Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Unavyoweza Kuacha Kuvuta Sigareti

Jinsi Unavyoweza Kuacha Kuvuta Sigareti

Jinsi Unavyoweza Kuacha Kuvuta Sigareti

SAWA na kujifunza kuendesha baiskeli, ni nadra sana kuacha tumbaku mara ya kwanza unapojaribu. Kwa hiyo, ikiwa umeazimia kuacha wapaswa kuwa tayari kujaribu tena na tena hadi utakapofaulu. Usiache hali ya kurudia uvutaji ikuvunje moyo. Ione kuwa somo, kikwazo kidogo tu katika programu inayoweza kufaulu. Hapa pana madokezo kadhaa ambayo yamewasaidia wengine. Huenda yakakusaidia pia.

Tayarisha Akili Yako Kuacha

■ Kwanza, ni sharti usadiki kwamba kuacha sigareti kunastahili jitihada. Orodhesha sababu ulizo nazo za kuacha, pamoja na faida zote. Baada ya kuacha, kupitia orodha hiyo kutaimarisha azimio lako. Tamaa ya kumpendeza Mungu ni kichocheo kikubwa cha kuacha. Biblia husema kwamba twapaswa kumpenda Mungu kwa akili, moyo, nafsi, na nguvu zetu zote. Hilo ni jambo tusiloweza kutimiza ikiwa tuna uraibu wa tumbaku.—Marko 12:30.

■ Changanua mazoea yako ya kuvuta sigareti ili ujue ni wakati gani na kwa nini wewe huvuta sigareti. Kuandika kwenye karatasi wakati na mahali unapovuta kila sigareti kwa siku moja kwaweza kukusaidia. Kufanya hivyo kutakusaidia utambue hali zinazoweza kukushawishi uvute sigareti baada ya kuacha.

Pangia Tarehe ya Kuacha

■ Teua tarehe ya kuacha, na uitie alama kwenye kalenda. Itakuwa vyema ukiteua siku ambayo hutabanwa na mkazo usiofaa. Siku hiyo iwadiapo, acha kabisa—mara moja na kabisa.

■ Kabla ya siku ya kuacha kufika, tupilia mbali visahani vya majivu na viberiti vya sigara. Fua nguo zako zote ili uondoe uvundo wa moshi wa tumbaku.

■ Omba msaada wa wafanyakazi wenzi, marafiki, na familia ili wakutie moyo katika jitihada zako za kuacha. Usihofu kuwaambia wengine waache kuvuta sigareti mahali ulipo.

■ Pangia shughuli nyingi katika siku utakayoacha kuvuta sigareti. Waweza kuzuru mahali ambapo kuvuta sigareti hakuruhusiwi, kama katika jumba la makumbusho au ukumbi wa maonyesho. Waweza pia kufanya mazoezi—kuogelea au kuendesha baiskeli au kufanya matembezi ya mbali.

Kukabiliana na Kuacha Sigareti

Iwapo wewe ni mvutaji-sigareti sugu, yaelekea utasumbuliwa na dalili za kuacha, ambazo huanza saa chache tu baada ya kuvuta sigareti ya mwisho. Zaweza kutia ndani kukasirika-kasirika, kukosa subira, uhasama, mahangaiko, mshuko-moyo, ukosefu wa usingizi, wasiwasi, hamu kubwa ya chakula, na hamu ya sigareti. Huenda daktari wako akakupa dawa zinazoweza kukusaidia kupunguza hali hizo. Kwa kuongezea, kuna mambo unayoweza kufanya ambayo yanaweza kukusaidia ushinde tatizo hilo.

■ Katika majuma machache magumu ya kwanza, kula vyakula vyenye kalori chache, na unywe maji mengi. Wengine wameona kwamba inasaidia kutafuna mboga mbichi, kama vile karoti au figili. Ukifanya mazoezi, utapunguza uzito wa mwili na kutuliza neva zinazotetema.

■ Epuka hali na mahali ambapo utashawishiwa uvute sigareti.

■ Pambana na mawazo yasiyofaa ambayo huenda yakakushawishi uvute sigareti. Haya ni baadhi ya mawazo ya kawaida unapoacha sigareti: ‘Nitavuta leo tu ili niweze kumudu hali hii ngumu.’ ‘Zoea baya pekee nililo nalo ni kuvuta sigareti!’ ‘Tumbaku haiwezi kuwa mbaya sana; baadhi ya wavutaji sugu huishi kwa miaka zaidi ya 90.’ ‘Hatimaye nitakufa kutokana na jambo fulani.’ ‘Maisha hayapendezi bila tumbaku.’

■ Unapokaribia kuridhiana na kishawishi, kawia. Kwa kusubiri kwa dakika kumi tu, hamu hiyo kali yaweza kwisha. Nyakati nyingine wazo la kutovuta sigareti tena laweza kulemea sana. Unapohisi hivyo, kazia sana kuacha sigareti leo tu.

■ Ikiwa wataka kumtumikia Mungu, sali upate msaada. Muumba wetu mwenye upendo aweza kuandaa “msaada katika wakati ufaao” kwa wale wanaojitahidi kupatanisha maisha yao na mapenzi yake. (Waebrania 4:16) Lakini usitarajie muujiza. Lazima utende kupatana na sala zako.

Dumu Ukiwa Mtu Asiyevuta Sigareti Tena

■ Miezi mitatu ya kwanza ndiyo migumu zaidi, lakini hata baada ya hiyo, epuka iwezekanapo wavutaji-sigareti na hali zinazoweza kukushawishi uvute sigareti.

■ Usijidanganye kwa kufikiri kwamba unaweza kuvuta sigareti mara kwa mara, hata baada ya kuacha kwa mwaka mmoja au zaidi.

■ Kinza kishawishi cha kuvuta “sigareti moja tu.” Sigareti moja tu yaweza kukuongoza kwa urahisi upate nyingine nyingi, na punde si punde utaharibu jitihada zako zote za kuacha. Hata hivyo, unaposhindwa kujiweza kisha unavuta sigareti moja, hakuna sababu ya kuvuta nyingine. Ukianza kuvuta sigareti tena, acha tena.

Mamilioni ya wavutaji-sigareti wamefaulu kuacha. Wewe pia waweza kuacha ukiazimia na kujitahidi bila kukoma!