Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wamepewa Tamaa ya Kuishi

Wamepewa Tamaa ya Kuishi

Wamepewa Tamaa ya Kuishi

MARY alikuwa na mshuko-moyo mkali sana kutia na matatizo mengine ya afya. Hata hivyo, hakuwa ametengwa na familia yake, wala kutumia vibaya vileo au dawa za kulevya. Kisa cha Mary chaonyesha kwamba jaribio hatari la kujiua halichangiwi tu na hali zinazoonwa kuwa visababishi.

Kwa muda fulani ilionekana kana kwamba Mary angehesabiwa katika takwimu zinazoshuhudia jambo la kwamba wazee-wazee hujiua sana. Alizimia kwa muda mrefu, bila fahamu, katika chumba cha wagonjwa mahututi katika hospitali ya karibu, uhai wake ulikuwa hatarini. Mume wake John mwenye wasiwasi hakubanduka ubavuni mwake. Madaktari walimwonya John na familia yao kwamba huenda Mary akafa na hata akinusurika atapatwa na madhara ya kudumu ya ubongo.

Mary alitembelewa kila siku na jiraniye, Sally, ambaye ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova. “Niliisihi sana familia yake isife moyo,” asema Sally. “Mama yangu anayeugua kisukari, alizimia kwa majuma mengi miaka kadhaa iliyopita. Madaktari waliiambia familia yetu kwamba angekufa, lakini hakufa. Ningeushika mkono wa Mary na kusema naye, kama nilivyomfanyia mama yangu, na nilihisi ni kana kwamba kulikuwa na itikio hafifu.” Kufikia siku ya tatu, itikio lilikuwa lenye nguvu zaidi, na ilionekana kwamba Mary angeweza kuwatambua watu, ingawa hangezungumza.

‘Je, Ningeweza Kumzuia Asijiue?’

“John alisumbuliwa sana na hisia ya hatia,” asema Sally. “Alikuwa na hakika kwamba yeye ndiye aliyekosea.” Hilo ni itikio la kawaida kwa kisa cha kujiua au kwa jaribio la kujiua la mtu umpendaye. “Nilimkumbusha kwamba Mary alikuwa akitibiwa mshuko-moyo mkali sana. Alikuwa mgonjwa na hangezuia mshuko-moyo kama ambavyo hangejizuia kuwa mgonjwa.”

Wale ambao wapendwa wao wanajiua mara nyingi huteswa na swali hili, Ningeweza kufanya nini ili nizuie jambo hilo? Kuwa macho kuona dalili za kuonya na mambo hatari kwaweza kuzuia jaribio la kujiua. Ikiwa sivyo, kumbuka kwamba tendo la mtu mwingine la kujiangamiza si daraka lako. (Wagalatia 6:5) Hili ni jambo muhimu kukumbuka hasa kuhusu visa ambavyo mshiriki wa familia mwenye nia ya kujiua anataka kimakusudi kuwafanya wengine wahisi wakiwa na hatia. Dakt. Hendin, aliyetajwa mapema, asema: “Yapasa ikumbukwe kwamba majaribio hatari ya kujiua mara nyingi hutekelezwa na watu ambao hutumaini kuathiri au kuelekeza hisia za watu wengine hata ingawa hawatakuwapo ili kushuhudia kufanikiwa au kushindwa kwa jitihada zao.”

Dakt. Hendin aendelea kusema hivi: “Wazee wenye nia ya kujiua, kwa kawaida hutaka kuathiri, kudhibiti, au kushurutisha watoto wao ambao ni watu wazima vilevile ndugu zao au wenzi wa ndoa watwae daraka la kumlinda. Kwa kawaida madai ya mhasiriwa hayawezi kamwe kutimizwa, mara nyingi anakuwa asiyeridhiana kuhusu madai hayo, na majaribio madogo ya kujiua hufuatwa mara nyingi na majaribio hatari.”

Washiriki wa familia wanaokabili hali hizo huenda wakahisi kwamba kwa kweli wamebanwa mno, zaidi ya uwezo wao. Lakini, usisahau kamwe kwamba Yehova Mungu hufufua wafu na kwamba aweza kufufua wapendwa wetu waliojiua kwa sababu ya mshuko-moyo, maradhi ya akili, au kukata tamaa.—Ona “Maoni ya Biblia: Kujiua—Kuna Ufufuo?” katika Amkeni! la Mei 8, 1991, ukurasa wa 22-23.

Ingawa kujiua hakuwezi kutetewa, inafariji kukumbuka kwamba matazamio ya wakati ujao ya wapendwa wetu yanamtegemea Mungu ambaye anafahamu kikamili kuwa udhaifu wetu na kupungukiwa kwetu kwaweza kumsukuma mtu atende kitendo hicho chenye kutamausha. Biblia husema hivi juu ya Yehova: “Maana mbingu zilivyoinuka juu ya nchi, kadiri ile ile rehema zake ni kuu kwa wamchao. Kama mashariki ilivyo mbali na magharibi, ndivyo alivyoweka dhambi zetu mbali nasi. Kama vile baba awahurumiavyo watoto wake, ndivyo BWANA anavyowahurumia wamchao. Kwa maana Yeye anatujua umbo letu, na kukumbuka ya kuwa sisi tu mavumbi.”—Zaburi 103:11-14.

