka au kama vyuma vya banda la simba vinavyokulinda kutokana na hatari? (Tazama fungu la 4)


5. (a) Unajiweka wakfu kwa Yehova jinsi gani? (b) Kuna tofauti gani kati ya kujiweka wakfu na kubatizwa? (Tazama pia picha.)

5 Unajiweka wakfu kwa Yehova jinsi gani? Unamwahidi katika sala kwamba utamwabudu yeye peke yake na kwamba utatanguliza mapenzi yake katika maisha yako. Kwa kweli, unamwahidi Yehova kwamba utaendelea kumpenda “kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote na kwa nguvu zako zote.” (Marko 12:30) Unajiweka wakfu ukiwa faraghani, na ni kati yako na Yehova. Tofauti na hilo, ubatizo hufanywa hadharani; unawaonyesha wengine kwamba tayari umejiweka wakfu kwa Yehova. Wakfu wako ni nadhiri takatifu. Lengo lako linapaswa kuwa kutimiza ahadi hiyo na Yehova anatarajia ufanye hivyo.—Mhu. 5:​4, 5.

Kujiweka wakfu kwa Yehova kunahusisha kumwahidi faraghani kwamba utamwabudu yeye peke yake na kutanguliza mapenzi yake katika maisha yako (Tazama fungu la 5)


KWA NINI UJIWEKE WAKFU KWA YEHOVA?

6. Ni nini kinachomchoea mtu ajiweke wakfu kwa Yehova?

6 Kumpenda Yehova ndiyo sababu kuu ya kujiweka wakfu kwake. Upendo wako hautegemei hisia tu. Badala yake, unategemea “ujuzi sahihi” na “utambuzi wa kiroho,” yaani, mambo uliyojifunza kumhusu Yehova ambayo yalifanya upendo wako kwake usitawi. (Kol. 1:9) Kujifunza Maandiko kulikusadikisha kwamba (1) Yehova ni halisi, (2) Biblia ni Neno lake lililoongozwa na roho, na (3) anatumia tengenezo lake kutimiza mapenzi yake.

7. Tunapaswa kufanya nini kabla ya kujiweka wakfu kwa Mungu?

7 Wale wanaojiweka wakfu kwa Yehova wanapaswa kujua mafundisho ya msingi yanayopatikana katika Neno la Mungu na kuishi kulingana na viwango vyake. Wanajitahidi kadiri wawezavyo kuwaambia wengine kuhusu mambo ambayo wamejifunza. (Mt. 28:​19, 20) Upendo wao kwa Yehova umekua, na tamaa yao ya kutoka moyoni ni kumtumikia yeye peke yake. Je, wewe unafanya hivyo? Ukiwa na upendo wa aina hiyo, hutajiweka wakfu na kubatizwa ili tu kumfurahisha mwalimu wako wa Biblia au wazazi wako; wala hutafanya hivyo kwa sababu tu marafiki wako wamefanya hivyo.

8. Kuonyesha shukrani kunakusaidiaje kufanya uamuzi wa kujiweka wakfu kwa Yehova? (Zaburi 116:​12-14)

8 Unapofikiria mambo yote ambayo Yehova amekufanyia utamthamini sana na utataka kujiweka wakfu kwake. (Soma Zaburi 116:​12-14.) Biblia inamwita kwa usahihi Yehova kuwa ndiye Mpaji wa “kila zawadi njema na kila tuzo kamilifu.” (Yak. 1:17) Zawadi bora zaidi kuliko zote ni dhabihu ya Yesu, Mwana wake. Hebu fikiria! Fidia imekuwezesha kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova. Na imekupatia tumaini la kuishi milele. (1 Yoh. 4:​9, 10, 19) Kujiweka wakfu kwa Yehova ni njia ya kuonyesha shukrani kwa ajili ya upendo huo mkubwa zaidi ambao amekuonyesha, pamoja na baraka nyingine ambazo Yehova amekupatia. (Kum. 16:17; 2 Kor. 5:15) Njia hiyo ya kuonyesha shukrani imekaziwa kwenye kitabu Furahia Maisha Milele! somo la 46, jambo kuu la 4, ambapo pia kuna video ya dakika tatu yenye kichwa Kumtolea Mungu Zawadi.

