Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Familia Yetu Ilivyoungana Tena

Jinsi Familia Yetu Ilivyoungana Tena

Jinsi Familia Yetu Ilivyoungana Tena

Kama ilivyosimuliwa na Lars na Judith Westergaard

NYUMBA yao yaonekana kuwa mahali pa kawaida kwa familia yoyote yenye furaha katika Denmark. Ni nyumba yenye starehe iliyo na bustani maridadi, iko katika kijiji kitulivu. Ndani yake mna picha kubwa ukutani ya watoto wenye afya na tabasamu wa familia hiyo.

Baba yao, Lars, ni mzee katika kutaniko moja la Mashahidi wa Yehova. Mkewe Judith, ni painia (mweneza-evanjeli wa wakati wote). Japo ni mume na mke wenye furaha, haijawa hivyo sikuzote. Lars na Judith walikuwa na matatizo na uhasama uliotokeza talaka na kusambaratisha familia yao. Ingawa hivyo, sasa familia yao imeungana tena. Kwa nini? Wenyewe wanasimulia kilichotendeka.

Lars na Judith wanakubali kusimulia kilichoharibu ndoa yao na jinsi walivyoungana tena. Wanahisi kwamba simulizi lao laweza kusaidia wengine.

Walikuwa na Mwanzo Mzuri Sana

Lars: Ndoa yetu ilikuwa na furaha sana mwanzoni, mwezi wa Aprili 1973. Tulitarajia kuishi kwa raha mustarehe. Hatukujua Biblia wala Mashahidi wa Yehova, lakini tulisadiki kwamba ulimwengu unaweza kuwa makao bora endapo kila mtu atajikakamua kuufanikisha. Kwa hiyo tulishiriki katika harakati nyingi za kisiasa. Furaha yetu iliongezeka tulipopata wavulana watatu wachangamfu na wenye afya—Martin, Thomas, na Jonas.

Judith: Nilikuwa na cheo katika shirika la kiserikali. Nilishiriki pia utendaji wa chama cha wafanyakazi na cha kisiasa. Punde si punde nikawa kiongozi.

Lars: Mimi nami, nilifanya kazi katika chama mashuhuri cha wafanyakazi, kisha nikapandishwa cheo. Tulipata madaraka zaidi kazini, na hatukuwazia kukabili magumu maishani.

Kutengana Hatua kwa Hatua

Lars: Lakini tulibanwa mno na shughuli zetu kiasi cha kutoweza kuwasiliana vyakutosha. Tulifanya kazi katika nyanja mbalimbali za chama kilekile cha kisiasa. Vijana wetu watatu walitunzwa na watu wengine, ama nyumbani ama katika vituo vya kutunzia watoto wadogo mchana. Maisha yetu ya familia yaliharibika kwa sababu kila mtu alihangaikia mambo yake binafsi. Mara nyingi ugomvi mbaya ulizuka sote tulipokutana nyumbani. Kisha nikaanza kunywa vileo ili kujituliza.

Judith: Bila shaka, bado tulipendana na kuwapenda watoto, lakini upendo wetu haukusitawishwa ipasavyo; ulikuwa ukififia. Uhusiano wetu ukawa na uhasama, na kama tokeo watoto waliteseka.

Lars: Niliamua kuacha kazi ili nijaribu mara ya mwisho kuifanikisha familia yetu tena. Mnamo mwaka wa 1985 tulihama mjini na kwenda kijijini tunakoishi sasa. Mambo yakawa nafuu kwa kitambo, lakini mimi na mke wangu tuliendelea kuhangaikia mambo yetu binafsi. Hatimaye, tulitalikiana mwezi wa Februari 1989, baada ya kuishi pamoja kwa miaka 16. Familia yetu ilisambaratika.

Judith: Lilikuwa jambo lenye kufadhaisha sana kuona familia yetu ikisambaratika na kuona watoto wakiteseka. Tulikuwa na uchungu mno kiasi cha kutoweza kushirikiana kulea wavulana wetu, kwa hiyo niliwachukua wote watatu.

