Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Nikaishi Ng’ambo?

Je, Nikaishi Ng’ambo?

Vijana Huuliza . . .

Je, Nikaishi Ng’ambo?

“Nilitaka kuishi mahali pengine.”—Sam.

“Nilitaka tu kujua. Nilitaka kuona kitu fulani kipya.”—Maren.

“Rafiki wa karibu aliniambia kwamba ningenufaika kwa kuondoka nyumbani kidogo.”—Andreas.

“Nilitamani sana kujasiria.” —Hagen.

JE, UMEPATA kuwazia kuishi katika nchi ya kigeni—labda kwa muda mfupi tu? Kila mwaka, maelfu ya vijana huweza kufanya hivyo. Andreas asema hivi baada ya mambo aliyojionea ng’ambo: “Ningependa kwenda huko tena.”

Vijana wengine huhama kwa muda mfupi kwa sababu wanataka kuchuma pesa au kujifunza lugha ya kigeni. Kwa mfano, katika nchi nyingi programu za kuchukua mtumishi wa nyumbani kutoka nchi za kigeni ni za kawaida sana. Hizo huwaruhusu wageni wachanga kufanya kazi ya nyumbani kwa familia fulani na kupatiwa mahali pa kulala na chakula, na huwawezesha kutumia wakati wao wa ziada kujifunza lugha ya huko. Kisha kuna vijana wanaohamia ng’ambo ili kuendelea na masomo. Wengine huhama ili kutafuta kazi kusudi wasaidie familia zao kifedha. Na bado wengine huhama kwa sababu hawana uhakika kuhusu jambo wanalotaka kufanya baada ya shule na hutaka kupata pumziko huko ng’ambo.

Jambo la kupendeza ni kwamba vijana wengine Wakristo wamehamia nchi zilizo na waeneza-evanjeli wachache, ili kupanua huduma yao. Hata sababu ya kuhama iwe ni gani, kuishi katika nchi ya kigeni kwaweza kukufunza kujitegemea kama mtu mzima. Kwaweza kupanua ujuzi wako kuhusu utamaduni. Hata waweza kujifunza lugha ya kigeni—jambo linaloweza kufanya upate kazi kwa urahisi zaidi.

Hata hivyo, si jambo linalopendeza sikuzote kuishi ng’ambo. Kwa mfano, Susanne alitumia mwaka mmoja chini ya mpango wa kubadilishana wanafunzi. Asema: “Nilikuwa na hakika kwamba lingekuwa jambo lenye kufurahisha kuanzia mwanzo hadi mwisho. Haikuwa hivyo.” Vijana fulani wametumiwa vibaya au kupatwa na matatizo makubwa. Kwa hiyo kabla ya kupakia mizigo yako, lingekuwa jambo la hekima kuketi chini na kufikiria faida na hasara.

Changanua Nia Yako

Bila shaka kufikiria faida na hasara kunatia ndani kuchanganua nia yako ya kutaka kwenda ng’ambo. Wengine huhama ili kufuatia masilahi ya kiroho au kutunza madaraka ya familia. Lakini kama vijana walionukuliwa mwanzoni, wengi hutamani kuhama kwa sababu wanataka kujasiria, kupata uhuru zaidi, au kujifurahisha. Kwa kweli si kosa kufanya hivyo. Kwani, Mhubiri 11:9 huwatia moyo vijana ‘waufurahie ujana wao.’ Hata hivyo, mstari wa 10 waonya: “Ondoa majonzi moyoni mwako, nawe uuondoe ubaya mwilini mwako.”

Ikiwa nia yako ya kuhamia nchi ya kigeni ni kuepuka vizuizi vya wazazi, huenda ukazidisha uwezekano wa kupatwa na “ubaya.” Je, wakumbuka mfano wa Yesu wa mwana mpotevu? Ulihusisha mwanamume kijana aliyesafiri ng’ambo kwa sababu ya ubinafsi, labda ili kupata uhuru zaidi. Ingawa hivyo, punde si punde, afa likatokea, na akajikuta akiwa na njaa, maskini, na mgonjwa kiroho.—Luka 15:11-16.

Kisha kuna wale wanaotaka kuhama kwa sababu wanataka kukwepa matatizo ya nyumbani. Lakini, kama aandikavyo Heike Berg katika kitabu chake What’s Up, “ukitaka kuhama kwa sababu tu huna furaha . . . na unaamini kwamba mambo yote yatakuwa sawa mahali pengine—puuza wazo hilo!” Kwa kweli, ni afadhali kukabili matatizo moja kwa moja. Mtu hafaidiki na chochote anapotoroka hali zisizofurahisha.

Nia nyingine iliyo hatari ni pupa na ufuatiaji wa vitu vya kimwili. Kwa kuchochewa na tamaa ya mali, vijana wengi husitawisha mawazo ya juu yasiyo halisi kuhusu jinsi maisha yalivyo katika nchi zilizositawi. Wengine hufikiri kwamba wakazi wote wa nchi za Magharibi ni matajiri. Lakini hiyo si kweli hata kidogo. Baada ya kuhama, vijana wengi hujikuta katika nchi ya kigeni, wakipambana na umaskini. * Biblia huonya: “Kupenda fedha ni mzizi wa mambo mabaya ya namna zote, na kwa kujitahidi kufikilia kupenda huku wengine wameongozwa wapotee njia kutoka kwenye imani na wamejichoma wenyewe kotekote kwa maumivu mengi.”—1 Timotheo 6:10.

Je, Uko Tayari?

