Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Naweza Kufanikishaje Maisha Yangu Ng’ambo?

Naweza Kufanikishaje Maisha Yangu Ng’ambo?

Vijana Huuliza . . .

Naweza Kufanikishaje Maisha Yangu Ng’ambo?

“Nilipofika kwenye uwanja wa ndege, nilitaka tu kurudi nyumbani! . . . Tamaa yangu ya kugundua mambo mapya ilikwisha na vilevile shangwe yangu yote ya uvumbuzi. Kwa ufupi, nilikuwa natamani sana nyumbani kuliko hapo awali.”—Uta.

INAOGOFYA sana kuwa peke yako katika nchi ya kigeni. Lakini kama vile makala iliyotangulia katika mfululizo huu ilivyoonyesha, vijana wengi wanachagua kwenda kuishi ng’ambo kwa muda fulani. Wengine huenda kupata elimu au mafunzo ya pekee. Wengine wanataka kujifunza lugha fulani. Wengine wanataka tu kuchuma fedha. Hata hivyo, wengine wamehamia katika nchi za kigeni ambazo zina uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme.

Tuseme kwamba unaishi ng’ambo kwa sababu zenye hekima—sababu ambazo zinatia ndani mahitaji yako ya kiroho na miradi yako *—unaweza kufanya nini ili kuhakikisha kwamba utafanikiwa?

Azimia Kubadilika ili Ufaane na Huko

Kwanza, lazima uwe tayari kubadilika ili ufaane na huko. Hiyo haimaanishi uache kanuni zako za Kikristo au utaratibu wako wa kiroho. Lakini huenda ikamaanisha kupenda vyakula vipya, kujifunza baadhi ya kanuni na adabu, au kujaribu njia mpya za kufanya mambo. Desturi hizo mpya huenda zikawa tofauti na jinsi ulivyofanya mambo kule nyumbani. Lakini amri ya Yesu ya ‘kutohukumu’ yaweza kutumika kuhusiana na hilo. (Mathayo 7:1) Kwa kweli, hakuna jamii au utamaduni ambao una haki ya kujitangaza kuwa bora kuliko wengine. (Matendo 17:26) Kama tu vile watu wazee wanavyopaswa kuepuka kulinganisha isivyofaa vijana wa zamani na wale wa siku hizi, vijana walio ng’ambo pia wapaswa kuepuka kulinganisha isivyofaa nchi ya kigeni na ile yao. (Mhubiri 7:10) Kazia fikira mambo yajengayo ambayo nchi hii mpya na utamaduni wake yaweza kuwa nayo. Pia, kadiri utakavyojifunza lugha ya nchi hiyo haraka, ndivyo utakavyoanza kuhisi kama uko kwenu.

Mtume Paulo alibadilika ili afaane na utamaduni mbalimbali katika kazi ya umishonari kwa sababu alikuwa tayari ‘kuwa mambo yote kwa watu wa namna zote.’ (1 Wakorintho 9:22) Mtazamo huohuo waweza kukusaidia ubadilike ili ufaane na huko. Adrianne ni mtumishi wa nyumbani wa kike anayeishi Ujerumani, akifanyia familia moja kazi za nyumbani kwa ujira wa chakula na malazi. Yeye aeleza hivi: “Lazima niwe mwenye kubadilika kwa sababu siwezi kutazamia wengine wabadilike ili wafaane nami.”

‘Natamani Sana Nyumbani!’

Wakati wa majuma machache ya kwanza, ni kawaida kuwa na huzuni na kutamani sana nyumbani. Biblia huonyesha kwamba Yakobo ‘alitamani sana nyumba ya baba yake,’ hata ingawa Yakobo alikuwa amekaa katika nchi ya kigeni kwa zaidi ya miaka 20! (Mwanzo 31:30) Kwa hiyo usishangae ikiwa nyakati nyingine utalazimika kulia. Bila shaka, mara nyingi ukiendelea kufikiria yale uliyoacha nyuma, utaongeza tu huzuni yako. (Hesabu 11:4, 5) Njia bora zaidi ya kushinda huzuni ni kujitahidi kuzoea utaratibu wako na mazingira yako mapya. Ijapokuwa inafaa kuwasiliana na familia yako kwa barua au simu, kupiga simu kila mara nyumbani kwaweza kukuzuia kuzoea makao yako mapya.

