Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wakati Ujao Wenye Tumaini Licha ya Udhaifu

Wakati Ujao Wenye Tumaini Licha ya Udhaifu

Wakati Ujao Wenye Tumaini Licha ya Udhaifu

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA KONSTANTIN MOROZOV

Nilipozaliwa Julai 20, 1936, sikuwa na mifupa yoyote iliyokomaa mwilini mwangu isipokuwa kwenye fuvu la kichwa na uti wa mgongo. Kiunzi changu chote kilifanyizwa na tishu dhaifu zisizo na nguvu kama tishu za sikio la mtu mzima. Nilikuwa na uzito unaopungua nusu kilogramu. Ishara pekee za uhai zilikuwa mpigo dhaifu wa moyo, kupumua kwa shida, na misogeo michache.

NILIKUWA wa saba kati ya watoto tisa katika familia iliyoishi katika kijiji cha Sara, huko Ul’yanovsk Oblast, sehemu ya kati ya Urusi. Nilipokuwa na umri wa majuma matatu, wazazi wangu walinipeleka kanisani ili nibatizwe. Kasisi alifanya haraka kuninyunyizia maji na kuwaambia wazazi wangu wanirudishe nyumbani haraka iwezekanavyo, kwa kuwa alisema ningekufa baada ya saa chache.

Katika Januari 1937, wazazi wangu walinipeleka kwenye jiji la Kazan’, jiji kuu la jamhuri ya Urusi ya Tatarstan, ili kuwaona wataalamu fulani. Wakati huo ningeweza kusema “Mama,” “Baba,” na “Babushka” (Nyanya), na nilijua majina ya ndugu zangu. Baada ya madaktari kunipima, waliwaambia wazazi wangu kwamba ningekufa katika mwaka mmoja. Walipendekeza kwamba niuawe na kuhifadhiwa ndani ya chupa ya maabara ili niwe wonyesho wa kutumiwa na wanafunzi wa tiba. Nawashukuru wazazi wangu wapendwa kama nini kwamba walikataa katakata!

Kuteseka Utotoni

Kadiri ninavyoweza kukumbuka, mwili wangu umekuwa ukikumbwa na maumivu. Hata hivyo, hata nilipokuwa mtoto nilijitahidi kudumisha maoni yanayofaa na kujaribu kucheka mara nyingi na kufurahia maisha. Nimedumisha maoni hayo. Kiunzi changu kilipata nguvu zaidi hatua kwa hatua, nikaweza kuketi na kutambaa kidogo. Sikukua kama watoto wa kawaida wakuavyo na nilikuwa nimelemaa vibaya sana. Lakini nilikuwa mwanafunzi mwenye uwezo, na nilipokuwa na umri wa miaka mitano, niliweza kusoma na kuandika.

Mama alinipeleka kanisani kwa mara ya pili mnamo Mei 1941. Kulikuwa na watu wengi, na wote walikuwa wamepiga magoti wakisali. Kijakazi mmoja alimjia Mama ili kujua ni kwa nini hakuwa amepiga magoti. Mama aliponionyesha kwa kijakazi huyo, alienda kuzungumza na kasisi. Aliporudi, kijakazi huyo alitusindikiza hadi mlangoni na kudokeza kwamba Mama aniache nje ya mlango na kuingia peke yake. Alidai kwamba kwa sababu ya dhambi za wazazi wangu, nilikuwa nimepokezwa kwao na “asiye safi.” Mama alirudi nyumbani akidondokwa na machozi. Nilifikiri juu ya jambo hilo kwa muda mrefu. Nilijiuliza, ‘Ni nani huyu “asiye safi”?’

Mnamo mwaka wa 1948, Mama alinipeleka kwenye kijiji cha Merenki katika Jamhuri ya Chuvash, kilometa 80 hivi kutoka nyumbani kwetu. Kulikuwa na chemchemi za dawa huko, na Mama alitumaini kwamba ningeponywa na maji hayo. Ili niponywe, baadhi ya masharti niliyowekewa na kasisi yalikuwa kwamba sikupaswa kula kwa muda wa siku tatu. Pia nilihitaji kupokea Komunyo kanisani. Ijapokuwa sikuitibari sana kanisa hilo, nilikubali masharti hayo. Safari yangu ilikuwa ndefu na ngumu, lakini nilivumilia, huku nikifurahia mandhari nzuri.

