Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Mitindo ya Maisha Isiyofaa Katika miezi michache iliyopita, afya yangu imezorota sana, kwa hiyo nilitiwa moyo kujua kwamba tunaweza kuboresha afya yetu kwa kubadili mtindo wetu wa maisha. Niliposoma mfululizo wa makala “Je, Mtindo Wako wa Maisha Unakuua?” (Julai 8, 1999) niliona uhitaji wa kupunguza kula vyakula fulani na kula mlo kamili unaotia ndani matunda na mboga zaidi.

E. P. M., Brazili

Itikio Lililokawia Nilitiwa moyo na makala “Mbegu Zilizozaa Matunda Miaka Mingi Baadaye.” (Julai 8, 1999) Huu ni mwaka wangu wa tatu nikiwa mweneza-evanjeli wa wakati wote, na ninapokosa kupata matokeo niliyotarajia, mimi huvunjika moyo na kukosa nia ya kuendelea. Kusoma makala haya kumenisaidia kufanya yaliyo bora zaidi sasa, nikimwachia Yehova matokeo.

T. N., Japani

Kudhihakiwa Vikali Nilifurahia makala ya Juni 22, 1999, “Vijana Huuliza . . . Naweza Kukabilianaje na Dhihaka Kali?” Tangu nilipokuwa katika shule ya watoto wadogo, wanashule wenzangu wameniuliza maswali kuhusu itikadi zangu. Nyakati nyingine wanaumiza hisia zangu kwa namna wanavyouliza. Nyakati nyingi nimekaribia kupoteza subira. Sasa natambua kwamba haya ni majaribu tu ya imani. Mbali na hilo, kuna wengine shuleni ambao nimewahubiria kwa mafanikio.

L. C., Marekani

Mimi pia nimedhihakiwa kwa kukataa kusherehekea sikukuu fulani za kidini au kujiunga na sherehe za kizalendo. Pia nimesumbuliwa kwa kuwa mwenye kufuatia haki na kwa kutegemeza viwango vya adili vya Biblia. Kutwaa ujuzi sahihi kumenisaidia kujitetea. Hilo hunisaidia kusema waziwazi bila kuona haya kueleza itikadi zangu.

H. C. Zambia

Ijapokuwa nilikuwa tineja zamani sana—nina umri wa miaka zaidi ya 50!—nilithamini makala hayo. Kuna nyakati ambapo upinzani tunaokabili kwenye huduma hutubabaisha na kutufanya tutake kulipiza kisasi. Ndiyo sababu nilithamini kikumbusha cha kwamba “jibu kali, hata liwe laonekana kuwa lafaa, litaongeza tu chuki na huenda hata likazidisha dhihaka.” Mimi hujaribu kujitetea bila kuonekana kuwa nalipiza kisasi, na kikumbusha hicho kilinisadikisha juu ya uhitaji wa kuendelea kufanya hivyo.

A. F., Marekani

Ishi Muda Mrefu Zaidi Nalazimika kutoa maoni kuhusu mfululizo wa makala zenu zenye kichwa “Jinsi ya Kuishi Muda Mrefu Ukiwa na Afya Bora.” (Julai 22, 1999) Hatimaye nimepata ufafanuzi unaohusu tofauti iliyopo kati ya muda wa kuishi wa wastani na taraja la kuishi. Pia, shauri zuri la jinsi ya kukabili madhara ya uzeeni ni vikumbusha ninavyoweza kuvitumia kwa busara kumsaidia babu yangu mwenye umri wa miaka 88, anayekabili hali ya kujisikitikia mara kwa mara.

T. N., Marekani

Mbwa Anayesikia Nataka kuwashukuru kwa ajili ya makala “Mbwa Wangu Husikiliza kwa Niaba Yangu!” (Julai 22, 1999) Kujua kwamba watu wenye matatizo ya kusikia wanakabili matatizo magumu namna hiyo kumenisaidia kuelewa hali zao zaidi. Nawapenda mbwa pia, kwa hiyo nilifurahi kujua jinsi wanavyoweza kutoa msaada na utegemezo kwa watu wengi.

L. B., Italia

Mimi pia hutegemea msaada wa mbwa. Mimi hutumia muda mwingi kwenye kiti chenye magurudumu, kwa kuwa uti wangu wa mgongo ni dhaifu na nina uyabisi wa misuli. Siwezi kueleza mambo yote ambayo mbwa wangu hunifanyia. Hunisaidia ninaponunua vitu au ninaposafisha nyumba. Hunisaidia pia kwenye huduma ya Kikristo kwa kunibebea vichapo.

K. W., Marekani