Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tabasamu Ni Yenye Manufaa Kwako!

Tabasamu Ni Yenye Manufaa Kwako!

Tabasamu Ni Yenye Manufaa Kwako!

NA MLETA-HABARI WA AMKENI! KATIKA JAPANI

INAPOKUWA ya kweli, huondoa shuku. Huondoa ubaguzi mwingi uliokuwako kwa miaka kadhaa. Hulainisha mioyo iliyofanywa migumu kwa kutoamini na kutotumaini. Huletea wengi kitulizo na shangwe. Hiyo husema, “Naelewa. Usijali.” Huomba hivi, “Natumaini twaweza kuwa marafiki.” Ni nini hiyo yenye nguvu? Ni tabasamu. Inaweza kuwa tabasamu YAKO.

Tabasamu ni nini? Kwa kawaida tabasamu hufafanuliwa na kamusi kuwa ‘ishara ya uso ambapo mdomo hujipinda kidogo pembeni kuelekea juu, hivyo kuonyesha furaha, kibali, au shangwe.’ Hiyo ndiyo siri ya tabasamu changamfu. Tabasamu ni njia ya kuonyesha hisia bila kutamka maneno au ya kuwasilisha hisia-moyo zako kwa wengine. Bila shaka, tabasamu yaweza pia kuonyesha mabezo au madharau, lakini hayo ni mambo mengine.

Je, kweli kutabasamu hubadili hali ya mambo? Je, wakumbuka wakati tabasamu ya mtu fulani ilipokufanya uhisi kitulizo au kukufanya uhisi umestarehe? Au mtu alipokosa kutabasamu kukakufanya uwe na wasiwasi au hata kuhisi umepuuzwa? Naam, tabasamu hubadili hali ya mambo. Huwa na matokeo kwa yule anayetabasamu na yule ambaye ameonyeshwa tabasamu. Yobu, anayetajwa katika Biblia alisema hivi kuhusu adui zake: “Kama nikiwacheka [“nikatabasamu nao,” NW] hawakuamini; wala hawakuangusha nuru ya uso wangu.” (Ayubu 29:24, Zaire Swahili Bible) “Nuru” ya uso wa Yobu huenda ilirejezea furaha au uchangamfu.

Matokeo mazuri ya tabasamu yangali hivyo mpaka leo. Tabasamu changamfu huenda ikasaidia kupunguza mkazo mwingi. Huenda ikathibitika kuwa kama vali ya usalama kwenye sufuria ya mvuke. Tunapohisi mkazo au tumevunjika moyo, tabasamu yaweza kutusaidia kupunguza mkazo huo na kukabiliana na hali yetu ya kuvunjika moyo. Kwa mfano, mara nyingi Tomoko aliona wengine wakimtazama. Alidhani kwamba wanamchambua walipoelekeza macho yao upande mwingine haraka walipotambua kuwa amegundua kwamba wanamtazama. Tomoko alikuwa mpweke na asiye na furaha. Siku moja, rafiki yake alimdokezea kwamba awe akitabasamu watu wakimtazama. Tomoko alijaribu kufanya hivyo kwa majuma mawili naye alistaajabu kwamba kila mtu alitabasamu! Mikazo ikatoweka. “Maisha yanafurahisha sasa kwelikweli,” asema. Naam, tabasamu hutufanya tustarehe tukiwa na wengine na hutusaidia tuwe wenye urafiki zaidi.

Matokeo Mazuri Kwako na kwa Wengine

Kutabasamu kwaweza kuathiri mtu kihisia-moyo. Husaidia mtu awe na hali inayofaa ya akili. Pia kwafaa afya ya kimwili. Kuna msemo usemao, “kicheko ni dawa nzuri.” Kwa kweli, wakuu wa kitiba wanasema kwamba hali ya mtu ya akili yahusika zaidi katika afya ya kimwili ya mtu. Uchunguzi mwingi waonyesha kwamba mkazo wa muda mrefu, hisia-moyo zisizofaa, na hali kama hizo hudhoofisha mfumo wetu wa kinga mwilini. Kwa upande mwingine, kutabasamu kwaweza kutufanya tuhisi vizuri, na kicheko hata huimarisha mfumo wetu wa kinga mwilini.

Tabasamu ina matokeo makubwa kwa wengine. Hebu wazia ukiwa katika hali ambayo unapokea shauri au onyo la upole. Ungependa kuona mshauri wako akiwa na sura ya aina gani? Sura isiyo ya kirafiki au ya ukali yaweza kuonyesha hasira, kuudhika, kupuuzwa, au hata uhasama. Lakini je, tabasamu ya kirafiki ya mshauri haitakufanya labda usiwe na wasiwasi na hivyo ukubali shauri vyepesi? Hakika, tabasamu husaidia kupunguza kutoelewana katika hali zenye mkazo.

