Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jilinde na Uwalinde Wapendwa Wako

Jilinde na Uwalinde Wapendwa Wako

Jilinde na Uwalinde Wapendwa Wako

INTERNET yaweza kuwa kifaa chenye mafaa. Lakini sawa na vifaa vinginevyo yaweza kutumiwa vibaya. Na cyberporn—ponografia kwenye Internet—ni njia moja ya kutumia vibaya Internet.

Kwa kuwa wazazi wanatambua athari za picha, wanapaswa kujitahidi sana kuzuia programu zisizofaa za Internet zisiwafikie watoto. Kijitabu Teen Safety on the Information Highway huandaa habari muhimu kuhusu suala hilo. Chasema hivi: “Sasa kuna huduma za kuainisha web site ikitegemea yaliyomo pamoja na kutia programu zinazowasaidia wazazi wafunge web site wanazoona hazifai. Programu hizo hutofautiana. Programu nyingine hufunga web site zinazojulikana kuwa na habari zisizofaa. Nyingine huwazuia watumiaji wasiingize habari fulani-fulani kama vile jina na anwani. Programu nyingine huwazuia watoto wako kujiunga na vituo vya mazungumzo au huwazuia kutuma au kupokea E-mail. Kwa kawaida programu hizo zaweza kutumiwa na mzazi ili kuzuia tu web site ambazo mzazi anaona hazifai.”—Ona pia sanduku “Kuwalinda Watoto Dhidi ya Ponografia.”

Hata hivyo, lazima tukiri kwamba wazazi hawawezi kufunga kila web site isiyofaa ambayo huenda watoto wao wakatazama. Hawawezi kuwachunga watoto wao kila dakika. Na mtoto au kijana asiyeweza kutazama ponografia nyumbani huenda akaitazama pasipo kizuizi akiwa shuleni au nyumbani mwa mwanashule mwenzake. Kwa hiyo, pamoja na kujitahidi sana kuwazuia watoto wao wasitazame ponografia, lazima wazazi wawasaidie kusitawisha dhamiri inayotenda itakayowachochea kuepuka ponografia bila kuamriwa.

Ni kosa kukata kauli kwamba watu wazima hawadhuriwi sana na ponografia kama watoto. Kama tulivyokwisha kuona katika makala iliyotangulia, ponografia haimfai mtu yeyote!

Hata hivyo, tuseme kwamba umekuwa ukitazama ponografia kwa muda fulani. Nawe watambua kwamba unalofanya halimpendezi Mungu, nawe wataka kuacha zoea hilo. Je, yawezekana? Ndiyo, yawezekana. Kila siku watu huacha mazoea mabaya. Ikiwa wataka kwelikweli kuacha kabisa ponografia, unaweza kufaulu.

Ikiwa Wataka Kuacha Kabisa

Hatua ya kwanza ni kuacha kutazama ponografia—mara moja! Kadiri unavyoahirisha kuacha, ndivyo iwavyo vigumu zaidi. Hata hivyo, kuacha si rahisi kama unavyowazia. Biblia husema waziwazi kwamba dhambi yaweza kufurahisha kwa muda. (Waebrania 11:25) Lakini dhambi yaweza kuongoza kwenye kifo pia. (Waroma 6:23) Mwanzoni, huenda ukatoa udhuru mbalimbali ili utazame ponografia mara moja tu. Usikubali kutoa udhuru! Na usishindwe na kishawishi cha kuendelea kutazama!

Kama tulivyotaja mapema katika mfululizo huu, kutazama ponografia kwaweza kuharibu kabisa maisha yako. Jichunguze kwa unyofu ili uone jinsi ambavyo zoea hilo linaathiri uhusiano wako na familia yako na marafiki. Je, wewe ni mume na baba? Yaelekea kwamba mke na watoto wako wameona mabadiliko fulani katika tabia yako. Tangu ulipoanza kutazama ponografia, huenda umekuwa mwenye kununa, mwepesi wa hasira, na msiri, au mwenye kujitenga—labda bila hata kujua. Nyakati nyingine huenda ukawafokea washiriki wa familia bila sababu. Ikiwa unatazama ponografia, basi labda tabia yako inadhihirisha jambo hilo. Marafiki na washiriki wako wa familia wameng’amua kwamba uko mashakani. Ni kwamba tu hawajui tatizo lako!

Iwapo unavutiwa kutazama ponografia tena na tena, usijaribu kupambana na tatizo hilo peke yako. Omba msaada. Ongea na rafiki mwenye uzoefu. Kwa kweli, kukubali kwamba una tatizo la kutazama ponografia kunahitaji ujasiri, lakini rafiki mkomavu aweza kuthamini jitihada zako za kuchukua hatua ya kukomesha zoea hilo.

