Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Ambavyo Familia Hukabiliana na Ugonjwa wa Kudumu

Jinsi Ambavyo Familia Hukabiliana na Ugonjwa wa Kudumu

Jinsi Ambavyo Familia Hukabiliana na Ugonjwa wa Kudumu

KUKABILIANA kwaweza kufasiliwa kuwa “uwezo wa kushughulika kwa matokeo na mikazo uliyo nayo.” (Taber’s Cyclopedic Medical Dictionary) Kwahusisha kukabili matatizo ya ugonjwa wa kudumu katika njia ambayo unaweza kuyadhibiti kwa kiasi fulani na kufurahia amani ya akili. Kwa sababu ugonjwa wa kudumu ni suala la familia, utegemezo mwaminifu na wenye upendo kutoka kwa kila mshiriki wa familia wahitajiwa ili familia ikabiliane kwa mafanikio na hali hiyo. Acheni tuchunguze baadhi ya njia ambazo familia hukabiliana na ugonjwa wa kudumu.

Thamani ya Ujuzi

Huenda isiwezekane kuponya ulemavu huo, lakini kujua namna ya kukabiliana kwaweza kupunguza athari za kiakili na za kihisia-moyo ziletwazo na ugonjwa huo. Hilo lapatana na mithali ya kale inayosema: “Mtu mwenye hekima ana nguvu.” (Mithali 24:5) Familia yaweza kupataje ujuzi kuhusu namna ya kukabiliana na hali hiyo?

Hatua ya kwanza ni kutafuta daktari aliye tayari kuwasiliana na kusaidia, ambaye yuko tayari kutumia wakati kumweleza mgonjwa na familia kila jambo kwa makini. “Daktari bora,” chasema kitabu A Special Child in the Family, “hujali familia yote nzima na vilevile huwa na stadi zote za kitiba zinazohitajika.”

Hatua ya pili ni kuendelea kuuliza maswali hususa mpaka uelewe kabisa hali kadiri uwezavyo. Hata hivyo, kumbuka kwamba unapokuwa na daktari, ni rahisi kupatwa na wasiwasi na kutatanika na hivyo kusahau kile ulichotaka kuuliza. Dokezo moja linalosaidia ni kuandika maswali kimbele. Huenda ukataka kujua kihususa ni nini unachoweza kutazamia kutokana na ugonjwa huo na matibabu yake na kile unachoweza kufanya. —Ona sanduku “Maswali Ambayo Familia Yaweza Kuuliza Daktari.”

Ni muhimu hasa kuandalia ndugu na dada za mtoto mwenye ugonjwa wa kudumu habari ya kutosha. “Eleza tatizo kuanzia siku za kwanza-kwanza,” apendekeza mama mmoja. “Wanaweza kuona kana kwamba wametengwa na familia ikiwa hawaelewi kile kinachotukia.”

Familia fulani pia zimepata habari inayosaidia kwa kufanya utafiti kwenye maktaba, duka la vitabu, au katika Internet—mara nyingi zimepata habari chungu nzima ihusuyo magonjwa hususa.

Kudumisha Maisha Bora kwa Kadiri Fulani

Ni jambo la asili kwa washiriki wa familia kutaka kudumisha maisha bora kwa kadiri fulani kwa ajili ya mgonjwa. Fikiria mfano wa Neil du Toit, aliyetajwa katika makala ya kwanza. Angali anafadhaishwa na udhaifu unaosababishwa na maradhi yake. Hata hivyo, yeye hutumia karibu saa 70 kwa mwezi katika utendaji unaomletea shangwe zaidi—kuzungumza na watu katika jumuiya yake kuhusu tumaini lake linalotegemea Biblia. “Mimi huridhika pia moyoni,” asema, “kufundisha kutaniko maagizo ya Biblia.”

Maisha bora pia hutia ndani kuonyesha na kuonyeshwa upendo, kufurahia utendaji unaopendeza, na kuwa na tumaini. Wagonjwa wangetaka kuendelea kufurahia maisha kadiri ugonjwa wao na matibabu yao yatakavyoruhusu. Baba mmoja ambaye familia yake imekabiliana na ugonjwa kwa zaidi ya miaka 25 asema: “Tunapenda kutalii, lakini kwa sababu ya udhaifu wa mwanangu, hatuwezi kusafiri kwa miguu. Kwa hiyo tunafanya hivyo kwa njia tofauti. Tunaenda katika sehemu ambazo hazihitaji utendaji wa kutumia nguvu.”

