Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Mageuzi Hupatana na Akili?

Je, Mageuzi Hupatana na Akili?

Je, Mageuzi Hupatana na Akili?

LEO, nadharia ya mageuzi husemwa kuwa ya kweli na wale wanaoitetea. Lakini, je, sababu wanazotoa mara nyingi zinapatana na akili? Fikiria mambo yafuatayo.

Hariri inayotokezwa na buibui ni mojawapo ya vitu vigumu zaidi vilivyopo. Gazeti New Scientist lasema kwamba, “kila uzi waweza kunyooka kwa asilimia 40 kupita urefu wake na kustahimili nishati inayopita ya feleji mara zaidi ya 100 bila kukatika.” Hariri hiyo ya kustaajabisha hutengenezwaje? Umajimaji wa protini wenye kunata, hupitia kwenye vifereji vidogo mno mwilini mwa buibui, kisha kubadilika kwa utaratibu wa molekuli za protini hugeuza umajimaji huo kuwa uzi mango, yaeleza Encyclopædia Britannica.

Gazeti New Scientist lamalizia hivi: “Buibui amebuni mbinu bora zaidi hata kuliko zile za mwanakemia mwenye ujuzi.” Je, haishangazi kwamba buibui amebuni mbinu ya utengenezaji bidhaa iliyo tata zaidi kwa mwanadamu kuweza kuelewa?

Makala moja katika jarida The Wall Street Journal, ya Phillip E. Johnson, profesa wa sheria katika Chuo Kikuu cha California, yasema kwamba watetezi wa mageuzi huendelea kudhihaki wale wanaopinga japo hakuna ushuhuda wa kutetea mageuzi. Makala hiyo yasema: “Nadharia ya mageuzi haiwezi kabisa kuthibitishwa—lakini watetezi wake hawataki mjadala wowote mnyoofu ambao waweza kudunisha maoni yao yenye kupendelea.”

Mfano mwingine unaoonyesha kwamba dhana ya mageuzi si jambo linalopatana na akili unahusiana na mimea. Wanasayansi wanaofanya utafiti huko Morocco walifukua visikuku 150 vya mimea ya archaeopteri, “mmea wa jamii inayokaribiana na ile ya mimea yenye mbegu iliyovumbuliwa kwanza, ambayo ilitokeza miti mingi iliyopo leo,” lasema The Daily Telegraph la London. Mhariri wa sayansi wa gazeti hilo asema kwamba mmea huo “ulibadili ulimwengu wetu kwa kubuni majani na matawi.” “Kubuni” ni “kutengeneza kitu baada ya kufikiri.” Je, kusema kwamba mmea una uwezo wa kufikiri na kubuni kunapatana na akili?

Solomoni, mmojawapo wa watu wenye hekima zaidi, atushauri ‘tulinde busara,’ tutumie uwezo wetu wa kufikiri. Tunahitaji kufanya hivyo sasa kuliko wakati mwingine wowote.—Mithali 5:2.