Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Usiathiriwe na Uenezaji-habari!

Usiathiriwe na Uenezaji-habari!

Usiathiriwe na Uenezaji-habari!

“Mjinga huamini kila neno.”—MITHALI 14:15.

KUNA tofauti kubwa sana kati ya elimu na uenezaji-habari. Elimu hukuonyesha jinsi ya kufikiri. Uenezaji-habari hukuambia utakachofikiri. Waelimishaji wazuri hutaja habari zote na kutia moyo mazungumzo. Waeneza-habari hukulazimisha daima kusikiliza maoni yao na hawapendi kuwe na mazungumzo. Mara nyingi ni vigumu kujua nia yao halisi. Huchanganua mambo hakika, wakitumia kwa faida yao mambo yenye mafaa na kuficha mengine. Pia hupotosha mambo, huku wakisema uwongo na kudanganya. Shabaha yao huwa ni hisia-moyo zako wala si uwezo wako wa kufikiri.

Mweneza-habari huhakikisha kwamba ujumbe wake waonekana kuwa wafaa na wa adili na kwamba utakufanya ujione kuwa mtu wa maana na anayethaminiwa unapoutii. Wewe ni mmojawapo wa watu walioerevuka, huko peke yako, huna shaka yoyote wala hofu—ndivyo wasemavyo.

Unaweza kujilindaje mwenyewe na aina ya watu ambao Biblia huwaita “waongeaji wa yasiyokuwa na faida” na “wadanganyi wa akili”? (Tito 1:10) Unapofahamu baadhi ya mbinu zao, utaweza kuchanganua ujumbe au habari yoyote unayopata. Zifuatazo ni baadhi ya njia za kufanya hivyo.

Uwe mteuzi: Akili inayopokea kila kitu yaweza kufananishwa na mfereji unaopitisha kitu chochote—hata maji machafu. Hakuna mtu yeyote anayetaka akili yake itiwe sumu. Solomoni, aliyekuwa mfalme na mwelimishaji wa kale alionya hivi: “Mjinga huamini kila neno; bali mwenye busara huangalia sana aendavyo.” (Mithali 14:15) Kwa hiyo twahitaji kuwa wateuzi. Twahitaji kuchanganua mambo tunayoonyeshwa, na kuamua tutakayokubali na tutakayokataa.

Hata hivyo, hatuhitaji kuwa na akili finyu hivi kwamba tukatae kufikiria mambo yawezayo kuboresha kufikiri kwetu. Twawezaje kuwa na usawaziko ufaao? Kwa kuwa na kiwango cha kupimia habari mpya. Kwa habari hiyo, Mkristo ana chanzo cha hekima kubwa sana. Ana Biblia inayoandaa mwongozo hakika kwa ajili ya kufikiri kwake. Kwa upande mmoja, ana akili iliyofunguka, ambayo hupokea habari mpya. Hupima kwa uangalifu habari hiyo mpya kwa kuilinganisha na viwango vya Biblia na kutumia yale yanayofaa katika kufikiri kwake. Kwa upande mwingine, yeye huona akilini mwake hatari ya habari ambayo haipatani kabisa na kanuni zake zinazotegemea Biblia.

Tumia ufahamu: Ufahamu ni “ustadi wa kuamua mambo.” Ni “nguvu au uwezo wa akili ambao hutofautisha kati ya jambo moja na jingine.” Mtu mwenye ufahamu huona mawazo au mambo yenye hila naye hufanya uamuzi timamu.

Kwa kutumia ufahamu, tutaweza kutambua wale wanaotumia tu “maongezi laini na usemi wa kusifu-sifu” ili ‘kushawishi mioyo ya wasio na hila.’ (Waroma 16:18) Ufahamu hukuwezesha utupilie mbali habari zisizokuhusu au zisizofaa na kupambanua umuhimu wa jambo. Lakini unaweza kujuaje jambo fulani linapokuwa lenye kupotosha?

Chunguza habari hiyo: “Wapendwa,” akasema Yohana, mwalimu Mkristo wa karne ya kwanza, “msiamini kila usemi uliopuliziwa, lakini jaribuni semi zilizopuliziwa.” (1 Yohana 4:1) Watu fulani leo ni kama sponji; hufyonza habari zozote wanazopata. Ni rahisi sana kupokea habari zozote zinazotuzunguka.

