Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutumia Habari Vibaya

Kutumia Habari Vibaya

Kutumia Habari Vibaya

“Kwa kutumia uenezaji-habari bila kukoma na kwa njia ya werevu watu waweza kusadikishwa kuwa mbingu ni helo, na kwa upande mwingine maisha yanayosikitisha zaidi yaonekane kuwa paradiso.”—ADOLF HITLER, MEIN KAMPF.

KWA kuwa njia za mawasiliano zimepanuka—kuanzia kwa uchapishaji hadi simu, redio, televisheni, na Internet—ujumbe wenye kushawishi umeongezeka sana. Mabadiliko hayo makubwa ya mawasiliano yamesababisha ongezeko kubwa la habari, huku watu wakilemewa na habari chungu nzima kutoka kila mahali. Wengi huitikia msongo huo kwa kukubali ujumbe upesi zaidi bila kuupima au kuuchanganua.

Mweneza-habari mjanja hupenda njia za mkato kama hizo—hasa zile zinazomfanya mtu akubali bila kufikiri. Uenezaji-habari huendeleza jambo hilo kwa kuchochea hisia-moyo, kutumia vibaya hali ya shaka, utata wa lugha, na kupotoa kanuni zinazopatana na akili. Historia yashuhudia kwamba mbinu kama hizo zaweza kuwa na matokeo sana.

Historia ya Uenezaji-Habari

Leo neno “uenezaji-habari” huonwa kwa njia isiyofaa, ukiashiria mbinu zisizo za haki, lakini hapo awali neno hilo halikunuiwa kumaanisha hivyo. Yaelekea neno la Kiingereza “propaganda” linatokana na jina la Kilatini la kikundi cha makadinali wa Kanisa Katoliki, Congregatio de Propaganda Fide (Kundi la Kueneza Imani). Kamati hiyo—iliyoitwa Propaganda kwa ufupi—ilianzishwa na Papa Gregory wa Kumi na Tano mwaka wa 1622 ili kusimamia wamishonari. Hatua kwa hatua, neno la Kiingereza “propaganda” likaja kumaanisha jitihada yoyote ya kueneza itikadi fulani.

Lakini dhana ya uenezaji-habari haikuanza katika karne ya 17. Tokea nyakati za kale, watu wametumia njia zozote zilizopo kueneza mawazo au kuboresha umashuhuri na uwezo. Kwa mfano, waeneza-habari wametumia sanaa kujifaidi tangu siku za mafarao wa Misri. Wafalme hao walijenga piramidi zao ili kuonyesha waziwazi mamlaka yao na kudumu kwao. Vivyo hivyo, usanifu-ujenzi wa Roma ulichangia kusudi la kisiasa—kutukuza taifa. Neno “uenezaji-habari” likatwaa maana isiyofaa wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza serikali zilipoanza kujihusisha katika kusimamia habari za vita zilizoenezwa na vyombo vya habari. Katika Vita ya Ulimwengu ya Pili, Adolf Hitler na Joseph Goebbels walithibitika kuwa waeneza-habari walio mahiri.

Baada ya Vita ya Ulimwengu ya Pili, uenezaji-habari ulizidi kuwa chombo kikuu cha kuendeleza sera ya kitaifa. Jumuiya ya Magharibi na ya Mashariki zilifanya kampeni kubwa kupita zote ili kujipatia wafuasi wengi kutoka kwa watu wasiounga mkono upande wowote. Kila upande wa maisha na sera ya kitaifa ulitumiwa kuendeleza uenezaji-habari. Katika miaka ya karibuni kusitawi kwa njia tata za uenezaji-habari kumedhihirika katika kampeni za uchaguzi, na vilevile katika matangazo ya biashara ya makampuni ya tumbaku. Wale wanaoitwa eti wataalamu na viongozi wengine wameajiriwa ili kuonyesha kuwa kuvuta sigareti huvutia na hufaa afya na wala hakutishi afya ya umma kama ilivyo kwa kweli.

Uwongo, Uwongo!

Bila shaka, mbinu iliyo rahisi zaidi kutumiwa na waeneza-habari ni uwongo wa waziwazi. Kwa mfano, fikiria uwongo ulioandikwa na Martin Luther mwaka wa 1543 kuhusu Wayahudi huko Ulaya: “Wametia sumu kwenye visima, wameua watu, wamewateka nyara watoto . . . Wamejaa sumu, ni watu wenye kinyongo, walipiza-kisasi, nyoka wenye hila, wauaji, na watoto wa ibilisi wanaochoma na kudhuru.” Aliwahimiza nini walioitwa eti Wakristo? “Chomeni moto masinagogi au shule zao . . . Nyumba zao pia [zapasa] kuchomwa na kuharibiwa.”