Naam, bado wagonjwa huwa na uwezo mbalimbali unaowapa uradhi wa kadiri fulani maishani. Ikitegemea asili ya ugonjwa wenyewe, bado wengi wanaweza kuthamini mandhari na sauti nzuri. Kadiri wawezavyo kushughulikia utendaji mbalimbali maishani, ndivyo wapatavyo maisha bora kwa kadiri fulani.

Kushughulika na Hisia-Moyo Zisizofaa

Sehemu muhimu ya kukabiliana na hali yatia ndani kujifunza namna ya kudhibiti hisia-moyo zenye kudhuru. Mojawapo ni hasira. Biblia hukiri kwamba mtu aweza kukasirika kwa sababu fulani. Hata hivyo, pia hutusihi tusiwe ‘wepesi wa hasira.’ (Mithali 14:29) Kwa nini ni jambo la hekima kufanya hivyo? Kulingana na kitabu kimoja cha marejezo, hasira “yaweza kukudhuru na kukufanya uwe na uchungu au kukufanya useme mambo yenye kuumiza utakayojutia baadaye.” Hata mfoko mmoja wa hasira waweza kusababisha madhara yanayoweza kuchukua muda mrefu sana kurekebishwa.

Biblia hupendekeza: “Msiache jua litue mkiwa katika hali ya kuchokozeka.” (Waefeso 4:26) Bila shaka, hatuwezi kufanya lolote ili kuchelewesha kutua kwa jua. Lakini tunaweza kuchukua hatua ili kushughulikia “hali [yetu] ya kuchokozeka” haraka ili tusiendelee kujidhuru wenyewe na kuwadhuru wengine. Unaweza kushughulikia hali kwa njia bora zaidi wakati ambapo umetulia.

Kama ilivyo na familia yoyote, yako pia itakuwa na heri na shari. Wengi huona kwamba wanaweza kukabiliana vyema na hali wanapokuwa na mtu wa kumwambia siri au kuzungumza na mtu mwingine mwenye huruma na hisia-mwenzi. Bila shaka Kathleen alipatwa na jambo kama hilo. Kwanza alimtunza mamake, aliyekuwa na kansa, na baadaye mumewe, aliyeugua mshuko-moyo wa kudumu na hatimaye maradhi ya Alzheimer. Akiri hivi: “Nilipata kitulizo na faraja nilipozungumza na marafiki wanaoelewa hali.” Rosemary, aliyemtunza mamake kwa miaka miwili, akubali. “Kuzungumza na rafiki mwenye moyo mweupe,” asema, “kulinisaidia nidumishe usawaziko.”

Hata hivyo, usishangae, ukidondokwa na machozi unapozungumza. “Kulia hupunguza mkazo na maumivu, na hukusaidia uondoe huzuni,” chasema kitabu A Special Child in the Family. *

Dumisha Mtazamo Unaofaa

“Nia yako ya kuishi inaweza kukutegemeza unapokuwa mgonjwa,” akaandika Mfalme Solomoni mwenye hekima. (Mithali 18:14, Today’s English Version) Watafiti wa kisasa wamesema kwamba matarajio ya wagonjwa—yawe yanafaa au hayafai—mara nyingi huathiri matokeo ya matibabu yao. Ingawa hivyo, familia yaweza kudumishaje mataraja mema inapokabili ugonjwa wa muda mrefu?

Bila kupuuza ugonjwa, familia zaweza kukabiliana vyema zinapoelekeza fikira kwenye mambo ambayo bado zinaweza kufanya. “Hali hiyo yaweza kukufanya uwe na mtazamo usiofaa kabisa,” akiri baba mmoja, “lakini wapaswa kutambua kwamba ungali na mengi sana. Ungali hai, una washiriki wa familia, na marafiki.”

Ingawa ugonjwa wa kudumu haupasi kuchukuliwa kivivi hivi, kuwa mcheshi huzuia mtazamo usiofaa. Jambo hilo laonyeshwa na wepesi wa ucheshi wa familia ya Du Toit. Collette, dadake Neil du Toit aliye mchanga zaidi, asema: “Kwa sababu tumejifunza kukabiliana na hali fulani, twaweza kuchekelea mambo yanayotupata ambayo huenda yakawaudhi sana wengine. Lakini kufanya hivyo kwa kweli husaidia kupunguza mkazo.” Biblia hutuhakikishia kwamba “moyo uliochangamka ni dawa nzuri.”—Mithali 17:22.