Kanisa lilikuwa limejaa watu furifuri. Mama alipokuwa akinibeba katikati ya umati, mwanamke mmoja mzee alinipa peremende. Niliichukua na kuitia mfukoni. Zamu yangu ya kupokea Komunyo ilipowadia, mwanamke huyo mzee alipaza sauti kwa kusema: “Kasisi, usimpe huyo Komunyo! Ametoka tu kula peremende!” Nilimweleza kwamba peremende hiyo ilikuwa mfukoni, lakini kasisi huyo alifoka: “Wewe kinyangarika mfidhuli! Je, ni lazima useme uwongo pia? Mwondoeni kanisani!” Hata hivyo, siku iliyofuata, kasisi mwingine aliongoza sherehe ya Komunyo na kuniosha kwa maji “ya muujiza.” Hata hivyo, hakukuwa na muujiza wowote. Nilibaki nikiwa dhaifu.

Mafanikio ya Kitaalamu

Ijapokuwa nilikuwa nimelemaa sana kimwili, nilipokuwa tineja nilifuatia miradi mingi ya kitaalamu na kielimu. Mnamo mwaka wa 1956, nilijiunga na Komsomol (Ushirika wa Vijana wa Ukomunisti) na, baada ya muda, nilifundisha vijana historia ya Komsomol. Nilikuwa mshiriki wa Tume ya Makazi na Utamaduni kwenye makao ya walemavu, na nilitumikia huko nikiwa mkurugenzi na mtangazaji wa redio.

Kwa kuongezea, nilikuwa msimamizi wa maktaba itembeayo ya vitabu vilivyorekodiwa vya vipofu, na nilikuwa nimechaguliwa kuwa mshiriki katika Tume ya Hakimu ya Kupambana na Uraibu wa Vileo. Pia nilishiriki kwenye klabu ya wasanii wasio stadi sana, niliimba, na kucheza ala kadhaa za muziki.

Kwenye Makao ya Walemavu

Mnamo mwaka wa 1957, nilipokuwa na umri wa miaka 21, nililazimika kuingia kwenye makao ya walemavu kwa sababu ya udhaifu wangu wa kimwili. Hata hivyo, niliazimia kutokata tamaa. Katika Oktoba mwaka wa 1963, nilijiunga na Taasisi ya Utafiti wa Sayansi ya Viungo Bandia ya Moscow. Hatimaye nikiwa huko nilipasuliwa mara 18 ili kunyoosha miguu yangu.

Kwanza, miguu yangu ilinyooshwa. Kisha, baada ya siku nane, nilifanyiwa upasuaji. Baada ya hapo nilitiwa plasta miguuni ili iimarike hadi wakati ambapo ningepasuliwa tena. Muuguzi angelia alipoona jinsi nilivyokuwa nikiteseka.

Miezi minne iliyofuata, nilijifunza kutembea kwa mikongojo. Kwa kutumia mikongojo, naweza kujiinua hadi kufikia urefu wa futi tatu na nusu hivi. Nina uzito unaopungua kilogramu 25. Nilipozoea kutembea kwa mikongojo, nilirudi kwenye makao ya walemavu mwaka wa 1964. Kwa kusikitisha, mifupa dhaifu ya miguu yangu haingeweza kutegemeza uzito wa mwili wangu, na baada ya muda mfupi nililazimika tena kutambaa au kutumia kiti chenye magurudumu. Mimi hutumia hasa kiti chenye magurudumu kwenda popote hadi leo hii.

