Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Upendo wa Kikristo Wakati wa Volkeno

Upendo wa Kikristo Wakati wa Volkeno

Upendo wa Kikristo Wakati wa Volkeno

NA MLETA-HABARI WA AMKENI! KATIKA KAMERUN

MLIPUKO mkubwa ulitokea mwaka jana katika nchi ya Afrika Magharibi ya Kamerun. Mlima Kamerun ni wenye urefu wa meta 4,070 juu ya usawa wa bahari. Mlipuko huo—ukiwa wa tano kutokea katika karne ya 20—uliripotiwa kuwa mbaya zaidi kufikia sasa.

Kwanza msiba huo ulitokea Jumamosi alasiri, Machi 27, 1999. Watu waliojionea katika mji wa Buea, ulio chini ya mlima huo, waliripoti kwamba kuta, nyumba, na hata miti ilitikisika vibaya sana. Jioni iliyofuata, saa mbili na nusu hivi, tetemeko kubwa lenye nguvu zaidi lilitikisa eneo hilo. Lilifikia umbali wa kilometa 70 huko Douala. Kichwa kikuu cha gazeti la Le Messager la Jumanne, Machi 30, 1999, kilitangaza hivi: “Mlipuko wa Mlima Kamerun—Watu 250,000 Wakabili Hatari ya Moto.” Gazeti hilo liliendelea kusema: “Dunia ilitetemeka mara 50 kwa siku mbili; tayari mashimo manne yametokea baada ya mlipuko; mamia ya nyumba zimeharibiwa; nyumba ya rais huko Buea imebomoka kabisa.”

Mashahidi wa Yehova wapatao 80 huishi Buea. Nyumba nyingi ziliharibiwa kabisa, kutia ndani moja iliyotumiwa kuwa Jumba la Ufalme. Hata hivyo, hakuna mtu aliyekufa.

Upendo wa Kikristo Waonekana

Upendo wa Kikristo ulionyeshwa mara moja kwa kurekebisha uharibifu uliosababishwa na mlipuko huo mbaya. Halmashauri ya kutoa msaada ilianzishwa, Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova lilipanga kuandaa fedha kadhaa zilizohitajiwa sana, na mamia ya Mashahidi walijitolea kwa hiari kutumia wakati, nishati, na pesa zao.

Makutaniko ya Mashahidi wa Yehova yalipeleka chakula. Shahidi mmoja alitoa matofali 1,000 ya saruji. Mwingine alipanga ununuzi wa mabati ya kuezeka kwa bei nafuu. Na mwingine alitembea kilometa 16 kupata mbao. Mwanamume mmoja kijana ambaye alikuwa ameweka pesa akibani ili kulipia mahari kwa wale ambao wangekuwa wakwe zake, aliahirisha harusi na kutumia pesa hizo kurekebisha msumeno wake wa mnyororo. Kisha akaenda msituni, ambapo kwa majuma matatu alikata magogo ya nyumba nzima! Ndugu vijana Wakristo walibeba mbao kwenye vichwa vyao kwa umbali wa kilometa tano, ambapo gari la kubebea mizigo lilizichukua.

Ujenzi ukaanza Aprili 24 wakati wajitoleaji 60 walipokutana penye msiba. Wakati wa miisho-juma iliyofuata, idadi iliongezeka hadi kufikia kilele cha watu 200. Mashahidi wawili wenye kazi za wakati wote walikuja baada ya kazi yao ya kawaida siku hiyo nao wakajenga hadi baada ya saa sita usiku. Shahidi mmoja kutoka Douala alikwenda kazini alikoajiriwa asubuhi yote; kisha akasafiri kwa pikipiki yake kilometa 70 naye akafanya kazi mpaka saa sita usiku kabla ya kurudi nyumbani. Nyumba sita zilikamilishwa kwa muda usiozidi miezi miwili. Wakati uleule, kutaniko la Buea liliendelea kufanya mikutano katika makao ya faragha, ingawa hudhurio la mkutano lilikuwa maradufu ya idadi ya washiriki wa kutaniko.

Wakati huohuo, halmashauri ya kutoa msaada iligawanya zaidi ya vidonge 40,000 vya kusafishia maji machafu na kuwatunza hospitalini watu kumi hivi waliokuwa na magonjwa ya kupumua yaliyosababishwa na gesi yenye sumu na jivu la volkeno. Matokeo yalikuwa nini kwa wale walioshuhudia upendo huo wa Kikristo?

Upendo wa Kikristo Watia Fora

Baada ya kuona mojawapo ya nyumba zilizojengwa na akina ndugu, mwanamume mmoja kutoka katika Baraza la Mkoa la Kilimo alisema: “Nyumba hiyo yenyewe ni ushahidi mkubwa . . . , wonyesho wa upendo.” Mwalimu mmoja alieleza hivi: “Sijapata kuona kamwe jambo kama hilo maishani mwangu. . . . Hiyo kwa kweli ni ishara ya Ukristo wa kweli.”

Wale walionufaika binafsi vilevile walieleza vivyo hivyo. Timothy, mwenye umri wa miaka 65 na mgonjwa-mgonjwa, aliandika: “Kila mara tuangaliapo nyumba yetu mpya, machozi ya shangwe hututiririka. Twaendelea kumshukuru Yehova kwa yale ambayo ametufanyia.” Mjane mwenye watoto wanne ambaye si mmoja wa Mashahidi wa Yehova alipoteza kila kitu nyumba yao ilipoporomoka. Kisha wale walioajiriwa kumsaidia wakaiba vifaa vyake vya kuezekea paa. Wajitoleaji Mashahidi walimsaidia. Yeye alisema hivi: “Sijui nishukuruje. Moyo wangu umejaa shangwe.” Elizabeth, mke wa mzee Mkristo, alisema hivi: “Ninafurahi kwamba kuna upendo katika tengenezo la Yehova. Yaonyesha kwamba twamtumikia Mungu aliye hai.”

Mlipuko wa volkeno ulikuwa mkubwa sana, lakini haungeweza kukomesha upendo wa Kikristo wa udugu huo. Kama vile mtume Paulo alivyopuliziwa kuandika, “upendo haushindwi kamwe.”—1 Wakorintho 13:8.

[Picha katika ukurasa wa 16]

Lava iliyoyeyuka iliyo kama mto ilisababisha uharibifu mkubwa sana

[Picha katika ukurasa wa 17]

Wenye kujitolea walifanya kazi kwa bidii kujenga upya nyumba zilizoharibiwa

[Picha katika ukurasa wa 16, 17]

Mlima Kamerun