Kanuni za Kiroho za Maana Zaidi

Sehemu muhimu ya hali njema ya kiroho kwa Wakristo wa kweli yahusisha ‘kuacha maombi yao ya bidii yajulishwe kwa Mungu kwa sala na dua.’ Tokeo litakuwa kama ilivyoahidiwa katika Biblia: “Amani ya Mungu izidiyo fikira yote kwa ubora italinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili.” (Wafilipi 4:6, 7) Baada ya miaka karibu 30 ya kuwatunza watoto wawili walio na ugonjwa wa kudumu, mama mmoja asema: “Tumejifunza kwamba Yehova hukusaidia kukabiliana na hali. Kwa kweli hukutegemeza.”

Zaidi ya hayo, wengi huimarishwa na ahadi za Biblia za dunia paradiso isiyo na maumivu na kuteseka. (Ufunuo 21:3, 4) “Kwa sababu ya ugonjwa wa kudumu ambao familia yetu imekabili,” asema Braam, “twapata maana zaidi ya ahadi ya Mungu ya kwamba ‘mtu aliye kilema ataruka-ruka kama kulungu, na ulimi wake aliye bubu utaimba.’ Kama ilivyo na wengine wengi, familia ya Du Toit yatazamia kwa hamu wakati ambapo katika Paradiso “hapana mwenyeji atakayesema, Mimi mgonjwa.”—Isaya 33:24; 35:6.

Jipe moyo. Maumivu na mateso yanayopata wanadamu ni uthibitisho wa kwamba hali bora zimekaribia. (Luka 21:7, 10, 11) Hata hivyo, kwa wakati uliopo, watunzaji wengi na wagonjwa wanaweza kuthibitisha kwamba kwa kweli Yehova ni “Baba ya rehema nyororo na Mungu wa faraja yote, ambaye hutufariji katika dhiki yetu yote.”—2 Wakorintho 1:3, 4.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 17 Kwa habari zaidi kuhusu jinsi ya kukabiliana na athari za kihisia-moyo ziletwazo na ugonjwa, tafadhali ona “Utunzaji—Kukabili Huo Ugumu,” katika Amkeni!, Februari 8, 1997, ukurasa wa 3-13.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 8]

Maswali Ambayo Familia Yaweza Kuuliza Daktari

• Ugonjwa utaendelea namna gani, kukiwa na tokeo gani?

• Kutakuwa na dalili gani, nazo zitadhibitiwa jinsi gani?

• Kuna matibabu gani mengine?

• Kuna athari, hatari, na manufaa gani za matibabu tofauti-tofauti?

• Ni nini kinachoweza kufanywa ili kuboresha hali, na ni nini kinachopasa kuepukwa?

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 11]

Jinsi Unavyoweza Kuandaa Utegemezo

Huenda watu fulani wakaepuka kuwatembelea au kuwapa msaada kwa sababu ya kutojua la kusema au namna ya kushughulikia hali hiyo. Huenda wengine wakajidukiza, na kuongeza mkazo kwa familia kwa kuishurutisha ifuate madokezo wanayofikiri yatasaidia. Basi, mtu aweza kuandaaje utegemezo kwa watu walio na mshiriki wa familia mwenye ugonjwa wa kudumu bila kuingilia hali yao ya faragha?

Onyesha hisia-mwenzi unaposikiliza. ‘Uwe mwepesi sana juu ya kusikia,’ yasema Biblia katika Yakobo 1:19. Onyesha upendezi kwa kuwa msikilizaji mzuri na kuruhusu washiriki wa familia wasema yaliyo moyoni ikiwa wanataka. Huenda wakaelekea kufanya hivyo wanapotambua kwamba una “hisia-mwenzi.” (1 Petro 3:8) Ingawa hivyo, kumbuka kwamba hakuna watu wawili au familia mbili zinazotenda kwa njia ileile zikabilipo ugonjwa wa kudumu. Kwa hiyo, “usitoe shauri isipokuwa uwe unajua kikamili habari kuhusu maradhi hayo au hali hiyo,” asema Kathleen, aliyemtunza mama yake na baadaye mume wake aliyepatwa na ugonjwa wa kudumu. (Mithali 10:19) Na kumbuka, hata ikiwa una ujuzi fulani kuhusu ugonjwa huo, huenda mgonjwa na familia wakakataa kuomba shauri lako au kulikubali.

Toa msaada unaotumika. Jitoe kikweli wanapokuhitaji, huku ukiwa mwangalifu sana kutoingilia faragha ya familia hiyo. (1 Wakorintho 10:24) Braam, ambaye amenukuliwa katika mfululizo huu wa makala, asema: “Marafiki wetu Wakristo walitupa msaada mkubwa kwelikweli. Kwa mfano, tulipolala hospitalini kwa sababu ya hali mbaya ya Michelle, sikuzote tulikuwa na marafiki kati ya wanne hadi sita walioketi pamoja nasi usiku kucha. Tulipohitaji msaada wakati wowote, tuliupata.” Mke wa Braam, Ann, aongezea hivi: “Yalikuwa majira ya baridi kali, na kwa majuma mawili tulipewa mchuzi wa aina tofauti kila siku. Tulilishwa mchuzi moto na kuonyeshwa upendo mwingi mchangamfu.”