Pasipo shaka, sababu kubwa zaidi ya kutufanya tupambane na ponografia ni ile ya kutaka kumpendeza Mungu. Tunapoishi kwa wema-adili, twaufurahisha moyo wa Mungu. (Mithali 27:11) Tunapoishi kwa njia isiyofaa, ‘tunamhuzunisha moyo.’ (Mwanzo 6:6) Ikiwa wewe ni Mkristo, bila shaka unahangaikia hisia za Mungu. Wapaswa pia kuhangaikia namna ambavyo unatumia akili na moyo wako, ambazo zimewekwa wakfu kwa Mungu na zapasa kuwekwa safi kwa ajili ya utumishi wake. (Ezekieli 44:23) Biblia huwahimiza Wakristo wajisafishe wenyewe ‘kila unajisi wa mwili na roho, wakikamilisha utakatifu katika hofu ya Mungu.’ (2 Wakorintho 7:1) Naam, hofu ifaayo ya kutompendeza Mungu, anayeona kila jambo, yaweza kukuchochea uache kabisa ponografia.

Lakini, tuseme kwamba unapojitahidi sana kuacha, bila kutarajia unafungua Web site inayoonyesha ponografia. Ifunge mara moja! Ikiwezekana, funga programu hiyo ya Internet! Unapopatwa na kishawishi cha kuirejelea, mfikie Mungu kwa sala ya kutoka moyoni, mwombe msaada ili ushinde kishawishi hicho. “Katika kila jambo,” yasema Biblia, “acheni maombi yenu ya bidii yajulishwe kwa Mungu.” Unaposumbuliwa na mawazo yasiyofaa, sali kwa Mungu hadi upatapo kitulizo. Kisha ‘amani ya Mungu izidiyo fikira yote kwa ubora italinda moyo wako na nguvu zako za akili.’ (Wafilipi 4:6, 7) Bila shaka, utahitaji kuondoa mawazo yasiyofaa na badala yake usitawishe yale yaliyo ‘ya kweli, ya hangaikio zito, ya uadilifu, yaliyo safi kiadili, ya kupendeka, na ya kusemwa vema.’—Wafilipi 4:8.

Huenda ukanufaika kwa kushika na kutafakari maandiko ya Biblia yafuatayo.

“Enyi mmpendao BWANA, uchukieni uovu.”—Zaburi 97:10.

“Napiga-piga mwili wangu ngumi na kuuongoza kama mtumwa, ili, baada ya mimi kuwa nimewahubiria wengine, mimi mwenyewe nisiwe mwenye kukataliwa kwa njia fulani.”—1 Wakorintho 9:27.

“Kwa hiyo, fisheni viungo vya mwili wenu vilivyo juu ya dunia kwa habari ya uasherati, ukosefu wa usafi, hamu ya ngono.”—Wakolosai 3:5.

“Kila mmoja wenu apaswe kujua jinsi ya kupata umiliki wa chombo chake mwenyewe katika utakaso na heshima, si katika hamu yenye tamaa ya ngono.”—1 Wathesalonike 4:4, 5.

“Kila mtu ambaye hufuliza kumtazama mwanamke ili kuwa na harara kwa ajili yake tayari amefanya uzinzi pamoja naye moyoni mwake.”—Mathayo 5:28.

“Waume wapaswa kuwa wakiwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. Yeye apendaye mke wake ajipenda mwenyewe.”—Waefeso 5:28.

Kuna sababu tele za kuepuka ponografia. Inaweza kuharibu kabisa maisha yako, kupotosha maoni yako, kuharibu uhusiano wako na wengine na, muhimu zaidi, kuharibu kabisa uhusiano wako na Mungu. Endapo huna zoea la kutazama ponografia, usianze. Iwapo umeanza, koma mara moja! Iwe yaonyeshwa kitabuni au gazetini au kwenye Internet, ponografia haiwafai Wakristo. Epuka ponografia kwa udi na uvumba!

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]

Kuwalinda Watoto Dhidi ya Ponografia

Madokezo yafuatayo yaweza kukusaidia uwalinde watoto wako dhidi ya hatari za ponografia kwenye Internet.

● Usimruhusu mtoto wako achunguze Internet akiwa katika chumba chake cha kulala. Ziweke kompyuta zozote zilizounganishwa na Internet katika chumba kilicho wazi kwa washiriki wote wa familia.

