Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Rafiki Yangu Aliniumiza?

Kwa Nini Rafiki Yangu Aliniumiza?

Vijana Huuliza . . .

Kwa Nini Rafiki Yangu Aliniumiza?

“Nilikuwa na marafiki kadhaa . . . Kisha wakaanzisha urafiki na msichana mmoja na nilipowakaribia, waliacha kuzungumza. . . . Wakaanza kunitenga kabisa. Niliumia hisia kwelikweli.”—Karen. *

INAWEZA kutukia kwa watu walio marafiki wakubwa sana. Siku moja hao wawili hawatengani; siku inayofuata hata hawazungumziani. “Rafiki apaswa kuwa mtu unayeweza kumtegemea na kumtumaini, mtu unayeweza kumwomba msaada chini ya hali zozote,” asema Nora mwenye umri wa miaka 17. Ingawa hivyo, nyakati fulani rafiki yako bora zaidi aweza kujiendesha kama adui yako mbaya zaidi.

Urafiki Watishwa

Ni nini hufanya urafiki wenye kupendeza ugeuke kuwa uhasama? Kuhusu Sandra, matatizo yalianza wakati rafiki yake Megan alipomwomba blauzi aliyoipenda sana. “Alipoirudisha,” asema Sandra, “ilikuwa chafu na ilikuwa imeraruka kidogo kwenye mkono. Hata hakutaja jambo hilo, ni kana kwamba singetambua.” Sandra alihisije kuhusu kukosa ufikirio kwa Megan? “Niliudhika kwelikweli,” asema. “Nilihisi kana kwamba haheshimu vitu vyangu . . . au hisia zangu.”

Unaweza kuumia pia ikiwa rafiki mkubwa afanya au asema jambo linalokuaibisha. Cindy alipatwa na jambo hilo alipoambia kikundi cha wanashule wenzi kwamba hakuwa amesoma kitabu ili kutayarisha taarifa yake. Kwa ghafula, rafiki yake Kate akaanza kumkemea. “Aliniaibisha mbele ya kikundi cha marafiki wangu,” akumbuka Cindy. “Alinikasirisha sana. Mambo yalibadilika kwelikweli baada ya hapo.”

Nyakati nyingine ugomvi hutokea rafiki anapoanza kushirikiana na waandamani wapya. “Nilikuwa na rafiki mzuri ambaye alijiunga na genge dogo,” asema Bonnie mwenye umri wa miaka 13. “Akaanza kunipuuza.” Au yawezekana unaanza kugundua kwamba rafiki yako hana nia inayofaa. “Mimi na Bobby tulikuwa marafiki wazuri kwelikweli,” asema Joe, mwenye umri wa miaka 13. “Nilifikiri alinipenda kwa sababu ya utu wangu, lakini nikagundua kwamba alinipenda tu kwa sababu baba yangu hutayarisha matangazo ya biashara na mara nyingi angeweza kupata tiketi nyingi za michezo na maonyesho.” Joe anahisije sasa? “Sitawahi kumtumaini Bobby tena!” asema.

Katika visa fulani huenda rafiki akawafunulia wengine habari uliyotaka ibaki ikiwa siri. Kwa mfano, Allison, alimtajia rafiki yake Sara tatizo la kibinafsi la mfanyakazi mwenzi. Siku iliyofuata Sara alitaja jambo hilo mbele ya mfanyakazi huyo. “Sikufikiri angeweza kuwa domokaya namna hiyo!” asema Allison. “Nilikasirika sana.” Rachel, mwenye umri wa miaka 16 alipatwa na jambo kama hilo wakati rafiki yake wa karibu alipotoboa siri ambayo waliizungumzia faraghani. “Nilihisi aibu na pia kusalitiwa,” asema Rachel. “Nilijiambia, ‘Nitawezaje kumwambia siri tena?’”

