Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yote Hayo Yamaanisha Nini?

Yote Hayo Yamaanisha Nini?

Yote Hayo Yamaanisha Nini?

IKIWA ungechanganua viwango vya maadili katika miaka ya karibuni, ungeona mwelekeo dhahiri. Bila shaka, viwango vya kiadili vinazidi kuzorota miongoni mwa idadi inayoongezeka ya watu. Maana halisi ya hilo ni nini?

Je, yamaanisha, kama wengine wadaivyo kwamba ustaarabu wetu wote na wanadamu wote wamehukumiwa maangamizi au wanakaribia kuangamizwa? Au je, mabadiliko hayo ni sehemu tu ya kuzorota na kuboreka kwa hali ambako ni kwa kawaida katika historia?

Watu wengi hufikiri hivyo. Wanaona kuvunjika kwa maadili katika siku zetu kuwa mojawapo tu kati ya mielekeo mingi, ambayo imekuwapo katika historia yote. Wanatarajia kabisa kwamba hatimaye mwelekeo wa kawaida utarudi na kwamba viwango vya juu vya maadili vitarejea. Je, wako sahihi?

“Siku za Mwisho”

Acheni tuzingatie mambo hakika kwa kufikiria kitabu ambacho kwa karne nyingi kilikuwa na mamlaka inayokubaliwa na wengi kuhusu masuala ya kiadili—Neno la Mungu, Biblia. Inaelimisha sana kulinganisha ulimwengu wa leo na ufafanuzi wa unabii unaotolewa katika Biblia kuhusu muhula wa kukata maneno katika historia ya kibinadamu. Hiki ndicho kipindi inachokiita “siku za mwisho” au “umalizio wa mfumo wa mambo.” (2 Timotheo 3:1; Mathayo 24:3) Kama idokezwavyo na semi hizo, kipindi hiki kitaashiria mwisho hususa wa kipindi maalumu na mwanzo wa kipindi kingine kipya.

Neno la Mungu lilitabiri kwamba siku za mwisho zingeashiriwa na “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” Ili kusaidia watazamaji walio makini watambue siku za mwisho, Biblia hutoa habari kadhaa ambazo kwa pamoja hufanyiza ufafanuzi dhahiri, au ishara yenye mambo mengi, ya kipindi hiki cha pekee.

Tabia Mbaya za Watu

Ona mojawapo ya ishara hizo ambayo ni yenye kutokeza zaidi leo: “Watu watakuwa na namna ya ujitoaji-kimungu lakini wakithibitika kuwa si kweli kwa nguvu ya hiyo.” (2 Timotheo 3:2, 5) Hakujawa na kipindi kingine katika historia kilichotiwa alama na kupuuzwa kabisa kwa dini kwa njia ya kupindukia. Mungu amepuuzwa kila mahali kuwa mamlaka pekee, na watu wengi hawaikubali Biblia kuwa chanzo pekee cha kweli. Bila shaka, kungali kuna dini, lakini nyingi zina uvutano mdogo. Zimekuwa wonyesho tu.

Biblia hutaja sehemu nyingine ya ishara hiyo: “Watu watakuwa . . . wasio na hali ya kujidhibiti, wakali,” na “kwa sababu ya kuongezeka kwa uasi-sheria upendo wa idadi iliyo kubwa zaidi utapoa.” (2 Timotheo 3:2, 3; Mathayo 24:12) Neno la Kigiriki lililotafsiriwa “kali” lamaanisha, miongoni mwa mambo mengine, “kukosa hisia-mwenzi za kibinadamu.” Leo watoto wachanga zaidi wanadhihirika kuwa “wakali” na wanafanya uhalifu unaozidi kuwa wenye jeuri.

Zaidi ya hilo, maendeleo ya haraka ya tekinolojia na ya kiuchumi na pupa ambayo imesababishwa nayo yamefanya watu wengi zaidi wapuuze maadili ya zamani. Bila kuwajali wengine, wanatumia njia yoyote ile, pamoja na njia zisizo za haki, kunyakua vitu vingi kadiri wawezavyo ili kutosheleza tamaa yao ya kichoyo. Ongezeko kubwa la kucheza kamari ni uthibitisho mwingine wa uchoyo, na takwimu za uhalifu uliofanywa miongo michache iliyopita zadhihirisha kabisa jambo hilo.

Jambo ambalo limeenea hasa katika kipindi chetu ni hili: “Watu watakuwa . . . wenye kuzipenda raha badala ya kuwa wapenda-Mungu.” (2 Timotheo 3:2, 4) Mfano mmoja wa hilo ni kwamba watu wanataka raha za kimwili, lakini hawataki daraka la kuishi na mwenzi mmoja wa ndoa maishani. Tokeo limekuwa visa vingi vya familia zilizovunjika, watoto wasio na furaha na ufungamano wa familia, wazazi wasio na wenzi, na maradhi ya kuambukizwa kingono.

Jambo jingine kuhusu ishara hiyo ni kwamba “watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wapenda-fedha.” (2 Timotheo 3:2) Kulingana na gazeti la Kijerumani Die Zeit, “ubinafsi ndio huchochea mfumo wa [kiuchumi wa leo].” Ufuatiaji wa pesa ndio jambo la maana zaidi maishani mwa wengi kuliko wakati mwingine wowote. Maadili mengine hupuuzwa katika ufuatiaji huu wa kibinafsi.

