Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Ulimwengu Utaungana?

Je, Ulimwengu Utaungana?

Je, Ulimwengu Utaungana?

KATIKA miaka ya hivi karibuni mamilioni ya watu katika Ulaya Mashariki na kwingineko wametaabishwa na vita yenye kugawanya. Ijapokuwa hivyo, hata wakati mapambano hayo ya kikatili yalipokuwa yakiendelea, maelfu ya watu katika nchi hizi zilizokumbwa na vita waliweza kusitawisha na kudumisha muungano wa kweli miongoni mwao. Fikiria mifano michache.

Katika mwaka wa 1991 umati wa watu wapatao 15,000 kutoka mataifa yote ulikutanika Zagreb, Kroatia. Polisi mmoja katika eneo hilo alichochewa kusema hivi: “Ingekuwa vyema kuwaonyesha waandishi wa habari mambo yanayoendelea katika stediamu hii, papa hapa, ambapo twaona Waserbia, Wakroatia, Waslovenia, Wamontenegro, na wengineo wakiketi pamoja kwa amani.” Ni nini huchangia muungano huo usio wa kawaida?

Katika mwaka wa 1993 mkusanyiko wa kimataifa mkubwa hata zaidi, wenye kichwa “Ufundishaji wa Kimungu,” ulifanywa Kiev, jiji kuu la Ukrainia. Kulikuwa na kilele cha wahudhuriaji wapatao 65,000. Ukurasa wa mbele wa gazeti la Evening Kiev uliripoti hivi: “Mashahidi wa Yehova . . . wameunganishwa, si na beji za buluu peke yake zilizoandikwa ‘Ufundishaji wa Kimungu,’ bali pia na imani ya kweli.”

Ufundishaji wa Kimungu —Kani ya Muungano

Je, unashangaa ni kwa nini Mashahidi wa Yehova hufurahia muungano huku ukosefu wa muungano ukiwa umeenea kila mahali? Profesa wa Poland Wojciech Modzelewski atambulisha sababu hiyo kwa kusema hivi kuhusu Mashahidi: “Jambo kuu linalochangia mtazamo wao wa amani ni azimio la kufuata kanuni ambazo kwa sasa zimefunuliwa katika Biblia.” Kwa kweli, Mashahidi wameunganishwa ulimwenguni pote na ufundishaji wa kimungu kuhusu Muumba, Yehova Mungu. Ni ufundishaji gani huo?

Yesu Kristo alitaja kanuni moja muhimu yenye kuunganisha aliposema hivi kuhusu wafuasi wake: “Wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile mimi si sehemu ya ulimwengu.” Ndiyo, Mashahidi wa Yehova kila mahali huunganishwa na msimamo wao wa kutokuwamo. Hilo lapatana na maneno ya Yesu aliposali hivi: “Nafanya ombi . . . ili wote wapate kuwa mmoja, kama vile wewe, Baba, umo katika muungano na mimi na mimi nimo katika muungano na wewe, ili wao pia wapate kuwa katika muungano na sisi.”—Yohana 17:16-21.

Msimamo huu wa kutokuwamo ni kani ya muungano kwa sababu huwachochea Mashahidi katika sehemu zote za ulimwengu waishi kupatana na maneno yaliyosemwa na nabii Isaya kuhusu wote ambao Mungu ‘atawafundisha . . . njia zake.’ Isaya alisema kwamba watu hao wangelazimika ‘kufua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu.’ Nabii huyo aliendelea kusema: “Taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe.”—Isaya 2:2-4.

Amani na muungano ulioonekana kwenye mikusanyiko ya Mashahidi wa Yehova katika Ulaya Mashariki katika mwongo uliopita waonyesha kwamba tayari unabii wa Isaya unatimizwa kwa kiwango kidogo. Katika Ulaya na kwingineko, Mashahidi wamefua panga zao kuwa majembe na mikuki yao kuwa miundu kwa njia ya kitamathali. Tokeo limekuwa kwamba wanafurahia amani na muungano katika ulimwengu huu usio na muungano. Si ajabu kwamba safu moja ya mhariri ilisema hivi: “Ikiwa ulimwengu wote ungeishi kwa imani ya [Biblia] ya Mashahidi [wa Yehova] umwagikaji wa damu na chuki ungekoma, na upendo ungetawala kama mfalme”! Je, hali itapata kuwa hivyo?

