Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maoni Yaliyosawazika juu ya Desturi Zinazopendwa

Maoni Yaliyosawazika juu ya Desturi Zinazopendwa

Maoni ya Biblia

Maoni Yaliyosawazika juu ya Desturi Zinazopendwa

“KILA ZOEA LIMEPATA KUSHUTUMIWA MAHALI FULANI NA PINDI FULANI, NA KATIKA PINDI NYINGINE NA MAHALI PENGINE LIKAONWA KUWA WAJIBU.”

KWA maoni hayo, mwanahistoria Muairishi William Lecky aeleza hali ya mwanadamu ya ugeugeu. Maelezo yake yaweza kuhusu pia desturi na mapokeo ya muda mrefu. Kwa kweli, mazoea mengi yaliyoonwa kuwa muhimu katika maisha ya kila siku yameshutumiwa baadaye. Si ajabu, kwa kuwa “mandhari ya ulimwengu huu inabadilika” kama alivyosema mtume Mkristo Paulo. —1 Wakorintho 7:31.

Naam, jamii ya kibinadamu hubadilika-badilika daima. Mara nyingi hilo hudhihirishwa na kubadilika sana kwa maoni na mazoea ya kijamii. Wakristo hawapaswi kuwa “sehemu ya ulimwengu”—yaani, wanajitenga na jamii ya kibinadamu iliyojitenga na Mungu. Hata hivyo, Biblia hukiri kwamba Wakristo wamo “ulimwenguni,” na haiwaamuru wajitenge na watu. Kwa hiyo, ni muhimu kuwa na maoni yaliyosawazika juu ya desturi.—Yohana 17:11, 14-16; 2 Wakorintho 6:14-17; Waefeso 4:17-19; 2 Petro 2:20.

Desturi Ni Nini?

Desturi ni mazoea yanayohusu maisha ya jamii na ambayo yanafuatwa na watu wa tabaka au mahali mahususi. Desturi fulani, kama vile adabu na taratibu za wakati wa mlo, huenda zilianzishwa kwa sababu ya uhitaji wa kuelekeza tabia ya watu katika utendaji wa kikundi, na kuwawezesha wachangamane kwa adabu na heshima. Katika hali hizo, adabu ya kijamii yaweza kulinganishwa na mafuta, kwa sababu inalainisha mahusiano ya kibinadamu.

Desturi zimeathiriwa sana na dini. Kwa kweli, desturi nyingi zilitokana na ushirikina wa kale na mawazo ya kidini yasiyo ya Kibiblia. Mathalani, kuwapa watu waliofiwa maua huenda kulitokana na ushirikina wa kidini. * Kwa kuongezea, rangi ya buluu—inayoshirikishwa kwa kawaida na watoto wavulana—ilidhaniwa kuwa ilifukuza roho waovu. Wanja ulitumiwa kuwa ulinzi dhidi ya kijicho, ilhali rangi ya midomo ilizuia roho waovu kuingia katika kinywa cha mwanamke na kumpagawa. Hata desturi ndogo kama vile kufunika kinywa unapopiga mwayo huenda ilitokana na wazo la kwamba nafsi ya mtu inaweza kutoroka kupitia kinywa kilicho wazi. Hata hivyo, ushirika wa kidini umetoweka baada ya muda, na mazoea na desturi hizo hazina maana yoyote ya kidini leo.

Linalowahangaisha Wakristo

Mkristo alazimikapo kuamua iwapo atafuata au hatafuata desturi fulani, anapaswa kuhangaikia sana swali hili, Maoni ya Mungu yaliyoonyeshwa kwenye Biblia ni yapi? Hapo awali Mungu alishutumu mazoea fulani ambayo huenda yalikubaliwa katika jamii nyingine. Yalitia ndani kudhabihu watoto, matumizi mabaya ya damu, na mazoea mbalimbali ya kingono. (Mambo ya Walawi 17:13, 14; 18:1-30; Kumbukumbu la Torati 18:10) Hali kadhalika, mazoea fulani ya kawaida leo kwa wazi hayapatani na kanuni za Biblia. Miongoni mwake ni mapokeo yasiyo ya Kibiblia yanayohusiana na sikukuu za kidini kama vile Krismasi na Ista au na mazoea ya kishirikina yanayohusiana na uwasiliani-roho.