Lars: Mimi na Judith tulijaribu kuokoa familia yetu isivunjike pasipo kufua dafu. Hata tulimwomba Mungu msaada. Lakini hatukumjua Mungu ipasavyo.

Judith: Sala zetu zilifanya tuhisi kwamba Mungu hakusikiliza. Twashukuru kwamba tangu wakati huo tumeona kwamba Mungu husikiliza sala.

Lars: Hatukujua kamwe kwamba tulihitaji kujitahidi kufanya mabadiliko sisi wenyewe. Kwa hiyo talaka yetu ilihuzunisha sana.

Lars Abadilika Isivyotazamiwa

Lars: Nilipokuwa nikiishi peke yangu, mambo yalibadilika kabisa nisivyotazamia. Siku moja nilipokea magazeti mawili kutoka kwa Mashahidi wa Yehova. Hapo awali nilikuwa nikiwafukuza Mashahidi. Lakini niliposoma magazeti hayo, niliona kwamba Mashahidi huitikadi kabisa Mungu na Yesu Kristo. Jambo hilo lilinishangaza sana. Sikudhani wao ni Wakristo.

Karibu wakati huo, nilianza kuishi na mwanamke mmoja niliyekutana naye. Kumbe zamani alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Nilipoanza kuuliza maswali, alinionyesha katika Biblia kwamba jina la Mungu ni Yehova. Kwa hiyo jina “Mashahidi wa Yehova” humaanisha “mashahidi wa Mungu”!

Mwanamke huyo alipanga nihudhurie hotuba ya watu wote katika Jumba la Kusanyiko la Mashahidi wa Yehova. Mambo niliyoona huko yalichochea upendezi wangu kwelikweli. Nilizuru Jumba la Ufalme la karibu ili nijifunze mengi, nikakubali funzo la Biblia. Punde si punde niling’amua kwamba niliishi maisha mapotovu, kwa hiyo nikamwacha yule mwanamke na nikaenda kuishi peke yangu katika mji wetu. Baada ya kusitasita kidogo niliwasiliana na Mashahidi wa Yehova wa huko na nikaendelea kujifunza Biblia.

Lakini bado nilikuwa na shaka. Je, kweli Mashahidi wa Yehova walikuwa watu wa Mungu? Vipi juu ya mambo yote niliyojifunza nikiwa mtoto? Kwa kuwa nililelewa katika kanisa la Seventh-Day Adventist, nilimfikia mhudumu wa kanisa la Adventist. Alikubali kujifunza nami kila Jumatano, ilhali Mashahidi wa Yehova walijifunza nami kila Jumatatu. Nilitaka tu kupata majibu wazi kutoka kwa vikundi vyote viwili kuhusu masuala manne mahususi: kurudi kwa Kristo, ufufuo, fundisho la Utatu, na mambo yanavyopasa kuendeshwa kanisani. Baada ya muda wa miezi michache sikuwa na shaka yoyote tena. Katika masuala yote manne—na katika mambo mengineyo yote—ni itikadi za Mashahidi wa Yehova tu zilizotegemea Biblia kikamili. Matokeo yakawa kwamba nilianza kushiriki utendaji wote wa kutaniko kwa furaha na muda si muda nikajiweka wakfu kwa Yehova. Nilibatizwa katika Mei 1990.

Namna Gani Judith?

Judith: Baada ya ndoa yetu kuvunjika, nilianza kwenda kanisani tena. Sikufurahi kusikia kwamba Lars alitaka kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Mwana wetu mchanga, Jonas mwenye umri wa miaka kumi, alimtembelea babake nyakati nyingine, lakini nilimkataza Lars kuandamana na Jonas kwenye mkutano wowote wa Mashahidi. Lars aliomba wenye mamlaka ruhusa, lakini waliniunga mkono.