Vijana wengi Wakristo huona kwamba kurudia utaratibu wao wa kiroho ndilo suluhisho bora zaidi la upweke. (Wafilipi 3:16) Amber akumbuka majuma yake ya kwanza-kwanza akiwa ng’ambo: “Hali ilikuwa ngumu wakati wa jioni, ambapo sikuwa na kitu cha kufanya, kwa hiyo nilijaribu kujifunza zaidi au kusoma kitabu.” Kijana Mwingereza Rachel, ambaye ni mtumishi wa nyumbani wa kike kwa ujira wa chakula na malazi huko Ujerumani, azungumzia jambo alilojionea mwenyewe anapotoa mawaidha haya: “Jihusishe bila kukawia. Anza kuhudhuria mikutano mara moja.” Mwanzoni, huenda ukahitaji msaada wa kufika mikutanoni. Lakini katika kutaniko la Kikristo, unaweza kupata marafiki wafaao ambao wanaweza kuwa kama “akina ndugu na akina dada na akina mama.”—Marko 10:29, 30.

Kushiriki katika kazi ya Kikristo ya kueneza evanjeli pia ni sehemu ya maana ya utaratibu mzuri wa kiroho. Kuhubiri hakutakunufaisha kiroho tu bali pia kutakusaidia uzoee utamaduni na lugha mpya.

Mwishowe, endeleza utaratibu wa sala na funzo la kibinafsi. Hayo ni mambo muhimu katika kuendeleza afya yako ya kiroho. (Waroma 12:12; 1 Timotheo 4:15) Kwa hiyo, Adrianne, aliyetajwa mwanzoni, alihakikisha kwamba alibeba vichapo vya Biblia vya lugha yake.

Kuishi na Familia Inayokukaribisha

Vijana fulani Wakristo wamepanga kuishi na familia zenye kuitikadi wakiwa huko ng’ambo. Ijapokuwa huwezi kutarajia familia inayokukaribisha ichukue daraka la wazazi wako, wanaweza kuwa mashirika mazuri na chanzo cha kitia-moyo cha kiroho.—Mithali 27:17.

Ijapokuwa hivyo, mawasiliano ya wazi pamoja na familia inayokukaribisha ni muhimu ili kudumisha uhusiano mzuri. (Mithali 15:22; 20:5; 25:11) Amber ataja hivi: “Wapaswa kuwa na mpango wa kile utakachohitaji kufanya. Wahitaji kujua matarajio ya wanaokukaribisha. Nao wapaswa kujua matarajio yako.” Pata kujua kanuni za familia za nyumba hiyo na kadiri unavyotazamiwa kushiriki kazi za nyumbani. Mambo hayo yapaswa kuzungumziwa kikamili.

Hali yako itakuwa ngumu hasa, ikiwa tuseme, unafanyia kazi familia ambayo haina itikadi kama zako. Kwa kuwa familia hiyo huenda isielewe msimamo wako kuhusu kanuni za Biblia, unaweza kujikuta katika hali za kuridhiana. (Mithali 13:20) Madai ya kutimiza kazi za nyumbani yanaweza kuhitilafiana na wajibu wako wa kiroho, kama vile kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Kwa hiyo hali zisizoepukika zikikufanya uishi na familia yenye itikadi tofauti na zako, basi wapaswa kujihadhari kwa mambo kadhaa.

Rachel apendekeza hivi: “Hakikisha kwamba wanajua wewe ni Mkristo. Ni afadhali uwaambie waziwazi mara moja.” Kueleza viwango vyako vya kidini na kiadili kwaweza kuwa ulinzi. Pia, wapaswa kueleza mwajiri wako jinsi mikutano ya Kikristo na kuhubiri kulivyo kwa maana kwako. Mwishowe, ni jambo la hekima kuhakikisha kwamba mambo ya maana kama vile muda wa saa za kufanya kazi, wakati wa kupumzika, na malipo yameandikwa kabla hujaanza. Kufanya hivyo kwaweza kuzuia matatizo baadaye.