JE, UKO TAYARI KUJIWEKA WAKFU NA KUBATIZWA?

9. Kwa nini mtu hapaswi kuhisi kwamba anashinikizwa kujiweka wakfu?

9 Huenda unahisi kwamba huko tayari kujiweka wakfu na kubatizwa. Labda bado unahitaji kufanya mabadiliko maishani mwako ili yapatane na viwango vya Yehova, au labda unahitaji muda zaidi ili kuimarisha imani yako. (Kol. 2:​6, 7) Si kila mwanafunzi atafanya maendeleo ya kiroho kwa kiwango kilekile, na si kila kijana atakuwa tayari kwa ajili ya kujiweka wakfu na kubatizwa katika umri uleule. Jitahidi kupima maendeleo yako ya kiroho kulingana na mambo unayoweza kufanya, na si kwa kujilinganisha na mtu mwingine.—Gal. 6:​4, 5.

10. Unaweza kufanya nini ikiwa huko tayari kwa ajili ya kujiweka wakfu na kubatizwa? (Tazama pia sanduku: “ Kwa Ajili ya Wale Wanaolelewa Katika Kweli.”)

10 Hata ikiwa umetambua kwamba huko tayari kujiweka wakfu kwa Yehova, endelea kufanya jambo hilo kuwa lengo lako. Sali kwa Yehova na umwombe abariki jitihada zako za kufanya mabadiliko yoyote unayohitaji kufanya. (Flp. 2:13; 3:16) Unaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atasikiliza sala yako na kuijibu.—1 Yoh. 5:14.

KWA NINI BAADHI YA WATU HUSITA?

11. Yehova atatusaidiaje kuendelea kuwa waaminifu kwake?

11 Baadhi ya watu ambao wako tayari kwa ajili ya ubatizo husita kujiweka wakfu na kubatizwa. Huenda wakajiuliza, ‘Namna gani nikifanya dhambi nzito na kutengwa na ushirika?’ Ikiwa una woga huo, uwe na uhakika kwamba Yehova atakupatia kila kitu unachohitaji ili ‘utembee kwa kumstahili yeye ili kumpendeza kikamili.’ (Kol. 1:10) Pia, atakupatia nguvu za kufanya yaliyo sawa. Tayari amethibitisha kwamba anaweza kufanya hivyo kwa kuwasaidia watu wengine wengi wafanye yaliyo sawa. (1 Kor. 10:13) Hiyo ni mojawapo ya sababu zinazofanya watu wachache tu watengwe na kutaniko la Kikristo. Yehova anawasaidia watu wake waendelee kuwa waaminifu.

12. Tunawezaje kuepuka kufanya dhambi nzito?

12 Kila mwanadamu ambaye si mkamilifu anashawishiwa kufanya mambo mabaya. (Yak. 1:14) Hata hivyo, wewe ndiye unayeamua ikiwa utatenda kulingana na kishawishi hicho au la. Ukweli ni kwamba wewe ndiye unayeamua jinsi utakavyoishi. Ingawa baadhi ya watu huenda wakadai haiwezekani, unaweza kujifunza kujidhibiti usinaswe na kishawishi. Hivyo, hata unaposhawishiwa, unaweza kuamua kutofanya jambo baya. Ili ufanikiwe, sali kila siku. Dumisha ratiba nzuri ya kujifunza kibinafsi Neno la Mungu. Hudhuria mikutano ya Kikristo. Wahubirie wengine kuhusu mambo uliyojifunza. Kufuata hatua hizo kwa ukawaida kutakupatia nguvu za kuendelea kuwa mwaminifu kwa Yehova. Na usisahau kwamba Yehova atakusaidia kufanya hivyo.—Gal. 5:16.

13. Yosefu alituwekea mfano gani mzuri?

13 Itakuwa rahisi zaidi kuishi kulingana na wakfu wako ikiwa utaamua mapema jambo utakalofanya utakaposhawishiwa. Biblia inatueleza kuhusu watu ambao walifanya hivyo, hata ingawa wao pia hawakuwa wakamilifu. Kwa mfano, mke wa Potifa alijaribu kumtongoza Yosefu siku baada ya siku. Lakini tayari Yosefu alijua jambo la kufanya. Biblia inasema kwamba ‘alikataa,’ na akasema: “Ninawezaje kufanya uovu huu mkubwa na kwa kweli nimtendee Mungu dhambi?” (Mwa. 39:​8-10) Kwa kweli, Yosefu alijua jambo ambalo angefanya hata kabla ya kushawishiwa na mke wa Potifa. Hilo lilifanya iwe rahisi zaidi kwake kufanya lililo sawa aliposhawishiwa.

