Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ponografia Yapatikana Kwenye Internet

Ponografia Yapatikana Kwenye Internet

Ponografia Yapatikana Kwenye Internet

MAMILIONI YA WATU KOTEKOTE ULIMWENGUNI hutumia Internet kila siku. Wengi huitumia kufanyia biashara, kupata habari za karibuni za ulimwengu, habari za halihewa, kujifunza kuhusu nchi mbalimbali, kupata habari za usafiri, au kuwasiliana na familia na marafiki katika sehemu mbalimbali ulimwenguni. Lakini wengine—waseja na waliofunga ndoa na vilevile idadi kubwa ya watoto hutumia Internet kwa sababu tofauti kabisa: KUTAZAMA PONOGRAFIA.

PONOGRAFIA KWENYE KOMPYUTA, inayoitwa pia cyberporn katika Kiingereza, inapendwa sana hivi kwamba imekuwa biashara inayochuma mamilioni ya dola. Gazeti The Wall Street Journal lilisema: “Web site yenye kuleta faida, ni ile inayofanya biashara ya ponografia.”

Gazeti Journal liliendelea kueleza kwa nini watu hutafuta ponografia kwenye Internet: “Wateja waweza kutazama mambo yenye kutia ashiki bila kunyemelea ndani ya duka la vitabu vichafu au katika chumba cha nyuma cha duka la karibu la vidio. Wateja waweza kutazama mambo machafu kupindukia wakiwa faraghani ama nyumbani mwao au ofisini.”

Ponografia na Watoto

Kwa kusikitisha, watazamaji wengi wa ponografia kwenye Internet ni watoto. Vijana wasioruhusiwa na sheria kununua vitabu vya ponografia au kukodi vidio za ponografia wanaweza kupata habari hizo mara moja kwa kubonyeza usukani wa kompyuta wakiwa nyumbani mwao. Kuna habari chungu nzima.

Watoto wengi hutazama Web site nyingi kwa kawaida pasipo wazazi wao kujua. Kwa hakika, gazeti The Detroit News lasema kwamba “zaidi ya watoto wawili kati ya watano wamejiandikisha kwenye web site fulani au huduma nyingine za Internet licha ya kwamba takriban asilimia 85 ya wazazi wameweka sheria zinazowakataza kufanya hivyo.”

Ingawa watoto wengi—na watu wazima vilevile—huficha sana zoea lao la kutazama ponografia, watu wengine hawafichi. Watu fulani huona zoea hilo kuwa tafrija isiyodhuru. Wengine hukiri kwamba ponografia si nzuri kwa watoto lakini wanasababu kwamba mazoea ya faraghani ya watu wazima hayamhusu yeyote.

Katika nchi fulani ubishi juu ya ponografia umegeuka kuwa pambano kali la kisiasa. Kwa upande mmoja, watetezi wa uhuru wa usemi wanatetea ponografia, na kwa upande mwingine, watetezi wa maadili ya familia hushawishi serikali zipige marufuku ponografia.

Gazeti Amkeni! haliungi mkono upande wowote katika masuala ya kisiasa. Kusudi la mfululizo huu ni kuwafahamisha wasomaji wetu juu ya hatari za kutazama ponografia, kudokeza njia ambazo wanaweza kutumia kujilinda wenyewe na wapendwa wao, na kuandaa madokezo yanayotegemea Biblia kwa mtu yeyote ambaye ametumbukia katika ponografia na ambaye anataka kuacha kabisa zoea hilo.