Kutatua Matatizo

Zijapokuwa jitihada zako za pekee, matata yanaweza kutokea. Kwa mfano, vipi wanaokukaribisha wakidai uondoke nyumbani kwao? Hilo laweza kutatiza sana. Kutoelewana kukitokea, unaweza kujaribu kuzungumzia mambo hayo na wanaokukaribisha kwa njia ya utulivu na ya kiasi. (Mithali 15:1) Uwe tayari kukubali makosa yoyote ambayo huenda ikawa ulifanya. Labda watabadili maoni yao. Ikiwa sivyo, utalazimika kutafuta mahali pengine pa kuishi.

Matatizo mengine huenda yakataka umwombe mtu fulani msaada. Kwa mfano, huenda ukapatwa na tatizo la fedha au ukawa mgonjwa. Ukiogopa kwamba wazazi wako wanaweza kukurudisha nyumbani, huenda ukasita kuwajulisha yaliyotokea. Isitoshe, wako kilometa nyingi sana kutoka mahali ulipo nao huenda wasijue jinsi ya kushughulika na hali fulani katika nchi ya kigeni. Hata hivyo, wazee wa kutaniko la hapo wanaweza kuwa na uzoefu wa kushughulikia matatizo hayo na huenda wakaweza kukupa mawaidha yenye kusaidia. Pia huenda wakaweza kukusaidia uamue kama hilo ni jambo ambalo wapaswa kujulisha wazazi wako.

Kurudi Nyumbani

Yajapokuwa magumu, kutumia wakati ng’ambo kwaweza kuwa jambo lenye kuthawabisha, hasa kama unaenda huko kwa madhumuni ya kiroho. Labda wakati utafika ambapo utahitaji kurudi nyumbani. Andreas asema hivi: “Nikiwa na mambo mengi mazuri ya kukumbuka—yasiyo mazuri yanasahaulika upesi—ilikuwa vigumu sana kuondoka.” Ijapokuwa hivyo, usitazamie rafiki zako au familia yako kule nyumbani ibadili ghafula njia yao ya kufanya mambo sasa kwa kuwa umerudi na mitazamo mipya ambayo umejifunza kule ng’ambo. Na zaidi ya hayo, usiwaudhi kwa kuwakumbusha kila mara jinsi ambavyo mambo hufanywa kwingineko. Kwa kawaida, utataka kuambia kila mtu mambo uliyoyaona, lakini usikate tamaa ikiwa si kila mtu atasisimuka.

Ni wazi basi, uamuzi wa kuishi katika nchi ya kigeni wapaswa kuchukuliwa kwa uzito. Ikiwa baada ya kuzungumza mambo pamoja na wazazi wako, waamua kwamba kuna sababu halali za kuhama, jitayarishe kukabiliana na magumu utakayokuta. Kama ilivyo na uamuzi wowote mkubwa utakaofanya maishani, ni jambo la hekima kuhesabu gharama kwanza.—Luka 14:28-30.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Ona makala “Vijana Huuliza . . . Je, Nikaishi Ng’ambo?” inayopatikana katika toleo la Juni 22, 2000.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 27]

Vidokezi vya Usalama

● Weka pasipoti yako, pesa, na tiketi yako ya kwenda na kurudi mahali salama.

● Fanya fotokopi za pasipoti yako na vilevile kibali chako cha kukaa na/au visa, tiketi yako ya kwenda na kurudi, na hati nyingine za maana. Weka seti moja ya nakala hizo, na seti nyingine uitume kwa wazazi wako au rafiki zako kule nyumbani.

● Sikuzote uwe na namba za simu za wazazi wako au rafiki zako kule nyumbani na za familia inayokukaribisha.

● Dumisha mwenendo safi na washiriki wa jinsia tofauti, wawe ni wa familia inayokukaribisha, shuleni, kazini, au mahali pengine.

● Jifunze angalau maneno na misemo ya msingi ya lugha ya nchi ya wale wanaokukaribisha.

● Pimwa na daktari kabla ya kuondoka. Hakikisha kwamba una dawa zozote za kutosha unazohitaji.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Ikiwa hali ya kutoelewana na familia inayokukaribisha yatokea, ongea nao kwa njia ya utulivu