Matokeo Yenye Kufurahisha

Kwa siku mbili Mary alipigania uhai wake, lakini akaokoka. Alirudiwa na fahamu pole kwa pole, kisha John akaenda naye nyumbani, na akafungia dawa zote. Sasa Mary huzuru wafanyakazi wa kijamii wa afya ya akili naye asema kwamba hawezi kueleza au kukumbuka wazo baya lililomchochea ajaribu kujiua.

Sasa Sally, jirani ya John na Mary, hujifunza nao Biblia kila juma. Wamejifunza kutoka kwa Biblia kwamba matatizo yanayoonekana kuwa bila utatuzi, hasa kwa wazee-wazee, yatatatuliwa na Mungu hivi karibuni. “Bila shaka funzo la Biblia peke yake haliondoi matatizo,” aeleza Sally. “Ni lazima uthibitishe kutoka kwenye Maandiko kuwa ahadi hizo ni halisi, kisha unahitaji kutumia yale unayojifunza. Lakini nafikiri John na Mary wanapata tumaini halisi la wakati ujao.”

Iwapo wakati wako ujao waonekana kuwa bila tumaini na ungependa kupata tumaini hakika, mbona usiwasiliane na Mashahidi wa Yehova? Sawa na John na Mary, acha wakuthibitishie kwamba Mungu anaweza na atatatua matatizo yote hivi karibuni. Bila kujali hali mbaya sana ya mambo sasa, kuna suluhisho. Tafadhali chunguza nasi tumaini hakika la wakati ujao ambalo limeamsha tena tamaa ya wengi ya kuishi.

[Sanduku katika ukurasa wa 6]

Mambo Yanayochangia Kujiua na Dalili za Kuonya

“Mambo yanayochangia kujiua hutofautiana kati ya wazee-wazee na vijana,” lasema jarida la The Journal of the American Medical Association. Mambo yanayochangia kujiua hutia ndani “kunywa vileo kupita kiasi na mshuko-moyo, kutumia sana njia zenye kufisha, na kujitenga na jamii. Kwa kuongezea, wazee-wazee . . . wana magonjwa mengi ya kimwili na matatizo ya kihisia-moyo.” Kitabu Suicide, cha Stephen Flanders, chaorodhesha mambo yafuatayo yanayochangia kujiua, kila jambo lahitaji kutiliwa maanani.

Mshuko-moyo mkali mno:

“Watafiti wanaripoti kwamba asilimia 50 au zaidi ya wale wanaojiua wana rekodi ya mshuko-moyo mkali mno.”

Kukata tamaa:

Uchunguzi fulani ulionyesha kwamba hata watu wasioonekana kuwa na mshuko-moyo wangefikiria kujiua endapo wangekosa tumaini la wakati ujao.

Matumizi mabaya ya vileo na dawa za kulevya:

“Inakadiriwa kwamba kati ya asilimia 7 na 21 [ya walevi sugu] hujiua, ikilinganishwa na asilimia inayopungua 1 ya watu kwa ujumla.”

Uvutano wa familia:

“Uchunguzi unaonyesha kwamba washiriki wa familia ambazo mtu alijiua wako katika hatari kubwa ya kujiua pia.”

Ugonjwa:

“Hofu ya kudhoofika kimwili na hatimaye kuzuiwa katika hospitali ya binafsi, yaweza kutosha kutokeza wazo la kujiua miongoni mwa wazee-wazee fulani.”

Hasara:

“Hasara yaweza kuwa dhahiri, kama vile kumpoteza mwenzi au rafiki, kazi, au kudhoofika kwa afya. Yaweza kuwa isiyoonekana. Mifano yatia ndani kupoteza staha, hadhi, au usalama.”

Pamoja na mambo hayo yanayochangia kujiua, kitabu cha Flander chaorodhesha dalili zifuatazo za kuonya ambazo hazipasi kupuuzwa kamwe.

Jaribio la awali la kujiua:

“Hii ni dalili kuu ya pekee ya kuweza kujiua.”

Kusema juu ya kujiua:

“Usemi kama vile ‘Sitawahangaisha tena’ au ‘Wataishi vyema bila mimi’ ni mifano ya vitisho vya wazi.”

Mipango ya mwisho:

“Tabia hizo zatia ndani kuandika wosia, kuwapa watu vitu vyake vya thamani, na kupangia utunzi wa wanyama-vipenzi.”

Kubadilika kwa utu au tabia:

Badiliko hilo “linapoandamana na usemi wa kujidunisha au kukata tamaa,” yaweza kuwa “dalili ya mshuko-moyo mkali sana kiasi cha kuweza kutokeza tabia ya kujiangamiza.”

[Picha katika ukurasa wa 7]

Kwa kawaida wale wanaobaki huhitaji msaada wa kukabiliana na kujiua kwa mwenzi wao