Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 44

Dumisha Tumaini Lako la Kikristo Likiwa Imara

Dumisha Tumaini Lako la Kikristo Likiwa Imara

“Mtumaini Yehova.”​—ZAB. 27:14.

WIMBO 144 Kaza Macho Kwenye Zawadi!

MUHTASARI *

1. Yehova ametupatia tumaini gani?

 YEHOVA ametupatia tumaini zuri ajabu la uzima wa milele. Baadhi ya Wakristo wana tumaini la kuishi milele mbinguni wakiwa viumbe wa roho wasioweza kufa. (1 Kor. 15:50, 53) Hata hivyo, wengi wana tumaini la kuishi milele duniani wakiwa na afya kamilifu na furaha. (Ufu. 21:3, 4) Iwe tunatarajia kuishi milele mbinguni au duniani, tumaini letu ni lenye thamani sana kwetu.

2. Tumaini letu linategemea nini, na kwa nini tunasema hivyo?

2 Neno “tumaini,” kama linavyotumiwa kwenye Biblia, linaweza kumaanisha “kutarajia kwamba mambo mazuri yatatokea.” Tumaini letu la wakati ujao ni hakika kwa sababu linatoka kwa Yehova. (Rom. 15:13) Tunajua mambo ambayo ameahidi, na pia tunajua kwamba sikuzote yeye hutimiza ahadi zake. (Hes. 23:19) Tunasadiki kwamba Yehova anatamani na pia ana uwezo wa kutimiza kila jambo analosema kwamba atafanya. Kwa hiyo, tumaini letu halitegemei ndoto au mambo ya kuwaziwa, bali linategemea uthibitisho na mambo halisi.

3. Tutazungumzia nini katika makala hii? (Zaburi 27:14)

3 Baba yetu wa mbinguni anatupenda, naye anataka tumtumaini. (Soma Zaburi 27:14.) Ikiwa tumaini letu katika Yehova ni imara, tutafaulu kuvumilia majaribu na kukabiliana na wakati ujao kwa ujasiri na shangwe. Acheni tuchunguze jinsi tumaini letu linavyotulinda. Kwanza, tutachunguza jinsi tumaini lilivyo kama nanga na kama kofia ya chuma. Kisha tutazungumzia jinsi tunavyoweza kuimarisha tumaini letu.

TUMAINI LETU NI KAMA NANGA

4. Tumaini linawezaje kulinganishwa na nanga? (Waebrania 6:19)

4 Katika barua ambayo aliwaandikia Waebrania, mtume Paulo alilinganisha tumaini letu na nanga. (Soma Waebrania 6:19.) Paulo alisafiri baharini mara nyingi, basi alijua kwamba nanga zilitumiwa kusaidia meli isipeperushwe. Pindi moja, alikuwa akisafiri kwenye meli wakati dhoruba kali ilipotokea. Wakati wa dhoruba hiyo, aliwaona mabaharia wakitupa nanga katika maji ili kuzuia meli isipeperushwe na kugonga miamba hatari. (Mdo. 27:29, 39-41) Kama vile nanga inavyosaidia meli kuwa thabiti, tumaini letu hutusaidia kuwa thabiti ili tusipeperushwe kutoka kwa Yehova tunapokabili misukosuko maishani. Tumaini letu imara hutusaidia kushinda majaribu yaliyo kama dhoruba kwa sababu tunasadiki kwamba wakati ujao hali zitakuwa bora zaidi. Kumbuka, Yesu alituonya kwamba tungeteswa. (Yoh. 15:20) Basi, kutafakari kuhusu thawabu tuliyoahidiwa ya wakati ujao, kutatusaidia kuendelea kumtumikia Yehova tukiwa imara.

5. Tumaini lilimwimarishaje Yesu alipokabili kifo?

5 Fikiria jinsi tumaini lilivyomsaidia Yesu aendelee kuwa imara licha ya kifo cha kikatili ambacho angekabili. Siku ya Pentekoste 33 W.K., mtume Petro alinukuu unabii huu kutoka kwenye kitabu cha Zaburi ambao unaeleza kwa njia nzuri jinsi Yesu alivyokuwa mwenye uhakika na utulivu: “Nitaishi katika tumaini; kwa sababu hutaniacha Kaburini, wala hutamruhusu mshikamanifu wako aone uharibifu. . . . Utanijaza shangwe nyingi mbele zako.” (Mdo. 2:25-28; Zab. 16:8-11) Ingawa Yesu alijua kwamba angekufa, alikuwa na tumaini imara kwamba Mungu angemfufua na kwamba angepata shangwe ya kuungana tena na Baba yake mbinguni.​—Ebr. 12:2, 3.

