Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Imani Thabiti Licha ya Mateso

Imani Thabiti Licha ya Mateso

Imani Thabiti Licha ya Mateso

YAPATA miaka 60 iliyopita, Mina Esch alipokea kadi kutoka kwa mume wake, Peter. Ujumbe ulioandikwa kwa mkono ulikuwa mfupi na usioonekana waziwazi. Hata hivyo, alifurahi na kupumzika baada ya kuupokea. Mume wa Mina alikuwa mfungwa katika kambi ya mateso ya Buchenwald, akiwa amepelekwa huko na serikali ya Nazi kwa kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Nyuma ya kadi hiyo kulikuwako taarifa hii fupi: “Mfungwa huyu angali Mwanafunzi wa Biblia mwenye kichwa kigumu [kama Mashahidi wa Yehova walivyojulikana wakati huo] . . . Kwa sababu hii, amenyimwa pendeleo la kuwasiliana.” Ujumbe huu ulimwambia Mina kwamba Peter alikuwa na imani thabiti.

Kadi hiyo, sasa ikiwa imechakaa na kubadilika rangi, imeombwa na Museum of Jewish Heritage—A Living Memorial to the Holocaust, iliyo katika Battery Park, huko New York City. Kadi hiyo, pamoja na picha ya Peter Esch, husaidia kufunua sehemu ndogo ya jambo lenye kuhuzunisha zaidi la binadamu—yale Maangamizi Makubwa—yaliyowaangamiza Wayahudi milioni sita. Maonyesho muhimu ya jumba la makumbusho yana picha 2,000 na sanaa za kihistoria 800 zinazoonyesha mambo waliyojionea jamii ya Wayahudi kuanzia miaka ya 1880 hadi wakati wa sasa, kutia ndani yale Maangamizi Makubwa. Kwa nini Museum of Jewish Heritage ni mahali pafaapo kuonyesha barua ya Peter Esch?

“Jumba hilo la makumbusho limeagizwa lionyeshe historia ya Wayahudi,” akaeleza mwanahistoria wa jumba la makumbusho Dakt. Jud Newborn. “Mashahidi wa Yehova walinyanyaswa kwa sababu ya dini yao. Mashahidi walinyanyaswa hasa kwa sababu ya itikadi zao za kidini na kwa sababu hawakuamini ubaguzi wa jamii, kuapa uaminifu wa kiraia kwa dikteta mwovu wa kilimwengu. Nao hawakuamini katika kupigana vita yake. . . . Wayahudi walijitahidi kudumisha viwango vyao na imani yao dhidi ya upinzani mkali zaidi. Jumba hilo la makumbusho lasherehekea ukinzaji huo wa kiroho. Kwa sababu hiyo, shirika hili pia latambua na kustaajabia imani ya Mashahidi wa Yehova wakati wa enzi ya Nazi.”

Ikiwa katika makao yake ya muda kwenye Museum of Jewish Heritage, barua sahili yaonyesha jitihada ya mwanamume mmoja ambaye uaminifu-mshikamanifu wake kwa Yehova ulitahiniwa. Peter Esch aliokoka mateso ya kambi ya Nazi akiwa na imani thabiti.

[Picha katika ukurasa wa 31]

Museum of Jewish Heritage, huko New York City

[Picha katika ukurasa wa 31]

Esch, mmoja wa Mashahidi wa Yehova, alifungwa gerezani kuanzia 1938 hadi 1945 kwa kukataa kukana itikadi zake