Sikuwahi kwenda kanisani tena. Dai la kwamba nilikuwa nimezaliwa na “asiye safi” liliendelea kukera nafsi yangu. Niliwapenda sana baba na mama yangu, na hivyo singeweza kukubali kwamba walikuwa wamemkosea Mungu na hivyo kuchangia hali yangu. Nilijitahidi kudumisha mtazamo unaofaa licha ya baa hilo. Nilitaka kuwatendea wengine mema, na zaidi ya yote, kujithibitishia mwenyewe kwamba ningeweza kufanya hivyo.

Kujitegemea Maishani

Mnamo mwaka wa 1970, nilimwoa Lidia, ambaye amepooza kwa sehemu tangu utotoni. Tulijipatia nyumba ndogo, tuliyoishi kwa miaka 15. Katika kipindi hicho sote tulifanya kazi ili kujiruzuku. Nilijifunza kurekebisha saa na vifaa vingine vidogo, vya kufanyiwa marekebisho.

Kwa muda fulani nilitumia mbwa aliyezoezwa kunitolea huduma mbalimbali zenye thamani. Kwa hakika, mimi na mtu fulani anayezoeza mbwa tulivumbua lijamu na hatamu ya pekee. Nilikuwa na mbwa wawili—mmoja aliitwa Vulkan na mwingine Palma. Palma alikuwa mwandamani mwaminifu kwa miaka mingi. Tukiwa dukani angechukua chakula na kunipa. Jambo pekee ambalo hakupenda kufanya lilikuwa kusimama kwenye foleni tulipokuwa tukilipa. Angebeba kibeti changu kwenye meno yake, na alikuwa na kulabu ndogo kwenye kola yake kwa ajili ya mfuko wangu wa kununulia vitu.

Mnamo mwaka wa 1973 mama yangu akawa mgonjwa sana. Kwa kuwa nilikuwa nyumbani sikuzote, mimi na mke wangu tuliamua kumleta aje kuishi nasi. Wakati huo baba na kaka zangu watano walikuwa wamekufa, na ndugu zangu wadogo waliishi katika sehemu nyingine za Urusi. Mama alipokuwa akiishi pamoja nasi, nilijaribu kufanya yote ambayo ningeweza kumfanyia. Hatimaye akafa akiwa na umri wa miaka 85.

Mnamo mwaka wa 1978, niliamua kujitengenezea gari. Baada ya kutengeneza magari mbalimbali ya majaribio, nilitengeneza gari lililofaa. Chama cha Taifa cha Kukagua Magari cha kwetu kiliniruhusu kufanya mtihani wa kuendesha gari na kusajili gari langu. Nililiita Osa (Nyigu). Mimi na mke wangu tulitengeneza trela ndogo ya gari hilo ambayo ingeweza kubeba uzito upatao kilogramu 300. Tuliweza kusafiri nalo mahali mbalimbali na kubeba vitu. Tulitumia gari hilo lililokuwa na mota hadi mwaka wa 1985.

Karibu wakati huo jicho langu la kushoto likapofuka, na la kulia likaanza kuzorota. Kisha Lidia akapatwa na maradhi ya moyo. Katika Mei 1985, kwa sababu ya udhaifu wetu, tulilazimika kuhamia makao ya walemavu katika jiji la Dimitrovgrad.

Sababu Inayofanya Nifurahie Sana Maisha Sasa

Katika kiangazi cha 1990, Mashahidi wa Yehova walizuru makao yetu ya walemavu. Nilipendezwa sana na mafundisho yao. Walinionyesha fungu katika Gospeli ya Yohana kuhusu yule mtu aliyezaliwa kipofu. Yesu alisema hivi kumhusu: “Mtu huyu hakufanya dhambi wala wazazi wake.” (Yohana 9:1-3) Nilielezwa kwamba tumerithi dhambi na magonjwa kutoka kwa mzazi wetu wa kale Adamu.—Waroma 5:12.

Hata hivyo, zaidi ya yote, nilivutiwa na uhakika wa kwamba hatimaye Mungu ataponya wote watakaopokea uhai chini ya utawala wa Ufalme wa Mwana wake, Yesu Kristo, Paradiso itakaporudishwa duniani. (Zaburi 37:11, 29; Luka 23:43; Ufunuo 21:3, 4) Nilidondokwa na machozi ya shangwe, na kunong’ona: “Nimepata kweli, kweli, kweli!” Nilijifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova kwa mwaka mmoja, na katika mwaka wa 1991, nilibatizwa ili kuonyesha wakfu wangu kwa Yehova Mungu.