Urafiki unaweza kuwa chanzo cha utegemezo wa kihisia-moyo, hasa kunapokuwa na kufikiriana, kutumainiana, na kuheshimiana. Na bado, hata urafiki wa karibu unaweza kupatwa na mkazo. Biblia husema hivi waziwazi: “Ajifanyiaye rafiki wengi ni kwa uangamivu wake mwenyewe.” (Mithali 18:24) Bila kujali sababu ni gani, unaweza kuvunjika moyo sana unapohisi kwamba umesalitiwa na rafiki. Kwa nini hilo hutukia?

Sababu Zifanyazo Urafiki Uvunjike

Hakuna uhusiano wa binadamu—uwe ni wa vijana au wa watu wazima—usiokuwa na matatizo. Kwa vyovyote vile, ni kama mwanafunzi Mkristo Yakobo alivyoandika: “Sisi sote hujikwaa mara nyingi. Ikiwa yeyote hajikwai katika neno, huyu ni mtu mkamilifu, awezaye kuuongoza kwa hatamu mwili wake wote pia.” (Yakobo 3:2; 1 Yohana 1:8) Kwa kuwa kila mtu hukosea, inatarajiwa kwamba wakati fulani ujao rafiki atafanya jambo fulani au kusema neno litakalokuumiza. Huenda hata ukakumbuka pindi ambapo ulimwumiza mtu huyo vilevile. (Mhubiri 7:22) “Sisi sote sio wakamilifu, na tutawaudhi wengine pindi fulani fulani,” asema Lisa msichana mwenye umri wa miaka 20.

Licha ya kutokamilika kwa binadamu, kuna mambo mengine yanayoweza kuhusika. Kumbuka, unapokua na kukomaa, mapendezi yako—vilevile yale ya rafiki zako—hubadilika. Hivyo, watu wawili ambao wakati mmoja walishirikiana kwa mambo mengi huenda wakajikuta wakitengana hatua kwa hatua. Tineja mmoja aliomboleza hivi kuhusu rafiki yake wa karibu zaidi: “Hatupigiani simu mara nyingi na tunapozungumza, hatukubaliani katika jambo lolote tena.”

Bila shaka, kutengana ni jambo moja. Lakini kwa nini watu wengine huumiza rafiki zao? Mara nyingi wivu huhusika. Kwa mfano, huenda ikawa rafiki yako anakuonea uchungu kwa sababu ya vipawa vyako au mafanikio yako. (Linganisha Mwanzo 37:4; 1 Samweli 18:7-9.) Kama Biblia isemavyo, “husuda ni ubovu wa mifupa.” (Mithali 14:30) Hutokeza wivu na ugomvi. Bila kujali sababu ni gani, unaweza kufanya nini unapoumizwa na rafiki?

Kutatua Matatizo

“Kwanza,” asema Rachel, “ningemchunguza mtu huyo na kujaribu kujua kama alifanya jambo hilo kimakusudi.” Unapokasirishwa na neno au kitendo fulani unachokiona kuwa cha madharau, usitende tu kwa kuchochewa na hisia za wakati huo. Badala yake, uwe mwenye subira na ufikirie kiini cha jambo hilo. (Mithali 14:29) Je, kutenda kwa haraka kuelekea madharau uliyotambua kutaboresha hali kikweli? Baada ya kufikiria mambo, huenda ukachagua kufuata shauri la Zaburi 4:4: “Mwe na hofu wala msitende dhambi, tafakarini vitandani mwenu na kutulia.” Kisha huenda ukaamua kuruhusu ‘upendo ufunike wingi wa dhambi.’—1 Petro 4:8.

