Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kusema Uwongo—Je, Kwaweza Kutetewa Wakati Wowote?

Kusema Uwongo—Je, Kwaweza Kutetewa Wakati Wowote?

Maoni ya Biblia

Kusema Uwongo—Je, Kwaweza Kutetewa Wakati Wowote?

“HABARI ISIYO SAHIHI KIDOGO WAKATI MWINGINE HUZUIA MAELEZO MENGI.”

ELEZO hilo laonyesha jinsi watu wengi wanavyohisi kuhusu kusema uwongo. Sababu yao ya msingi ni kwamba si vibaya kusema uwongo ikiwa haudhuru mtu yeyote. Hata kusababu huko kuna jina la kitaalamu—kufikiria hali bila kuzingatia maadili, jina linalosema kwamba sheria pekee unayohitaji kufuata ni ile inayoitwa eti sheria ya upendo. Yaani, aeleza mwandishi Diane Komp, “ikiwa kichocheo na nia yako ni sawa (basi) uhakika wa kwamba umesema uwongo . . . si jambo la maana.”

Maoni hayo ni ya kawaida katika ulimwengu wa leo. Kashfa zinazohusu uwongo uliosemwa na wanasiasa mashuhuri na viongozi wengine wa ulimwengu zimeshtua jamii. Kwa kuathiriwa na mazingira ya namna hiyo, watu wengi hawaoni uzito wa kusema kweli. Katika maeneo fulani kusema uwongo hata kumekuwa sera rasmi. “Ninalipwa ili kusema uwongo. Kila mwaka mimi hushinda mashindano ya kibiashara na kusifiwa sana na magazeti ninaposema uwongo. . . . Hii yaonekana kuwa sehemu kuu ya mazoezi ya biashara ya rejareja kila mahali,” alalamika karani mmoja wa mauzo. Wengi wanaamini kwamba hakuna ubaya wowote katika ule unaoitwa eti uwongo mdogo wa kujiokoa. Je, hiyo ni kweli? Je, kuna pindi ambazo Wakristo waweza kuwa na sababu halali ya kusema uwongo?

Kiwango cha Biblia Kilichokwezwa

Biblia hushutumu kwa dhati namna zote za uwongo. “[Mungu] ataharibu wasemao uongo,” atangaza mtunga-zaburi. (Zaburi 5:6; ona Ufunuo 22:15.) Kwenye Mithali 6:16-19, Biblia inaorodhesha vitu saba vinavyomchukiza Yehova. “Ulimi wa uongo” na “shahidi wa uongo asemaye uongo” vinatajwa waziwazi katika orodha hiyo. Kwa nini? Kwa sababu Yehova huchukia madhara yanayosababishwa na uwongo. Hiyo ni sababu moja iliyomfanya Yesu amwite Shetani mwongo na muua-binadamu. Uwongo wake ulitumbukiza jamii ya binadamu katika taabu na kifo.—Mwanzo 3:4, 5; Yohana 8:44; Waroma 5:12.

Kisa kilichowapata Anania na Safira hukazia jinsi ambavyo Yehova huona kusema uwongo kuwa jambo zito. Watu hao wawili walisema uwongo kimakusudi mbele za mitume wakijaribu kujionyesha kuwa wakarimu sana kuliko walivyokuwa. Tendo lao lilikuwa la kimakusudi na lililopangwa kimbele. Hivyo mtume Petro alitangaza hivi: “Umefanya isivyo kweli, si kwa wanadamu, bali kwa Mungu.” Kwa sababu hiyo, wote wawili waliangamizwa na Mungu.—Matendo 5:1-10.

Miaka mingi baadaye mtume Paulo aliwaonya Wakristo kwa upole hivi: “Msiwe mkiambiana uwongo.” (Wakolosai 3:9) Himizo hilo ni muhimu hasa katika kutaniko la Kikristo. Yesu alisema kwamba upendo unaoongozwa na kanuni ungekuwa alama ya kutambulisha wafuasi wake wa kweli. (Yohana 13:34, 35) Upendo huo usio na unafiki unaweza kukua na kusitawi tu katika hali zenye ufuatiaji-haki na itibari kamili. Ni vigumu kumpenda mtu ikiwa hatuwezi kuwa na hakika kwamba atatuambia kweli sikuzote.