6. Ndugu mmoja alisema nini kuhusu tumaini?

6 Tumaini letu la Kikristo limewasaidia ndugu na dada zetu wengi wavumilie. Fikiria mfano wa Leonard Chinn, ndugu mwaminifu aliyeishi huko Uingereza. Wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, alifungwa gerezani kwa sababu ya kukataa kujiunga na jeshi. Kwa miezi miwili, aliwekwa kwenye kifungo cha upweke, kisha akalazimishwa kufanya kazi ngumu sana kwa muda fulani. Baadaye aliandika hivi: “Mambo niliyojionea yalinisaidia kutambua kwamba tunahitaji kuwa na tumaini ili kuvumilia. Tuna mfano wa Yesu, mitume, manabii, na pia tuna ahadi zenye thamani zilizo katika Biblia. Mambo hayo yote hutusaidia kuwa na tumaini lenye nguvu la wakati ujao, na kutuimarisha ili tuvumilie.” Tumaini lilikuwa kama nanga kwa Leonard, na linaweza kuwa kama nanga kwetu pia.

7. Majaribu yanawezaje kuimarisha tumaini letu? (Waroma 5:3-5; Yakobo 1:12)

7 Tumaini letu huimarika zaidi tunapovumilia majaribu na kujionea msaada wa Yehova na kupata kibali chake. (Soma Waroma 5:3-5; Yakobo 1:12.) Na hivyo, tunakuwa na tumaini lenye nguvu zaidi, kuliko tumaini tulilokuwa nalo mwanzoni tulipokubali habari njema. Shetani anataka tulemewe na majaribu yetu, lakini Yehova anaweza kutusaidia tuvumilie kila jaribu kwa mafanikio.

TUMAINI LETU NI KAMA KOFIA YA CHUMA

8. Kwa nini tumaini letu ni kama kofia ya chuma? (1 Wathesalonike 5:8)

8 Pia, Biblia inalinganisha tumaini letu na kofia ya chuma. (Soma 1 Wathesalonike 5:8.) Mwanajeshi huvaa kofia ya chuma ili kulinda kichwa chake dhidi ya mashambulizi ya adui zake. Katika vita vyetu vya kiroho, tunahitaji kulinda akili yetu dhidi ya mashambulizi ya Shetani. Anatushambulia kwa vishawishi na mawazo mbalimbali ambayo yamekusudiwa kupotosha njia yetu ya kufikiri. Kama vile kofia ya chuma inavyolinda kichwa cha mwanajeshi, tumaini letu linalinda fikira zetu ili tuendelee kuwa waaminifu kwa Yehova.

9. Matokeo yanakuwaje watu wanapokosa tumaini?

9 Tumaini letu la uzima wa milele litatusaidia tutende kwa hekima na utambuzi. Ikiwa tumaini letu litadhoofika na turuhusu fikira zetu ziongozwe na mawazo ya kimwili, tunaweza kupoteza tumaini letu la kupata uzima wa milele. Fikiria kisa cha baadhi ya Wakristo walioishi katika jiji la kale la Korintho. Walipoteza imani katika ahadi muhimu ya Mungu, yaani, tumaini la ufufuo. (1 Kor. 15:12) Paulo alisema kwamba watu wasio na tumaini la kuishi wakati ujao hukazia fikira tu kutosheleza tamaa zao za sasa. (1 Kor. 15:32) Leo, watu wengi ambao hawatumaini ahadi za Mungu wanakazia fikira maisha ya sasa, wakijitahidi kufuatilia kila jambo wanaloweza kufurahia sasa. Hata hivyo, sisi tunaweka tumaini letu katika wakati ujao tulioahidiwa na Mungu. Tumaini letu ni kama kofia ya chuma ya mfano ambayo inalinda njia yetu ya kufikiri na kutuzuia tusijiingize kwenye maisha ya kutosheleza tu tamaa za kibinafsi, ambayo yanaweza kuharibu uhusiano wetu na Yehova.​—1 Kor. 15:33, 34.