14. Tunawezaje kujifunza kukataa kishawishi?

14 Unawezaje kuiga mfano wa Yosefu unaposhawishiwa? Unaweza kuamua sasa jambo utakalofanya kishawishi kitakapotokea. Jifunze kukataa mara moja mambo ambayo Yehova anachukia, na kuepuka kuendelea kuyafikiria. (Zab. 97:10; 119:165) Kwa njia hiyo, hutatenda dhambi unaposhawishiwa. Tayari utakuwa unajua jinsi utakavyotenda. Tayari utakuwa umefanya uamuzi.

15. Mtu anawezaje kuonyesha kwamba ‘anamtafuta Yehova kwa bidii’? (Waebrania 11:6)

15 Huenda unajua kwamba umeipata kweli na unataka kumtumikia Yehova kwa moyo wako wote, lakini bado kuna kitu kinachokuzuia kujiweka wakfu na kubatizwa. Unaweza kujifunza kutokana na mfano wa Mfalme Daudi. Mwombe Yehova hivi: “Nichunguze kabisa, Ee Mungu, uujue moyo wangu. Nipime, uyajue mawazo yangu yanayonihangaisha. Angalia ikiwa kuna njia yoyote yenye madhara ndani yangu, uniongoze katika njia ya milele.” (Zab. 139:​23, 24) Yehova huwabariki wale “wanaomtafuta kwa bidii.” Kujitahidi kufikia lengo lako la kujiweka wakfu na kubatizwa kunamwonyesha kwamba unamtafuta kwa bidii.—Soma Waebrania 11:6.

ENDELEA KUMKARIBIA YEHOVA

16-17. Yehova anawavuta jinsi gani wale wanaolelewa katika kweli? (Yohana 6:44)

16 Yesu alisema kwamba wanafunzi wake huvutwa na Yehova. (Soma Yohana 6:44.) Fikiria kuhusu wazo hilo nzuri na jinsi linavyokuhusu. Yehova huona jambo fulani zuri ndani ya kila mtu anayemvuta kwake. Anamwona mtu huyo kuwa “mali yake ya pekee,” au “mali yake anayothamini sana.” (Kum. 7:6; maelezo ya chini) Hivyo ndivyo Yehova anavyokuona pia.

17 Inawezekana kwamba wewe ni kijana ambaye unalelewa katika kweli. Huenda ukahisi kwamba unamtumikia Yehova kwa sababu tu wazazi wako wanafanya hivyo, na si kwa sababu Yehova amekuvuta kwake. Hata hivyo, Biblia inasema hivi: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.” (Yak. 4:8; 1 Nya. 28:9) Unapochukua hatua ya kwanza ya kumkaribia Yehova, yeye hukukaribia pia. Yehova hakuoni wewe kuwa tu sehemu ya kikundi cha watu. Anamvuta kila mtu kibinafsi—kutia ndani kila mtu anayelelewa katika kweli. Mtu huyo anapochukua hatua ya kwanza ya kumkaribia Yehova, Yeye humkaribia pia kama tulivyoona kwenye Yakobo 4:8.—Linganisha 2 Wathesalonike 2:13.

18. Tutazungumzia nini katika makala inayofuata? (Zaburi 40:8)

18 Unapojiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa, unaiga mtazamo wa Yesu. Alijitoa kwa hiari kwa Baba yake ili afanye chochote ambacho Baba yake alimwagiza. (Soma Zaburi 40:8; Ebr. 10:7) Katika makala inayofuata, tutazungumzia kitakachokusaidia kuendelea kumtumikia Yehova kwa uaminifu baada ya ubatizo wako.

UNGEJIBUJE?

  • Kujiweka wakfu kwa Yehova kunamaanisha nini?

  • Kuonyesha shukrani kunahusianaje na kujiweka wakfu?

  • Ni nini kitakachokusaidia kuepuka dhambi nzito?

WIMBO 38 Atakupa Nguvu