Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 36

WIMBO 89 Sikiliza, Tii, Upate Baraka

“Iweni Watendaji wa Neno”

“Iweni Watendaji wa Neno”

“Iweni watendaji wa neno, na si wasikiaji tu.”YAK. 1:22.

JAMBO KUU

Makala hii itatusaidia kuimarisha tamaa yetu ya kusoma Neno la Mungu kila siku, kulitafakari, na kulitumia kikamili maishani mwetu.

1-2. Ni nini kinachofanya watumishi wa Mungu wawe na furaha? (Yakobo 1:​22-25)

 YEHOVA na Mwana wake mpendwa wanataka tuwe na furaha. Mwandikaji wa Zaburi 119:2 anasema hivi: “Wenye furaha ni wale wanaoshika vikumbusho vyake, wanaomtafuta kwa moyo wao wote.” Yesu alitupatia uhakikisho zaidi aliposema hivi: “Wenye furaha ni wale wanaolisikia neno la Mungu na kulishika!”Luka 11:28.

2 Tukiwa waabudu wa Yehova, sisi ni watu wenye furaha. Kwa nini? Tuna sababu nyingi, lakini sababu moja muhimu ni kwamba tunasoma Neno la Mungu kwa ukawaida na tunajitahidi kutumia mambo tunayojifunza.—Soma Yakobo 1:​22-25.

3. Tunanufaikaje tunapotumia mambo tunayojifunza katika Neno la Mungu?

3 Kuna njia kadhaa ambazo tunanufaika tunapokuwa “watendaji wa neno.” Jambo moja tunalojua ni kwamba hiyo ni hatua muhimu ili kumpendeza Yehova. Kutambua hilo kunatufanya tuwe na furaha. (Mhu. 12:13) Tunapotumia mambo ambayo tunasoma katika Neno la Mungu lililoongozwa na roho, tunaboresha maisha yetu ya familia na kuimarisha urafiki pamoja na waabudu wenzetu. Huenda umejionea jambo hilo maishani mwako. Zaidi ya hayo, tunaepuka matatizo mengi ambayo yanawapata watu wasiofuata njia za Yehova. Kwa kweli, tunakubaliana na Mfalme Daudi. Baada ya kutaja sheria, maagizo, na hukumu za Yehova katika wimbo, alimalizia hivi: “Anapozishika anapata thawabu kubwa.”—Zab. 19:​7-11.

4. Kwa nini si rahisi kuwa watendaji wa Neno la Mungu?

4 Kihalisi, si rahisi sikuzote kuwa watendaji wa Neno la Mungu. Ingawa tuna shughuli nyingi, ni lazima tutenge wakati wa kusoma na kujifunza Biblia ili tuelewe mambo ambayo Yehova anataka tufanye. Acheni tuchunguze baadhi ya mapendekezo ambayo yanaweza kutusaidia kusoma Neno la Mungu kwa ukawaida. Pia, tutachunguza mambo ambayo yatatusaidia kutafakari yale tunayosoma na kuona njia za kutumia mambo hayo maishani.

TENGA WAKATI WA KUSOMA NENO LA MUNGU

5. Ni majukumu gani yanayochukua muda wetu mwingi?

5 Watumishi wengi wa Yehova wana shughuli nyingi. Tunatumia muda mwingi kushughulikia majukumu muhimu yanayotajwa katika Biblia. Kwa mfano, wengi wetu tunafanya kazi ya kimwili ili kupata mahitaji yetu na kuandalia familia zetu. (1 Tim. 5:8) Wakristo wengi wanawatunza watu wa ukoo ambao ni wagonjwa au waliozeeka. Na sisi sote tunahitaji kutunza afya zetu, jambo ambalo huchukua muda. Zaidi ya majukumu hayo, tuna migawo mbalimbali kutanikoni. Jukumu moja muhimu ni kushiriki kwa bidii katika kazi ya kuhubiri. Kwa kuwa una majukumu hayo mbalimbali, unawezaje kupata muda wa kusoma Biblia kwa ukawaida, kutafakari mambo unayosoma, na kuyatumia?

