Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Uhuru Zaidi wa Dhamiri Utaruhusiwa Mexico?

Je, Uhuru Zaidi wa Dhamiri Utaruhusiwa Mexico?

Je, Uhuru Zaidi wa Dhamiri Utaruhusiwa Mexico?

NA MLETA-HABARI WA AMKENI! KATIKA MEXICO

UHURU wa kidini unaruhusiwa kisheria katika Mexico. Hata hivyo, sheria ingali na vizuizi fulani kuelekea uhuru wa ibada. Kwa mfano, wazo la kukataa utumishi wa jeshi kwa sababu ya dhamiri halijulikani sana katika nchi hii. Ndiyo sababu Taasisi ya Uchunguzi wa Kisheria, ya National Autonomous University of Mexico (UNAM), ikaamua kupanga kongamano la kimataifa lenye kichwa “Kukataa kwa Kudhamiria Katika Mexico na Ulimwenguni.” Taasisi ya Uchunguzi wa Kisheria ya UNAM inaelekezwa na serikali, lakini kusudi lake ni kuchunguza sheria zilizotungwa na matumizi yake. Mashahidi wa Yehova wa Mexico waliombwa watume mwakilishi atakayetoa hotuba yenye kichwa “Mashahidi wa Yehova na Kukataa kwa Kudhamiria.”

Maprofesa Wasema Waziwazi

Hotuba yenye kichwa “Kukataa kwa Kudhamiria Katika Sheria za Kimataifa,” iliyotolewa na Dakt. Javier Martínez Torrón, profesa katika Chuo Kikuu cha Sheria cha Granada, huko Hispania, ilieleza kwamba uhuru wa dhamiri na haki ya kukataa kutii sheria fulani au wajibu kwa sababu ya dhamiri tayari inatambuliwa ulimwenguni pote. Alitaja hali ya Mashahidi wa Yehova huko Hispania na kesi ya Kokkinakis huko Ugiriki. *

Dakt. José Luis Soberanes Fernández, profesa katika Taasisi ya Uchunguzi wa Kisheria ya UNAM, alizungumzia kichwa “Mexico na Suala Hilo.” “Lazima tutaje kwamba Sheria ya Mexico ya Ushirika wa Kidini na Ibada ya Hadharani hupinga kabisa kukataa kwa kudhamiria,” akasema, huku akirejezea Kifungu cha Kwanza, kinachotaarifu hivi: “Masadikisho ya kidini hayamzuii mtu yeyote kutii sheria za nchi hii katika njia yoyote. Hakuna mtu atakayetumia sababu za kidini kuwa kisingizio cha kuepuka wajibu na utumishi wa kisheria.” Akimalizia, Dakt. Soberanes alisema: “Twaamini kwamba kukubali kisheria suala la kukataa kwa kudhamiria katika Mexico ni jambo la dharura.”

Alirejezea jambo la kwamba kila mwaka mamia ya watoto walio Mashahidi katika Mexico hukabili matatizo shuleni kwa sababu ya msimamo wao unaotegemea Biblia wa kutoisalimu bendera. Baadhi ya watoto walio Mashahidi hata wanazuiwa kujiandikisha shuleni. Hata hivyo, kwa sababu ya kukata rufani kupitia kwa Tume ya Haki za Kibinadamu, wengi wao wamepata tena haki ya kujiunga na shule. Maofisa fulani wa elimu wamechukua hatua ya kuzuia watoto wasifukuzwe shuleni, lakini walimu wengine hupuuza jitihada hizo. Wenye mamlaka wamevumilia msimamo wa Mashahidi, lakini hakuna kiwango kilichowekwa kinachoweza kufuatwa na shule katika Mexico.

Kongamano hilo lilijadili pia kukataa kwa kudhamiria kwa dini nyingine, kama vile kushurutishwa kufanya kazi siku wanazoona kuwa takatifu, kutarajiwa wawe na mavazi ya kazini yanayokiuka itikadi zao za kidini, na kadhalika. Kukataa utumishi wa jeshi na matibabu fulani hususa pia kulijadiliwa.