Nilikuwa na mwanamume mwingine. Pia, nilijishughulisha sana na siasa na kazi nyingine za kijamii. Kwa hiyo, kama mtu yeyote angezungumzia kuungana tena kwa familia yetu wakati huo, lingeonekana kuwa jambo lisilowezekana.

Ili kuwapinga Mashahidi wa Yehova, nilimwendea mhudumu wa parokia ya karibu, ambaye alikiri mara moja kwamba hakujua jambo lolote kuhusu Mashahidi wala hakuwa na kichapo chochote kuwahusu. Alinitahadharisha tu nijitenge nao. Pasipo shaka, jambo hilo halikubadili maoni yangu mabaya juu ya Mashahidi wa Yehova. Lakini hali zilinilazimu kukutana nao nisivyotarajia.

Ndugu yangu aishiye Sweden alikuwa amekuwa Shahidi wa Yehova, na nilialikwa kwa arusi yake kwenye Jumba la Ufalme! Tukio hilo lilibadili kabisa maoni yangu juu ya Mashahidi. Nilishangaa kuona kwamba hawakuwa watu wasiopendeza kama nilivyodhania sikuzote. Walikuwa wenye fadhili na furaha, hata walikuwa wacheshi.

Wakati huohuo, Lars, aliyekuwa mume wangu, alikuwa amebadilika kabisa. Alichukua wajibu wake kwa uzito zaidi, alitumia wakati wake pamoja na watoto, alikuwa mwenye fadhili na hakuongea ovyoovyo, pia hakuwa mlevi kama awali. Utu wake ulivutia sana! Sasa alikuwa mwanamume mwenye sifa nilizokuwa nikitaka awe nazo. Nilikerwa sana na wazo la kwamba hakuwa mume wangu na kwamba huenda siku moja akaoa mwanamke mwingine!

Kisha nikapanga “kumnasa” kwa werevu. Wakati mmoja Jonas alipokuwa akiishi na baba yake, nilipanga kusafiri na dada zangu wawili kwenda kuwaona Jonas na Lars kwa kisingizio cha kwamba shangazi hao wawili wapaswa kumwona mpwa wao. Tulikutana katika uwanja wa burudani. Mimi na Lars tuliketi kwenye benchi moja huku shangazi wakiburudika na kijana wetu.

Mara tu nilipotaja wakati wetu ujao, nilishangaa kumwona Lars akitoa kitabu mfukoni mwake. Kiliitwa Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha. * Alinipokeza kitabu hicho na kudokeza nisome sura zinazohusu fungu la mume na mke katika familia. Alipendekeza hasa nisome maandiko.

Mwishowe mimi na Lars tuliponyanyuka kutoka kwenye benchi, nilitaka kumshika mkono, lakini akakataa kwa fadhili. Lars hakunuia kuanzisha uhusiano mpya nami pasipo kujua maoni yangu juu ya imani yake mpya. Hilo liliniudhi kwa kadiri fulani, lakini nikatambua kwamba alikuwa na mtazamo unaofaa kwa kuwa mimi ndimi ningenufaika endapo angekubali kuwa mume wangu tena.

Yote hayo yalinichochea nitake kujua mengi sana juu ya Mashahidi wa Yehova. Siku iliyofuata, niliwasiliana na mwanamke mmoja ambaye nilijua alikuwa Shahidi, tukapanga kwamba yeye na mumewe wanifunze mambo niliyotaka kujua kuhusu dini yao. Walijibu maswali yangu mengi wakitumia Biblia. Niliweza kuona kwamba mafundisho ya Mashahidi wa Yehova yanategemea kabisa Biblia. Nililazimika kukiri kwamba kila jambo tulilojifunza lilikuwa kweli.

Wakati huo nilijiuzulu kutoka kwa Evangelical Lutheran Church na nikaacha mambo ya kisiasa. Hata niliacha kuvuta sigareti. Hilo lilikuwa jambo gumu zaidi ya yote. Nilianza kujifunza Biblia katika Agosti 1990, na nikabatizwa kuwa Shahidi wa Yehova mwezi wa Aprili 1991.

