Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Mungu Ni Kigeugeu?

Je, Mungu Ni Kigeugeu?

Maoni ya Biblia

Je, Mungu Ni Kigeugeu?

MWANA anthropolojia George Dorsey alimweleza Mungu wa “Agano la Kale” kuwa “Mungu katili.” Aliongezea hivi: “Yahweh . . . hana upendo kabisa. Yeye ni Mungu wa waporaji, wa watesaji, wa wapiganaji, wa ushindi.” Wengine wamefikia mkataa kama huo kuhusu Mungu wa “Agano la Kale”—Yahweh, au Yehova. Hivyo, wengine leo hujiuliza kama kweli Yehova alikuwa Mungu katili ambaye hatimaye alibadili utu wake na kuwa Mungu mwenye upendo na rehema wa “Agano Jipya.”

Wazo hilo kuhusu Mungu wa Biblia si jipya. Lilitokezwa mara ya kwanza na Marcion, Mwagnosti kwa kadiri fulani, aliyeishi karne ya pili W.K. Marcion alikataa katakata Mungu wa “Agano la Kale.” Alimwona Mungu huyo kuwa mwenye jeuri na asiyesamehe, dikteta aliyethawabisha kimwili wale wanaomwabudu. Kwa upande mwingine, Marcion alimweleza Mungu wa “Agano Jipya”—kama alivyojifunua kupitia kwa Yesu Kristo—kuwa Mungu mkamilifu, Mungu mwenye upendo kamili na rehema, mwema na anayesamehe.

Yehova Hutenda Kulingana na Jinsi Hali Zinavyobadilika

Jina lenyewe la Mungu, Yehova, humaanisha “Yeye Husababisha Iwe.” Hilo ladokeza kwamba Yehova hujisababisha kuwa Mtimizaji wa ahadi zake zote. Musa alipomwuliza Mungu jina lake, Yehova alifafanua maana yake kwa njia hii: “Mimi niko ambaye niko.” (Kutoka 3:14) Tafsiri ya Rotherham husema hivi: “Nitakuwa chochote Ninachopenda kuwa.”

Kwa hiyo Yehova huchagua kuwa, au huthibitika kuwa, chochote ahitajiwacho kuwa ili kutimiza makusudi na ahadi zake za uadilifu. Hilo lathibitishwa na uhakika wa kwamba ana majina mengi ya cheo na mitajo ya kumweleza: Yehova wa Majeshi, Hakimu, Mwenye Enzi Kuu, Mwenye Wivu, Bwana Mwenye Enzi Kuu, Muumba, Baba, Mfunzi Mtukufu, Mchungaji, Msikiaji wa sala, Mkombozi, Mungu mwenye furaha, na mengine mengi. Amekusudia kuwa yote hayo—na zaidi—ili atekeleze makusudi yake yenye upendo.—Kutoka 34:14; Waamuzi 11:27; Zaburi 23:1; 65:2; 73:28; 89:26; Isaya 8:13; 30:20; 40:28; 41:14; 1 Timotheo 1:11, linganisha NW.

Basi, je, hilo lamaanisha kwamba utu au viwango vya Yehova hubadilika? La. Kuhusu Mungu, Yakobo 1:17 husema: “Kwake yeye hakuna badiliko-badiliko la kugeuka kwa kivuli.” Mungu angeweza kukabilianaje na ugumu wa hali zenye kubadilika huku yeye si kigeugeu?

Twaweza kueleza jambo hilo kwa kutumia mfano wa wazazi wenye kujali ambao huchukua madaraka mbalimbali kwa ajili ya watoto wao. Katika siku moja, mzazi aweza kuwa mpishi, mtunzaji-nyumba, fundi wa umeme, muuguzi, rafiki, mshauri, mwalimu, mtoa-nidhamu, na kadhalika. Mzazi habadili utu wake anapochukua madaraka hayo; yeye hubadilikana tu ili kufaana na hali zinazotokea. Ndivyo na Yehova, lakini yeye hufanya hivyo kwa kiwango kikubwa zaidi. Hana mpaka wowote wa kumzuia awe kile ajisababishacho kuwa ili atimize kusudi lake na ili anufaishe viumbe wake.—Waroma 11:33.

Kwa mfano, Maandiko ya Kiebrania na ya Kigiriki ya Kikristo, humwonyesha Yehova kuwa Mungu wa upendo na rehema. Nabii Mika aliyeishi karne ya nane K.W.K. aliuliza hivi kuhusu Yehova: “Ni nani aliye Mungu kama wewe, mwenye kusamehe uovu, na kuliachilia kosa la watu wa urithi wake waliosalia? Hashiki hasira yake milele, kwa maana yeye hufurahia rehema.” (Mika 7:18) Vivyo hivyo, mtume Yohana aliandika maneno yanayojulikana sana: “Mungu ni upendo.”—1 Yohana 4:8.

Kwa upande mwingine, katika sehemu zote mbili za Biblia, Yehova huonyeshwa kuwa Hakimu mwadilifu wa wale ambao kwa kurudia-rudia, kwa kupita kiasi, na bila kutubu hukiuka sheria zake na kuwadhuru wengine. “Wote wasio haki [Yehova] atawaangamiza,” akasema mtunga-zaburi. (Zaburi 145:20) Vivyo hivyo, Yohana 3:36 husema: “Yeye ambaye hudhihirisha imani katika Mwana ana uhai udumuo milele; yeye ambaye hukosa kutii Mwana hataona uhai, bali hasira ya kisasi ya Mungu hukaa juu yake.”

Sifa Zake Hazibadiliki

Utu wa Yehova na sifa zake za msingi—upendo, hekima, haki, na nguvu—hazijabadilika. Aliwaambia Waisraeli hivi: “Mimi, BWANA, sina kigeugeu.” (Malaki 3:6) Hiyo ilikuwa miaka ipatayo 3,500 baada ya Mungu kuumba wanadamu. Kupatana na taarifa hiyo ya Mungu, tunapoichunguza Biblia nzima kikamili yafunua Mungu asiyebadili viwango na sifa zake. Kupita kwa karne hizi zote hakujabadili utu wa Yehova, kwa kuwa badiliko hilo halikuhitajiwa.

Kama inavyoonyeshwa kotekote katika Biblia, upendo wa Mungu na kushikilia kwake haki hakujaongezeka wala kupungua tangu aliposhughulika na wanadamu katika Edeni. Zile zinazoonekana kuwa tofauti katika utu wake kwenye sehemu mbalimbali za Biblia kwa kweli ni sifa tofauti-tofauti za utu uleule usiobadilika. Hizo husababishwa na hali na watu tofauti-tofauti anaoshughulika nao, waliofanya iwe lazima kuwa na mtazamo au mahusiano tofauti.

Hivyo, Maandiko huonyesha waziwazi kwamba utu wa Mungu haujabadilika katika karne nyingi zilizopita na hautabadilika wakati ujao. Yehova ni mfano mkuu zaidi ulio halisi wa udumifu na uthabiti. Yeye ni mwenye kutegemeka na mwenye kutumainika nyakati zote. Twaweza kumtegemea daima.

[Picha katika ukurasa wa 16]

Mungu yuleyule aliyeharibu Sodoma na Gomora . . .

. . . ataleta ulimwengu mpya wenye uadilifu