6. Unawezaje kuhakikisha kwamba unatanguliza usomaji wako wa Biblia? (Tazama pia picha.)

6 Kusoma Biblia ni mojawapo ya “mambo muhimu zaidi” kwa Wakristo, hivyo, tunahitaji kutanguliza jambo hilo. (Flp. 1:10) Zaburi ya kwanza inasema hivi inapozungumza kumhusu mwanamume mwenye furaha: “Anapendezwa na sheria ya Yehova, naye huisoma sheria Yake kwa sauti ya chini mchana na usiku.” (Zab. 1:​1, 2) Ni wazi kwamba hilo linamaanisha tunahitaji kutenga wakati ili kusoma Biblia. Ni wakati gani unaofaa zaidi kusoma Biblia? Huenda kila mmoja wetu akawa na jibu tofauti. Lakini jibu rahisi ni wakati ambao unaweza kufanya hivyo kwa ukawaida. Ndugu anayeitwa Victor anasema hivi: “Ninapenda kusoma Biblia asubuhi. Ingawa sipendi kuamka asubuhi na mapema, wakati huo hakuna vikengeusha fikira vingi. Akili yangu inakuwa imetulia na ninaweza kukaza fikira zaidi.” Huenda hata wewe unahisi hivyo. Jiulize hivi, ‘Ni wakati gani unaonifaa mimi kusoma Biblia?’

Ni wakati gani unaofaa zaidi kusoma Biblia? Ni wakati gani unaoweza kufanya hivyo kwa ukawaida? (Tazama fungu la 6)


TAFAKARI KUHUSU KILE UNACHOSOMA

7-8. Ni jambo gani ambalo huenda likatuzuia tusinufaike kikamili na mambo tunayosoma? Toa mfano.

7 Ukweli ni kwamba huenda tukasoma mambo mengi sana kwa ukawaida bila kuyatafakari. Je, umewahi kusoma kitu fulani na baada ya muda mfupi hukumbuki ulichosoma? Sisi sote tumewahi kupatwa na jambo kama hilo. Kwa kusikitisha, hilo linaweza kutokea tunaposoma Biblia. Huenda umejiwekea lengo la kusoma sura kadhaa za Biblia kila siku. Unastahili pongezi. Tunapaswa kujiwekea malengo na kujitahidi kushikamana nayo. (1 Kor. 9:26) Hata hivyo, kusoma Biblia ni mwanzo mzuri—lakini ni mwanzo tu. Tunahitaji kufanya mengi zaidi ili tunufaike kikamili na usomaji wa Neno la Mungu.

8 Fikiria mfano huu: Maji ya mvua ni muhimu ili mimea isitawi. Lakini mvua nyingi ikinyesha kwa muda mfupi, huenda ardhi ikawa na maji mengi. Mvua nyingi zaidi ikinyesha haitakuwa na manufaa kwa mimea. Udongo unahitaji muda ili ufyonze maji ya mvua na kuisaidia mimea ikue. Vivyo hivyo, tunapaswa kuepuka kusoma Biblia kwa mwendo wa kasi, yaani, kwa haraka hivi kwamba tunashindwa kutafakari, kukumbuka, na kutumia mambo tunayosoma.—Yak. 1:24.

Kama tu ambavyo ardhi inahitaji muda wa kutosha ili ifyonze na kutumia maji ya mvua, ndivyo tunavyohitaji muda wa kutosha kutafakari na kutumia mambo tunayosoma katika Neno la Mungu (Tazama fungu la 8)