Profesa wa serikali na mafunzo ya jamii aliyechunguza enzi hiyo asema: “Kwa msingi kuchukia Wayahudi hakuhusiani kabisa na matendo yao, kwa hiyo hakuhusiani kwa vyovyote na ikiwa wanaochukia Wayahudi wanajua asili yao ya kweli.” Pia asema: “Wayahudi waliwakilisha kila kitu kilichopotoka, hivi kwamba jambo lolote baya la asili au la kijamii lilisemekana kuwa limetendwa na Myahudi.”

Kujumuisha Mambo

Mbinu nyingine ya uenezaji-habari inayofaulu sana ni kujumuisha mambo. Kujumuisha mambo ni kuficha habari muhimu kuhusu suala linalobishaniwa, na mara nyingi hutumiwa kutweza kikundi kizima cha watu. Mathalani, msemo “wahamaji-wazururaji ni wezi” husikika sana katika nchi fulani za Ulaya. Lakini je, ni kweli?

Richardos Someritis, mwandishi-habari, asema kwamba katika nchi moja maoni hayo yalisababisha “hofu ya namna fulani kuelekea wageni na mara nyingi uchokozi” dhidi ya wageni. Hata hivyo, kuhusu uvunjaji wa sheria imeonyeshwa kwamba, wanaohusika katika nchi hiyo huenda wakawa ni wazaliwa au wageni. Kwa mfano, Someritis asema kwamba uchunguzi waonyesha kuwa katika Ugiriki, “kati ya visa vya uhalifu 96 kwa 100 hufanywa na [Wagiriki].” “Uhalifu husababishwa na mambo yanayohusu uchumi na jamii,” asema, “wala si ya ‘ubaguzi wa rangi.’” Analaumu vyombo vya habari “kwa kuchochea kwa ustadi chuki dhidi ya wageni na ubaguzi wa rangi” kwa kutoa habari bandia kuhusu uhalifu.

Kukashifu Watu

Watu wengine huwatukana wale wasiokubaliana nao kwa kushuku sifa au nia zao badala ya kukazia fikira mambo hakika. Kukashifu mtu ni kupachika mtu, kikundi, au wazo fulani jina lisilofaa linaloweza kukumbukwa kwa urahisi. Mkashifu-watu hutumaini kwamba jina hilo litadumu kwa muda mrefu. Mbinu ya kukashifu hufua dafu watu wanapokataa mtu huyo au wazo hilo kwa kutegemea tu sifa mbaya badala ya kuchanganua uthibitisho wao wenyewe.

Kwa mfano, katika miaka ya karibuni kumekuwa na maoni mengi mabaya sana dhidi ya madhehebu katika nchi nyingi za Ulaya na kwingineko. Mwelekeo huo umechochea hisia, ukatokeza uadui, na kuimarisha ubaguzi uliopo dhidi ya dini ndogo-ndogo. Mara nyingi, “madhehebu” huwa neno linalorudiwa-rudiwa. “‘Neno jingine la madhehebu ni ‘mzushi,’” akaandika profesa Mjerumani Martin Kriele katika mwaka wa 1993, “na leo katika Ujerumani kama ilivyokuwa hapo zamani mzushi [apasa kuangamizwa]—ikiwa si kuchomwa . . . , basi aharibiwe sifa, atengwe na watu na kufilisishwa.”

Taasisi ya Kuchunguza Uenezaji-Habari yasema kwamba “kushushia wengine hadhi kumechangia fungu kubwa sana katika historia ya ulimwengu na kusitawisha utu wetu wenyewe. Kumeharibu sifa, . . . kukawapeleka [watu] gerezani, na kuchochea watu wakasirike vya kutosha kwenda vitani na kuua wanadamu wenzao.”

Kutumia Hisia-Moyo ili Kujifaidi

Hisia hutimiza fungu kubwa katika kushawishi, hata ingawa huenda zisihusike kwa habari ya madai hakika au hoja mantiki. Jitihada za kuchochea hisia-moyo hufanywa na maajenti wa habari wazoefu, ambao hutumia vibaya hisia kwa njia stadi sawa na mpiga-piano aliye stadi.

