Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Inafaa Kumwabudu Yesu?

Je, Inafaa Kumwabudu Yesu?

Maoni ya Biblia

Je, Inafaa Kumwabudu Yesu?

KATIKA karne zote, watu wengi katika Jumuiya ya Wakristo wamemwabudu Yesu Kristo kana kwamba ni Mungu Mweza Yote. Hata hivyo, Yesu mwenyewe alielekeza uangalifu na ibada kwa Yehova Mungu peke yake. Kwa mfano, aliposihiwa afanye tendo la ibada kwa Ibilisi, Yesu alisema: “Ni Yehova Mungu wako ambaye lazima uabudu, na ni kwake peke yake lazima utoe utumishi mtakatifu.” (Mathayo 4:10) Baadaye Yesu aliwaagiza wanafunzi wake hivi: “Msiite yeyote baba yenu duniani, kwa maana mmoja ni Baba yenu, Aliye wa kimbingu.”—Mathayo 23:9.

Akizungumza na mwanamke Msamaria, Yesu alieleza namna ya ibada ambayo watu wapaswa kumpa Mungu. Lazima ibada yao iwe ya roho na kweli. Kwa kweli, “Baba anawatafuta wa namna hiyo wamwabudu yeye.” (Yohana 4:23, 24) Naam, ibada yapasa kuelekezwa kwa Mungu pekee. Kumwabudu mtu yeyote au kitu chochote kungekuwa namna ya ibada ya sanamu, inayolaumiwa katika Maandiko ya Kiebrania na ya Kigiriki.—Kutoka 20:4, 5; Wagalatia 5:19, 20.

‘Lakini,’ huenda wengine wakabisha, ‘je, Biblia haionyeshi kwamba lazima tumwabudu Yesu pia? Je, Paulo hakusema kwenye Waebrania 1:6: “Acheni kila malaika wa Mungu amwabudu yeye [Yesu]”?’ (King James Version) Twaweza kuelewaje andiko hili kwa kufikiria isemavyo Biblia kuhusu ibada ya sanamu?

Ibada Katika Biblia

Kwanza, lazima tuelewe alilomaanisha Paulo kwa neno ibada. Alitumia neno la Kigiriki pro·sky·neʹo. Kamusi ya Unger’s Bible Dictionary husema kwamba kihalisi neno hilo lamaanisha ‘kubusu mkono wa mtu fulani kama ishara ya staha au shikamoo.’ Kichapo An Expository Dictionary of New Testament Words, cha W. E. Vine, chasema kwamba neno hili “lamaanisha tendo la staha, liwe linafanyiwa mwanadamu . . . au Mungu.” Katika nyakati za Biblia, mara nyingi neno pro·sky·neʹo lilitia ndani kuinamia kihalisi mtu fulani mwenye mamlaka.

Fikiria mfano ambao Yesu alitoa wa mtumwa aliyeshindwa kumlipa bwana wake kiasi kikubwa cha fedha alichowiwa. Namna moja ya neno hili la Kigiriki huonekana katika mfano huu, na inapolitafsiri King James Version yasema kwamba “kisha mtumwa huyo akaanguka chini, na kumwabudu [namna ya pro·sky·neʹo] [mfalme], akisema, Bwana, uwe mwenye subira kwangu, nami nitakulipa kila kitu.” (Mathayo 18:26, italiki ni zetu.) Je, mtu huyo alikuwa akijihusisha na tendo la ibada ya sanamu? Sivyo kamwe! Alikuwa akionyesha tu staha aliyostahili kupewa mfalme ambaye ni bwana na mkubwa wake.

Matendo hayo ya kusujudu, au wonyesho wa staha, yalikuwa ya kawaida katika Nchi za Mashariki katika nyakati za Biblia. Yakobo aliinama mara saba alipokutana na ndugu yake, Esau. (Mwanzo 33:3) Ndugu za Yosefu waliinama kifudifudi mbele zake, au kumsujudia ili kuonyesha staha kwa cheo alichokuwa nacho katika nyumba ya mfalme wa Wamisri. (Mwanzo 42:6) Kwa kufikiria mambo hayo twaweza kuelewa vyema kilichotukia wanajimu walipompata mtoto mchanga Yesu, ambaye walimtambua kuwa “yule aliyezaliwa kuwa mfalme wa Wayahudi.” Kama inavyotafsiriwa kwenye King James Version, simulizi hilo latuambia kwamba “walianguka chini, wakamsujudia [pro·sky·neʹo].”—Mathayo 2:2, 11.

Ni wazi, basi, neno pro·sky·neʹo, lililotafsiriwa “abudu” katika tafsiri fulani za Biblia, halirejezei tu namna ya ibada anayostahili Yehova Mungu. Laweza pia kurejezea staha na heshima anayopewa mtu mwingine. Katika jitihada ya kuepuka kueleweka vibaya kokote, tafsiri fulani za Biblia hutafsiri neno pro·sky·neʹo kwenye Waebrania 1:6 kuwa “kumpa heshima” (New Jerusalem Bible), “kumheshimu” (The Complete Bible in Modern English), “kuinama mbele zake” (Twentieth Century New Testament), au “kumsujudu” (Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo).

Yesu Anastahili Kusujudiwa

Je, Yesu anastahili kusujudiwa? Bila shaka, ndiyo! Katika barua yake kwa Waebrania, mtume Paulo aeleza kwamba akiwa “mrithi wa vitu vyote,” Yesu ‘ameketi kwenye mkono wa kuume wa Ukuu katika mahali palipoinuka sana.” (Waebrania 1:2-4) Hivyo, “katika jina la Yesu kila goti likunjwe la wale walio mbinguni na wale walio duniani na wale walio chini ya ardhi, na kila ulimi ukiri waziwazi kwamba Yesu Kristo ni Bwana kwa utukufu wa Mungu Baba.”—Wafilipi 2:10, 11.

Kwa njia yenye kutokeza, karibuni Kristo atatumia cheo chake kilichokwezwa na mamlaka yake kubwa inayohusiana nacho kugeuza dunia hii kuwa paradiso ya tufeni pote. Chini ya mwelekezo wa Mungu, na kwa sababu ya dhabihu ya fidia ya Yesu, ataondoa huzuni yote ulimwenguni, maumivu, na majonzi ili kunufaisha wale wanaonyenyekea utawala wake wa uadilifu. Kwa hiyo, je, hastahili heshima, staha, na utii kutoka kwetu?—Zaburi 2:12; Isaya 9:6; Luka 23:43; Ufunuo 21:3, 4.

“Mungu Mwenye Kudai Ujitoaji Usiohusisha Wengine”

Hata hivyo, Biblia huonyesha waziwazi kwamba ibada yetu—katika maana ya staha ya kidini na ujitoaji—lazima ielekezwe kwa Mungu peke yake. Musa alimfafanua kuwa “Mungu mwenye kudai ujitoaji usiohusisha wengine.” Nayo Biblia hutuhimiza ‘tumwabudu Yeye aliyezifanya mbingu na dunia na bahari na mabubujiko ya maji.’—Kumbukumbu la Torati 4:24, NW; Ufunuo 14:7.

Hakika Yesu anashiriki sehemu ya maana katika ibada ya kweli, kama mmoja anayestahili heshima na staha. (2 Wakorintho 1:20, 21; 1 Timotheo 2:5) Yeye ndiye njia pekee ambayo kupitia hiyo twaweza kumkaribia Yehova Mungu. (Yohana 14:6) Kupatana na hilo, Wakristo wa kweli hufanya vyema kumwabudu Yehova Mungu Mweza Yote pekee.