Mashahidi wa Yehova na Kaisari

Mshiriki mmoja wa ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova katika Mexico alitoa muhtasari wa itikadi zao za msingi. Alieleza kutii kwao kanuni hizo za Biblia kama ile inayoonyeshwa katika Luka 20:25, inayowaagiza Wakristo ‘wamlipe Kaisari vitu vya Kaisari.’ Alirejezea pia Waroma 13:1, linalosema kwamba ni lazima Wakristo wastahi mamlaka za kiserikali. Alikazia kwamba Mashahidi wa Yehova ni watu wa kawaida, raia wanaotii sheria ambao wanajitahidi kulipa kodi zao, wanaoishi kwa utaratibu, wenye kuzingatia usafi nyumbani, na wanaopeleka watoto wao shuleni.

Kisha akakazia msingi wa Kimaandiko wa kutosalimu bendera wa Mashahidi, unaopatikana katika zile Amri Kumi, katika Kutoka 20:3-5: “Usiwe na miungu mingine ila mimi. Usijifanyie sanamu ya kuchonga, wala mfano wa kitu cho chote kilicho juu mbinguni, wala kilicho chini duniani, wala kilicho majini chini ya dunia. Usivisujudie wala kuvitumikia.”

Mashahidi wa Yehova humwabudu Mungu peke yake, na hawaabudu sanamu kwa vyovyote vile. Hata hivyo, hawatawahi kamwe kutenda tendo lolote la kukosea staha nembo ya kitaifa wala kuikosea staha kwa usemi.

Ili kukazia maoni ya Mashahidi wa Yehova kuelekea swali hilo, vidio ya Purple Triangles ilionyeshwa. Vidio hiyo inaonyesha msimamo thabiti wa Mashahidi wa Yehova katika Ujerumani ya Nazi (1933-1945). Inaonyesha yaliyoipata familia ya Kusserow, ambayo ilishikilia itikadi zao kwa uthabiti wakati wa utawala wa Nazi. *

Kisha, msingi wa Kimaandiko wa Mashahidi wa Yehova kukataa kutiwa damu mishipani ukatolewa. (Mwanzo 9:3, 4; Matendo 15:28, 29) Mpango wa Halmashauri za Uhusiano na Hospitali ulimwenguni pote ulielezwa. Pia, mafanikio ya madaktari wanaoshirikiana katika kupasua Mashahidi wa Yehova bila damu yalitajwa.

Kila siku watu wapatao 100 walihudhuria mhadhara huo, wengi wao wakiwa wanasheria. Wawakilishi wa Ofisi ya Mambo ya Dini katika Mexico walihudhuria pia. Wote waliokuwapo waliweza kusikiliza maoni ya wataalamu kuhusu kustahi watu wanaokataa kwa kudhamiria. Hii ni dhana ngeni kwa watunga-sheria katika Mexico, japo inakubaliwa katika nchi nyingi za kidemokrasia, kama vile Hispania, Marekani, Ufaransa, na Ureno kutia ndani baadhi ya nchi zilizokuwa za Kikomunisti, kama vile Czechia na Slovakia.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Ona makala “Mahakama ya Juu ya Ulaya Yaunga Mkono Haki ya Kuhubiri Katika Ugiriki” na “Kulinda Kisheria Habari Njema,” katika toleo la Septemba 1, 1993, na Desemba 1, 1998, la Mnara wa Mlinzi.

^ fu. 13 Ona Mnara wa Mlinzi, Septemba 1, 1985, la Kiingereza, “Familia Yangu Yampenda Yehova Licha ya Jela na Kifo.” Ona pia toleo la Januari 15, 1994, ukurasa wa 5.

[Picha katika ukurasa wa 21]

Mashahidi wa Yehova katika Mexico huthamini sana uhuru wao wa kuhubiri