Kwa mfano, hofu ni hisia inayoweza kumzuia mtu asitumie ufahamu. Sawa na husuda, hofu yaweza kutumiwa kwa kujifaidi. Gazeti la Kanada The Globe and Mail, la Februari 15, 1999, liliripoti habari ifuatayo kutoka Moscow: “Wasichana watatu walipojiua huko Moscow juma lililopita, upesi vyombo vya habari vya Urusi vilidokeza kwamba walikuwa wafuasi shupavu wa Mashahidi wa Yehova.” Ona neno “shupavu.” Kwa kawaida, watu wataogopa tengenezo la kidini la kishupavu linalodhaniwa kuwa huchochea vijana wajiue. Je, kwa kweli wasichana hao wa kusikitikiwa walikuwa Mashahidi wa Yehova kwa njia fulani?

Gazeti Globe liliendelea kusema: “Baadaye polisi walikiri kwamba wasichana hao hawakuwa na uhusiano wowote na [Mashahidi wa Yehova]. Lakini kufikia wakati huo kituo kimoja cha televisheni huko Moscow tayari kilikuwa kimeanzisha mashambulizi mapya dhidi ya madhehebu hayo, kikiwaambia watazamaji kwamba Mashahidi wa Yehova walishirikiana na Adolf Hitler katika Ujerumani ya Nazi—licha ya uthibitisho wa kihistoria kwamba maelfu ya washiriki wao waliuawa kwenye kambi za kifo za Nazi.” Watu wasiojua ukweli au wenye kuhofu, waliwaona Mashahidi wa Yehova kuwa ama madhehebu ya kujiua au washirika wa Nazi!

Chuki ni hisia kali inayotumiwa vibaya na waeneza-habari. Usemi unaodokeza mambo yasiyofaa huwa na matokeo sana katika kuianzisha. Inaonekana kwamba hakuna mwisho wa maneno machafu yanayoendeleza na kutumia vibaya chuki dhidi ya vikundi hususa vya kimbari, kikabila, au kidini.

Waeneza-habari fulani hutumia kiburi ili kujifaidi. Mara nyingi twaweza kutambua mambo yanayochochea kiburi kwa kuangalia maneno makuu kama vile: “Mtu yeyote aliye na akili anajua kwamba . . . ” au, “Mtu aliye na elimu kama wewe hawezi kukosa kuona kwamba . . . ” Tunaogopa kuonekana wapumbavu kwa hiyo kiburi kinatumiwa kutuchochea. Wataalamu wa kushawishi wanafahamu vizuri jambo hilo.

Shime na Ishara

Shime ni taarifa zisizo wazi zinazotumiwa hasa kuonyesha nyadhifa au miradi. Kwa sababu ya kutokuwa wazi, ni rahisi kuzikubali.

Kwa mfano, wakati wa msukosuko au mapambano ya kitaifa, huenda viongozi wakatumia shime kama vile “Ninaunga mkono nchi yangu, iwe iko sawa ama la,” “Nchi ya Kuzaliwa, Dini, Familia,” au “Uhuru au Kifo.” Lakini je, watu wengi huchanganua kwa makini masuala halisi yanayohusika katika tatizo au pambano hilo? Au wao hukubali tu wanaloambiwa?

Akiandika kuhusu Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, Winston Churchill alisema: “Ni kichocheo kimoja tu kinachohitajika ili kufanya umati huu wa wakulima na wafanyakazi wenye amani uwe jeshi lenye nguvu litakalouana.” Pia aliendelea kusema kwamba watu wengi huitikia bila kufikiri wanapoambiwa jambo la kufanya.

Pia mweneza-habari ana ishara za namna nyingi za kupitisha ujumbe wake—kufyatua risasi nyingi kwa pamoja, kupiga saluti ya kijeshi, bendera. Kuwapenda wazazi kwaweza kutumiwa vibaya pia. Hivyo, ufananisho kama vile nchi ya kuzaliwa, au kanisa la wazazi ni zana zinazotumiwa vilivyo na mshawishi mwerevu.

Kwa hiyo mbinu yenye hila ya uenezaji-habari yaweza kukandamiza mawazo, kufikiri vizuri na ufahamu, na kufanya watu watende kwa pamoja. Unaweza kujilindaje?

[Blabu katika ukurasa wa 8]

Mbinu yenye hila ya uenezaji-habari yaweza kukandamiza mawazo na kumfanya mtu asifikiri vizuri

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7]

JE, KAZI YA MASHAHIDI WA YEHOVA NI UENEZAJI-HABARI POTOVU?

