Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Utumwa wa Kisasa—Mwisho Wake Wakaribia!

Utumwa wa Kisasa—Mwisho Wake Wakaribia!

Utumwa wa Kisasa—Mwisho Wake Wakaribia!

“Uhuru wa mtu mmoja ni sehemu muhimu ya uhuru wa ulimwenguni pote. Huwezi kuhalifu uhuru wa mtu na wakati huohuo ukose kuhatarisha uhuru wa ulimwenguni pote.”-Victor Schoelcher, Mwandishi Wa Habari Na Mwanasiasa Mfaransa, 1848.

“NI UOVU gani unaomchochea mwanadamu daima kudharau, kushinda, na kushushia heshima wanadamu wenzake?” wauliza wahariri wa The UNESCO Courier. “Na imekuwaje kwamba uhalifu huo dhidi ya binadamu haujaadhibiwa hata tangu Haki za Kibinadamu zianzishwe?”

Jibu ni tata. Pupa ndiyo huchochea kuajiriwa kwa watoto ili walipwe mshahara mdogo na pia hali ya kufungwa na deni. Umaskini na kukosa elimu vimelaumiwa kwa kufanya wasichana wauzwe kwenye ukahaba na kwenye ndoa za kiutumwa. Desturi za kidini na mawazo ya kitamaduni ndiyo huchangia utumwa wa kidesturi. Na kuhusu wanaume wanaozuru Bangkok au Manila ili kutafuta wavulana au wasichana wachanga wasio na UKIMWI, nia yao ni upotovu wa kingono na ukosefu wa adili ulio wazi. Yote hayo ni sehemu ya ulimwengu wa watu ambao ni “wenye kujipenda wenyewe, wapenda-fedha, . . . wasio na shauku ya kiasili, . . . wasio na hali ya kujidhibiti, wakali,” kupatana na maneno ya mtume Paulo, mwanafunzi wa sheria wa karne ya kwanza. (2 Timotheo 3:1-5) Ni sehemu ya ulimwengu ambamo “yaliyopotoka hayawezi kunyoshwa, wala yasiyokuwapo hayahesabiki,” kupatana na maneno ya mtawala wa kale anayeitwa Solomoni.—Mhubiri 1:15.

Badiliko la Akili

Je, hilo lamaanisha kwamba hakuna jambo lolote linaloweza kufanywa au litakalofanywa ili kukomesha utumwa daima—ama kwa namna yake ya kale ama kwa namna ya kisasa zaidi? Sivyo kamwe!

Ofisi ya UM ya Mjumbe Mkuu wa Haki za Kibinadamu (OHCHR) yasema kwamba utumwa ni “hali ya akili,” ikiongezea hivi: “Hata unapokomeshwa, utumwa huacha alama fulani. Unaweza kudumu akilini—miongoni mwa wale walioathiriwa pamoja na wazao wao na pia miongoni mwa warithi wa watu waliotumikisha wengine—muda mrefu baada ya kutoweka rasmi.”

Hivyo njia moja ya kukomesha utumwa ingekuwa kuanzisha badiliko la kufikiri—badiliko la moyo—ulimwenguni pote. Na hilo lahusisha badiliko la elimu—kufundisha watu wapendane na kustahi adhama ya wengine. Inamaanisha kusaidia watu wang’oe pupa mioyoni mwao na kufuata viwango vya juu vya adili. Ni nani anayeweza kuandaa elimu hiyo? Shirika la OHCHR lasema kwamba “kila mtu apaswa kuchangia utengamano wa ulimwengu unaopinga kuwatumia vibaya wanadamu.”

Fikiria programu ya elimu ambayo imetekelezwa ulimwenguni pote na kikundi cha Kikristo cha Mashahidi wa Yehova. Programu hiyo imefanikiwa kufundisha watu wenye moyo wa haki wasivumilie au kuruhusu kutumiwa vibaya kwa wanadamu. Kupitia programu hiyo, mamilioni ya watu katika nchi zaidi ya 230 wamefundishwa kutendea wanadamu wenzao kwa adhama. Kwa nini programu hiyo imefaulu?