10. Tumaini linawezaje kutulinda dhidi ya mawazo ya uwongo?

10 Tumaini letu lililo kama kofia linaweza kutulinda dhidi ya kufikiria kwamba hatuwezi kumfurahisha Yehova na hivyo kuhisi kwamba hatuhitaji kujitahidi. Kwa mfano, huenda wengine wakafikiria hivi: ‘Mimi sitawahi kamwe kuwa kati ya wale watakaoishi milele. Mimi sistahili. Sitawahi kamwe kufikia viwango vya Mungu.’ Kumbuka kwamba Elifazi, mfariji wa uwongo wa Ayubu, alijaribu kumshawishi Ayubu kwa kutumia njia hiyo. Elifazi alisema hivi: “Mwanadamu anayeweza kufa ni nini hata awe safi?” Kisha akasema hivi kumhusu Mungu: “Tazama! Hana imani na watakatifu wake, na hata mbingu si safi machoni pake.” (Ayu. 15:14, 15) Huo ulikuwa uwongo mkubwa! Kumbuka kwamba Shetani ndiye anayeendeleza njia hiyo ya kufikiri. Anajua kwamba ukijiruhusu kuendelea kukazia fikira mawazo hayo, utapoteza tumaini lako. Badala yake, kataa uwongo huo na ukazie fikira ahadi za Yehova. Usitilie shaka kamwe kwamba anataka uishi milele, naye atakusaidia ufikie lengo hilo.​—1 Tim. 2:3, 4.

DUMISHA TUMAINI LAKO LIKIWA IMARA

11. Kwa nini tunapaswa kuwa na subira tunapongoja tumaini letu litimizwe?

11 Si rahisi kudumisha tumaini letu likiwa imara sikuzote. Huenda tukachoka kusubiri Mungu atimize ahadi zake. Hata hivyo, Yehova anaishi milele, naye anaona wakati kwa njia tofauti na sisi. (2 Pet. 3:8, 9) Atatimiza kusudi lake kwa njia bora kabisa, lakini huenda asichukue hatua wakati ambao sisi tunatarajia. Ni nini ambacho kitatusaidia kudumisha tumaini letu likiwa imara tunapongoja kwa subira Mungu atimize ahadi zake?​—Yak. 5:7, 8.

12. Kulingana na Waebrania 11:1, 6, tumaini linahusianaje na imani?

12 Tutadumisha tumaini letu likiwa imara ikiwa tutaendelea kukaa karibu na Yehova ambaye anatupatia uhakika wa tumaini letu. Hata Biblia inaonyesha kwamba tumaini linahusiana kwa ukaribu na imani kwamba Mungu yupo na kwamba yeye ni “mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.” (Soma Waebrania 11:1, 6.) Kadiri Yehova anavyokuwa halisi kwetu, ndivyo uhakika wetu unavyozidi kuongezeka kwamba atatimiza mambo yote aliyoahidi. Acheni tuchunguze njia hususa ambazo tunaweza kuimarisha uhusiano wetu pamoja na Yehova na hivyo kudumisha tumaini letu likiwa imara.

Kusali na kutafakari kutatusaidia kudumisha tumaini letu likiwa imara (Tazama fungu la 13 hadi 15) *

13. Tunawezaje kumkaribia Mungu?

13 Sali kwa Yehova, na usome Neno lake. Ingawa hatuwezi kumwona Yehova, tunaweza kumkaribia. Tunaweza kuzungumza naye katika sala, tukiwa na uhakika kwamba atatusikiliza. (Yer. 29:11, 12) Tunaweza kumsikiliza Mungu kwa kusoma Neno lake na kulitafakari. Tunaposoma jinsi Yehova alivyowatunza wale waliokuwa washikamanifu kwake zamani, tumaini letu litazidi kuwa imara. Mambo yote yaliyo katika Neno la Mungu yaliandikwa “ili kutufundisha, ili kupitia uvumilivu wetu na kupitia faraja kutoka kwa Maandiko tuwe na tumaini.”​—Rom. 15:4.

14. Kwa nini tunapaswa kutafakari mambo ambayo Yehova aliwatendea watu wengine?

14 Tafakari jinsi ambavyo Yehova ametimiza ahadi zake. Fikiria jambo ambalo Yehova aliwafanyia Abrahamu na Sara. Walikuwa wamefika umri ambao hawangeweza kupata watoto. Ingawa hivyo, Mungu aliwaahidi kwamba wangepata mtoto. (Mwa. 18:10) Abrahamu alitendaje? Biblia inasema hivi: “Alikuwa na imani kwamba angekuwa baba ya mataifa mengi.” (Rom. 4:18) Ingawa kulingana na maoni ya wanadamu hawakuwa na tumaini lolote, Abrahamu alikuwa na uhakika kwamba Yehova angetimiza ahadi yake. Mwanamume huyo mwaminifu hakukatishwa tamaa. (Rom. 4:19-21) Masimulizi kama hayo yanatufundisha kwamba sikuzote tunaweza kumtegemea Yehova atimize ahadi zake, hata inapoonekana kwamba hilo haliwezekani.

