Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Ukumbi wa hekalu la Sulemani ulikuwa na kimo gani?

Ukumbi huo ulikuwa sehemu ya mwingilio wa chumba cha Patakatifu katika hekalu. Kulingana na matoleo yaliyochapishwa kabla ya 2023 ya tafsiri ya Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya, “ukumbi wa mbele ulikuwa na urefu wa mikono 20, nao ulilingana na upana wa nyumba, na kimo chake kilikuwa 120.” (2 Nya. 3:4) Pia, tafsiri nyingine zinasema kwamba ukumbi huo ulikuwa na kimo cha “mikono 120,” hivyo inamaanisha ulikuwa na kimo cha mita 53!

Hata hivyo, toleo la Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya lililochapishwa mwaka wa 2023 linasema hivi kuhusu ukumbi wa hekalu la Sulemani: “Kimo chake kilikuwa mikono 20,” au kimo cha mita 9 hivi. a Fikiria sababu chache za rekebisho hilo.

Kimo cha ukumbi hakitajwi kwenye 1 Wafalme 6:3. Katika mstari huo, Yeremia, mwandikaji wa kitabu hicho, anataja urefu na kina cha ukumbi huo, lakini hataji kimo chake. Kisha, katika sura inayofuata anatoa habari nyingi kuhusu sehemu za pekee za hekalu, kutia ndani Bahari ya madini yaliyoyeyushwa, magari kumi, na nguzo mbili za shaba zilizosimamishwa nje ya ukumbi. (1 Fal. 7:​15-37) Ikiwa kwa kweli ukumbi huo ulikuwa na kimo cha zaidi ya mita 50, kimo ambacho kinazidi sana sehemu nyingine za hekalu, basi kwa nini Yeremia hakutaja kimo hicho? Hata karne kadhaa baadaye, wanahistoria wa Kiyahudi waliripoti kwamba ukumbi huo haukuwa na kimo kirefu kuliko sehemu nyingine za hekalu la Sulemani.

Wasomi wa Biblia wanatilia shaka ikiwa kuta za hekalu zingeweza kutegemeza ukumbi wenye kimo cha mikono 120. Katika nyakati za Biblia, majengo marefu sana yaliyojengwa kwa mawe na matofali, kama vile malango ya hekalu huko Misri, chini yalikuwa na msingi wenye upana mkubwa na juu yalikuwa membamba. Lakini hekalu la Sulemani lilikuwa tofauti. Wasomi wa Biblia wanaamini kwamba upana wa kuta za hekalu haukuzidi mikono 6, au mita 2.7. Mwanahistoria anayeitwa Theodor Busink alisema hivi: “Kwa kutegemea upana wa kuta za [mwingilio wa hekalu], ukumbi haungeweza kuwa na [kimo cha] mikono 120.”

Huenda maandishi ya 2 Mambo ya Nyakati 3:4 hayakunakiliwa kwa usahihi. Ingawa baadhi ya hati za Biblia za kale zinataja “120” katika mstari huo, hati nyingine zinazotegemeka, kama vile Kodeksi ya Alexandria ya karne ya tano na Kodeksi ya Ambrosia ya karne ya sita, zilitaja “mikono 20.” Kwa nini huenda mwandishi angeandika kimakosa “120”? Katika Kiebrania neno linalotafsiriwa “mia moja” na neno “mikono” yanafanana. Hivyo, huenda mwandishi aliandika neno “mia moja” badala ya “mikono.”

Bila shaka, tunapojitahidi kuelewa habari hizo hususa na kuonyesha kwa usahihi hekalu la Sulemani, tunakazia hasa kile ambacho hekalu hilo lilifananisha—hekalu kubwa la kiroho. Tunashukuru sana kwamba Yehova amewaalika watumishi wake wote wamwabudu katika hekalu hilo!—Ebr. 9:​11-14; Ufu. 3:12; 7:​9-17.

a Maelezo ya chini yanafafanua kwamba “baadhi ya hati za kale zinataja ‘120,’ huku hati nyingine na baadhi ya tafsiri zinataja ‘mikono 20.’”