Ingawa hivyo, namna gani ukihisi kwamba huwezi kuachilia mwenendo wenye kuumiza? Katika kisa hicho, huenda ikafaa kumfikia mtu huyo. “Ketini pamoja, nyinyi wawili tu na kusuluhisha jambo lililotokea,” asema Frank mwenye umri wa miaka 13. “Usipofanya hivyo utafungia kinyongo.” Susan mwenye umri wa miaka 16, alikuwa na maoni hayohayo. “Jambo bora zaidi kufanya,” asema, “ni kumwambia kwamba ulimtumaini lakini akakufadhaisha.” Jacqueline pia hupendelea kusuluhisha mambo kwa kumfikia mtu binafsi. “Mimi hujaribu kusema mambo waziwazi,” asema. “Kwa kawaida, mtu huyo hukuambia mambo waziwazi na mnaweza kutatua matatizo karibu mara hiyohiyo.”

Bila shaka, unapaswa kujihadhari kutomwendea rafiki yako ukiwa na hasira. Biblia husema: “Mtu wa hasira huchochea ugomvi; bali asiye mwepesi wa hasira hutuliza mashindano.” (Mithali 15:18) Kwa hiyo, subiri hadi unapotulia kabla ya kujaribu kutatua tatizo hilo. “Mwanzoni unakuwa na hasira kali,” akiri Lisa, “lakini unapaswa kujiruhusu utulie. Ngoja mpaka hasira kali dhidi ya mtu huyo zinapokwisha. Kisha unaweza kumwendea mtu huyo na kuketi na kuzungumzia mambo kwa njia ya amani.”

Jambo kuu ni “amani.” Kumbuka, lengo lako si kumshambulia rafiki yako kwa maneno. Ni kusuluhisha mambo kwa njia ya amani, na ikiwezekana kwa vyovyote, kurudisha urafiki. (Zaburi 34:14) Kwa hiyo, sema kutoka moyoni. “Unaweza kusema, ‘mimi ni rafiki yako, nawe ni rafiki yangu; lakini nahitaji tu kujua ni nini kilichotokea,’” adokeza Lisa. “Unahitaji kujua sababu zilizochochea tendo hilo. Unapojua, kwa kawaida haiwi vigumu kushughulikia hali hiyo.”

Kwa hakika lingekuwa kosa kujaribu kulipiza kisasi, labda kwa kupiga porojo juu ya mtu huyo na kujaribu kushawishi wengine wakuunge mkono. Mtume Mkristo Paulo aliwaandikia Waroma hivi: “Msirudishe ovu kwa ovu kwa yeyote.” (Waroma 12:17) Kwa kweli, hata iwe umeumizwa kadiri gani, kulipiza kisasi kutaharibu tu mambo. “Haifai kulipiza kisasi,” asema Nora, “kwa sababu hamtapata kuwa marafiki tena.” Tofauti na hilo, aongezea kwamba kujitahidi kadiri uwezavyo ili kurekebisha uhusiano “hukufanya uhisi kuwa mtu bora zaidi.”

Lakini vipi ikiwa rafiki yako haitikii jitihada zako za upatanisho? Katika kisa hicho, kumbuka kwamba urafiki hutofautiana sana. “Si kila rafiki atakayekuwa wa karibu,” asema mshauri wa familia Judith McCleese. “Ujue kwamba unaweza kuwa na uhusiano wa aina mbalimbali.” Hata hivyo, unaweza kupata faraja kwamba umefanya sehemu yako ili kurudisha amani. Mtume Paulo aliandika hivi: “Ikiwezekana, kwa kadiri itegemeavyo nyinyi, iweni wenye kufanya amani na watu wote.”—Waroma 12:18.

Hata urafiki bora zaidi utapatwa na matatizo. Ukiweza kustahimili matatizo hayo bila kuyaruhusu yaharibu maoni yako kuelekea wengine au kujistahi mwenyewe, unafanya maendeleo ya kuwa mtu mzima mkomavu. Ijapokuwa watu fulani huenda wakawa ‘wanaangamiza wengine,’ pia Biblia hutuhakikishia kwamba “yuko rafiki aambatanaye na mtu kuliko ndugu.”—Mithali 18:24.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Baadhi ya majina katika makala haya yamebadilishwa.

[Picha katika ukurasa wa 15]

Huenda ukarudisha urafiki kwa kuzungumzia jambo lililotokea