Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Naweza Kuepukaje Hatari Katika Internet?

Naweza Kuepukaje Hatari Katika Internet?

Vijana Huuliza . . .

Naweza Kuepukaje Hatari Katika Internet?

JIWAZIE ukiwa katika maktaba kubwa zaidi ulimwenguni. Unazingirwa na vitabu, magazeti, katalogi, picha, na rekodi za kila namna—zinazozungumzia karibu kila jambo. Waweza kupokea mara moja habari yote ya karibuni na hata vichapo vya karne zilizopita.

Kwa kweli, waweza kupokea habari hizo zote mara moja kwenye Internet. * Humwezesha mtu atumie kompyuta yake kuwasiliana na kompyuta nyingine na watumiaji wengine wa kompyuta mahali popote ulimwenguni. Huwawezesha watumiaji wauze na kununua bidhaa, waendeshe shughuli za benki, wazungumze, wasikilize miziki ya karibuni zaidi—wafanye yote hayo faraghani katika nyumba zao.

Si ajabu kwamba, wataalamu fulani wanatabiri ya kuwa zaidi ya watu milioni 320 watakuwa wakitumia Internet mwishoni mwa mwaka huu. Hivyo, kutumia Internet kumeanza kuenea katika sehemu nyingi ulimwenguni. Mamilioni ya vijana wanaitumia kwa sababu ya juhudi kabambe za shule na maktaba za kuendeleza utumiaji wake. Huko Marekani, takriban asilimia 65 ya vijana wenye umri wa kati ya miaka 12 na 19 tayari wameitumia au ni wateja wa huduma za Internet.

Internet itumiwapo kwa njia inayofaa inaweza kuwa chanzo cha habari muhimu ya halihewa, usafiri, na mambo mengineyo. Unaweza kununua vitabu, spea za gari, na vitu vinginevyo kupitia Internet. Wengi huitumia kufanya mazoezi ya shule.

Ingawa Internet yaweza kuwa yenye mafaa, yaweza pia kuwa kama maktaba isiyokuwa na wakutubi au watazamaji wengine. Mtu aweza kupitia-pitia vitabu akihisi kwamba hakuna mtu mwingine yeyote karibu. Lakini hii ni mojawapo ya hatari kubwa zaidi za kutumia Internet. Kwa nini? Kwa sababu Web site nyingi zina habari zinazopotosha maadili na zenye kuangamiza kiroho. Hivyo, Internet yaweza kuwatia vijana Wakristo katika kishawishi. Kwa vyovyote vile, wanadamu ni wadadisi kwa asili—naye Shetani Ibilisi ametumia mwelekeo huo kujifaidi kwa muda mrefu. Bila shaka Shetani alitumia udadisi wa Hawa na ‘akamshawishi kwa ujanja wake.’—2 Wakorintho 11:3.

Vivyo hivyo, endapo kijana Mkristo hataazimia kulinda hali yake ya kiroho anaweza kushawishwa kwa urahisi na habari isiyofaa. Makala moja katika kichapo Better Homes and Gardens ilieleza hivi: “Internet ni fani yenye kusisimua inayotumiwa na wabunifu werevu ili kusambaza habari mpya; hata hivyo watu wanaovutiwa na watoto kingono, walaghai, washupavu, na watu wengine wafidhuli hutumia pia Internet.”

Kijana aitwaye Javier * asema: “Web site fulani zinashtua. Zaweza kuzuka ghafula bila onyo.” Aongezea: “Zinajaribu kukunasa. Zinataka kukushawishi—ili zitwae fedha zako.” Kijana Mkristo aitwaye John akiri: “Mara tu unapoanza kutazama habari isiyofaa, ni vigumu kuacha—inakuvutia sana.” Baadhi ya vijana Wakristo wamekuwa wakitazama Web site fulani zisizofaa, na hilo limewatumbukiza katika matatizo makubwa sana. Wengine hata wameharibu uhusiano wao na Yehova. Hilo laweza kuepukwaje?

