Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 37

WIMBO 118 “Tusaidie Tuwe na Imani Zaidi”

Barua Inayoweza Kutusaidia Kuvumilia kwa Uaminifu Mpaka Mwisho

Barua Inayoweza Kutusaidia Kuvumilia kwa Uaminifu Mpaka Mwisho

“Tunashikilia imara mpaka mwisho uhakika tuliokuwa nao mwanzoni.”EBR. 3:14.

JAMBO KUU

Kujifunza mambo hususa kutoka katika barua kwa Waebrania kutatusaidia kuvumilia kwa uaminifu hadi mwisho wa mfumo huu wa mambo.

1-2. (a) Hali ilikuwaje huko Yudea mtume Paulo alipowaandikia barua Waebrania? (b) Kwa nini barua hiyo iliyoongozwa na roho iliandikwa kwa wakati uliofaa?

 KATIKA miaka iliyofuata baada ya kifo cha Yesu, Wakristo Waebrania walioishi jijini Yerusalemu na Yudea walikabili hali ngumu. Kutaniko la Kikristo lilikabili mateso makali muda mfupi baada ya kuanzishwa. (Mdo. 8:1) Kisha, baada ya miaka 20 hivi, wafuasi wa Kristo walikabili hali ngumu sana za kiuchumi, ambazo inaelekea zilisababishwa na kipindi cha njaa ambacho kilikuwa kimeathiri eneo hilo. (Mdo. 11:​27-30) Hata hivyo, karibu mwaka wa 61 W.K., Wakristo walikuwa na kipindi cha amani ya kadiri, tofauti na hali ambayo wangekabili wakati ujao. Katika kipindi hicho, walipokea barua iliyoongozwa na roho ya Mungu kutoka kwa mtume Paulo—barua ambayo ilikuja kwa wakati uliofaa kabisa.

2 Barua hiyo kwa Waebrania iliandikwa kwa wakati uliofaa kwa sababu amani ambayo Wakristo hao walifurahia isingedumu. Paulo aliwapatia ushauri hususa ambao ungewasaidia Wakristo hao kuvumilia dhiki ambayo wangekabili muda mfupi baadaye. Kuharibiwa kwa mfumo wa mambo wa Kiyahudi ambao Yesu alikuwa ametabiri kulikuwa kumekaribia. (Luka 21:20) Bila shaka, Paulo na Wakristo walio Yudea hawakujua wakati hususa ambapo uharibifu huo ungetokea. Hata hivyo, Wakristo hao wangeweza kutumia muda uliobaki ili wajitayarishe kwa kusitawisha sifa kama vile, imani na uvumilivu.—Ebr. 10:25; 12:​1, 2.

3. Kwa nini kitabu cha Waebrania ni muhimu sana kwa Wakristo leo?

3 Hivi karibuni, tutakabili dhiki kuu zaidi kuliko ile ambayo Wakristo Waebrania walikabili. (Mt. 24:21; Ufu. 16:​14, 16) Basi, acheni tuchunguze ushauri hususa ambao Yehova aliwapatia Wakristo hao unaoweza kutunufaisha sisi pia.

“TUSONGE MBELE KUELEKEA UKOMAVU”

4. Wakristo Wayahudi walikabili changamoto gani? (Tazama pia picha.)

4 Wakristo Wayahudi walikabili changamoto kubwa. Awali, Wayahudi walikuwa watu ambao Yehova alikuwa amewachagua. Jiji la Yerusalemu lilikuwa kiti cha Ufalme wa Mungu hapa duniani, na hekalu lilikuwa kitovu cha ibada safi. Wayahudi wote waaminifu walifuata Sheria ya Musa kama ilivyofafanuliwa na viongozi wao wa kidini. Mafundisho hayo yaliongoza maamuzi yao kuhusu chakula, maoni yao kuhusu tohara, na hata jinsi walivyowatendea Watu wa Mataifa. Hata hivyo, baada ya kifo cha Yesu, Yehova hakuendelea kukubali dhabihu ambazo Wayahudi walitoa. Hilo lilitokeza changamoto kwa Wakristo Wayahudi ambao walizoea kufuata Sheria ya Musa. (Ebr. 10:​1, 4, 10) Ilikuwa vigumu kufanya baadhi ya mabadiliko, hata kwa Wakristo wakomavu kama vile, mtume Petro. (Mdo. 10:​9-14; Gal. 2:​11-14) Kwa sababu ya imani yao mpya, Wakristo hao waliteswa na viongozi wa dini ya Kiyahudi.

