Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Imani ya Kweli—Ni Nini?

Imani ya Kweli—Ni Nini?

Maoni ya Biblia

Imani ya Kweli—Ni Nini?

“BILA IMANI HAIWEZEKANI KUMPENDEZA VEMA, KWA MAANA AMKARIBIAYE MUNGU LAZIMA AAMINI KWAMBA YEYE YUKO NA KWAMBA YEYE HUWA MTHAWABISHAJI WA WALE WANAOMTAFUTA KWA BIDII.”—WAEBRANIA 11:6.

IMANI ni nini? Watu fulani hufafanua imani kuwa itikadi ya kidini katika Mungu bila uthibitisho thabiti wa kuwapo kwake. Mwandishi-habari Mmarekani H. L. Mencken alifafanua imani kuwa “itikadi isiyo ya kiakili ya mambo yasiyoelekea kutukia.” Je, hii ni imani ya kweli kama ifafanuliwavyo katika Biblia? Ni muhimu kuelewa imani waziwazi kwa sababu, kama ilivyonukuliwa juu, ‘bila imani haiwezekani kumpendeza Mungu.’

Biblia husema: “Imani ni kuwa na hakika juu ya mambo tunayotumaini.” (Waebrania 11:1, The New Testament in the Language of Today) Kwa hiyo, imani hutegemea ujuzi sahihi, mambo hakika ambayo hutegemeza maamuzi yanayofaa. Imani haihusishi tu itikadi bali pia sababu ya kuitikadi.

Kwa kielelezo: Labda una rafiki unayeweza kusema hivi juu yake: “Namtumaini mtu huyo. Ahadi zake zinategemeka. Najua kwamba niwapo na tatizo, atanisaidia.” Haielekei kwamba ungesema hivyo kuhusu mtu fulani uliyemjua kwa siku moja au mbili, sivyo? Angehitaji kuwa mtu ambaye amethibitika kuwa mwenye kutegemeka tena na tena. Ndivyo ilivyo na imani ya kidini, inayopaswa kutokeza tumaini na usadikisho unaotegemea uthibitisho wenye kutegemeka.

Je, Ni Imani au Ni Wepesi wa Kuamini Bila Ushuhuda?

Kati ya imani nyingi zinazokubaliwa leo kwa kweli ni wepesi wa kuamini bila ushuhuda—utayari wa kuamini bila msingi au sababu halali. Mara nyingi wepesi wa kuamini bila ushuhuda hutegemea hisia-moyo na ushirikina unaobadilika-badilika. Hiyo si imani yenye msingi mzuri kwa sababu haina msingi wenye kutegemeka wa kuitikadi.

Wepesi wa kuamini bila ushuhuda waweza kumfanya mtu afikie haraka mkataa ambao haupatani na kweli ya Biblia. Basi, Biblia huonya dhidi ya imani isiyo na msingi: “Mjinga huamini kila neno; bali mwenye busara huangalia sana aendavyo.” (Mithali 14:15) Mtume Paulo aliandika hivi: “Hakikisheni mambo yote; shikeni sana lililo bora.” (1 Wathesalonike 5:21) Biblia haipendekezi wepesi wa kuamini bila ushuhuda. Hupendekeza imani yenye uthibitisho.

Ni jambo zito kuweza kupambanua imani ya kweli na wepesi wa kuamini bila ushuhuda. Mtu aweza kuwa wa kidini lakini akose imani ya kweli. Paulo alisema hivi: “Imani si miliki ya watu wote.” (2 Wathesalonike 3:2) Lakini imani inayotegemea Biblia ni miliki ya watu fulani, nayo huathiri maisha yao.

Imani ya Kweli Huunganisha Mwanadamu na Mungu

Imani yaweza kufananishwa na mnyororo unaofanyizwa na uhakika na itibari ambayo humuunganisha mwanadamu na Mungu. Lakini imani ya aina hiyo ni kitu kinachositawishwa; si kitu tunachozaliwa nacho. Unaweza kusitawishaje imani ya kweli? Biblia hueleza hivi: “Imani hufuata jambo lisikiwalo. Nalo jambo lisikiwalo ni kupitia neno juu ya Kristo.”—Waroma 10:17.

Kwa hiyo, unahitaji kuchukua muda wa kumjua Mungu na mafundisho ya Mwanaye, Yesu Kristo. Ujuzi huo haupatikani bila jitihada. (Mithali 2:1-9) Lazima ujikakamue kujua kile isemacho Biblia kusudi usadikishwe na kutegemeka kwake.

Hata hivyo, imani ya kweli, huhusisha zaidi ya kuwa na ujuzi au kuamini kwamba jambo fulani ni kweli. Inahusisha moyo pia—kiti cha msukumo. Waroma 10:10 husema: “Kwa moyo mtu hudhihirisha imani.” Hilo lamaanisha nini? Unapotafakari juu ya mambo ya kimungu, na kujenga uthamini kuyaelekea, unaruhusu ujumbe wa Biblia upenye ndani kabisa ya moyo wako. Imani hukua na kuimarika kadiri uchochewavyo kutenda kupatana na ahadi za Mungu na uonapo uthibitisho wa baraka zake.—2 Wathesalonike 1:3.

Imani ya kweli ni kitu chenye thamani kama nini! Twanufaika kwa kuweza kukabili hali ngumu tukiwa na uhakika katika Mungu, tukiitibari uwezo wake wa kuelekeza hatua zetu na utayari wake wa kushughulikia mahitaji yetu. Kwa kuongezea, Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, alitaja manufaa moja ya muda mrefu ya imani: “Kwa maana Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akatoa Mwana mzaliwa-pekee wake, ili kila mtu anayedhihirisha imani katika yeye asipate kuangamizwa bali awe na uhai udumuo milele.” (Yohana 3:16) Uhai udumuo milele—ni zawadi kubwa jinsi gani kwa wale walio na imani!

Imani katika ahadi ya Mungu ya kuthawabisha watumishi wake hufanya mtu awe na maoni mapya ya akilini kuelekea maisha. Waebrania 11:6 husema kwamba imani ya kweli hutia ndani kuitikadi uwezo wa Mungu wa kuthawabisha “wale wanaomtafuta kwa bidii.” Kwa wazi, basi, imani ya kweli si wepesi wa kuamini bila ushuhuda na inahusisha mengi zaidi ya kuamini tu kwamba Mungu yuko. Inahusisha kukubali uwezo wa Mungu wa kutenda akiwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii. Je, kwa kweli ungependa kumjua Mungu kwa unyofu wa moyo? Ikiwa ndivyo, basi jipatie ujuzi sahihi kutoka kwa Neno lake, Biblia, na imani yako itathawabishwa.—Wakolosai 1:9, 10.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 26]

Drawings of Albrecht Dürer/Dover Publications, Inc.