Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Vasco da Gama Nilifurahia sana ile makala “Safari ya Baharini Yenye Kutokeza ya Vasco da Gama.” (Machi 22, 1999) Ilielezwa vizuri sana na ilikuwa yenye kuarifu. Mwataja kwamba alikuwa na meli tatu ndogo katika safari yake ya baharini, lakini kwa hakika zilikuwa nne. Pia, mnasema kwamba Da Gama alirudi Lisbon Septemba 8, 1499. Hata hivyo, aliwasili kuelekea mwisho wa Agosti.

P. N., Kenya

Ni kweli kwamba safari ya Da Gama ilianza na meli nne. Hata hivyo, sehemu ya safari ya baharini inayosimuliwa katika utangulizi ilitukia baada ya meli ya nne kuharibiwa. Kwa habari ya tarehe yake ya kuwasili huko Lisbon, vyanzo vingi husema ni mwanzo-mwanzo wa Septemba. Kwa kupendeza, kitabu “Portugal and the Discoveries” chasema: “Vasco da Gama aliwasili mnamo au karibu na Agosti 29, akipokewa kwa njia inayofaa na Mfalme mnamo Septemba 8.” Hili laweza kupatanisha jambo hilo linaloonekana kuwa hitilafu.—Mhariri.

 

 

Comenius Ninafunza kikundi cha watu wazima kusoma. Makala yenu bora kabisa “Comenius—Mwanzilishi wa Elimu ya Kisasa” (Mei 8, 1999) ilinisaidia kuelewa kwa nini wengine walikuwa na matatizo ya kujifunza. Habari iliyo kwenye sanduku linaloandamana nayo, “Baadhi ya Kanuni za Kufundisha za John Comenius,” zitasaidia sana.

N. A. F., Brazili

Asanteni sana kwa makala hiyo yenye kuarifu. Nilijifunza mengi kuhusu Comenius kutoka kwa kurasa nne za Amkeni! kuliko niliyokuwa nimejifunza kutoka kwa mihadhara kumi wakati wa mafunzo yangu kwenye chuo kikuu.

H. P., Ujerumani

Biblia ya Wazaliwa wa Amerika Niliposoma ile makala “Wazaliwa wa Amerika na Biblia” (Mei 8, 1999), upendezi wangu ulichochewa hasa na marejezo yenu kwa Biblia ya John Eliot kwa ajili ya Wahindi wa Massachusett. Mimi na mume wangu tuliona nakala ya Biblia hiyo tulipotembelea Maktaba ya Huntington huko San Marino, California. Ilikuwa imefunguliwa kwenye kitabu cha Zaburi, na jina Yehova lilionekana kwa kurudiwa-rudiwa. Ilisisimua jinsi gani kuona jina la Mungu katika Biblia hii ya karne ya 17!

B. J., Marekani

Kuajiriwa kwa Watoto Asanteni kwa ule mfululizo wa makala “Kuajiriwa kwa Watoto—Mwisho Wake Wakaribia!” (Mei 22, 1999) Nilipoona jalada kwa mara ya kwanza, maoni yangu kwa kweli yalikuwa makala hizi hazihusu nchi yangu. Lakini mara tu nilipoanza kuzisoma, sikuweza kuacha. Kusema wazi, niliogopeshwa. Hivi karibuni nilinunua mwanasesere wa dubu aliyefumwa kwa mkono kwa bei ya chini zaidi kuliko kiasi ambacho angegharimu iwapo angetengenezewa Japani. Ni jambo la kuhuzunisha kufikiri kwamba watoto wachanga wanatendwa kinyama ili kupata vitu kwa bei nafuu.

S. O., Japani

Uzito Nina umri wa miaka kumi. Asanteni kwa ile makala “Vijana Huuliza . . . Naweza Kushindaje Kuhangaikia Sana Uzito?” (Mei 22, 1999) Sikuzote nimejifikiria kuwa mzito sana. Baada ya kusoma makala hii nilikuja kuelewa kwamba umbo la mtu si ndilo jambo la maana. Jambo la maana zaidi ni sifa zake.

M. S., Urusi