Wakristo walihitaji kushikamana kwa uthabiti na kweli, wakikataa mawazo ya uwongo kutoka kwa viongozi wa dini ya Kiyahudi waliowapinga (Tazama fungu la 4-5)


5. Kwa nini Wakristo Waebrania walihitaji kujihadhari?

5 Wakristo Waebrania walikuwa wakipingwa na vikundi viwili vya watu. Kikundi cha kwanza kilikuwa cha viongozi wa dini ya Kiyahudi ambao waliwaona Wakristo hao kuwa waasi-imani. Kwa kuongezea, baadhi ya Wakristo walikuwa wakisisitiza kwamba wafuasi wa Kristo waendelee kufuata mambo fulani katika Sheria ya Musa, huenda ili waepuke kuteswa. (Gal. 6:12) Ni jambo gani ambalo lingewasaidia Wakristo waaminifu washikamane na kweli?

6. Paulo aliwatia moyo waabudu wenzake wafanye nini? (Waebrania 5:14–6:1)

6 Katika barua yake kwa Waebrania, Paulo aliwatia moyo waabudu wenzake wajifunze kwa kina Neno la Mungu. (Soma Waebrania 5:14–6:1.) Akitumia Maandiko ya Kiebrania, Paulo alijadiliana na ndugu zake kuhusu ubora wa njia ya ibada ya Kikristo kwa kulinganisha na ibada ya Kiyahudi. a Paulo alijua kwamba ikiwa Wakristo hao wangeongeza ujuzi wao na kuwa na uelewaji wenye kina zaidi wa kweli, wangeweza kutambua na kukataa mawazo ya uwongo na hivyo hawangeweza kupotoshwa.

7. Tunakabili changamoto gani leo?

7 Kama Wakristo Waebrania, sisi pia tunakutana na watu wanaosambaza habari na mawazo yanayopingana na viwango vya Yehova vya uadilifu. Mara nyingi, wale wanaopinga mambo tunayoamini kuhusu maadili yanayotegemea Biblia, wanadai kwamba sisi tuna ubaguzi na ni wakatili. Mitazamo na maoni ya ulimwengu huu yanazidi kutofautiana sana na maoni makamilifu ya Mungu. (Met.17:15) Hivyo, ni lazima tuimarishe uwezo wetu wa kutambua na kukataa mawazo ambayo wale wanaotupinga wanatumia ili kujaribu kutuvunja moyo au hata kutupotosha.—Ebr. 13:9.

8. Ni nini kitakachotusaidia kuendelea kukomaa kiroho?

8 Itafaa ikiwa tutazingatia ushauri ambao Paulo aliwapatia Wakristo Waebrania wa kusonga mbele kuelekea ukomavu. Hilo linatia ndani kuwa na ujuzi wenye kina wa kweli na kuiga njia ya Yehova ya kufikiri. Tunaendelea kufuata hatua hizo hata baada ya kujiweka wakfu na kubatizwa. Hata ikiwa tumekuwa katika kweli kwa muda mrefu kadiri gani, ni lazima sisi sote tusome na kujifunza Neno la Mungu kwa ukawaida. (Zab. 1:2) Ratiba nzuri ya kujifunza kibinafsi itatusaidia kuimarisha sifa ambayo mtume Paulo alikazia katika barua yake kwa Waebrania: imani.—Ebr. 11:​1, 6.