Ijapokuwa nilisitawisha tamaa kubwa ya kumtumikia Yehova na kuhubiri juu ya makusudi yake ya ajabu, nilikabili vizuizi vingi. Hapo awali, sikuwa na uhitaji mkubwa wa kwenda huku na huko, lakini sasa nilihitaji kwenda na kushiriki imani yangu pamoja na wengine. Eneo langu la kwanza kuhubiri lilikuwa makao yetu ya walemavu, ambamo mliishi watu zaidi ya 300. Ili nikutane na watu wengi kadiri iwezekanavyo, niliomba nipewe mgawo wa kutumikia katika chumba cha mambo yahusuyo makao hayo.

Kila asubuhi niliketi mahali pangu pa kazi na kutunza migawo yangu. Ninapokuwa nikifanya kazi, nimejipatia marafiki wengi wapya ambao tunazungumza nao vichwa vya Biblia vyenye kupendeza. Wengi wao wamekubali vitabu na magazeti na vimewasaidia kuelewa Biblia. Wageni wamezoea kunisikiliza nikiwasomea kutoka kwa Biblia na vichapo vinavyotegemea Biblia. Wakati wa mchana, aghalabu kunakuwa na watu wengi chumbani ninamoishi na mke wangu hivi kwamba nyakati fulani kunakuwa hakuna nafasi ya mtu mwingine zaidi.

Ndugu na dada zangu Wakristo kutoka kwenye kutaniko la Mashahidi wa Yehova wamenisaidia sana katika kazi ya kuhubiri. Wao huniletea vichapo vya Biblia na kutumia wakati pamoja nami na mke wangu. Pia hunisaidia kufika kwenye mikutano ya kutaniko katika Jumba la Ufalme. Shahidi mmoja alinunua pikipiki yenye kigari kwa kusudi tu la kunisafirisha. Wengine walio na magari, hufurahia kuja na kunichukua wakati wa miezi ya baridi kali.

Kwa sababu ya utunzaji huo wenye upendo, nimeweza kuhudhuria makumi ya mikusanyiko, au semina za elimu, za Mashahidi wa Yehova. Wa kwanza ulikuwa mkusanyiko wa kimataifa huko Moscow, Julai 1993, ambapo kilele cha wahudhuriaji kilikuwa 23,743, kutoka nchi zaidi ya 30. Nilihitaji kufunga safari ya kilometa 1,000 hivi ili kuhudhuria mkusanyiko huo. Tangu wakati huo sijakosa mkusanyiko hata mmoja wa watu wa Yehova.

Wasimamizi wa makao yetu hunistahi sana, nami nawashukuru kwa ajili ya hilo. Mwenzi wangu, Lidia, ambaye tumeishi kwa upatano kwa miaka 30, pia hunitegemeza na kunisaidia, ijapokuwa hashiriki maoni yangu ya kidini. Lakini zaidi ya yote, Yehova hunitegemeza kwa mkono wake wenye nguvu na kunipa baraka zake nyingi. Hivi karibuni, katika Septemba 1, 1997, niliwekwa rasmi kuwa painia, kama waitwavyo wahudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova.

Kumekuwa na pindi nyingi maishani mwangu ambapo moyo wangu ungeacha kupiga na ningekufa. Ninafurahi jinsi gani kwamba jambo hilo halikutukia na nimepata kumjua na kumpenda Yehova Mungu, Chanzo cha uhai! Nataka kuendelea kumtumikia pamoja na ndugu na dada zangu wa kiroho ulimwenguni pote maadamu moyo wangu unaendelea kupiga.

[Picha katika ukurasa wa 20]

Nikiwa na mke wangu, Lidia

[Picha katika ukurasa wa 21]

Kumfundisha mwanafunzi katika makao yetu ya walemavu