Ingawa uwongo wote unashutumiwa, uwongo fulani huwa na uzito kuliko mwingine. Kwa mfano, huenda mtu fulani akasema uwongo kwa sababu ya aibu au hofu. Huenda mwingine akawa na zoea la kusema uwongo akiwa na nia ya kudhuru. Kwa sababu ya nia yake ya kudhuru, mwongo huyo wa kukusudia huhatarisha wengine na hata angetengwa na ushirika wa kutaniko asipotubu. Kwa kuwa uwongo wote hauwi wenye nia ya kudhuru, lazima kuwa waangalifu kutolaumu isivyo lazima bali kuwa na hakika kwamba umefahamu mambo yote yanayohusika mtu fulani anaposema uwongo. Nia na hali zisizo za kawaida zapasa kufikiriwa.—Yakobo 2:13.

“Wenye Hadhari Kama Nyoka”

Bila shaka, kusema kweli hakumaanishi kwamba tunawajibika kufunua habari zote kwa mtu yeyote anayetuuliza. “Msiwape mbwa kilicho kitakatifu, wala msitupe lulu zenu mbele ya nguruwe, ili wasipate kamwe . . . kugeuka kabisa na kuwararua nyinyi,” akaonya Yesu, kwenye Mathayo 7:6. Kwa mfano, huenda watu wenye nia mbovu wasiwe na haki ya kujua mambo fulani. Wakristo wanaelewa kwamba wanaishi katika ulimwengu wenye uhasama. Hivyo, Yesu alishauri wanafunzi wake wawe “wenye hadhari kama nyoka” na bado wakiwa ‘bila hatia kama njiwa.’ (Mathayo 10:16; Yohana 15:19) Yesu hakufunua ukweli wote daima, hasa wakati kufunua mambo yote kungeleta madhara yasiyo ya lazima kwake yeye au kwa wanafunzi wake. Na bado, hata katika pindi hizo, hakusema uwongo. Badala yake, aliamua kunyamaza au kubadili kichwa cha mazungumzo.—Mathayo 15:1-6; 21:23-27; Yohana 7:3-10.

Wanaume na wanawake waaminifu wanaotajwa katika Biblia, kama vile Abrahamu, Isaka, Rahabu, na Daudi, vilevile walikuwa na busara na wenye hadhari walipokuwa wakishughulika na watu ambao wangeweza kuwa maadui. (Mwanzo 20:11-13; 26:9; Yoshua 2:1-6; 1 Samweli 21:10-14) Biblia huwataja wanaume na wanawake hao kuwa waabudu waaminifu ambao maisha yao yalionyesha utii. Jambo hilo lafanya wastahili kuigwa.—Waroma 15:4; Waebrania 11:8-10, 20, 31, 32-39.

Huenda kukawa na nyakati ambapo kusema uwongo huonekana kukitokeza utatuzi rahisi. Lakini Wakristo leo hufanya vyema kumwiga Yesu na kutii dhamiri yao iliyozoezwa na Biblia wanapokabili hali ngumu hasa.—Waebrania 5:14.

Biblia hututia moyo tuseme kweli na kufuatia haki. Kusema uwongo ni kosa, na twapaswa kufuata shauri la Biblia: “Semeni kweli kila mmoja wenu pamoja na jirani yake.” (Waefeso 4:25) Kwa kufanya hivyo, tutadumisha dhamiri safi, tutaendeleza amani na upendo katika kutaniko, na kuendelea kumheshimu “Mungu wa kweli.”—Zaburi 31:5; Waebrania 13:18.

[Picha katika ukurasa wa 20]

Anania na Safira walikufa kwa sababu ya kusema uwongo