Mawazo Yenye Kujenga Hufanya Iwe Rahisi Zaidi Kutabasamu

Bila shaka, wengi wetu si kama waigizaji wa kulipwa ambao wanaweza kutabasamu haraka dakika yoyote ile; wala hatutaki kuwa hivyo. Twataka tabasamu zetu ziwe halisi na za kweli. Mfunzi wa shule ya maelewano alieleza hivi: ‘Ni jambo la maana kustarehe na kutabasamu kwa moyo wako wote, la sivyo, tabasamu yako yaweza kuonekana isiyo halisi.’ Twawezaje kutabasamu kwa moyo wote? Biblia yaweza kutusaidia katika jambo hili. Kuhusu usemi wetu Biblia hutuambia hivi katika Mathayo 12:34, 35: “Kwa maana kutoka katika wingi wa moyo kinywa husema. Mtu mwema kutoka katika hazina yake njema hupeleka nje mambo mema, lakini mtu mwovu kutoka katika hazina yake mbovu hupeleka nje mambo maovu.”

Kumbuka kwamba, tabasamu ni njia ya kuwasilisha hisia zetu bila kutamka maneno. Tukikumbuka kwamba twasema “kutoka katika wingi wa moyo” na kwamba “mambo mema” hutoka katika “hazina njema,” ni dhahiri kwamba kiini cha tabasamu ya kweli hutokana na mawazo yetu na hisia-moyo zetu. Naam, wakati mwingine, kilicho ndani ya mioyo yetu bila shaka kitaonyeshwa kwa maneno na matendo yetu na vilevile sura ya uso wetu. Hivyo, twahitaji kuendelea kujitahidi kudumu tukiwaza mambo yajengayo. Sura ya uso wetu huathiriwa sana na mawazo yetu kuhusu wengine. Kwa hiyo acheni tukazie fikira sifa njema zaidi za washiriki wa familia, jirani zetu, na rafiki zetu wa karibu. Tutaona ikiwa rahisi kuwaonyesha tabasamu. Itakuwa tabasamu ya kweli, kwa kuwa itakuwa imechochewa na moyo uliojaa mema, huruma, na fadhili. Macho yetu yatakuwa maangavu, na wengine watajua kwamba twamaanisha hivyo.

Ingawa hivyo, ni lazima itambuliwe kwamba kwa sababu ya malezi yao au mazingira yao, watu fulani huona likiwa jambo gumu kutabasamu kuliko wengine. Hata kama wana nia njema kuelekea jirani zao, hawajazoea kuwaonyesha tabasamu. Kwa mfano, kidesturi wanaume Wajapani wanatazamiwa kuwa na hali ya utulivu kamili nyakati zote. Kwa hiyo, wengi wao hawajazoea kuwaonyesha wageni tabasamu. Huenda ikawa hivyo pia na tamaduni nyinginezo. Au watu fulani huenda wakawa wenye haya kiasili na huenda wasione kuwa jambo rahisi kuonyesha wengine tabasamu. Kwa hiyo, hatupaswi kuhukumu wengine kwa jinsi tabasamu yao ilivyo kubwa au kadiri ambavyo hutabasamu. Watu wako tofauti, na ndivyo zilivyo tabia zao na njia zao za kuwasiliana na wengine.

Hata hivyo, ikiwa waliona kuwa jambo gumu kuonyesha wengine tabasamu, kwa nini usilifanyie kazi? Biblia hushauri hivi: “Acheni tusife moyo katika kufanya lililo bora . . . Acheni sisi tufanye lililo jema kuelekea wote.” (Wagalatia 6:9, 10) Njia moja ya kufanya “lililo jema” kuelekea wengine ni kuwaonyesha tabasamu—nawe waweza kufanya hivyo! Kwa hiyo chukua hatua kusalimu wengine ukiwatia moyo kwa tabasamu. Itathaminiwa sana. Pia, utatambua kwamba kutabasamu huwa rahisi zaidi unapoendelea kusitawisha zoea hilo.

[Sanduku katika ukurasa wa 12]

Uwe Mwangalifu

Inasikitisha kwamba si kila tabasamu huwa ya kweli. Walaghai, wauzaji wasio wanyoofu, na wengine huenda wakaonyesha tabasamu zenye kuvutia sana. Wanajua kwamba tabasamu yaweza kutiisha watu na kuwazubaisha. Watu wenye maadili yenye kutiliwa shaka au mitazamo isiyo safi huenda pia wakawa na tabasamu yenye kutongoza. Hata hivyo, tabasamu zao hazifai kitu; ni zenye udanganyifu. (Mhubiri 7:6) Kwa hiyo ingawa hatupaswi kuwashuku sana wengine, twahitaji kufahamu kwamba kwa kuwa tunaishi katika “siku za mwisho,” ambazo ni ngumu kushughulika nazo, twahitaji ‘kujithibitisha wenyewe kuwa wenye hadhari kama nyoka na bado kuwa wasio na hatia kama njiwa,’ kama Yesu mwenyewe alivyopendekeza.—2 Timotheo 3:1; Mathayo 10:16.

[Picha katika ukurasa wa 13]

Chukua hatua ya kuwasalimu wengine kwa tabasamu