TUWE NA “IMANI YA KUHIFADHI UHAI WETU”

9. Kwa nini Wakristo Waebrania walihitaji imani yenye nguvu?

9 Wakristo Waebrania wangehitaji imani yenye nguvu ili kuokoka dhiki iliyokuwa karibu kuipata Yudea. (Ebr. 10:​37-39) Yesu alikuwa amewaonya wafuasi wake kwamba watakapoona Yerusalemu limezingirwa na majeshi yaliyopiga kambi, wangehitaji kukimbilia milimani. Shauri hilo la Yesu liliwahusu Wakristo wote, iwe waliishi katika jiji hilo au eneo la mashambani. (Luka 21:​20-24) Wakati huo, watu waliovamiwa na jeshi fulani, kwa kawaida wangekimbilia katika jiji lenye kuta, kama Yerusalemu, ili kupata ulinzi. Agizo la kukimbilia milimani huenda lingeonekana kuwa halipatani na akili, hivyo, watu hao wangehitaji imani kubwa ili kutii agizo hilo.

10. Imani yenye nguvu ingewachochea Wakristo wafanye nini? (Waebrania 13:17)

10 Wakristo Waebrania pia wangehitaji kuwatumaini wale ambao Yesu alikuwa akiwatumia kuliongoza kutaniko. Inawezekana kwamba wale walioongoza walitoa maagizo hususa ili kuwasaidia watu wote kutanikoni wafuate mwongozo wa Yesu kwa wakati unaofaa na kwa njia inayofaa. (Soma Waebrania 13:17.) Neno la Kigiriki lililotumiwa kwenye Waebrania 13:17 linalotafsiriwa “watiini,” linaonyesha kwamba mtu anachochewa kutii kwa sababu anamtumaini mtu anayetoa mwongozo. Hilo linahusisha mengi zaidi ya kumtii mtu huyo kwa sababu tu ana mamlaka ya kutoa mwongozo. Hivyo, Wakristo Waebrania walihitaji kujifunza kuwatumaini wale walioongoza, kabla ya dhiki hiyo. Ikiwa Wakristo hao wangewatii wale walioongoza katika kipindi cha amani, ingekuwa rahisi zaidi kwao kufanya hivyo katika kipindi cha dhiki.

11. Kwa nini Wakristo leo wanahitaji kuwa na imani yenye nguvu?

11 Kama Wakristo Waebrania, sisi pia tunahitaji kuwa na imani. Tunaishi katika wakati ambao watu wengi wanakataa—na hata kudhihaki—onyo la Biblia kuhusu mwisho wa mfumo huu wa mambo. (2 Pet. 3:​3, 4) Isitoshe, ingawa Biblia inafunua habari mbalimbali kuhusu jinsi dhiki kuu itakavyokuwa, kuna mambo mengi ambayo hatujui. Tunahitaji kuwa na imani yenye nguvu kwamba mwisho wa mfumo huu wa mambo utafika kwa wakati na kwamba Yehova atatutunza.—Hab. 2:3.

12. Ni jambo gani litakalotusaidia kuokoka dhiki kuu?

12 Pia, ni lazima tuimarishe imani yetu katika njia ambayo Yehova anatumia kutuongoza leo—“mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mt. 24:45) Dhiki kuu itakapoanza, huenda tukapokea maagizo hususa yanayookoa uhai, kama yale ambayo huenda Wakristo Waebrania walipokea jeshi la Roma lilipozingira jiji la Yerusalemu. Sasa ndio wakati wa kuendelea kuwatumaini wale wanaoongoza katika tengenezo la Yehova na kuimarisha uhakika wetu katika mwongozo tunaopata kutoka kwao. Hatuwezi kutarajia kwamba tutatumaini na kutii mwongozo wao wakati wa dhiki kuu, ikiwa sasa tunashindwa kufanya hivyo.