‘Kutazama Visivyofaa’

Nyakati nyingine anwani tu ya Web site huonyesha waziwazi kwamba ina habari zenye kuchukiza. * Mithali 22:3 huonya hivi: “Mwenye busara huyaona mabaya na kujificha; bali wajinga huendelea mbele wakaumia.”

Ingawa kwa kawaida, tatizo ni kwamba watu wanaweza kufungua Web site yenye kuchukiza bila kutarajia. Sehemu ya home page yaweza kuwa na picha zenye kutisha zilizochorwa kwa uangalifu ili kuweza kukushawishi uchunguze Web site hiyo—na kuitazama tena na tena! *

Kevin aeleza kilichompata rafikiye mmoja: “Hakuwa na kazi ya kufanya naye alikuwa mdadisi. Punde si punde akazoea kutazama ponografia.” Jambo la kupendeza ni kwamba kijana huyo Mkristo alimwendea mzee na kupata msaada.

Je, umeazimia utakavyotenda iwapo utafungua kimakosa Web site ya aina hiyo? Jambo ambalo Mkristo anapaswa kutenda ni dhahiri: Funga Web site hiyo mara moja—au funga kabisa programu inayokuelekeza kwenye Internet! Uwe kama mtunga-zaburi aliyesali hivi: “Unigeuze macho yangu nisitazame visivyofaa.” (Zaburi 119:37; linganisha Ayubu 31:1.) Kumbuka kwamba hata ikiwa hakuna mwanadamu mwingine anayetuchunguza, kuna mwingine anayetuona. Biblia hutukumbusha kwamba vitu vyote viko “uchi na vikiwa vimefunuliwa wazi machoni pake ambaye kwake sisi tuna kutoa hesabu.”—Waebrania 4:13.

Kuzungumza na wazazi wako au na Wakristo wengine wakomavu kwaweza kuimarisha azimio lako la kutotazama tena Web site zisizofaa. Kwa vyovyote vile, endapo ungetumbukia katika mchanga-didimizi, je, ungekazana hadi uzamapo kufikia shingoni ndipo uombe msaada?

Namna Gani juu ya Ushirika Kwenye Internet?

Vituo vya maongezi huwawezesha watumiaji wa Internet ulimwenguni kote wawasiliane wakati mmoja. Mashirika ya kibiashara huvitumia kufanya mikutano kwenye Internet na kuwahudumia wateja. Vituo fulani vya maongezi huwawezesha watumiaji wajadili habari za kiufundi, kama vile urekebishaji-magari au utayarishaji wa programu za kompyuta. Vituo fulani vya maongezi huwezesha marafiki na washiriki wa familia wawasiliane kwa faragha pasipo gharama za kupiga simu mbali. Ingawa kwaweza kuwa na sababu nzuri za kutumia mfumo huo, je, kuna hatari zozote?

Kuna uhitaji mkubwa wa kutahadhari inapohusu vituo vya maongezi ya umma, kwani vituo hivi vyaweza kuwa na hatari fulani. Mwandikaji Leah Rozen alisema hivi: “Vijana walio na ujuzi wa tekinolojia wanatumia wakati mwingi wakizungumza kwa Internet na watu wasiowajua kutoka kila mahali nchini na, hata ulimwenguni. Kwa kusikitisha, baadhi ya watu hao wasiojulikana ambao vijana wanawasiliana nao kwenye Internet ni watu wazima wapotovu wanaotafuta miadi ya kingono na watoto.” Makala moja katika kichapo Popular Mechanics yaonya kuwa “unahitaji kuwa mwangalifu sana” unapotumia vituo vya maongezi ya umma. Kumpa mtu usiyemjua jina au anwani yako kwaweza kukuletea matatizo makubwa! Kwa nini ujihatarishe?