Sali pamoja nao. Nyakati nyingine huenda kusiwe na jambo unaloweza kufanya. Hata hivyo, kuna mambo machache yanayotia moyo kama vile kushiriki wazo la Kimaandiko linalojenga au sala ya kutoka moyoni pamoja na wagonjwa na familia zao. (Yakobo 5:16) “Usipuuze kamwe uwezo wa kusali kwa ajili ya—na pamoja na—watu walio na ugonjwa wa kudumu na familia zao,” asema Nicolas mwenye umri wa miaka 18, ambaye mama yake anaugua mshuko-moyo wa kudumu.

Naam, utegemezo unaofaa waweza kusaidia sana familia zikabiliane na mkazo unaoletwa na ugonjwa wa kudumu. Biblia husema hivi: “Rafiki ni mwandamani anayependa nyakati zote, na ndugu huzaliwa kushiriki taabu.”—Mithali 17:17, The New English Bible.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 12]

Ugonjwa Usipotibika

Huenda familia fulani zikasitasita kuzungumzia kifo kinachokaribia cha mpendwa aliye na ugonjwa usiotibika. Hata hivyo, kitabu Caring—How to Cope chasema kwamba “unapojua jambo unalotazamia na unalopaswa kufanya, huenda ikasaidia kupunguza wasiwasi.” Ingawa hatua mahususi zitatofautiana ikitegemea sheria na desturi za mahali, yafuatayo ni madokezo kadhaa ambayo huenda familia ikayafikiria inapomtunza mpendwa aliye na ugonjwa usiotibika nyumbani.

Mapema vya Kutosha

1. Mwulize daktari mambo unayopaswa kutazamia siku na saa za mwisho-mwisho na kile kipasacho kufanywa ikiwa kifo kitatukia usiku.

2. Tayarisha orodha ya wale watu wanaohitaji kujulishwa juu ya kifo.

3. Fikiria njia tofauti-tofauti za maziko:

• Mgonjwa angependa kufanyiwa nini?

• Kuzikwa au kuchomwa? Linganisha gharama na huduma za watu mbalimbali wanaotia maiti dawa isioze.

• Maziko yapasa kufanywa lini? Ruhusu wakati kwa ajili ya mipango ya kusafiri.

• Ni nani atakayeongoza maziko au hotuba ya maziko?

• Yatafanywa wapi?

4. Hata ikiwa mgonjwa ametulizwa kwa dawa huenda bado akawa anajua kile kinachosemwa na kufanywa karibu naye. Uwe mwangalifu usiseme jambo lolote mbele yake ambalo hungependa asikie. Huenda ukataka kumpa uhakikishio kwa kuzungumza naye kwa utulivu na kushika mkono wake.

Mpendwa Anapokufa

Haya ni baadhi ya mambo ambayo wengine wanaweza kufanya ili kusaidia familia:

1. Ruhusu familia iwe na wakati wa kutosha ikiwa peke yake pamoja na aliyekufa ili iweze kukabiliana na kifo.

2. Sali pamoja na familia.

3. Familia inapokuwa tayari, huenda ikathamini msaada wa kujulisha watu wafuatao:

• Daktari ili kuthibitisha kifo na kutoa hati ya kifo.

• Mtu anayetia maiti dawa isioze, chumba cha kuhifadhi maiti, au mahali pa kuchomea maiti, ili kuchukua mwili.

• Jamaa na marafiki. (Huenda ukasema jambo kama hili kwa busara: “Napiga simu kuhusu [jina la mgonjwa]. Nasikitika kusema kwamba nina habari mbaya. Kama ujuavyo, amepambana na [ugonjwa] kwa muda fulani, na alikufa [lini na wapi].)

• Ofisi ya kampuni ya kuchapisha magazeti ili kuweka tangazo la kifo wakipenda.

4. Huenda familia ikataka kuandamana na mtu fulani ili kuwasaidia kukamilisha mipango ya maziko.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Washiriki wa familia wapaswa kufanya yote wawezayo ili kudumisha maisha bora kwa kadiri fulani

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kusali pamoja na familia hiyo kwaweza kuwasaidia wakabiliane na hali