Matukio ya Ulimwengu

Mbali na kufafanua kuporomoka kwa maadili ya kibinadamu, Biblia pia ilitabiri kwamba siku za mwisho zingetiwa alama na mabadiliko makubwa yasiyo ya kawaida ambayo yangeathiri familia ya kibinadamu. Kwa mfano, inasema kwamba “taifa litainuka dhidi ya taifa, na ufalme dhidi ya ufalme; na kutakuwa na matetemeko makubwa ya dunia, na katika mahali pamoja baada ya pengine magonjwa ya kuambukiza na upungufu wa chakula.”—Luka 21:10, 11.

Mbali na karne ya 20, hakujawa na kipindi kingine katika historia ambapo watu wengi sana wamehusika na misiba mikuu katika kipindi kifupi kama hicho. Mathalani, zaidi ya watu milioni 100 walikufa katika vita wakati huo, idadi iliyo kubwa zaidi kuliko idadi ya makafara wa vita katika karne kadhaa zilizopita wanapojumlishwa pamoja. Karne ya 20 ilitokeza vita viwili vilivyokuwa tofauti kabisa na vingine hivi kwamba vikaitwa vita vya ulimwengu. Mapambano ya ulimwenguni pote kama hayo hayakuwa yamepata kutokea.

Kichocheo Kutoka kwa Kani Mbovu

Biblia hufunua pia kuwepo kwa kiumbe mwovu wa roho mwenye nguvu, “aitwaye Ibilisi na Shetani,” ambaye kusudi lake ni kushawishi watu waache maadili ya kweli na kuwatumbukiza kwenye ufisadi wa kiadili. Inasema kwamba katika siku za mwisho, ameteremka kwenye dunia, “akiwa na hasira kubwa, akijua ana kipindi kifupi cha wakati.”—Ufunuo 12:9, 12.

Katika Biblia Ibilisi hufafanuliwa kuwa “mtawala wa mamlaka ya hewa, roho ambayo sasa hutenda katika wana wa kutotii.” (Waefeso 2:2) Hilo ladokeza kwamba Ibilisi hudhihirisha uvutano wenye nguvu juu ya wanadamu wengi, kwa kawaida bila wao kutambua, kama vile huenda nyakati nyingine tukakosa kuona kichafuzi katika hewa.

Kwa mfano, uvutano wa Shetani huonekana katika njia nyingi za mawasiliano ya kisasa: vidio, sinema, televisheni, Internet, matangazo ya biashara, vitabu, na magazeti. Habari nyingi, hasa ile inayoelekezwa kwa vijana wasio na ujuzi, imejaa mielekeo yenye kuchukiza, kama vile ubaguzi wa rangi, uchawi, ukosefu wa adili, na jeuri ya kikatili.

Watu wengi wenye moyo mweupe wamevutiwa na ufanano kati ya ufafanuzi wa Biblia kuhusu siku za mwisho na hali halisi katika ulimwengu wa leo. Ni kweli kwamba kumekuwa na matukio fulani katika historia kabla ya karne ya 20 ambayo kwa kadiri ndogo yalilingana na ufafanuzi wa Biblia. Lakini mambo yote yahusuyo ile ishara yameonekana tu katika karne ya 20, na sasa katika karne ya 21.

Kipindi Kipya Maalumu Kinachokuja

Wale wanaoamini kwamba wanadamu wataangamizwa, na wale wanaodai kwamba mambo yataendelea kama kawaida wamekosea. Badala yake, Biblia huonyesha waziwazi kwamba mahali pa jamii ya ulimwengu ya sasa inayotawala dunia patachukuliwa na kitu fulani kipya kabisa.

Baada ya Yesu kuorodhesha idadi kadhaa ya matukio ya ishara ya siku za mwisho, alisema: “Katika njia hii nyinyi pia, wakati mwonapo mambo hayo yakitukia, jueni kwamba ufalme wa Mungu uko karibu.” (Luka 21:31) Ufalme wa Mungu wa kimbingu ndio uliokuwa kichwa kikuu cha mahubiri ya Yesu. (Mathayo 6:9, 10) Naye Mungu alimteua awe Mfalme wa Ufalme huo, ambao ni serikali itakayotawala dunia yote hivi karibuni.—Luka 8:1; Ufunuo 11:15; 20:1-6.

Mwishoni mwa siku za mwisho, Ufalme wa Mungu wa kimbingu mikononi mwa Kristo utaondoa wote ambao ni maadui wake—Ibilisi na wale wanaomuunga mkono—na kuleta ulimwengu mpya wa uadilifu badala ya jamii ya sasa iliyozorota kiadili. (Danieli 2: 44) Katika ulimwengu huo mpya, watu wenye moyo mzuri watafurahia uhai udumuo milele katika dunia iliyogeuzwa kuwa paradiso.—Luka 23:43; 2 Petro 3:13; Ufunuo 21:3, 4.

Wale ambao wanachukia sana kupotoka kwa sasa kwa maadili na kutambua kwamba ishara yenye mambo mengi ya siku hizi za mwisho inatimizwa kwa matukio ya kisasa wanaweza kutazamia wakati ujao mtukufu. Kwa sababu hiyo tunamshukuru Mungu Mweza Yote, anayetujali sisi wanadamu na ambaye ana kusudi tukufu kwa uumbaji wake, dunia.—Zaburi 37:10, 11, 29; 1 Petro 5:6, 7.

Mashahidi wa Yehova wanakualika ujifunze mengi kuhusu Muumba wetu mwenye upendo na tazamio la uhai katika ulimwengu safi kiadili, aliotayarishia wote wanaomtafuta. Kama isemavyo Biblia, ‘hii yamaanisha uhai udumuo milele, wao kuendelea kutwaa ujuzi juu yako wewe, Mungu pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.’—Yohana 17:3.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Watu wenye moyo mnyoofu watafurahia uhai usiokoma katika dunia paradiso