13. Kwa nini shauri lililo kwenye Waebrania 13:5 lilifaa?

13 Walipokuwa wakisubiri ishara ili wakimbie, Wakristo Waebrania walihitaji pia kurahisisha maisha yao na kujilinda dhidi ya “upendo wa pesa.” (Soma Waebrania 13:5.) Baadhi yao walikuwa wamekabili njaa na umaskini. (Ebr. 10:​32-34) Ingawa mwanzoni walikuwa tayari kuvumilia hali ngumu kwa ajili ya habari njema, huenda baadhi yao walianza kuona mali kuwa ulinzi dhidi ya hatari au umaskini. Lakini hakuna kiwango chochote cha pesa ambacho kingeweza kuwalinda dhidi ya uharibifu uliokuwa ukikaribia. (Yak. 5:3) Ukweli ni kwamba huenda ingekuwa vigumu zaidi kwa mtu yeyote ambaye alipenda vitu vya kimwili, kukimbia na kuacha nyumba na mali zake.

14. Imani yenye nguvu itatusaidiaje kufanya maamuzi mazuri inapohusu vitu vya kimwili?

14 Ikiwa tuna imani yenye nguvu kwamba hivi karibuni Yehova atauharibu mfumo huu wa mambo, tutachochewa kuepuka kupenda mali. Watu “watatupa fedha yao barabarani” kwa sababu watatambua kwamba “fedha yao wala dhahabu yao haitaweza kuwaokoa katika siku ya ghadhabu ya Yehova.” (Eze. 7:19) Badala ya kukazia fikira kujikusanyia pesa nyingi iwezekanavyo, tunahitaji kufanya maamuzi yatakayotusaidia kuishi maisha rahisi na yenye usawaziko. Hilo linatia ndani kukataa kishawishi cha kuwa na madeni yasiyo ya lazima au kutumia muda mwingi sana kuhangaikia vitu vyetu vya kimwili. Pia, ni lazima tuwe waangalifu ili mali zetu zisiwe jambo muhimu zaidi maishani mwetu. (Mt. 6:​19, 24) Huenda imani yetu ikajaribiwa inapohusu vitu vya kimwili na mambo mengine tunaposubiri mwisho wa mfumo huu wa mambo ufike.

“MNAHITAJI UVUMILIVU”

15. Kwa nini Wakristo Waebrania walihitaji hasa kuwa wavumilivu?

15 Wakristo Waebrania wangehitaji kuvumilia majaribu ya imani kadiri hali zilivyozidi kuzorota huko Yudea. (Ebr. 10:36) Ingawa baadhi ya Wakristo Waebrania walikuwa wamekabili mateso makali, wengi wao walikuwa wamekubali Ukristo katika kipindi ambacho kulikuwa na amani ya kadiri. Paulo aliwaeleza kwamba ingawa walikuwa wamevumilia majaribu makali ya imani, kufikia wakati huo hawakuwa wameteseka kama Yesu, yaani, hadi kufikia kifo. (Ebr. 12:4) Hata hivyo, kadiri Ukristo ulivyokuwa ukienea, ndivyo Wayahudi waliowapinga walivyozidi kuwa na uchungu na wenye msimamo mkali. Miaka michache tu mapema, kikundi cha watu wenye hasira kilimshambulia Paulo alipokuwa akihubiri jijini Yerusalemu. Zaidi ya Wayahudi 40 ‘walijifunga kabisa kwa laana kwamba hawatakula chochote mpaka watakapomuua Paulo.’ (Mdo. 22:22; 23:​12-14) Licha ya kuzungukwa na watu wenye chuki na msimamo mkali wa kidini, bado Wakristo hao wangehitaji kukutana kwa ajili ya ibada, kuhubiri habari njema, na kuendelea kuimarisha imani yao.

16. Barua kwa Waebrania inawezaje kutusaidia kuwa na mtazamo unaofaa inapohusu mateso? (Waebrania 12:7)

16 Ni jambo gani ambalo lingewasaidia Wakristo Waebrania wavumilie upinzani waliokabili? Paulo alijua kwamba walihitaji kuwa na mtazamo unaofaa kuelekea majaribu yao. Hivyo, alifafanua kwamba huenda Mungu akaruhusu majaribu ya imani kuwa sehemu ya mazoezi ya Mkristo. (Soma Waebrania 12:7.) Mazoezi hayo yanaweza kumsaidia mtu kusitawisha na kuboresha sifa muhimu za Kikristo. Kwa kukazia fikira matokeo mazuri ya majaribu yao, ingekuwa rahisi zaidi kwa Wakristo hao Waebrania kuvumilia.—Ebr. 12:11.