Jinsi Muungano wa Ulimwenguni Pote Utakavyopatikana

Ili kuleta muungano duniani pote, mengi zaidi yahitajiwa kuliko kikundi kidogo tu cha watu wenye nia njema. Pia kunahitajika serikali yenye uwezo wa kudhibiti uvutano wa watu wanaopinga amani na muungano. Kwa hakika, Yesu alifunza wafuasi wake waombe ili kupata serikali hiyo: “Acha ufalme wako uje. Mapenzi yako na yatendeke, kama ilivyo katika mbingu, pia juu ya dunia.” (Mathayo 6:10) Ndiyo, Yesu alionyesha kwamba ni serikali ya Mungu, “ufalme wa kimbingu,” uwezao kutatua matatizo ya ulimwengu—kutia ndani tatizo la ukosefu wa muungano.—Mathayo 4:17.

Yesu Kristo ndiye Mfalme wa Ufalme huu wa kimbingu. Chini ya utawala wake watu watafurahia amani na muungano usio na kifani duniani. Muungano huo wa ulimwenguni pote hautaletwa na marekebisho ya kiuchumi ya binadamu. Ni serikali ya ulimwengu chini ya “Mfalme wa amani” itakayoweza kufanya jambo hilo.—Isaya 9:6, 7.

Mfalme wa Amani hatavumilia ukosefu wa haki uliopo, ambao mara nyingi husababishwa na umaskini na kutumia mamlaka vibaya. Biblia yaahidi: “Wafalme wote na wamsujudie; na mataifa yote wamtumikie. Kwa maana atamkomboa mhitaji aliapo, na mtu aliyeonewa iwapo hana msaidizi. Atawakomboa nafsi zao na kuonewa na udhalimu . . . Na uwepo wingi wa nafaka katika ardhi juu ya milima; matunda yake na yawaye-waye.”—Zaburi 72:11, 12, 14, 16.

Pia ukosefu wa kazi ya kuajiriwa hautakuwapo chini ya utawala wa Kristo. Nabii Isaya asema: “Hawatajenga akakaa mtu mwingine ndani yake; hawatapanda akala mtu mwingine; maana kama siku za mti ndivyo zitakavyokuwa siku za watu wangu, na wateule wangu wataifurahia kazi ya mikono yao muda wa siku nyingi.” (Isaya 65:22) Wazia, kila mtu duniani ataweza kufanya kazi ya maana yenye kuridhisha!

Muungano wa Kweli—Lini?

Lakini utawala wa Kristo juu ya dunia utaanza lini? Katika kujibu swali hilo, Yesu Kristo alitaja kipindi ambacho kingekuwa na vita, ripoti za vita, maradhi, matetemeko ya dunia, na matukio mengine. Hata hivyo, alitaja pia utendaji unaofaa—kuhubiriwa kwa habari njema za Ufalme wa Mungu ulimwenguni pote. (Mathayo 24:3-14; Luka 21:11) Yesu alisema matukio haya yatafikia upeo kwenye “dhiki kubwa” itakayotangulia badiliko kamili la utawala wa dunia. (Mathayo 24:21) Soma hotuba hiyo iliyorekodiwa katika Mathayo sura ya 24 na Luka sura ya 21. Linganisha hali anazotabiri na yale unayoona ulimwenguni. Unaweza kuona waziwazi kwamba sasa tunaishi karibu sana na siku ambayo Mungu ataingilia kati utawala wa wanadamu. Ufalme wake, Yesu Kristo akiwa Mfalme, utaanza kutawala. Ulimwengu ulioungana uko mbele!

Swali labaki, Unapaswa kufanya nini ili kuona utimizo wa ahadi hii? Kwa kuwa Biblia huchangia fungu la maana katika mataraja ya wakati ujao ya wanadamu, ni jambo la hekima kujitahidi kujua Biblia vyema. Kwa hiyo, Mashahidi wa Yehova watafurahi kukutembelea nyumbani ili wajifunze Biblia nawe bila malipo. * Ukikubali funzo hilo, karibuni utaona kwamba muungano wa ulimwengu unaweza kupatikana na kwamba hata wewe pia unaweza kuufurahia!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 17 Ikiwa ungependa kupokea habari zaidi kuhusu programu hiyo ya funzo la Biblia, wasiliana na wachapishaji wa gazeti hili au Mashahidi wa Yehova katika jumuiya yenu.

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Mashahidi wa Yehova hufurahia muungano usio wa kawaida ulimwenguni kote

Kiev, Ukrainia

Zagreb, Kroatia

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kusudi la Mungu ni kwamba wanadamu wawe familia moja ya ulimwenguni pote iliyoungana