● Pata kujua programu zote za kompyuta zinazotumiwa na mtoto wako.

● Chunguza ujue kama mtoto wako amefungua Web site yake binafsi pasipo kukujulisha. Fanya hivyo kwa kujaribu kutafuta jina lake katika programu zinazochunguza Internet yote. Andika jina lake kamili likiwa na alama za mnukuo ili uepuke kufungua Web site usizotaka.

● Usimruhusu mtoto wako awasiliane moja kwa moja na mtumiaji mwingine wa kompyuta usiyemfahamu.—Ona sanduku “Ni Zaidi ya Kupiga Gumzo.”

● Usijibu kamwe ujumbe au taarifa za habari zenye kushawishi, chafu, zenye kuudhi, au zenye vitisho.

● Waonye watoto wako wasitazame programu zisizofaa kwenye Internet. Wafunze kutofautisha programu zinazofaa na zisizofaa hata usipokuwa karibu. Kumbuka kwamba kompyuta zilizo shuleni au katika nyumba ya rafiki huenda zisiwe zimefungwa ili kuzuia watoto kutazama ponografia.

[Hisani]

Habari hii inategemea kwa sehemu, broshua Child Safety on the Information Highway na makala katika gazeti Los Angeles Times, Julai 5, 1999.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 10]

Ni Zaidi ya Kupiga Gumzo

Mtu anahitaji kutahadhari sana anapotumia kituo cha maongezi kwenye kompyuta. Kituo cha maongezi ni mfumo unaowawezesha watumiaji wa Internet wawasiliane. Bila shaka, watu wengi huwasiliana na marafiki wa karibu kupitia E-mail. Wengine wanaoishi mbali na washiriki wa familia huweza kuwasiliana kwa ukawaida kupitia njia hiyo. Lakini kuna tofauti baina ya kumtumia mtu unayemjua E-mail na kuwasiliana na mtu usiyemjua. Je, ungefikiria kupiga nambari yoyote ya simu kisha kufanya urafiki na yeyote anayejibu simu hiyo? Bila shaka la! Basi kwa nini usitawishe uhusiano kwenye Internet na mtu usiyemjua?

Tatizo moja la kuwasiliana na mtu usiyemjua ni kwamba huenda asiwe kama unavyofikiria. Kwa mfano, huenda akawa ni mtu anayevutiwa kingono na watoto anayetumaini kumnasa mtoto au kijana asiye mwangalifu.

Parry Aftab, mwanasheria aliye mtaalamu wa visa vinavyohusiana na Internet, alieleza namna jambo hilo lilivyo rahisi. Alisema: “Kwa kawaida watoto hutumia vituo vya maongezi. Watu wanaovutiwa kingono na watoto wanajua hivyo, wao husoma ujumbe unaotumwa na kuwatafuta watoto walio wapweke. Mtoto aweza kutuma ujumbe kama huu ‘Wazazi wangu wanatalikiana . . . Namchukia mama yangu, haninunulii mchezo wa kompyuta ninaotaka.’ . . . Mtu huyo anayevutiwa kingono na watoto hujibu ujumbe huo kwa kusema ‘Wazazi wangu wanatalikiana . . . Namchukia mama yangu . . . Sikuweza kupata mchezo niliotaka hadi Mjomba Timmy aliponinunulia. . . . Unalohitaji kufanya ni kukutana na Mjomba Timmy kwenye jengo kubwa lenye maduka.’” “Mjomba Timmy” kwa kweli ndiye mtu anayevutiwa kingono na watoto na anayewavizia.

Hivyo basi, wazazi wapaswa kudumisha uhusiano mchangamfu, na wenye upendo pamoja na watoto wao. Wasilianeni waziwazi ili watoto wasitafute utegemezo wa kihisia-moyo kusikofaa.

Watu wazima walio wapweke au walio na matatizo ya ndoa hawapaswi kujiunga na vituo vya maongezi kwenye kompyuta ili kupata utegemezo wa kihisia-moyo. Kuwasiliana na watu usiowajua ni hatari sana. Watu wazima fulani wametengana na wenzi wao kwa sababu ya “kukutana” na mtu fulani kwenye Internet. *

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 38 Kwa habari zaidi kuhusu vituo vya maongezi kwenye kompyuta, tafadhali ona makala “Vijana Huuliza . . . Naweza Kuepukaje Hatari Katika Internet?” katika Amkeni! la Januari 22, 2000.

[Picha katika ukurasa wa 8]

Sala yaweza kumsaidia mtu ashinde kishawishi