Hata hivyo, hatari isiyoonekana inahusiana na kushirikiana isivyofaa na watu usiowajua ambao hawastahi kanuni za Biblia. * Watafiti wanasema kwamba mazungumzo mengi ya vijana katika vituo vya maongezi hukazia sana masuala ya ngono. Hivyo shauri la Biblia katika 1 Wakorintho 15:33 linafaa: “Msiongozwe vibaya. Mashirika mabaya huharibu mazoea yenye mafaa.” Mashirika mabaya kupitia kwa mawasiliano ya kompyuta ni hatari. Je, kijana anayemhofu Mungu apaswa kujihatarisha kwa njia hiyo bila kujali?

Ulinzi

Ni lazima Internet itumiwe kwa tahadhari kwa sababu ya hatari zake. Kwa kielelezo, familia fulani huweka kompyuta mahali palipo wazi, kama vile sebuleni. Waweza hata kuweka sheria ya kwamba Internet yapasa kutumiwa wengine wanapokuwa nyumbani. Shirikiana na wazazi wako wanapoweka vizuizi kama hivyo. (Mithali 1:8) Miongozo iliyo wazi huthibitisha upendo wao.

Iwapo ni lazima utumie Internet kufanya mazoezi ya shule, mbona usipime wakati unaotumia? Jaribu kuamua kimbele muda utakaotumia, saa ya kengele yaweza kukumbusha muda unapokwisha. Tom adokeza hivi: “Panga kimbele, fahamu kikamili habari unayotafuta, shikamana na mpango huo—hata mambo mengine yawe yenye kuvutia namna gani.”

Tahadhari yahitajiwa pia inapohusu matumizi ya E-mail. Vijana Wakristo huwa waangalifu kuhusu kusoma mno kiasi kikubwa cha E-mail, hasa inapokuwa na habari nyingi za kipuuzi au zisizo sahihi. Kutumia E-mail kupita kiasi kwaweza kupoteza wakati muhimu unaohitajiwa kwa ajili ya mazoezi ya shule na utendaji wa kiroho.

Mfalme Solomoni alisema: “Hakuna mwisho wo wote wa kutunga vitabu vingi; na kusoma sana huuchosha mwili.” (Mhubiri 12:12) Maneno hayo yaweza kuhusu Internet pia. Usitafute mno mambo hakika na tarakimu hata upuuze funzo la kibinafsi la Biblia na kushiriki huduma ya Kikristo. (Mathayo 24:14; Yohana 17:3; Waefeso 5:15, 16) Kumbuka pia kwamba ingawa mawasiliano ya kompyuta yana mahali pake, hakuna jambo linalochukua mahali pa kuonana uso kwa uso na Wakristo wenzetu. Kwa hiyo ikiwa unahitaji kikweli kutumia Internet, fanya uamuzi thabiti wa kuitumia kwa hekima. Epuka Web site hatari, na usitumie wakati mwingi kupita kiasi kwenye Internet. “Linda moyo wako,” na usiwe kamwe mtumwa wa Internet.—Mithali 4:23.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Ona mfululizo Internet—Je, Yakufaa?” katika toleo la Amkeni! la Julai 22, 1997.

^ fu. 9 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

^ fu. 11 Anwani ya Web-site ni herufi zinazofuatana zinazotumiwa ili kufungua Web site. Nyakati nyingine anwani huwa na maneno yanayotambulisha kusudi la Web site hiyo.

^ fu. 12 Sehemu ya home page ni kama njia ya elektroni ya kufikia yaliyomo. Hueleza mambo yaliyo katika Web site hiyo, aliyeibuni, na kadhalika.

^ fu. 19 Hatari kama hizo zaweza kuwako katika vituo vya maongezi ya umma vilivyoanzishwa na Wakristo wenye nia nzuri kwa madhumuni ya kuzungumzia mambo ya kiroho. Watu wasio-haki na waasi-imani nyakati nyingine wamejiunga na mazungumzo hayo na kwa njia ya siri wamejaribu kuwashawishi wengine wakubali mawazo yao yasiyo ya Kimaandiko.

[Blabu katika ukurasa wa 20]

“Web site fulani zinashtua. Zaweza kuzuka ghafula bila onyo”

[Blabu katika ukurasa wa 21]

Familia fulani huweka kompyuta mahali palipo wazi