Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Uzito Ninataka kuwashukuru kwa moyo wote kwa ile makala “Vijana Huuliza . . . Naweza Kushindaje Kuhangaikia Sana Uzito?” (Mei 22, 1999) Kwa muda fulani sasa, nimekuwa nikifikiria tu kuhusu umbo langu na uzito wangu. Ninapojitazama kwenye kioo mimi hujiaibikia, na siku hizi sijipimi uzito kwa ukawaida. Lakini, baada ya kusoma makala hii, nilitambua kwamba ni utu wa ndani ulio wa maana.

L. R., Ufaransa

Ulemavu Mimi hutumia muda mwingi kwenye kiti chenye magurudumu. Mke wangu ana ugonjwa wa uchovu wenye kudumu na pia mshuko-moyo mbaya sana. Ule mfululizo “Tumaini kwa Walemavu” (Juni 8, 1999) ulionyesha kwamba huzuni ni itikio la kawaida baada ya kupatwa na mapungukio makubwa. Pia, picha kwenye ile makala “Ulemavu Wote Utakapotoweka” zilinisadikishia kwamba kuponywa kwa ulemavu tulio nao ni jambo hakika.

C. W., Marekani

Nilipoteza wayo wangu wa kushoto katika aksidenti ya gari nilipokuwa na umri wa miaka minne tu. Mfululizo wenu ulinisaidia kuweza kukabiliana na vipindi vingi vya mshuko-moyo. Tafadhali endeleeni na kazi yenu nzuri ya kushinda upendeleo.

A.J.T.P., Brazili

Watu wanahitaji kujua kwamba walemavu wana hisia na hisia-moyo kama watu wengine na kwamba wanaweza kuumizwa nao huumia. Wakati mwingine watu huona kana kwamba wewe ni mtu asiye wa kawaida na kusema maneno yasiyo na fadhili, au kutenda kana kwamba haupo. Walemavu si wajinga wala wavivu wala wasiojiweza. Wengi wetu tukipewa fursa tunaweza kupika, kusafisha, kununua vitu, kutunza familia, kudumu kazini, na hata kuendesha gari. Jambo moja ambalo limenisaidia kuendelea ni kujifunza kuhusu Yehova na njia zake zenye fadhili na upendo. Kwa sasa mimi si mmoja wa Mashahidi wa Yehova lakini natumaini kuwa shahidi wakati ujao.

A. G., Marekani

Thamani Machoni pa Mungu Mara nyingi mimi huhisi nikiwa nimeshuka moyo na asiyefaa, wakati mwingine hata hufikiria kuwa sistahili kuwa mweneza-evanjeli wa wakati wote kwa sababu jitihada zangu hazitoshi. Ile makala “Maoni ya Biblia: Una Thamani Machoni pa Mungu!” (Juni 8, 1999) ilinifanya nihisi vema zaidi. Ilinisaidia kuona kwamba Shetani hujaribu kwa bidii kutufanya tuhisi hivyo ili atufanye tuache kumtumikia Yehova.

L. W., Kanada

Makala hiyo ilikuwa yenye kufariji sana. Kufikia sasa, nimekuwa nikihisi kana kwamba Yehova hakuwa akisikiliza sala zangu. Lakini tangu niliposoma makala yenu, nimekuwa na uhakika zaidi kwa Yehova na kwangu mwenyewe. Tafadhali endeleeni kuchapisha makala zenye kufariji kama hiyo.

R. V.T., Ubelgiji

Nina makovu ya mambo machungu niliyoyapitia—makosa ambayo yamenipokonya hali yangu ya kujistahi. Leo uhusiano wangu na Yehova na ujuzi wa kwamba upendo wake unapita ufahamivu wa binadamu hunipa hisia ya furaha na usalama.

V.S.C., Brazili

Nimemaliza kusikiliza makala hiyo kwenye kaseti. Nimekuwa kipofu kwa miaka 44 hivi, na hata baada ya kubatizwa kuwa Mkristo, sikufikiria kuwa nilikuwa na thamani sana. Makala hii ilinigusa moyo sana. Namshukuru Mungu sana kwa sababu hatuoni jinsi tunavyojiona wenyewe.

A. K., Italia

Nimekumbwa sana na hisia zisizofaa. Lakini kadiri nilivyoendelea kusoma makala hiyo, ilikuwa ni kana kwamba Yehova alikuwa akizungumza nami kwa uanana. Ni vigumu sana kubadili namna ya kufikiri, lakini nitajaribu kutosahau vile makala hiyo ilivyosema: “Yehova, kama mzazi mwenye upendo, ‘yu karibu’—akituchunguza daima, akitupa uangalifu, na tayari kusaidia.—Zaburi 147:1, 3.”

K. F., Japani