Kuna jambo jingine la kufikiria: Je, umekomaa vyakutosha kushughulika na magumu, matatizo, na mapambano yatakayotokea huko ng’ambo? Yaelekea utalazimika kuishi na mtu mwingine katika chumba kimoja au na familia fulani na kujipatanisha na ratiba yao. Umefanikiwa kadiri gani katika uhusiano wako na familia yenu sasa? Je, wazazi wako hulalamika kwamba wewe huwafikirii wengine na kwamba una ubinafsi? Je, wewe huchagua chakula utakachokula? Unakuwa tayari kadiri gani kufanya kazi za nyumbani? Ikiwa mambo hayo ni magumu kwako sasa, wazia jinsi yanavyoweza kuwa magumu utakapohamia nchi ya kigeni!

Ikiwa wewe ni Mkristo, je, utafaulu kudumisha hali yako ya kiroho? Au je, wazazi wako hulazimika kukukumbusha daima usipuuze funzo la Biblia, mikutano ya Kikristo, na kuhubiri? Je, utakuwa na nguvu za kiroho vyakutosha kukinza misongo na vishawishi huko ng’ambo ambavyo huenda usikabili nchini kwenu? Siku yake ya kwanza shuleni katika nchi ya kigeni, kijana mmoja Mkristo, mwanafunzi wa programu ya kubadilishana, alielezwa mahali anapoweza kupata dawa za kulevya haramu. Baadaye msichana mmoja aliyekuwa mwanashule mwenzake alimwomba wawe pamoja kwa muda fulani. Katika nchi ya kwao, msichana hangeweza kamwe kueleza upendezi wake waziwazi namna hiyo. Kijana mmoja Mwafrika aliyehamia Ulaya pia asema: “Katika nchi yetu huwezi kamwe kuona picha zisizo za adili hadharani. Lakini hapa unaziona kila mahali.” Kuhamia ng’ambo kwaweza kuongoza kwenye kuharibika kwa hali ya kiroho ikiwa mtu si “thabiti katika imani.”—1 Petro 5:9.

Tafuta Habari!

Kabla ya kuhamia ng’ambo unahitaji kutafuta habari zote. Usitegemee uvumi tu. Kwa mfano, ikiwa unafikiria mpango wa kubadilishana wanafunzi, utagharimu kiasi gani? Huenda ukashangaa kujua kwamba mara nyingi unagharimu maelfu ya dola. Pia unahitaji kujua ikiwa elimu utakayopata ng’ambo itakuwa na thamani yoyote nchini kwenu. Pia, pata habari nyingi kadiri uwezavyo kuhusu nchi hiyo—sheria zake, utamaduni wake, mapokeo yake. Inagharimu kiasi gani kuishi huko? Utahitaji kulipa kodi zipi? Je, kuna hatari za kiafya unazopaswa kufikiria? Huenda ukanufaika kwa kuzungumza na watu ambao wameishi huko.

Kisha wapaswa kufikiria mahali utakapoishi. Mara nyingi wazazi wanaokaribisha wanafunzi wa programu ya kubadilishana hawatarajii kulipwa. Hata hivyo, kuishi na watu wasioheshimu kanuni za Biblia kwaweza kusababisha mikazo na misongo mingi. Huenda ukaamua kuishi na marafiki au watu wa jamaa. Lakini uwe mwangalifu usiwe mzigo kwao—hata wakikusihi uishi nao. Hilo laweza kuleta mkazo au hata kuharibu uhusiano wako pamoja nao.—Mithali 25:17.

Ikiwa unapanga kuchuma pesa unapokuwa ng’ambo, usisahau wajibu wako wa Kikristo wa kutii mamlaka za kilimwengu. (Waroma 13:1-7) Je, unaruhusiwa kisheria kufanya kazi katika nchi hiyo? Ikiwa ndivyo, chini ya hali gani? Ukifanya kazi kwa njia haramu unaweza kuridhiana msimamo wako wa kuwa Mkristo mwenye kufuatia haki na kukosa ulinzi wa msingi, kama vile bima ya aksidenti. Hata ikiwa ni halali kufanya kazi, utahitaji kutahadhari na kutumia busara. (Mithali 14:15) Mara nyingi waajiri wafidhuli hutumia wageni vibaya.

Kufanya Uamuzi

Basi, ni wazi kwamba uamuzi wa kuhamia nchi ya kigeni ni mzito—nao haupasi kuchukuliwa kivivi hivi. Keti pamoja na wazazi wako na kufikiria kwa makini manufaa unayoweza kupata na hatari unazoweza kukabili. Usiruhusu shauku yako ifanye ukose kutumia ufahamu. Uwe mnyoofu unapochanganua nia yako. Wasikilize wazazi wako kwa makini. Kwani, bado wanaona kuwa wana daraka kukuelekea, hata unapokuwa mbali sana. Labda utahitaji wakutegemeze kifedha.

Baada ya kufikiria mambo yote, huenda ukaona kwamba halitakuwa jambo la hekima kuhama—angalau kwa sasa. Huenda ukatamauka, lakini kuna mambo mengi yenye kusisimua unayoweza kufanya. Kwa mfano, je, umefikiria uwezekano wa kuzuru sehemu zenye kupendeza katika nchi yako? Au kwa nini usianze kujifunza lugha ya kigeni? Baada ya muda, huenda fursa ya kusafiri ng’ambo ikajitokeza.

Ingawa hivyo, vipi ikiwa umeamua kuhama? Makala ya wakati ujao itazungumzia jinsi unavyoweza kufanikiwa kuishi ng’ambo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 15 Ona makala “Kuhesabu Gharama ya Kuhamia Nchi Yenye Utajiri,” katika toleo la Aprili 1, 1991, la Mnara wa Mlinzi, lililochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

[Picha katika ukurasa wa 13]

Vijana wengine huhama ili kuendeleza kazi ya kuhubiri Ufalme

[Picha katika ukurasa wa 14]

Zungumza pamoja na wazazi wako juu ya manufaa na hatari za kuhama