Lakini ni afadhali kila mtu achague kile atakacholisha akili yake. Sisi huathiriwa na kile tunacholisha mwili na akili. Hata iwe unasoma au unatazama au unasikiliza nini, chunguza uone ikiwa huo ni uenezaji-habari au ni habari ya kweli.

Isitoshe, ikiwa twataka kuwa wenye kufuatia haki, lazima tujaribu maoni yetu daima tunapojifunza habari mpya. Lazima tutambue kwamba hayo ni maoni tu. Yaweza kutumainika ikitegemea habari tulizo nazo, ubora wetu wa kusababu, na kanuni au viwango tunavyochagua kutumia.

Uliza maswali: Kama tulivyoona, kuna wengi leo ambao wangependa ‘kutupotosha kwa hoja zenye kushawishi.’ (Wakolosai 2:4) Kwa hiyo, tunapokabili hoja zenye kushawishi, twapaswa kuuliza maswali.

Kwanza, chunguza uone ikiwa kuna ubaguzi. Ni nini kusudi la ujumbe huo? Ikiwa ujumbe huo ni wa kukashifu watu na una usemi unaodokeza mambo yasiyofaa, ni kwa nini uko hivyo? Mbali na usemi unaodokeza mambo yasiyofaa, ujumbe huo una wema gani? Pia, ikiwezekana, jaribu kuchunguza rekodi ya wale wanaosema. Je, ni watu ambao husema kweli? Ikiwa wananukuu “mamlaka,” ni akina nani au ni gani? Kwa nini unaona mtu huyo—au shirika au kichapo—kuwa na ujuzi wa kitaalamu au habari yenye kutegemeka kuhusu jambo linalozungumziwa? Ukiona hisia zako zinachochewa, jiulize, ‘Unapoangalia ujumbe huo bila kupendelea upande wowote, una wema gani?’

Usifuatane tu na umati: Uking’amua kwamba kile ambacho kila mtu hufikiri si lazima kiwe sahihi, unaweza kupata nguvu za kufikiri tofauti. Ingawa huenda ikaonekana kwamba watu wote wanafikiri kwa njia ileile, je, hilo lamaanisha kwamba wewe wapaswa kufanya hivyo? Maoni yanayopendwa na wengi si kipimio kinachotegemeka cha kuamua ukweli. Katika karne nyingi maoni mengi yamekubaliwa na umma na baadaye yakaja kuthibitishwa kuwa bandia. Hata hivyo, kuna mwelekeo wa kufuatana na umati. Amri iliyotolewa kwenye Kutoka 23:2 ni kanuni ifaayo: “Usiandamane na mkutano kutenda uovu.”

Kulinganisha Ujuzi wa Kweli na Uenezaji-Habari

Hapo awali, ilitajwa kwamba Biblia ni mwongozo hakika kwa ajili ya kufikiri kuzuri. Mashahidi wa Yehova huamini na kukubali waziwazi taarifa ya Yesu kwa Mungu: “Neno lako ni kweli.” (Yohana 17:17) Hivyo ndivyo ilivyo kwa sababu Mungu, Mtungaji wa Biblia, ni “Mungu wa kweli.”—Zaburi 31:5.

Naam, katika kizazi hiki cha uenezaji-habari potovu wa hali ya juu, twaweza kutegemea kwa hakika Neno la Yehova kuwa chanzo cha kweli. Hatimaye hilo litatulinda na wale wanaotaka ‘kututumia kujifaidi kwa maneno bandia.’—2 Petro 2:3.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Ufahamu hukuwezesha utupilie mbali habari zisizokuhusu au zisizofaa

[Picha katika ukurasa wa 10]

Chunguza unachosoma au kutazama, kuona ikiwa ni habari ya kweli

[Picha katika ukurasa wa 11]

Maoni yanayopendwa na wengi hayategemeki sikuzote

[Picha katika ukurasa wa 11]

Twaweza kutegemea kwa hakika Neno la Mungu kuwa chanzo cha kweli