9. Tunapaswa kufanya nini ikiwa tumesitawisha zoea la kusoma Biblia haraka-haraka?

9 Je, umetambua kwamba kuna nyakati ambazo unasoma Biblia haraka-haraka? Ikiwa ndivyo, unapaswa kufanya nini? Punguza mwendo. Jitahidi kutafakari mambo unayosoma au ambayo umesoma. Huenda wengine wakahisi ni vigumu kufanya hivyo. Ikiwa unahisi kwamba kutafakari ni jambo gumu kwako, huenda ukahitaji kuona kutafakari kuwa ni kufikiria tu jambo ambalo umesoma. Huenda ukaamua kuongeza muda wa kujifunza ili uwe na wakati wa kufikiria, au kutafakari. Kwa upande mwingine, huenda ukaamua kusoma mistari michache na kutumia muda unaobaki kutafakari mambo ambayo umesoma. Victor aliyetajwa mwanzoni anasema hivi: “Huwa ninasoma sehemu fupi ya Biblia, labda sura moja. Kwa kuwa ninasoma asubuhi na mapema, ninaweza kutafakari kwa siku nzima kile nilichosoma.” Unaweza kutumia mbinu yoyote, lakini jambo muhimu ni kusoma Biblia kwa mwendo utakaokuruhusu unufaike kikamili na mambo unayosoma.—Zab. 119:97; tazama sanduku “ Maswali ya Kufikiria.”

10. Toa mfano wa jinsi unavyoweza kutumia mambo unayojifunza. (1 Wathesalonike 5:​17, 18)

10 Licha ya wakati unaochagua kusoma Biblia na muda unaotumia kuisoma, jitahidi kutafuta njia za kutumia mambo unayosoma. Unaposoma sehemu fulani ya Neno la Mungu, jiulize hivi, ‘Ninawezaje kutumia habari hii sasa au wakati ujao?’ Kwa mfano, tuseme katika usomaji wako wa Biblia unasoma 1 Wathesalonike 5:​17, 18. (Soma.) Baada ya kusoma mistari hiyo miwili, unaweza kutua na kufikiria unasali mara ngapi, na sala zako ni zenye kina kadiri gani. Pia, unaweza kutafakari kuhusu mambo ya kumshukuru Yehova. Na huenda unaamua kwamba utamshukuru Yehova kwa mambo matatu hususa. Ukitumia hata dakika chache kukaza fikira kwa njia hiyo, kwa kadiri fulani utakuwa msikiaji na mtendaji wa Neno la Mungu. Fikiria jinsi utakavyonufaika kwa kurudia hatua hizo kila siku unaposoma sehemu nyingine za Biblia! Naam, utakuwa mtendaji mzuri zaidi wa Neno la Mungu. Namna gani ikiwa unahisi kwamba una mambo mengi sana ya kufanyia kazi?

ONYESHA KIASI UNAPOJIWEKEA MALENGO

11. Kwa nini huenda nyakati nyingine ukahisi umelemewa? Toa mfano.

11 Unaposoma Biblia na kutafuta njia za kutumia mwongozo wake, huenda nyakati nyingine ukalemewa kwa sababu unahisi kwamba una mambo mengi ya kufanyia kazi. Fikiria mfano huu: Leo, usomaji wako wa Biblia unatia ndani shauri la kuepuka kuonyesha upendeleo. (Yak. 2:​1-8) Unaona uhitaji wa kuboresha jinsi unavyowatendea wengine, hivyo unaamua kufanya mabadiliko fulani. Hongera sana! Kisha, kesho unasoma habari inayokazia umuhimu wa kudhibiti maneno unayosema. (Yak. 3:​1-12) Unatambua kwamba kuna pindi fulani ambazo umekuwa ukiongea maneno yasiyofaa. Hivyo, unaazimia kwamba unapozungumza na wengine utatumia maneno yanayofaa na yenye kujenga. Siku inayofuata, usomaji wako wa Biblia unatia ndani onyo kuhusu kutokuwa rafiki ya ulimwengu. (Yak. 4:​4-12) Unatambua kwamba unapaswa kuwa mwangalifu zaidi unapochagua burudani. Inapofika siku ya nne, huenda ukahisi umelemewa na mambo unayohitaji kufanyia kazi.

12. Kwa nini hupaswi kuvunjika moyo ikiwa usomaji wako wa Biblia unafunua kwamba unahitaji kufanya mabadiliko? (Tazama pia maelezo ya chini.)

12 Ikiwa unahitaji kufanya mabadiliko au marekebisho kadhaa, usivunjike moyo. Huo ni uthibitisho kwamba una hali nzuri ya moyoni. Mtu ambaye ni mnyenyekevu na mnyoofu, anasoma Maandiko akiwa na lengo la kujichunguza na kutafuta mambo ya kufanyia kazi. a Kumbuka kwamba ni lazima tuendelee kujitahidi kuvaa “utu mpya.” (Kol. 3:10; linganisha habari za utafiti za Kiingereza is being made new,” nwtsty.) Ni jambo gani litakalokusaidia kuendelea kuwa mtendaji wa Neno la Mungu?