Wapinzani fulani wa Mashahidi wa Yehova wamewashtaki kuwa waeneza-habari za Kiyahudi. Wengine wamedai kwamba huduma ya Mashahidi huendeleza Ukomunisti. Na bado kuna wengine ambao wamedai kwamba kazi ya Mashahidi wa Yehova huendeleza mawazo na masilahi ya “ubepari wa Kimarekani.” Pia kuna wale wanaosisitiza kwamba Mashahidi ni wapinzani wa serikali, wanaotokeza mvurugo wakiwa na lengo la kubadili utaratibu wa kijamii, kiuchumi, kisiasa, au kisheria. Bila shaka, mashtaka yote hayo yanayopingana hayawezi kuwa ya kweli.

Ukweli ni kwamba Mashahidi wa Yehova hawako kama inavyodokezwa juu. Mashahidi hufanya kazi yao kwa kutii kwa uaminifu amri ya Yesu Kristo kwa wafuasi wake: “Mtakuwa mashahidi wangu . . . hadi sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia.” (Matendo 1:8) Kazi yao hukazia kwa njia ya pekee habari njema za Ufalme wa kimbingu—chombo atakachotumia Mungu kuleta amani duniani pote.—Mathayo 6:10; 24:14.

Watu wanaowatazama Mashahidi wa Yehova hawajapata uthibitisho wowote kwamba kikundi hiki cha Kikristo kimewahi kuwa kani inayovuruga utaratibu mzuri wa nchi yoyote.

Waandishi-habari, mahakimu, na wengine wengi wametoa maelezo kuhusu mambo mazuri ambayo Mashahidi wa Yehova wamefanyia jumuiya wanamoishi. Fikiria baadhi ya mifano hiyo. Baada ya kuhudhuria mkusanyiko wa Mashahidi wa Yehova, ripota mmoja kutoka kusini mwa Ulaya alitoa maelezo haya: “Hawa ni watu walio na vifungo imara vya familia, wanafundishwa kupenda na kuishi kupatana na dhamiri zao ili wasiwadhuru wengine.”

Mwandishi-habari mwingine ambaye hapo awali alikuwa na maoni yasiyofaa kuhusu Mashahidi, alisema: “Maisha yao ni ya kuigwa. Hawavunji viwango vya maadili na mambo yaliyo sawa.” Vivyo hivyo, mwanasayansi mmoja wa siasa alisema hivi kuhusu Mashahidi: “Wanawatendea watu wengine kwa fadhili nyingi, kwa njia ya upendo na uanana.”

Mashahidi wa Yehova hufundisha ni kwa nini inafaa kunyenyekea mamlaka. Wakiwa raia wanaotii sheria, wanafuata viwango vya Biblia vya kufuatia haki, ukweli, na usafi. Wanasaidia familia zao kufuata maadili yafaayo, nao huwasaidia wengine wajifunze namna wanavyoweza kufanya vivyo hivyo. Wanaishi kwa amani na watu wote, bila kujihusisha na maandamano yanayoleta mvurugo au mapinduzi ya kisiasa. Mashahidi wa Yehova hujitahidi kuweka kielelezo katika kutii sheria za mamlaka zilizo kubwa za kibinadamu, huku wakingoja kwa saburi Mamlaka Kuu Kuliko Zote, Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, arudishe amani kamili na serikali yenye uadilifu kwenye dunia hii.

Wakati huohuo, kazi ya Mashahidi ni ya kuelimisha watu. Wakitumia Biblia kama msingi, wao wanafundisha watu ulimwenguni pote kusababu juu ya kanuni za Biblia na hivyo kusitawisha viwango vifaavyo vya mwenendo na uaminifu wa kiadili. Wanaendeleza kanuni zinazoboresha maisha ya familia na kusaidia vijana wakabiliane na misongo ya kipekee. Pia wanasaidia watu wapate nguvu za kuacha mazoea mabaya na kusitawisha uwezo wa kupatana na wengine. Kwa hakika kazi hiyo haiwezi kuwa “uenezaji-habari potovu.” Kama kisemavyo The World Book Encyclopedia, mahali palipo na uhuru wa kujieleza, “uenezaji-habari hutofautiana na elimu.”

[Picha]

Vichapo vya Mashahidi wa Yehova hukazia kanuni za familia na viwango vya juu vya maadili

[Picha katika ukurasa wa 5]

Uenezaji-habari unaoendeleza vita na kuvuta sigareti umesababisha vifo vya watu wengi