Lakini namna gani desturi ambazo huenda awali zilihusiana na mazoea yenye kutiliwa shaka na ambazo leo zinaonwa kuwa adabu ya kawaida? Kwa mfano, desturi nyingi za arusi zinazopendwa—kutia ndani kuvishana pete na ulaji wa keki—huenda zilianzishwa na wapagani. Je, hilo lamaanisha kwamba Wakristo hawapaswi kuzingatia desturi hizo? Je, Wakristo wapaswa kuchunguza kwa makini kila desturi katika jamii ili kuona endapo haikufaa mahali fulani au wakati fulani?

Paulo asema kwamba “iliko roho ya Yehova, kuna uhuru.” (2 Wakorintho 3:17; Yakobo 1:25) Mungu hataki tutumie uhuru huu kuwa kichocheo cha tamaa za ubinafsi, bali tuzoeze nguvu zetu za ufahamu kutofautisha lililo sahihi na lililo kosa. (Wagalatia 5:13; Waebrania 5:14; 1 Petro 2:16) Kwa hiyo, kuhusu jambo ambalo kwa wazi halivunji kanuni za Biblia, Mashahidi wa Yehova hawatokezi sheria isiyobadilika. Badala yake, ni lazima kila Mkristo achunguze kwa uangalifu hali inayohusika na kufanya uamuzi wake binafsi.

Tafuta Faida ya Wengine

Je, hili lamaanisha kwamba inafaa sikuzote kushiriki desturi fulani maadamu haikiuki mafundisho ya Biblia moja kwa moja? La. (Wagalatia 5:13) Paulo alisema kwamba Mkristo apaswa kutafuta si faida yake mwenyewe “bali ile ya walio wengi.” Yeye apaswa ‘kufanya mambo yote kwa utukufu wa Mungu’ na kuepuka kuwa sababu ya kuwakwaza wengine. (1 Wakorintho 10:31-33) Kwa hiyo, mtu anayetafuta kibali cha Mungu atajiuliza hivi: ‘Wengine huionaje desturi hii? Je, jumuiya huihusianisha na mambo yenye kuchukiza? Je, kuishiriki kutadokeza kwamba ninaunga mkono mazoea au mawazo yasiyompendeza Mungu?’—1 Wakorintho 9:19, 23; 10:23, 24.

Ijapokuwa kwa ujumla hazidhuru, desturi fulani zinazofuatwa na jamii inayotuzunguka zaweza kuzoewa kwa njia inayopingana na kanuni za Biblia. Kwa mfano, kutoa maua kwenye pindi fulani mahususi huenda kukawa na maana ya pekee inayopingana na mafundisho ya Biblia. Kwa hiyo, Mkristo apaswa kuhangaikia nini hasa? Japo kwaweza kuwa na sababu ya kuchunguza mwanzo wa desturi hususa, wakati mwingine ni muhimu zaidi kuzingatia desturi hiyo humaanisha nini kwa watu wakati huo na mahali unapoishi. Ikiwa desturi ina maana isiyo ya Kimaandiko au isiyofaa katika pindi fulani ya mwaka au katika hali fulani, Wakristo waweza kuamua kwa busara kuiepuka wakati huo.

Paulo alisali kwamba upendo wa Wakristo upate kuzidi pamoja na ujuzi sahihi na ufahamu kamili. Kwa kuwa na maoni yaliyosawazika juu ya desturi zinazopendwa, Wakristo ‘huhakikisha mambo yaliyo ya maana zaidi, ili wapate kuwa bila dosari na kutowakwaza wengine.’ (Wafilipi 1:9, 10) Wakati huohuo, ‘hali yao ya kukubali sababu itajulikana kwa watu wote.’—Wafilipi 4:5.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Kulingana na wanaanthropolojia fulani, shada za maua zilitolewa kwa wafu nyakati nyingine ili kuwazuia wasisumbue walio hai.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Desturi fulani za kale, kama vile kufunika kinywa unapopiga mwayo na kuwapa watu waliofiwa maua, zimepoteza maana yake ya awali