13. Unawezaje kujiwekea malengo machache? (Tazama pia picha.)

13 Badala ya kujaribu kutumia mambo yote ambayo umejifunza kwa wakati mmoja, jiwekee malengo machache. (Met. 11:2) Unaweza kutumia njia hii: Andika orodha ya mambo ambayo unahitaji kufanyia kazi. Kisha, chagua jambo moja au mawili ambayo unaweza kuanza kufanyia kazi, halafu wakati ujao unaweza kufanyia kazi mambo mengine. Unapaswa kuanzia wapi?

Badala ya kujaribu kutumia mambo yote ambayo umejifunza kwa wakati mmoja, kwa nini usijiwekee malengo machache? Unaweza kuchagua kufanyia kazi jambo moja au mawili (Tazama fungu la 13-14)


14. Unaweza kuanza na malengo gani?

14 Unaweza kuamua kuanza na lengo ambalo ni rahisi kwako kulifikia. Au unaweza kuchagua kuanza na mambo ambayo unahisi yanahitaji mabadiliko makubwa. Baada ya kujiwekea lengo unalotaka kufikia, fanya utafiti katika machapisho yetu, labda kwa kutumia Fahirisi au Mwongozo wa Utafiti wa Mashahidi wa Yehova. Sali kuhusu lengo lako, na umwombe Yehova akupe “hamu na nguvu za kutenda.” (Flp. 2:13) Kisha, tumia mambo ambayo umejifunza. Unapojitahidi kufikia lengo la kwanza ulilojiwekea na kuona matokeo mazuri, unaweza kuchochewa zaidi kufanyia kazi malengo yako mengine. Ukweli ni kwamba unapofanikiwa kuboresha sehemu moja ya maisha yako ya Kikristo au sifa moja ya Kikristo, utaona ikiwa rahisi zaidi kufanya hivyo katika sehemu nyingine za maisha yako.

LIRUHUSU NENO LA MUNGU ‘LIFANYE KAZI NDANI YAKO’

15. Watu wa Yehova wana tofauti gani na watu wengi wanaoisoma Biblia? (1 Wathesalonike 2:13)

15 Baadhi ya watu wanadai kwamba wamesoma Biblia yote mara nyingi. Lakini je, kweli wanaiamini Biblia? Je, wanaishi kulingana na mafundisho yake na kuiruhusu ibadili maisha yao? Inasikitisha kwamba mara nyingi jibu ni hapana. Watu wa Yehova ni tofauti kabisa! Kama Wakristo wa karne ya kwanza, tunaikubali Biblia “kama [ilivyo] kwa kweli, neno la Mungu.” Zaidi ya hilo, tunajitahidi kuonyesha kwamba Neno la Mungu linafanya kazi katika maisha yetu.—Soma 1 Wathesalonike 2:13.

16. Ni mambo gani yanayoweza kutusaidia kuwa watendaji wa Neno?

16 Si rahisi sikuzote kusoma na kutumia Neno la Mungu. Huenda tukapambana ili kupata muda wa kuisoma. Au huenda tukasoma kwa mwendo wa kasi sana hivi kwamba hatupati wakati wa kutafakari tunachosoma. Au huenda tukahisi tumelemewa na mambo mengi ambayo tunahitaji kufanyia marekebisho. Hata iwe unakabili changamoto gani, unaweza kukabiliana nayo. Kwa msaada wa Yehova, unaweza kuishinda. Acheni tuazimie kukubali msaada wake na kuwa, si wasikiaji wasahaulifu, bali watendaji wa lile Neno. Bila shaka, kadiri tunavyosoma zaidi Neno la Mungu na kulitumia katika maisha yetu, ndivyo tutakavyokuwa wenye furaha zaidi.—Yak. 1:25.

WIMBO 94 Kulithamini Neno la Mungu