15. Kwa nini tunapaswa kutafakari mambo ambayo Mungu ametufanyia?

15 Fikiria mambo ambayo Yehova amekutendea. Fikiria jinsi ambavyo tayari umenufaika kibinafsi kutokana na kutimizwa kwa ahadi zilizo katika Neno la Mungu. Kwa mfano, Yesu aliahidi kwamba Baba yake atakuandalia mahitaji muhimu maishani. (Mt. 6:32, 33) Pia, Yesu amekuhakikishia kwamba Yehova atakupatia roho takatifu ikiwa utamwomba. (Luka 11:13) Yehova ametimiza ahadi hizo. Labda unaweza kufikiria ahadi nyingine ambazo amekutimizia. Kwa mfano, anaahidi kwamba atakusamehe, atakufariji, na kukulisha kiroho. (Mt. 6:14; 24:45; 2 Kor. 1:3) Unapotafakari mambo ambayo tayari Mungu amekufanyia, utaimarisha tumaini lako katika mambo ambayo atakufanyia wakati ujao.

SHANGILIENI KATIKA TUMAINI

16. Kwa nini tumaini ni zawadi yenye thamani sana?

16 Tumaini letu la uzima wa milele ni zawadi yenye thamani kutoka kwa Mungu. Tunatarajia wakati ujao mzuri ajabu, na tuna uhakika kwamba hilo litatimizwa. Tumaini letu ni kama nanga, ambayo inatuimarisha ili tufaulu kuvumilia majaribu, kuvumilia mateso, na hata kukabili kifo. Tumaini letu ni kama kofia ya chuma, inayolinda mawazo yetu ili tufaulu kukataa mambo yasiyofaa na kushikamana na mambo yanayofaa. Tumaini letu linalotegemea Biblia linatusaidia kumkaribia zaidi Mungu na linafunua kina cha upendo wake kutuelekea. Tunanufaika sana tunapodumisha tumaini letu likiwa jangavu na imara.

17. Kwa nini tumaini letu linaweza kufanya tushangilie?

17 Katika barua yake kwa Waroma, mtume Paulo alitutia moyo hivi: “Shangilieni katika tumaini.” (Rom. 12:12) Paulo angeweza kushangilia kwa sababu alikuwa na uhakika kwamba ikiwa angeendelea kuwa mwaminifu angepata uzima wa milele mbinguni. Sisi pia tunaweza kushangilia katika tumaini letu kwa sababu tuna uhakika kwamba Yehova atatimiza ahadi zake. Na kama mtunga zaburi alivyoandika, “mwenye furaha ni yule ambaye . . . anamtumaini Yehova Mungu wake, . . . Yeye ambaye ni mwaminifu daima.”​—Zab. 146:5, 6.

WIMBO 139 Wazia Wakati Vitu Vyote Vitakuwa Vipya

^ Yehova ametupatia tumaini zuri ajabu la wakati ujao. Tumaini hilo linatusaidia kuwa na maisha yenye kusudi na kuepuka kukazia fikira matatizo tunayokabili sasa. Linatutia nguvu ili tuendelee kuwa waaminifu licha ya hali ngumu tunazokabili. Pia linaweza kutulinda ili tusinaswe na mawazo yanayoweza kupotosha njia yetu ya kufikiri. Kama tutakavyojifunza katika makala hii, hizo ni sababu nzuri za kuendelea kudumisha tumaini letu la Kikristo likiwa imara.

^ MAELEZO YA PICHA: Kama vile kofia ya chuma inavyolinda kichwa cha mwanajeshi na nanga inavyosaidia meli kuwa thabiti, tumaini letu hulinda mawazo yetu na kutusaidia tuwe thabiti tunapokabili majaribu. Dada anasali kwa Yehova akiwa na uhakika. Ndugu anatafakari jinsi Mungu alivyotimiza ahadi zake kwa Abrahamu. Ndugu mwingine anatafakari jinsi ambavyo Yehova amembariki.