Kwa sababu inategemea Biblia, kitabu kilichopuliziwa na Muumba wa mwanadamu. Ni kitabu kinachotegemeza adhama ya kibinadamu. Watu waliofundishwa na Biblia kupitia programu ya elimu ya Mashahidi wa Yehova hujifunza kwamba Muumba wetu, Yehova, ni Mungu wa adhama. (1 Mambo ya Nyakati 16:27) Huwapa adhama viumbe wake wote. Hao hutia ndani wanaume na wanawake, kutoka rangi zote, malezi ya kijamii, na hali za kiuchumi.—Ona sanduku “Uhuru na Adhama ya Kibinadamu—Kutoka Chanzo Gani?”

Usawa na Kuheshimu Adhama

Biblia hufundisha kwamba Mungu “alifanya kutoka kwa mtu mmoja kila taifa la watu, ili wakae juu ya uso mzima wa dunia.” (Matendo 17:26) Hivyo, hakuna mtu anayeweza kudai kuwa juu ya wanadamu wenzake au haki ya kuonea au kutumia wengine vibaya. Watu walio tayari kujifunza hupata kuthamini uhakika wa kwamba “Mungu si mwenye ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye humhofu na kutenda uadilifu akubalika kwake.” (Matendo 10:34, 35) Wanatambua kwamba upendo wa Mungu huhusisha wote, kwa kuwa pendeleo la uhusiano wa karibu naye hupatikana kwa watu wote. Kwa hakika, “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akatoa Mwana mzaliwa-pekee wake, ili kila mtu anayedhihirisha imani katika yeye asipate kuangamizwa bali awe na uhai udumuo milele.”—Yohana 3:16.

Elimu hii inayotegemea Biblia huathiri sana nyutu za watu. Kupitia elimu hiyo mioyo na akili za watu zaweza “kufanywa upya kabisa.” (Waefeso 4:22-24, Today’s English Version) Huwachochea wawatendee wanadamu wenzao kwa adhama na staha. Wameazimia ‘kufanya lililo jema kuelekea wote.’ (Wagalatia 6:10) Hakuna mtu awezaye kuwa Mkristo wa kweli na ashiriki kutumia vibaya na kuonea wanadamu wenzake. Mashahidi wa Yehova wanafurahi kuwa kikundi cha Kikristo kama vile kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza, ambapo ‘hakukuwa Myahudi wala Mgiriki, na hakukuwa mtumwa wala mtu huru. Wote walikuwa mtu mmoja katika muungano na Kristo Yesu.’—Wagalatia 3:28.

Badiliko la Serikali

Hata hivyo, ili utumwa wa namna zote ukomeshwe kabisa, badiliko kubwa katika jamii ya kibinadamu lahitajiwa. Shirika la Wafanyakazi Ulimwenguni lasema kwamba ili kukomesha kutumiwa vibaya kwa wanadamu, kuna uhitaji wa “kubadili hali ambazo huruhusu kuwepo” kwa mazoea hayo. Hatua za kimataifa, ushirikiano wa kimataifa, na uwajibikaji wa jumuiya ya ulimwengu ni miongoni mwa madokezo zaidi yaliyotolewa na shirika hilo.

Hilo lingehitaji serikali itakayodhibiti kabisa sayari yetu, serikali itakayohakikisha uhuru ulimwenguni pote. Boutros Boutros-Ghali aliyekuwa katibu-mkuu wa UM, alisema kwamba matatizo halisi yanayokumba sayari yetu lazima yatatuliwe “ulimwenguni pote.” Lakini si kila mtu aliye na hakika kwamba jambo hilo linaweza kutukia. Mambo ya kale yaonyesha kwamba watu wengi walio mamlakani ni wachoyo sana na ni wenye kufikiria mapendezi na miradi yao sana hivi kwamba ni vigumu kufikia ushirikiano wa kimataifa.

Hata hivyo, Biblia—kitabu kilekile ambacho kimefundisha mamilioni ya watu kuheshimu adhama ya wanadamu wenzao—yaonyesha kwamba Mungu anakusudia kusimamisha serikali ya ulimwengu ya namna hiyo. Katika Biblia utapata ahadi nyingi za ulimwengu mpya wa uadilifu. (Isaya 65:17; 2 Petro 3:13) Mungu anakusudia kuondoa kabisa duniani mtu yeyote asiyempenda Mungu na jirani. Mungu amefunua kusudi lake la kusimamisha serikali ya ulimwenguni pote juu ya wanadamu ili itawale dunia kwa uadilifu. Yesu alituambia tusali kwa ajili ya serikali hiyo katika ile inayoitwa kwa kawaida Sala ya Bwana au Baba Yetu.—Mathayo 6:9, 10.