17. Paulo alikuwa amejifunza nini kuhusu kuvumilia mateso?

17 Paulo aliwahimiza Wakristo Waebrania waazimie hata zaidi kuvumilia majaribu. Mtume Paulo angeweza kutoa ushauri mzuri kuhusu kuvumilia mateso. Kabla ya kuwa Mkristo aliwatesa Wakristo na alikuwa ameona jinsi walivyotendewa kwa ukatili. Pia, alijua jinsi ya kuvumilia mateso. Isitoshe, alikuwa amekabili aina mbalimbali za upinzani baada ya kuwa Mkristo. (2 Kor. 11:​23-25) Hivyo, Paulo angeweza kuzungumza akiwa na uhakika kuhusu mambo yanayohitajika ili kuvumilia. Aliwakumbusha Wakristo hao kwamba walipovumilia majaribu, walihitaji kumtegemea Yehova, si nguvu zao wenyewe. Hivyo, Paulo angeweza kusema hivi kwa ujasiri: “Yehova ni msaidizi wangu; sitaogopa.”—Ebr. 13:6.

18. Ni jambo gani litakalotupata sisi sote, na tunapaswa kufanya nini sasa?

18 Baadhi ya ndugu zetu wanavumilia mateso sasa. Tunaweza kuwategemeza kwa ushikamanifu kwa kusali kwa ajili yao, na nyakati nyingine kuwapatia msaada hususa. (Ebr. 10:33) Hata hivyo, Biblia inaeleza wazi kwamba “wote wanaotamani kuishi kwa ujitoaji-kimungu katika ushirika na Kristo Yesu watateswa pia.” (2 Tim. 3:12) Kwa sababu hiyo, sisi sote tunahitaji kujitayarisha kwa ajili ya mambo yatakayotokea wakati ujao. Acheni tuendelee kumtumaini kikamili Yehova, tukiwa na uhakika kwamba atatusaidia kuvumilia jaribu lolote ambalo huenda tukakabili. Kwa wakati unaofaa, ataleta kitulizo kwa waabudu wake wote waaminifu.—2 The. 1:​7, 8.

19. Ni hatua zipi hususa zitakazotusaidia kujitayarisha kwa ajili ya dhiki kuu? (Tazama pia picha.)

19 Bila shaka, barua ya Paulo kwa Waebrania iliwasaidia Wakristo wa karne ya kwanza kujitayarisha kwa ajili ya majaribu ambayo wangekabili. Paulo aliwahimiza ndugu zake wawe na ujuzi na uelewaji wenye kina wa Maandiko. Kufanya hivyo kungewasaidia waweze kutambua na kukataa mafundisho ambayo yangedhoofisha imani yao. Aliwatia moyo waimarishe imani yao ili wafuate bila kukawia mwongozo wa Yesu na wa wale walioongoza katika kutaniko. Na aliwasaidia Wakristo wasitawishe uvumilivu kwa kuwa na mtazamo unaofaa kuelekea majaribu, na kuyaona kuwa fursa ya kuzoezwa na Baba yao mwenye upendo. Acheni sisi pia tutumie shauri hilo lililoongozwa na roho. Kisha, tutaweza kuvumilia kwa uaminifu mpaka mwisho.—Ebr. 3:14.

Wakristo waaminifu walibarikiwa kwa sababu ya uvumilivu wao. Walipokimbia kutoka Yudea, waliendelea kukutanika pamoja. Tunaweza kujifunza nini kutokana na jambo hilo? (Tazama fungu la 19)

WIMBO 126 Uwe Macho, Simama Imara, Uwe na Nguvu

a Katika sura ya kwanza pekee, Paulo ananukuu angalau sehemu saba mbalimbali kutoka katika Maandiko ya Kiebrania ili kuthibitisha kwamba njia ya ibada ya Kikristo ni bora kuliko ibada ya Kiyahudi.—Ebr. 1:​5-13.