Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tumaini Hakika

Tumaini Hakika

Tumaini Hakika

YAPATA miaka 2,000 iliyopita, Yesu, ambaye mara nyingi huitwa mtu mkuu zaidi aliyepata kuishi, alihukumiwa kifo isivyo haki. Alipokuwa ametundikwa kwenye mti wa mateso, mtenda-maovu aliyetundikwa karibu naye alimwambia hivi kwa kumdhihaki: “Wewe ndiwe Kristo, sivyo? Jiokoe mwenyewe na sisi.”

Ndipo, mtenda-maovu mwingine aliyehukumiwa kifo pia akamkemea yule mwingine: “Je, wewe humhofu Mungu hata kidogo, kwamba sasa wewe umo katika hukumu ileile? Nasi, kwa kweli, tuko hivyo kwa haki, kwa maana sisi tunapokea kwa ukamili kile tustahilicho kwa mambo tuliyofanya; lakini mtu huyu hakufanya jambo lolote lisilopaswa.” Kisha akamgeukia Yesu na kusihi hivi: “Nikumbuke mimi uingiapo katika ufalme wako.”

Yesu akajibu: “Kwa kweli mimi nakuambia wewe leo, Utakuwa pamoja na mimi katika Paradiso.”—Luka 23:39-43.

Yesu alikuwa amewekewa tumaini zuri ajabu mbele yake. Mtume Paulo alionyesha jinsi tumaini hilo lilivyomwathiri Yesu, aliposema: “Kwa ajili ya shangwe iliyowekwa mbele yake alivumilia mti wa mateso, akidharau aibu.”—Waebrania 12:2.

“Shangwe” hiyo iliyowekwa mbele ya Yesu ilitia ndani kuishi tena mbinguni na Baba yake na hatimaye kutumikia akiwa Mtawala wa Ufalme wa Mungu. Isitoshe, angekuwa pia na shangwe ya kuwakaribisha mbinguni wafuasi wake waliothibitishwa na wanaotumainika ambao watatawala pamoja naye wakiwa wafalme juu ya dunia. (Yohana 14:2, 3; Wafilipi 2:7-11; Ufunuo 20:5, 6) Hivyo basi, Yesu alimaanisha nini alipomwahidi yule mtenda-maovu kwamba angekuwa katika Paradiso?

Kuna Tumaini Gani kwa Yule Mtenda-Maovu?

Yule mtu hakustahili kutawala pamoja na Yesu mbinguni. Yeye hatiwi miongoni mwa wale walioambiwa hivi na Yesu: “Nyinyi ndio mmeshikamana nami katika majaribu yangu; nami nafanya agano pamoja nanyi, sawa na vile Baba yangu amefanya agano pamoja nami, kwa ajili ya ufalme.” (Luka 22:28, 29) Lakini, Yesu alimwahidi yule mtenda-maovu kwamba angekuwa pamoja naye katika Paradiso. Ahadi hiyo itatimizwaje?

Mwanamume na mwanamke wa kwanza, Adamu na Hawa, waliwekwa katika Paradiso na Yehova Mungu, bustani ya raha inayoitwa Edeni. (Mwanzo 2:8, 15) Edeni ilikuwa duniani, na Mungu alikusudia kwamba dunia nzima iwe paradiso. Hata hivyo, Adamu na Hawa walikosa kumtii Mungu nao wakafukuzwa kutoka kwa makao yao mazuri. (Mwanzo 3:23, 24) Lakini Yesu alifunua kwamba Paradiso ingerudishwa na kwamba ingeenea duniani pote.

Mtume Petro alipomuuliza Yesu kuhusu thawabu ambayo yeye na mitume wenzake wangepokea kwa kumfuata yeye, Yesu aliahidi: “Katika uumbaji-upya wakati Mwana wa binadamu aketipo juu ya kiti chake cha ufalme chenye utukufu, nyinyi ambao mmenifuata mtaketi nyinyi wenyewe pia juu ya viti vya ufalme kumi na viwili.” (Mathayo 19:27, 28) Kwa wazi, katika simulizi la Luka la mazungumzo hayo, badala ya kusema “katika uumbaji-upya,” Yesu anukuliwa akisema “katika mfumo wa mambo unaokuja.”—Luka 18:28-30.

Kwa hiyo, Yesu Kristo aketipo juu ya kiti chake cha ufalme chenye utukufu, pamoja na watawala-wenzi wake, atafanyiza mfumo mpya wa mambo ulio mwadilifu. (2 Timotheo 2:11, 12; Ufunuo 5:10; 14:1, 3) Kupitia utawala wa kimbingu wa Kristo, kusudi la awali la Mungu la dunia nzima kuwa paradiso litatimizwa!

Wakati wa utawala huo wa Ufalme, Yesu atatimiza ahadi yake kwa yule mhalifu aliyekufa kando yake. Atamfufua, na mtu huyo atakuwa raia wa kidunia wa Yesu. Kisha yule mtenda-maovu atapewa fursa ya kutimiza matakwa ya Mungu na kuishi milele chini ya utawala wa huo Ufalme. Kwa kweli twaweza kushangilia tazamio linalotegemea Biblia la kuishi milele katika Paradiso duniani!

Maisha Yaweza Kuwa na Kusudi

Ebu wazia kusudi ambalo tumaini hilo tukufu laweza kuleta maishani mwetu. Laweza kulinda akili zetu kutokana na matokeo yenye msiba ya fikira zisizofaa. Mtume Paulo alilinganisha tumaini hilo na kifaa muhimu cha silaha za kiroho. Alisema kwamba ni lazima tuvae “tumaini la wokovu” kama “kofia ya chuma.”—1 Wathesalonike 5:8; Zaburi 37:29; Ufunuo 21:3, 4.

Tumaini hilo linaendeleza uhai. Katika Paradiso inayokuja, badala ya upweke kutakuwapo machozi ya shangwe wapendwa wetu wanapofufuliwa na “Mungu awafufuaye wafu.” (2 Wakorintho 1:9) Kisha kuvunjika moyo kunakosababishwa na udhaifu wa kimwili, maumivu, na ulemavu kutasahauliwa, kwa kuwa “mtu aliye kilema ataruka-ruka kama kulungu.” ‘Nyama ya mwili wa [mtu] itakuwa laini kuliko ya mtoto,’ naye ‘atarudia siku za ujana wake.’—Isaya 35:6; Ayubu 33:25.

Wakati huo, wakati ambapo “hapana mwenyeji atakayesema, ‘Mimi mgonjwa,’” kukata tamaa kwa sababu ya maradhi sugu kutakuwa tu kumbukumbu linalodidimia. (Isaya 33:24) Utupu unaosababishwa na mshuko-moyo mkali sana utageuzwa kuwa “furaha ya milele.” (Isaya 35:10) Kukatishwa tumaini na habari za kwamba una ugonjwa unaofisha kutatokomea pamoja na kifo, adui wa kale wa wanadamu.—1 Wakorintho 15:26.

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Zingatia akilini tumaini zuri ajabu la ulimwengu mpya wa Mungu