Kutumiwa vibaya kwa wanadamu na kila namna ya utumwa itakomeshwa chini ya utawala wa serikali hiyo kwa sababu Kristo Mfalme atatawala “kwa hukumu na kwa haki.” (Isaya 9:7) Wale walioonewa watafunguliwa chini ya utawala wake wa haki, kwa kuwa Biblia husema: “Kwa maana atamkomboa mhitaji aliapo, na mtu aliyeonewa iwapo hana msaidizi. Atamhurumia aliye dhaifu na maskini, na nafsi za wahitaji ataziokoa. Atawakomboa nafsi zao na kuonewa na udhalimu.”—Zaburi 72:12-14.

Ikiwa unatamani kuona mwisho wa utumwa—namna zote za utumwa—twakualika ujifunze mengi zaidi kuhusu kusudi la Mungu la kusimamisha serikali hiyo ya ulimwengu itakayoleta uhuru. Mashahidi wa Yehova katika eneo lenu watafurahi kukusaidia kufanya hivyo.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 11]

UHURU NA ADHAMA YA KIBINADAMU—KUTOKA CHANZO GANI?

Sote tumezaliwa tukiwa na uhitaji na tamaa ya asili ya adhama na uhuru. Kofi Annan, katibu-mkuu wa UM, alirudia maoni yanayojulikana ulimwenguni pote alipouliza hivi: “Ni nani awezaye kukanusha kwamba sote twataka maisha yasiyo na hofu, mateso na ubaguzi? . . . Ni lini uliposikia mtu aliye huru akitaka uhuru ukomeshwe? Ni wapi uliposikia mtumwa akitetea utumwa?”

Mawazo hayo si mapya kamwe. Akikanusha wazo la kwamba watu fulani walizaliwa wawe watumwa, mwanafalsafa Mroma wa karne ya kwanza Seneca, katika kichapo chake Letters to Lucilius, aliandika hivi: “Tafadhali kumbuka kwamba mtu unayemwita mtumwa wako alitokana na mbegu ileile, anga zuri lilelile liko juu yake, hupumua kama wewe, huishi kama wewe, hufa kama wewe!”

Imam ʽAlī, anayeonwa kuwa mwandamizi wa nne wa Muḥammad, alisema kwamba watu wote ni “sawa katika uumbaji.” Saʽdī, mshairi Mwajemi wa karne ya 13, alitangaza hivi: “Watoto wa Adamu ni viungo vya mmoja na mwenzake na wameumbwa kwa kitu kimoja. Ulimwengu unapoumiza mshiriki mmoja, washiriki wengine huumia pia.”

Historia iliyopuliziwa na Mungu iliyo katika Biblia hukazia adhama ya wanadamu wote. Kwa mfano, Mwanzo 1:27 hueleza kuumbwa kwa mwanadamu, isemapo: “Mungu akaumba mtu kwa mfano wake, kwa mfano wa Mungu alimwumba, mwanamume na mwanamke aliwaumba.” Muumba wetu ni Mungu wa uhuru. “Iliko roho ya Yehova, kuna uhuru,” akasema mtume Paulo. (2 Wakorintho 3:17) Kwa kumwumba mtu kwa mfano wake, Yehova aliwapa wanadamu kiasi fulani cha kujiona wanafaa, kujistahi, na adhama. Kwa kuweka huru uumbaji wake kutoka kwa “utumwa wa uharibifu,” pia atahakikisha kwamba watu watafurahia uhuru huo na adhama hiyo milele.—Waroma 8:21.

[Picha katika kurasa za 9, 10]

Kila mtu ana haki ya kuwa na adhama na uhuru

[Picha katika ukurasa wa 10]

ELIMU YA BIBLIA HUKAZIA STAHA KWA ADHAMA YA KIBINADAMU NA HUTOKEZA TUMAINI LA WAKATI UJAO LA ULIMWENGU MPYA UJAO

Funzo la Biblia la familia katika Papua New Guinea

Umaridadi wa maporomoko haya ya Blue Nile katika Ethiopia ni mmweko wa kimbele wa paradiso iliyorudishwa