Arusi Yao ya Pili

Judith: Sasa sote tulikuwa Mashahidi waliobatizwa. Ijapokuwa tulitengana, sote tulijifunza Biblia. Mafundisho bora ya Biblia yalitubadili kabisa tukawa tofauti na awali. Bado tulipendana, labda kwa undani zaidi kuliko mbeleni. Sasa tulikuwa huru kufunga ndoa tena—na ndivyo tulivyofanya. Tuliweka nadhiri zetu kwa mara ya pili, lakini wakati huu katika Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova.

Lars: Amini usiamini—familia yetu iliungana tena! Lilikuwa jambo la furaha na shangwe kama nini!

Judith: Wana wetu, watu wa ukoo, na marafiki wengi wapya na wa zamani walihudhuria arusi yetu. Ilikuwa sherehe yenye kufana. Baadhi ya watu waliotujua wakati wa ndoa yetu ya kwanza walihudhuria pia; walifurahi kutuona tukiwa tumeungana tena na walistaajabia shangwe ya kweli ya Mashahidi wa Yehova.

Watoto

Lars: Tangu tulipobatizwa tumefurahi kuona wana wetu wawili wakiamua kujiweka wakfu kwa Yehova.

Judith: Jonas amethamini sana kweli ya Biblia tangu utotoni alipomzuru baba yake. Alikuwa na umri wa miaka kumi tu aliponiambia kwamba alitaka kuishi na baba yake, alisema ni kwa sababu, “Baba hufuata Biblia.” Jonas alibatizwa akiwa na umri wa miaka 14. Amekamilisha masomo yake, na sasa yeye ni mhudumu wa wakati wote.

Lars: Mwana wetu mkubwa, Martin, sasa ana umri wa miaka 27. Alifikiri sana alipoona mabadiliko tuliyofanya. Alihama nyumbani na sasa anaishi katika sehemu tofauti nchini. Miaka miwili iliyopita alianza kujifunza Biblia katika kutaniko la karibu la Mashahidi wa Yehova katika sehemu hiyo. Baada ya miezi mitano tu, alikuwa tayari kubatizwa. Akiwa Mkristo angali anaweka miradi mizuri ya wakati wake ujao.

Mwana wetu wa pili, Thomas, hivi sasa si Shahidi wa Yehova. Bila shaka tungali tunampenda, na tuna uhusiano mzuri pamoja naye. Anafurahi kwa sababu ya mabadiliko ya maisha yetu ya familia. Sote tunakubali kwamba familia yetu imeunganishwa tena na kanuni za Biblia tulizojifunza tukiwa wazazi. Sasa tuna baraka kama nini ya kuweza kukutana pamoja tukiwa familia, vijana wote watatu na wazazi pia!

Maisha Yetu Leo

Lars: Hatusemi kwamba tumekuwa wakamilifu. Lakini tumejifunza jambo fulani—kwamba upendo na kuheshimiana ni mambo muhimu katika ndoa yenye fanaka. Msingi wa ndoa yetu sasa ni tofauti kabisa na msingi wa awali. Sasa sote wawili tumejitiisha kwa mamlaka kuu zaidi, kwa kuwa sote twang’amua kwamba twaishi kwa ajili ya Yehova. Mimi na Judith twahisi kwamba tumeunganika kikweli na twatazamia wakati ujao tukiwa na uhakika.

Judith: Nadhani tumetoa uthibitisho hakika kwamba Yehova ni mshauri wa ndoa na familia aliye bora kupita wote.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 30 Kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc., mwaka wa 1978; sasa hakichapishwi tena.

[Picha katika ukurasa wa 20]

Lars na Judith wakati wa ndoa yao ya kwanza, mnamo 1973

[Picha katika ukurasa wa 21]

Vijana watatu wa familia iliyosambaratika ambayo baadaye iliungana tena

[Picha katika ukurasa wa 23]

Lars na Judith leo, wameungana tena kwa kufuata kanuni za Biblia