Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Dawa za Kulevya Mfululizo wa makala “Je, Dawa za Kulevya Zinaudhibiti Ulimwengu?” (Novemba 8, 1999) ulifanyiwa utafiti vizuri. Mimi ni ofisa wa majaribio wa wahalifu waliofunguliwa katika sehemu yenye waraibu wengi wachanga wa dawa za kulevya. Toleo hilo litawasaidia wengi kuacha zoea la kutumia dawa za kulevya.

J. T., Ujerumani

Kisa cha Pedro na mkewe Ana kilinitia moyo sana. Kwa muda wa miaka sita dawa za kulevya ziliharibu maisha yangu. Kupitia funzo la Biblia na kwa kuzungumza na wengine juu ya yale ninayojifunza nimepata nguvu ya kiroho niliyohitaji ili kuacha zoea la kutumia dawa za kulevya.

D. J., Marekani

Nimekuwa nikifundisha masomo ya afya shuleni kwa muda wa miaka 15. Kwa kuwa sasa tunajifunza kuhusu alkoholi, dawa za kulevya na udereva, toleo hilo la Amkeni! lilikuja kwa wakati unaofaa kabisa. Kwa hakika nitakuwa nikitumia habari kutoka toleo hilo!

C. J., Marekani

Kokwa ya Tagua Nimesoma kila nakala ya gazeti lenu tangu mwaka wa 1954, na sikuzote nastaajabia makala ambazo hueleza juu ya matumizi mengi mbalimbali ya vitu vilivyoumbwa na Yehova. Mojawapo ya makala ya aina hiyo ilikuwa “Kokwa ya Tagua—Je, Yaweza Kuokoa Tembo?” (Novemba 8, 1999) Asanteni kwa kutusaidia kuthamini zaidi na zaidi hekima ya ajabu ya Mungu wetu.

D. H., Marekani

Uchawi Asanteni sana kwa makala yenye kichwa “Ni Nini Husababisha Uchawi?” (Novemba 8, 1999) Zamani watu wengi walifikiri kwamba wachawi walikuwa wazee wenye sura isiyovutia. Lakini, leo harakati ya Wicca yavutia wavulana na wasichana wengi. Binti yangu mwenyewe alianza kupendezwa na harakati hiyo. Hata hivyo, alikuwa ameomba andikisho lake mwenyewe la Amkeni!, na toleo la kwanza alilopata lilikuwa na makala hiyo! Lilifika wakati unaofaa.

B. H., Marekani

Malaika Pongezi kwa mfululizo wa makala “Ukweli Ni Nini Kuhusu Malaika?” uliotoa habari hii waziwazi. (Novemba 22, 1999) Mwishowe, hatari za kuwa na maoni yaliyopotoka kuhusu malaika zilifichuliwa waziwazi kwa njia ya heshima na ujasiri. Nilipendezwa hasa na picha kwenye ukurasa wa 9, ionyeshayo jinsi malaika wenyewe wanavyokataa sifa isiyostahilika na umashuhuri wanaopewa leo.

J. L. A. H., Brazili

Majaribu ya Kitiba Simulizi kuhusu familia ya Major katika makala yenye kichwa “Tulijifunza Kumtegemea Mungu Kupitia Majanga” (Novemba 22, 1999) lilinitia moyo. Mwana wetu alikuwa na kasoro kadhaa za moyo zilizo hatari, naye alihitaji kupasuliwa. Madaktari walituambia, ‘Asipotiwa damu mwana wenu atakufa!’ Isitoshe, madaktari walitutenganisha mimi na mume wangu ili watushurutishe kukubali mwana wetu atiwe damu mishipani. Lakini, kama vile familia ya Major, tulisali ili tupate nguvu na ujasiri. Upasuaji wote mbalimbali ulifaulu, mwana wetu alipona na sasa ana afya nzuri. Alisema kwamba anatamani kubatizwa awe mmoja wa Mashahidi wa Yehova.

B. C., Marekani

Mume wangu alikuwa amelazwa hospitalini, na madaktari walisema kwamba, huenda angelazwa kwa miezi kadhaa. Nilikuwa nimechoka sana kwa kujaribu kuwatunza watoto watatu huku nikimtembelea mume wangu kila siku. Ninathamini sana jinsi ndugu na dada zangu Wakristo walivyonisaidia kutunza watoto. Nilipokuwa karibu kusalimu amri, mume wangu akarudi nyumbani. Niliposoma makala hiyo yenye kutia moyo, nililia machozi ya hisia-mwenzi kwa kuwa niliweza kuelewa yote ambayo yalikuwa yameipata familia ya Major. Nafurahi sana kuona jinsi walivyomtegemea Yehova kabisa!

J. A., Marekani