Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi ya Kukabiliana na Hali ya Kukata Tamaa

Jinsi ya Kukabiliana na Hali ya Kukata Tamaa

Maoni ya Biblia

Jinsi ya Kukabiliana na Hali ya Kukata Tamaa

KUKATA tamaa ni jambo la kawaida kwa wanadamu wote, angalau kwa kiasi fulani. Hata hivyo, kwa wengine, hali ya kukata tamaa huwa mbaya sana hivi kwamba inakuwa afadhali kufa kuliko kuishi.

Biblia huonyesha kwamba hata watumishi waaminifu wa Mungu hupatwa na matatizo na mikazo inayoongoza kwenye kukata tamaa. Kwa mfano, fikiria Eliya na Yobu—wote wawili walifurahia uhusiano mzuri na Mungu. Baada ya kukimbia ili asiuawe na Malkia mwovu Yezebeli, Eliya ‘aliomba afe.’ (1 Wafalme 19:1-4, Biblia Habari Njema) Mwanadamu mwadilifu Yobu alipatwa na misiba mingi, kutia ndani maradhi ya kuchukiza na kufa kwa watoto kumi. (Ayubu 1:13-19; 2:7, 8) Hali yake ya kukata tamaa ilimfanya aseme: “Ni afadhali nife kuliko kupata mateso haya yote.” (Ayubu 7:15, The New English Bible) Bila shaka, watumishi hao waaminifu wa Mungu walikuwa na mahangaiko mengi sana.

Huenda watu fulani leo wakakata tamaa kwa sababu ya athari zenye kuumiza za uzee, kifo cha mwenzi wa ndoa, au magumu ya kifedha. Wengine huona kwamba mkazo wa daima, kuendelea kukumbuka mambo yenye kuvuruga, au matatizo ya familia huwafanya wahisi kana kwamba wanatatanika katikati ya bahari, kila wimbi likifanya iwe vigumu zaidi kufika ukingoni. Mtu mmoja alisema: “Unahisi hufai kabisa—kana kwamba hakuna mtu atakayekukumbuka ukifa. Nyakati nyingine mtu huhisi upweke usiovumilika.”

Katika visa fulani hali hubadilika na kuwa bora, na kupunguza mkazo huo mkubwa. Lakini vipi ikiwa hali zetu hazitabadilika? Biblia inaweza kutusaidiaje kukabiliana na hali ya kukata tamaa?

Biblia Inaweza Kusaidia

Yehova alikuwa na uwezo na nguvu za kumtegemeza Eliya na Yobu katika magumu yao. (1 Wafalme 19:10-12; Ayubu 42:1-6) Ni faraja iliyoje leo kutambua jambo hilo! Biblia husema: “Mungu kwetu sisi ni kimbilio na nguvu; msaada utakaoonekana tele wakati wa mateso.” (Zaburi 46:1; 55:22) Ingawa huenda ikaonekana kwamba tunalemewa na kukata tamaa, Yehova anaahidi kwamba atatushika kwa mkono wa kuume wa haki yake. (Isaya 41:10) Twaweza kunufaikaje na msaada huo?

Biblia hueleza kwamba kupitia sala “amani ya Mungu izidiyo fikira yote kwa ubora italinda mioyo [yetu] na nguvu [zetu] za akili kwa njia ya Kristo Yesu.” (Wafilipi 4:6, 7) Kwa sababu ya msononeko wetu huenda tusione utatuzi wa matatizo yetu. Hata hivyo, ‘tukidumu katika sala,’ Yehova anaweza kulinda mioyo na akili zetu, akitupa nguvu tunayohitaji ili kuvumilia.—Waroma 12:12; Isaya 40:28-31; 2 Wakorintho 1:3, 4; Wafilipi 4:13.

Tutanufaika tukisema mambo waziwazi katika sala zetu. Ingawa huenda ikawa vigumu kueleza mawazo yetu, twapaswa kuwa huru kuzungumza na Yehova kuhusu jinsi tunavyohisi na kile tunachoona kuwa kiini cha tatizo. Twahitaji kumwomba nguvu ya kututegemeza kila siku. Tuna uhakikisho huu: “Atawafanyia wamchao matakwa yao, naye atasikia kilio chao na kuwaokoa.”—Zaburi 145:19.

Mbali na kusali, twapaswa kuepuka kujitenga na wengine. (Mithali 18:1) Wengine wamepata nguvu kwa kutumia wakati na nguvu zao kusaidia wengine. (Mithali 19:17; Luka 6:38) Mfikirie mwanamke anayeitwa Maria, * ambaye, mbali na kupambana na kansa alipoteza washiriki wanane wa familia katika kipindi cha mwaka mmoja tu. Ilimbidi Maria ajilazimishe kutoka kitandani na kurudia utendaji wa kawaida. Alienda kuwafundisha wengine Biblia karibu kila siku, na alihudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida. Baada ya kurudi nyumbani, Maria angepatwa na msononeko mkubwa sana. Hata hivyo, kwa kukazia jinsi anavyoweza kusaidia wengine, Maria anaweza kuvumilia.

Lakini vipi ikiwa twaona ugumu kusali na hatuwezi kushinda hali ya upweke? Katika hali hiyo lazima tutafute msaada. Biblia hututia moyo tuwaendee “wanaume wazee wa kutaniko.” (Yakobo 5:13-16) Mtu mmoja anayepambana na mshuko-moyo mbaya sana unaoendelea alisema: “Nyakati fulani kuzungumza na mtu unayemtumaini husaidia kutuliza akili na moyo, na hukuwezesha ufikiri kwa njia ya busara.” (Mithali 17:17) Bila shaka, wakati hali ya kukata tamaa inapoendelea kwa muda mrefu na kuonyesha kuwa kuna tatizo la kitiba, huenda msaada kutoka kwa wataalamu ukahitajiwa pia. *Mathayo 9:12.

Ijapokuwa hakuna utatuzi rahisi, hatupaswi kudharau uwezo wa Mungu wa kutusaidia kukabiliana na matatizo yetu. (2 Wakorintho 4:8) Kudumu katika sala, kuepuka hali ya upweke, na kupokea msaada kutoka kwa wataalamu kutatusaidia tupate kujiimarisha tena. Biblia huahidi kwamba Mungu atakomesha kabisa kiini cha kukata tamaa sana. Wakristo wameazimia kumtegemea wanapongojea siku ambayo “mambo [haya] ya kwanza hayatakumbukwa.”—Isaya 65:17; Ufunuo 21:4.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 11 Si jina lake halisi.

^ fu. 12 Amkeni! haliungi mkono tiba yoyote hususa. Wakristo wapaswa kuhakikisha kwamba tiba yoyote wanayopokea haipingani na kanuni za Biblia. Kwa habari zaidi, ona Mnara wa Mlinzi, Oktoba 15, 1988, ukurasa wa 25-29.